Ubatizo Wa Roho Mtakatifu

Sura Ya Kumi Na Moja

 

Mtu anaposoma kitabu cha Matendo ya Mitume, utendaji wa Roho Mtakatifu katika kanisa la kwanza ni dhahiri kwenye kila ukurasa. Ukiondoa kazi ya Roho Mtakatifu katika kitabu cha Matendo, huna kitu kilichobaki. Kweli, aliwatia nguvu wanafunzi wa kwanza ili “kuupindua ulimwengu” (tazama Matendo 17:6).

Siku hizi katika dunia yetu, mahali ambapo kanisa linakua kwa haraka ni pale ambapo wafuasi wa Yesu wmejitoa kwa Roho Mtakatifu kabisa na kuwezeshwa Naye. Hili lisitushangaze. Roho Mtakatifu anaweza kufanikisha mambo mengi kwa muda wa nukta kumi kuliko tunayoweza kufanikisha sisi kwa muda wa miaka elfu kumi, kwa juhudi zetu. Kwa hiyo, ni kitu muhimu sana kwamba mtumishi anayefanya watu kuwa wanafunzi aelewe Maandiko yanafundisha nini juu ya kazi ya Roho Mtakatifu katika maisha na huduma za waamini.

Mara kwa mara katika kitabu cha Matendo ya Mitume tunapata mifano ya waamini wakibatizwa kwa Roho Mtakatifu na kuwezeshwa kufanya huduma. Tuwe na busara kujifunza somo hili ili ikiwezekana, hata sisi tupate walichopata na kufurahia msaada wa kimuujiza waliopata wao kutoka kwa Roho Mtakatifu. Ingawa kuna wanaodai kwamba matendo hayo ya miujiza ya Roho Mtakatifu ilikuwa ni kwa ajili ya wakati wa mitume wenyewe tu, mimi sipati hoja ya kiMaandiko, kihistoria wala ya kiakili, yenye kuunga mkono maoni hayo. Wale wanaoamini kinachoahidiwa katika Neno la Mungu watapata baraka zilizotajwa. Sawa na Waisraeli ambao hawakuamini, walioshindwa kuingia katika Nchi ya Ahadi, wale wasioamini ahadi za Mungu kwa leo watashindwa kuingia katika yote ambayo Mungu amewaandalia. Je, wewe uko kundi gani? Mimi niko miongoni mwa wenye kuamini!

Kazi Mbili Za Roho Mtakatifu

Kila mtu aliyemwamini Bwana Yesu Kristo kabisa amefanyiwa kazi na Roho Mtakatifu maishani mwake. Utu wake wa ndani – au roho – umezaliwa upya kwa Roho Mtakat ifu (ona Tito 3:5), na Roho Mtakatifu anaka andani yake (ona Warumi 8:9; 1Wakor. 6:19). Yeye “amezaliwa kwa Roho” (Yohana 3:5).

Kwa kutoelea hili, Wakristo wengi wa Pentekoste na Karizmatiki wamekosea kwa kuwaambia waamini fulani kwamba hawakuwa na Roho Mtakatifu kama hawakuwa wamebatizwa kwa Roho Mtakat ifu na kunena kwa lugha. Hili ni kosa kutokana na Maandiko na hata ujuzi halisi wa maisha. Waamini wengi wasiokuwa WaPentekoste au WaKarizmatiki wana ushuhuda zaidi kwamba Roho anakaa ndani yao kuliko baadhi ya waamini wa KiPentekoste au KiKarizmatiki! Wanaonyesha matunda ya Roho yaliyotajwa na Paulo katika Wagalatia 5:22-23 kwa kiwango kikubwa sana, kitu ambacho kisingewezekana bila kuwa na Roho Mtakatifu ndani.

Kwa kuwa tu mtu amezaliwa na Roho si uhakikisho kwamba amebatizwa pia kwa Roho Mtakatifu. Kulingana na Biblia, kuzaliwa na Roho Mtakatifu na kubatizwa kwa Roho Mtakatifu ni vitu viwili tofauti.

Tunapoanza kuchambua mada hii, hebu kwanza tutazame yale ambayo Yesu aliyasema wakati fulani kuhusu Roho Mtakatifu, kwa mwanamke asiyeokoka, huko kisimani Samaria.

Kama ungeliijua karama ya Mungu naye ni nani akuambiaye, ‘Nipe maji ninywe’, ungalimwomba yeye naye angelikupa maji yaliyo hai. … Kila anywaye maji haya [kutoka kisimani] ataona kiu tena; walakini yeyote atakayekunywa maji yale nitakayompa mimi hataona kiu milele; bali yale maji nitakayompa yatakuwa ndani yake chemchemi ya maji, yakibubujikia uzima wa milele (Yohana 4:10, 13-14).

Ni halali kufikiri kwamba yale maji yanayokaa ndani ya mtu ambayo Yesu alizungumzia ni Roho Mtakatifu, anayekaa ndani ya wale wanaoamini. Baadaye katika Injili ya Yohana, Yesu alitumia tena maneno “maji yaliyo hai”, na hapo hakuna shaka kwamba alikuwa anazungumza juu ya Roho Mtakatifu.

Hata siku ya mwisho, siku ile kubwa ya sikukuu, Yesu akasimama na kupaza sauti yake, akasema hivi: ‘Mtu akiona kiu na aje kwangu anywe. Aniaminiye mimi kama vile maandiko yalivyonena, mito ya maji yaliyo hai itatoka ndani yake.’ Na neno hilo alilisema kwa habari ya Roho, ambaye wale wamwaminio watampokea baadaye; kwa maana Roho alikuwa hajaja, kwa sababu Yesu alikuwa hajatukuzwa (Yohana 7:37-39, TLR. Maneno mepesi kukazia).

Hapa, Yesu hakuzungumza juu ya maji yaliyo hai kuwa “chemchemi ya maji, yakibubujikia uzima wa milele”. Badala yake, hayo maji yaliyo hai yanafanyika mito ibubujikayo kutoka ndani ya mwenye kupokea.

Mafungu haya mawili ya Maandiko kutoka Injili ya Yohana huonyesha vizuri sana tofauti kati ya kuzaliwa kwa Roho na kubatizwa kwa Roho Mtakatifu. Kuzaliwa kwa Roho ni kwa faida ya yule aliyezaliwa upya, ili aweze kufurahia uzima wa milele. Mtu anapozaliwa tena kwa Roho, anapata hifadhi ya Roho ndani yake yenye kumpa uzima wa milele.

Lakini kubatizwa kwa Roho Mtakatifu ni kwa faida ya wengine, maana inawawezesha waamini kuwahudumia watu wengine kwa nguvu za Roho. “Mito ya maji yaliyo hai” itabubujika kutoka ndani yao, ikileta baraka za Mungu kwa wengine kwa nguvu za Roho Mtakatifu.

Ubatizo Wa Roho Mtakatifu Unahitajika Kwa Nini?

Tunahitaji sana msaada wa Roho Mtakatifu ili tuweze kuwahudumia wengine! Bila msaada Wake, hatuwezi kutumaini kuwafanya watu wote kuwa wanafunzi. Hiyo ndiyo sababu hasa iliyomfanya Yesu kuahidi kuwabatiza waamini kwa Roho Mtakatifu – ili dunia ipate kusikia Injili. Aliwaambia hivi wanafunzi Wake:

Na tazama, nawaletea juu yenu ahadi ya Baba yangu, lakini kaeni humu mjini hata mvikwe uwezo utokao juu (Luka 24:49 – Maneno mepesi kutilia mkazo).

Luka tena anaandika maneno mengine ya Yesu, kwamba:

Si kazi yenu kujua nyakati wala majira, Baba aliyoyaweka katika mamlaka yake mwenyewe. Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi (Matendo 1:7-8. Maneno mepesi kutilia mkazo).

Yesu aliwaambia wanafunzi Wake hata wasiondoke Yerusalemu mpaka “wavikwe uwezo kutoka juu.” Alijua wasingekuwa na uwezo kama si hivyo, na wangeshindwa kabisa kutekeleza kazi aliyokuwa amewapa. Tunaona kwamba mara baada ya kubatizwa kwa Roho Mtakatifu, Mungu alianza kuwatumia wao kwa njia ya ajabu sana kueneza Injili.

Wakristo milioni nyingi duniani, baada ya kubatizwa na Roho Mtakatifu, wamefahamu na kutambua kiwango kipya cha nguvu, hasa wakati wa kuwashuhudia watu ambao hawajaokoka. Waligundua kwamba maneno yao yalikuwa na maana zaidi, na kwamba wakati mwingine walitaja maandiko ambayo hawakujua waliyafahamu. Baadhi yao walijikuta wenyewe wakiwa wameitwa na kupewa karama kwa ajili ya huduma fulani, kama vile uinjilisti. Wengine waligundua kwamba Mungu aliwatumia kama alivyopenda katika karama mbalimbali za Roho Mtakatifu. Ujuzi wao ni wa KiBiblia kabisa. Wale wanaopinga ujuzi wao hawana msingi wowote KiBiblia kwa ajili ya kuwapinga. Ukweli ni kwamba wanapingana na Mungu.

Isitushangaze sisi ambao tumeitwa kumwiga Kristo kwamba tumeitwa kuiga ujuzi Wake na ROho Mtakatifu. Yeye alitungwa mimba tumboni mwa Mariamu kwa Roho Mtakatifu (ona Mathayo 1:20). Yeye aliyezaliwa kwa Roho alikuja kubatizwa na Roho kabla ya kuanza huduma Yake (ona Mathayo 3:16). Kama Yesu alihitaji kubatizwa na Roho Mtakatifu ili kumwezesha katika huduma, sisi je?

Ushahidi Wa Kwanza Kwamba Mtu Amebatizwa Katika Roho Mtakatifu

Mwamini anapobatizwa katika Roho Mtakatifu, ushahidi wa kwanza wa ujuzi wake ni kwamba ananena kwa lugha mpya, au kama Maandiko yanavyosema wakati mwingine, “lugha nyingine.” Kuna maandiko mengi sana yanayothibitisha jambo hilo. Hebu tuyatazame.

Kwanza – Muda mfupi tu kabla ya kupaa Kwake, yesu alisema kwamba mojawapo ya ishara zitakazofuatana na waamini ni kwamba wangesema kwa lugha mpya.

Enendeni ulimwenguni mwote, mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe. Aaminiye na kubatizwa ataokoka, asiyeamini atahukumiwa. Na ishara hizi zitafuatana na hao waaminio: kwa jina langu watatoa pepo, watasema kwa lugha mpya (Marko 16:15-17. Maneno mepesi kutilia mkazo).

Kuna waandishi wa vitabu vya mafafanuzi vya Biblia wanaodai kwamba maandiko hayo hayapaswi kuwa katika Biblia zetu kwa sababu baadhi ya magombo fulani ya zamani ya Agano Jipya hayana fungu hilo. Lakini, mengi katika magombo ya kale yana fungu hilo, na hakuna tafsiri nyingi za Kiswahili za Biblia ambazo hazina fungu hilo. Tena, yale ambayo Yesu alisema katika maandiko haya yanalingana vizuri tuna ujuzi wa kanisa la kwanza kama tunavyopata habari zake katika kitabu cha Matendo ya Mitume.

Kuna mifano mitano katika kitabu cha Matendo, yenye kuonyesha waamini wakibatizwa kwa mara ya kwanza na Roho Mtakatifu. Hebu tuitazame yote, na tutakapokuwa tunafanya hivyo, tutajiuliza maswali mawili yafuatayo: (1) Je, Ubatizo kwa Roho Mtakatifu ulikuwa ni kitu baada ya wokovu? Na (2) Je, waliopokea walinena kwa lugha mpya? Hii itatusaidia kuelewa mapenzi ya Mungu kwa ajili ya waamini siku za leo.

Yerusalemu

Mfano wa kwanza unapatikana katika Matendo sura ya 2, wakati wale wanafunzi mia na ishirini walipobatizwa kwa Roho Mtakatifu siku ya Pentekoste.

Hata ilipotimia siku ya Pentekoste walikuwako wote mahali pamoja. Kukaja ghafula toka mbinguni uvumi kama uvumi wa upepo wa nguvu ukienda kasi, ukaijaza nyumba yote waliyokuwa wameketi. Kukawatokea ndimi zilizogawanyikana, kama ndimi za moto uliowakalia kila mmoja wao. Wote wakajazwa Roho Mtakatifu, wakaanza kusema kwa lugha nyingine, kama Roho alivyowajalia kutamka (Matendo 2:1-4. Maneno mepesi kutilia mkazo).

Hakuna shaka yoyote kwamba wale waamini mia na ishirini walikuwa wamekwisha okoka na kuzaliwa mara ya pili kabla ya wakati huo. Basi, walipokea ubatizo wa Roho Mtakatifu baada ya wokovu. Hata hivyo isingewezekana kwao kubatizwa katika Roho Mtakatifu kabla ya wakati huo kwa sababu Roho Mtakatifu hakuwa ametolewa kwa kanisa kabla ya siku hiyo.

Ni dhahiri basi kwamba ishara iliyoambatana na tendo hilo ilikuwa kunena kwa lugha nyingine.

Samaria

Mfano wa pili wa waamini kubatizwa kwa Roho Mtakatifu unapatikana katika Matendo sura ya 8, wakati Filipo alipokwenda jijini Samaria na kuhubiri Injili huko.

Lakini [WaSamaria] walipomwamini Filipo, akizihubiri habari njema za ufalme wa Mungu na jina lake Yesu Kristo, wakabatizwa, wanaume na wanawake. … Na mitume waliokuwako Yerusalemu waliposikia ya kwamba Samaria imelikubali neno la Mungu, wakawapelekea Petro na Yohana, ambao waliposhuka, wakawaombea wampokee Roho Mtakatifu, kwa maana bado hajawashukia hata mmoja wao, ila wamebatizwa tu kwa jina lake Bwana Yesu (Matendo 8:12-16).

Ni wazi kwamba Wakristo WaSamaria walipokea ubatizo wa Roho Mtakatifu kama kitu cha zaidi baada ya wokovu wao. Biblia inasema wazi kabisa kwamba kabla Petro na Yohana hawajafika, WaSamaria tayari walikuwa “wamelipokea neno la Mungu,” wameiamini Injili na kubatizwa katika maji. Lakini, wakati Petro na Yohana walipokuja kuwaombea, Maandiko yanasema ni ili wampokee Roho Mtakatifu.” Iwekwe wazi zaidi kuliko hapo jamani?

Je, waamini wa Samaria walinena kwa lugha mpya walipobatizwa kwa Roho Mtakatifu? Biblia haisemi, lakini inasema kwamba kitu cha kushangaza kilitokea kwao. Wakati mtu aitwaye Simoni alipoona yaliyotokea baada ya Petro na Yohana kuweka mikono yao juu ya Wakristo wa Samaria, alijaribu kununua kutoka kwao uwezo huo huo wa kumtoa Roho Mtakatifu.

Ndipo wakaweka mikono yao juu yao, nao wakampokea Roho Mtakatifu. Hata Simoni alipoona ya kuwa watu wanapewa Roho Mtakatifu kwa kuwekewa mikono ya mitume, akataka kuwapa fedha akisema, ‘Nipeni na mimi uwezo huu, ili kila mtu nitakayemweka mikono yangu apokee Roho Mtakatifu’ (Matendo 8:17-19).

Je, Simoni aliona nini kilichomshika hivyo? Tayari alikwisha ona miujiza mingi tu mingine, kama vile watu wakitolewa mapepo na waliolemaa na viwete wakiponywa (ona Matendo 8:6-7). Yeye mwenyewe alikuwa amehusika katika uchawi hapo kwanza, akiwashangaza watu wote wa Samaria (ona Matendo 8:9-10). Kama ni hivyo, alichokiona wakati Petro na Yohana walipoomba lazima kingekuwa kitu cha ajabu sana. Ingawa hatuwezi kusema kwa uhakika kabisa, inaonekana ni sawa kufikiri kwamba aliona kitu cha kushangaza kile kile kilichokuwa kinatokea kila mara ambapo Wakristo walipokea Roho Mtakatifu katika kitabu cha Matendo ya Mitume – aliona na kuwasikia watu wa Samaria wakinena kwa lugha nyingine.

Sauli Huko Dameski

Mara ya tatu katika kitabu cha Matendo kunapotajwa mtu akimpokea Roho Mtakatifu ni kwa habari ya Sauli wa Tarso, ambaye baadaye alijulikana kama mtume Paulo. Aliokolewa akiwa njiani kwenda Dameski, na alikuwa amepofuka kwa muda. Siku tatu baada ya kuokoka kwake, mtu aitwaye Anania alitumwa kwake na Mungu.

Anania akaenda zake, akaingia mle nyumbani, akamwekea mikono akisema, ‘Ndugu Sauli! Bwana amenituma, Yesu, yeye aliyekutokea katika njia uliyoijia, upate kuona tena, ukajazwe Roho Mtakatifu.’ Mara vikaanguka machoni pake vitu kama magamba, akapata kuona, akasimama, akabatizwa (Matendo 9:17, 18).

Hapana shaka kwamba Sauli aliokoka kabla ya Anania kufika kumwombea. Alimwamini Bwana Yesu alipokuwa yungali njiani kwenda Dameski, na mara moja akatii maagizo ya Bwana wake mpya. Tena, wakati Anania alipokutana na Sauli mara ya kwanza alimwita “Ndugu Sauli.” Ona kwamba Anania alimwambia Sauli kwamba amekuja ili apate kuona na kujazwa na Roho Mtakatifu. Basi kwa Sauli, kujazwa na Roho Mtakatifu – au kubatizwa basi – kulitokea siku tatu tu baada ya kuokoka kwake.

Maandiko hayasemi tukio hilo la Sauli kubatizwa na Roho Mtakatifu, lakini bila shaka lilifanyika muda mfupi tu baada ya Anania kufika mahali Sauli alipokuwa. Hakuna shaka kwamba Sauli alinena kwa lugha kwa sababu, baadaye anasema katika 1Wakor. 14:18 hivi: “Namshukuru Mungu kwamba mimi nanena kwa lugha kuliko ninyi wote” (TLR).

Kaisaria

Mara ya nne ambapo waamini wanatajwa kwamba wamebatizwa kwa Roho Mtakatifu ni katika Matendo 10. Mtume Petro alikuwa ameagizwa na Mungu kwenda kuhubiri Injili huko Kaisaria, nyumbani kwa Kornelio. Mara tu baada ya Petro kudhihirisha kwamba wokovu hupokelewa kwa imani katika Yesu, wasikilizaji wake wote waliokuwa si Wayahudi (yaani, WaMataifa) waliitikia kwa imani, na Roho Mtakatifu akawashukia.

Petro alipokuwa akisema maneno hayo Roho Mtakatifu akawashukia wote waliolisikia lile neno. Na wale waliotahiriwa, walioamini, wakashangaa, watu wote waliokuja pamoja na Petro, kwa sababu Mataifa nao wamemwagiwa kipawa cha Roho Mtakatifu. Kwa maana waliwasikia wakisema kwa lugha na kumwadhimisha Mungu. Ndipo Petro akajibu, ‘Ni nani awezaye kuzuia maji, hawa wasibatizwe, watu waliopokea Roho Mtakatifu vile vile kama sisi?’ Akaamuru wabatizwe kwa Jina lake Yesu Kristo (Matendo 10:44-48a).

Hapa, inaonekana kwamba watu wote wa nyumbani mwa Kornelio, waliokuwa wasiokuwa Wayahudi wa kwanza kumwamini Yesu, walizaliwa mara ya pili na kubatizwa hapo hapo.

Tukijifunza maandiko yanayoambatana na hayo pamoja na mantiki kihistoria, kuna sababu iliyo dhahiri kabisa iliyomfanya Mungu asingojee Petro na waamini wenzake wawawekee mikono waamini wale wasiokuwa Wayahudi, ili wapokee Roho Mtakatifu. Petro na waamini wanzake wa Kiyahudi walikuwa na shida sana kuamini kwamba wasiokuwa Wayahudi wanaweza kuokoka – achilia mbali kumpokea Roho Mtakatifu! Yawezekana wasingewaombea familia ya Kornelio wapokee ubatizo wa Roho Mtakatifu. Basi Mungu akafanya kwa enzi Yake. Mungua likuwa anamfundisha Petro na wenzake kitu kuhusu neema Yake ya ajabu kwa wasiokuwa Wayahudi.

Kilichomshawishi Petro na wale waamini wengine Wayahudi kwamba familia ya Kornelio walipokea Roho Mtakatifu kweli ni nini? Luka anaandika hivi: “Kwa maana waliwasikia wakisema kwa lugha” (Luka 10:46). Petro akatamka kwamba wasiokuwa Wayahudi wamempokea Roho Mtakatifu kama wale mia na ishirini walivyofanya siku ya Pentekoste (ona 10:47).

Efeso

Mara ya tano ambapo waamini wanatajwa kubatizwa katika Roho Mtakatifu ni katika Matendo sura ya 19. Alipokuwa anasafiri na kupitia Efeso, mtume Paulo alikutana na wanafunzi fulani, akawauliza hivi: “Je, mlipokea Roho Mtakatifu mlipoamini?” (Matendo 19:2, TLR).

Paulo, mtu aliyeandika sehemu kubwa ya nyaraka za Agano Jipya aliamini dhahiri kabisa kwamba inawezekana kumpokea Yesu na usiwe umempokea Roho Mtakatifu.Vinginevyo, asingeuliza swali alilouliza.

Wale ndugu wakajibu kwamba hawakuwa hata wamesikia kuhusu Roho Mtakatifu. Ni kwamba walikuwa wamesikia kuhusu Masiye anayekuja tu kupitia Yohana Mbatizaji, ambaye alikuwa amewabatiza. Paulo mara moja akawabatiza tena kwa maji, na wakati huu wakawa wamebatizwa Kikristo. Hatimaye, Paulo akawawekea mikono ili wapokee Roho Mtakatifu.

Waliposikia haya wakabatizwa kwa jina la Bwana Yesu. Na Paulo, alipokwisha kuweka mikono yake juu yao, Roho Mtakatifu akaja juu yao, wakaanza kunena kwa lugha, na kutabiri. Na jumla yao walipata wanaume kumi na wawili (Matendo 19:5-7).

Hapa tena ni kitu wazi kwamba ubatizo wa Roho Mtakatifu ulikuwa baada ya wokovu, bila kujali kama hao watu kumi na mbili walikuwa wameokoka kabla ya kukutana na Paulo. Tena, ishara iliyoambatana na wao kubatizwa kwa Roho Mtakatifu ilikuwa kunena kwa lugha (na hapa, kutabiri pia).

Sawa – Hebu tuitazame tena ile mifano mitano. Katika mifano minne, ubatizo kwa Roho Mtakatifu ulikuwa kitu kilichotokea baada ya wokovu.

Katika mifano mitatu, Maandiko yanasema wazi kabisa kwamba wahusika walinena kwa lugha nyingine. Tena, Paulo alipokutana na Anania, yeye kubatizwa kwa Roho Mtakatifu hakuelezwi, lakini tunajua kwamba hatimaye alikuja kunena kwa lugha. Huo ni mfano wa nne.

Katika mfano uliosalia, kitu kisicho cha kawaida kilitokea wakati waamini huko Samaria walipompokea Roho Mtakatifu kwa sababu, Simoni alijaribu kununua nguvu za kumtoa Roho Mtakatifu.

Basi, ushahidi uko wazi kabisa. Katika kanisa la kwanza, waamini waliozaliwa mara ya pili walipata kitu kingine na Roho Mtakatifu, na walipofanya hivyo, walinena kwa lugha nyingine. Hii isitushangaze kwa sababu Yesu alisema wale wanaomwamini watanena kwa lugha nyingine.

Tunao ushahidi thabiti kabisa kwamba kila mtu aliyezaliwa mara ya pili anatakiwa pia kupokea kazi nyingine ya Roho Mtakatifu – kubatizwa katika Roho Mtakatifu. Tena, kila mwamini anapaswa kutazamia kunena kwa lugha nyingine wakati anapobatizwa kwa Roho Mtakatifu.

Jinsi Ya Kupokea Ubatizo Wa Roho Mtakatifu

Roho Mtakatifu hupokelewa kwa imani (Wagal. 3:5), sawa tu na zawadi nyingine zote za Mungu. Ili kuwa na imani ya kupokea, mwamini anatakiwa kwanza ashawishike kwamba ni mapenzi ya Mungu kwake kubatizwa kwa Roho Mtakatifu. Kama ana mashaka au wasiwasi, hatapokea (ona Yakobo 1:6-7).

Hakuna mwamini yeyote mwenye sababu nzuri ya kuamini kwamba si mapenzi ya Mungu kwake kupokea Roho Mtakatifu, kwa sababu Yesu alieleza waziwazi mapenzi ya Mungu kuhusu swala hilo.

Basi, ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Baba aliye mbinguni hatazidi sana kuwapa Roho Mtakatifu hao wamwombao? (Luka 11:13).

Ahadi hiyo kutoka kwa Yesu inapaswa kumwaminisha kila mtoto wa Mungu kwamba ni mapenzi ya Mungu yeye apokee Roho Mtakatifu.

Mstari huo huo pia unathibitisha ukweli kwamba kubatizwa kwa Roho Mtakatifu hutokea baada ya wokovu, kwa sababu hapa Yesu aliwaahidi watoto wa Mungu (watu pekee ambao Mungu ndiye “Baba yao wa mbinguni”) kwamba angewapa Roho Mtakatifu, wakiomba. Bila shaka ni kwamba, kama ujuzi pekee na Roho Mtakatifu ambao mtu angepata ni kuzaliwa mara ya pili wakati wa wokovu tu, basi ahadi ya Yesu isingekuwa na maana. Kinyume na kikundi cha wanatheolojia wachache wa kisasa ambacho kinaelekea kutoweka, Yesu aliamini kwamba ni sawa kabisa kwa watu waliokwisha zaliwa mara ya pili kumwomba Mungu awape Roho Mtakatifu.

Kwa maneno ya Yesu, kuna masharti mawili tu ambayo lazima mtu atimize ikiwa anataka kupokea Roho Mtakatifu. Kwanza – Mungu lazima awe Baba, na ndivyo ilivyo kama umezaliwa mara ya pili. Pili – umwombe Roho Mtakatifu.

Pamoja na kwamba kumpokea Roho Mtakatifu kwa kuwekewa mikono ni kitu kinachoungwa mkono na Maandiko (ona Matendo 8:17; 19:6), si lazima. Mkristo yeyote anaweza kumpokea Roho Mtakatifu akiwa peke yake katika faragha yake ya maombi. Anachohitaji kufanya ni kuomba tu, kupokea kwa imani, na kuanza kunena kwa lugha kama Roho atakavyomwezesha kutamka.

Hofu Za Wengi

Kuna watu wenye kuogopa kwamba wakiomba Roho Mtakatifu, wanaweza kujiweka wazi kuingiwa na pepo. Hakuna msingi wowote wa hofu kama hiyo. Yesu aliahidi hivi:

Maana ni yupi kwenu aliye baba, ambaye mwanamwe akimwomba mkate atampa jiwe, au samaki, badala ya samaki atampa nyoka? Au akiomba yai, atampa nge? Basi, ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Baba yenu wa mbinguni hatazidi sana kuwapa Roho Mtakatifu hao wamwombao? (Luka 11:11-13).

Tukiomba Roho Mtakatifu, Mungu atatupa Roho Mtakatifu. Tusiwe na hofu kwamba tutapokea kitu kingine chochote!

Kuna wengine wenye kuogopa kwamba, wakinena kwa lugha, ni kitu chao watakachokuwa wametunga badala ya lugha ya kimuujiza itolewayo na Roho Mtakatifu. Sawa – ila, kama utajaribu kutunga lugha ya hakika kabla ya kubatizwa na Roho Mtakatifu utagundua kwamba ni kitu kigumu sana, kisichowezekana. Ila, ni lazima uelewe kwamba kama utanena kwa lugha nyingine, itakubidi utumie midomo yako, ulimi, na ngano za sauti. Roho Mtakatifu hakusemei – anakupa lugha. Yeye ni msaidizi wetu, si anayetenda. Inakupasa wewe useme. Ni kama Biblia inavyofundisha, kwamba:

Wote wakajazwa Roho Mtakatifu, wakaanza kusema kwa lugha nyingine, kama Roho alivyowajalia kutamka (Matendo 2:4 – Maneno mepesi kutilia mkazo).

Na Paulo, alipokwisha kuweka mikono yake juu yao, Roho Mtakatifu akaja juu yao; wakaanza kunena kwa lugha (Matendo 19:6 – Maneno mepesi kutilia mkazo).

Baada ya mwamini kuomba zawadi ya Roho Mtakatifu, anatakiwa kuamini na kutazamia kunena kwa lugha nyingine. Kwa kuwa Roho Mtakatifu anapokelewa kwa imani, mwenye kupokea asitazamie hisia za namna fulani au msisimko kimwili. Anatakiwa kufungua kinywa chake tu na kuanza kutamka zile sauti mpya na silabi zitakazosababisha ile lugha mpya ambayo Roho Mtakatifu anampa. Mwamini asipoanza kusema kwa imani, hakuna maneno yatakayotokea kinywani mwake. Ni lazima yeye aseme, ndipo Roho Mtakatifu atakapomjalia kutamka.

Mahali Lugha Inapotoka

Kulingana na Paulo – aaminiye anapoomba kwa lugha – si akili yake iombayo bali ni roho yake.

Maana nikiomba kwa lugha,roho yangu huomba, lakini akili zangu hazina matunda. Imekuwaje, basi? Nitaomba kwa roho, tena nitaomba kwa akili pia, nitaimba kwa roho, tena nitaimba kwa akili pia (1Wakor. 14:14-15).

Paulo alisema kwamba alipoomba kwa lugha, akili yake haikuwa na matunda. Maana yake ni kwamba akili yake ilikuwa haihusiki, wala hakuelewa alichokuwa anaomba kwa lugha. Basi, anachosema ni kwamba, badala ya kuomba kwa lugha wakati wote na huku haelewi anachosema, alikuwa pia anaomba kwa akili, kwa lugha yake mwenyewe. Alitumia muda mwingi kuimba kwa lugha na kuimba kwa akili yake pia. Ipo nafasi kwa maombi ya aina zote hizo mbili pamoja na kuimba kwa aina zote hizo mbili, nasi tuwe na busara kufuata mfano wa Paulo.

Ona pia kwamba, kwa Paulo, kunena kwa lugha kulikuwa chini ya mamlaka ya mapenzi yake, sawa na jinsi kuzungumza lugha yake kulivyokuwa. Alisema hivi: “Nitaomba kwa roho na nitaomba kwa akili pia” (TLR). Mara nyingi wakosoaji hudai kwamba kama kunena kwa lugha siku hizi ni zawadi kweli kutoka kwa Mungu, hakuna mtu ambaye angeweza kuitawala, maana kufanya hivyo ni sawa na kumtawala Mungu. Wazo kama hilo halina msingi wowote. Kunena kwa lugha zamani na siku hizi kuko chini ya mamlaka ya mtu binafsi, na ndivyo Mungu alivyopanga. Wakosoaji hao ni vizuri waendelee na kusema kwamba watu wenye mikono ambayo imeumbwa na Mungu kweli hawana mamlaka na utawala juu ya mikono yao, na watu wenye kufanya maamuzi ya kutumia mikono yao wanamtawala Mungu.

Ukisha batizwa kwa Roho Mtakatifu, ni rahisi sana kuthibitisha kwamba kunena kwa lugha kwako kunatoka rohoni na si akilini mwako. Kwanza – Hebu jaribu kuzungumza na mtu huku unasoma kitabu hiki. Utaona kwamba huwezi kufanya yote mawili kwa wakati mmoja. Lakini, utagundua kwamba unaweza kuendelea kunena kwa lugha unapoendelea kusoma hiki kitabu. Sababu ni hii: hutumii akili yako kunena kwa lugha – tendo la kunena hutoka rohoni mwako. Basi, unapotumia roho yako kuomba, waweza pia kutumia akili yako kusoma na kuelewa.

Sasa – Kwa Kuwa Umebatizwa Kwa Roho Mtakatifu

Usisahau sababu kuu ya Mungu kukupa ubatizo wa Roho Mtakatifu – ni ili kukutia nguvu kwa ajili ya kuwa shaiidi Wake, kwa madhihirisho ya tunda na karama (au zawadi) za Roho Mtakatifu (ona 1Wakor. 12:4-11; Wagal. 5:22-23). Unapoishi maisha yanayofanana na Kristo na kujonyesha upendo Wake, furaha na amani Yake kwa dunia pamoja na kudhihirisha karama zisizo za kawaida za Roho, Mungu atakutumia kuwavuta wengine Kwake. Uwezo wa kunena kwa lugha ni sehemu moja tu ya “mito ya maji yaliyo hai” inayotakiwa kububujika kutoka ndani mwako.

Pia kumbuka kwamba Mungu alitupa Roho Mtakatifu atuwezeshe kuwafikishia Injili watu wote duniani (ona Matendo 1:8). Tunaponena kwa lugha zingine, tunapaswa pia kutambua kwamba lugha tunayosema inaweza kuwa lugha ya kabila fulani au nchi fulani ya kigeni. Kila mara tunapoomba kwa lugha, tukumbuke kwamba Mungu anataka watu wa kila lugha wasikie habari za Yesu. Tunapaswa kumwomba Bwana kuhusu jinsi anavyotaka sisi tuhusike kutimiza Agizo Kuu la Yesu Kristo.

Kunena kwa lugha ni kitu tunachopaswa kufanya mara nyingi iwezekanavyo. Paulo – mtu wa hali ya juu sana kiroho – aliandika hivi: “Ninamshukuru Mungu kwamba mimi nanena kw alugha zaidi yenu wote” (1Wakor. 14:18, TLR). Aliandika maneno hayo kwa kanisa lililokuwa linanena sana kwa lugha (japo kwa nyakati zisizofaa). Basi, Paulo bila shaka alinena kwa lugha mara nyingi sana mpaka akawazidi. Kuomba kwa lugha hutusaidia kumtambua Roho Mtakatifu anayeishi ndani yetu, na itatusaidia “kuomba bila kukoma” kama Paulo alivyofundisha katika 1Wathes. 5:17.

Vile vile Paulo alifundisha kwamba kunena kwa lugha zingine humjenga mwamini (ona 1Wakor. 14:4). Maana yake ni kwamba inatujenga kiroho. Kwa kuomba kwa lugha, tunatia nguvu utu wetu wa ndani kwa njia tusizoelewa kabisa. Kunena kwa lugha kunatakiwa kuleta utajiri mpya kila siku katika maisha ya kiroho ya kila aaminiye, wala si tukio la wakati mmoja tu tunapojazwa na Roho Mtakatifu mara ya kwanza.

Ukiisha batizwa kwa Roho Mtakatifu, ninakutia moyo utumie muda mwingi kila siku kumwomba Mungu kwa lugha yako mpya. Itakusaidia sana katika maisha yako ya kiroho na kukua kwako kiroho.

Majibu Kwa Maswali Kadhaa Ya Kawaida

Je, tunaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba wote ambao hawajawahi kunena kwa lugha hawajabatizwa na Roho Mtakatifu? Mimi nadhani sivyo.

Sikuzote nimewatia watu moyo watazamie kunena kwa lugha wakati nilipowaombea kubatizwa kwa Roho Mtakatifu, nami nadhani asilimia 95 ya hao walifanya hivyo baada ya kuwaombea kwa nukta chache. Ni maelfu ya watu kwa kipindi cha miaka mingi sana.

Lakini siwezi kusema kwamba Mkristo aliyeomba kubatizwa kwa Roho na ambaye hajanena kwa lugha hajabatizwa na Roho Mtakatifu. Hii ni kwa sababu ubatizo wa Roho hupokelewa kwa imani, na kunena kwa lugha ni kitu cha hiari. Ila, nipatapo nafasi ya kuzungumza na mwamini ambaye ameomba kubatizwa na Roho Mtakatifu lakini hajawahi kunena kwa lugha, ninachoanza nacho ni kumwonyesha mtu huyo maandiko yote katika kitabu cha Matendo kuhusu swala lenyewe. Isha, ninamwonyesha huyo mwamini jinsi ambavyo Paulo aliandika, kwamba yeye husimamia wakati wa kunena na wakati wa kutonena kwa lugha. Kama Paulo, mimi mwenyewe naweza kunena kwa lugha wakati wowote ninaotaka, na hivyo naweza kuamua, nikitaka, kutonena tena kwa lugha. Kama ni hivyo, inawezekana nikawa nimebatizwa kwa Roho Mtakatifu na kutonena kwa lugha kwa kutoshirikiana na tamko analoleta Roho Mtakatifu.

Basi – ninapokuwa na nafasi ya kuzungumza na Mkristo ambaye ameomba kwa imani apokee ubatizo wa Roho Mtakatifu lakini hajawahi kunena kwa lugha, simwambii jinsi ambavyo kunena kwa lugha si kitu Roho anachofanya bila sisi. Ninajaribu kumweleza kwamba Roho Mtakatifu ndiye ajaliaye kutamka, lakini sisi lazima tuseme – au tunene – sawa tu na jinsi ambavyo inakuwa mtu anaposema lugha ya kawaida. Kisha ninamtia moyo mtu huyo kushirikiana na Roho Mtakatifu na kuanza kunena kwa lugha. Mara nyingi baada ya hayo, watu hao hunena baadaye.

Je, Paulo Hakuandika Kwamba Si Wote Wanenao Kwa Lugha?

Swali la Paulo – “Kwani ni wote wanenao kwa lugha?” (1Wakor. 12:30) – ambalo jibu lake dhahiri ni “Hapana” lazima litazamwe kwa kuangalia Agano Jipya kwa jumla. Swali lake linapatikana katika mantiki ya mafundisho aliyotoa juu ya karama za kiroho, ambazo zinadhihirishwa kadiri Roho apendavyo tu (1Wakor. 12:11). Paulo alikuwa anaandika kuhusu karama ile ya “aina za lugha” (1Wakor. 12:10), ambayo, kulingana na Paulo, lazima kila mara iambatane na karama ya kiroho ya tafsiri za lugha. Hii karama isingeweza kuwa ile ambayo Wakorintho waliitumia mara kwa mara kanisani mwao, kwa sababu wao walikuwa wananena kwa lugha hadharani pasipo kuwepo na mtu wa kutafsiri. Tunatakiwa kujiuliza hivi: Kwa nini Roho Mtakatifu atoe karama ya lugha kwa mtu katika ibada ya hadhara, bila ya kumpa mtu mwingine karama ya kutafsiri? Jibu ni kwamba hawezi kufanya hivyo, maana akifanya, hawi anaendeleza mapenzi ya Mungu.

Bila shaka Wakorinto walikuwa wanaomba kwa lugha kwa sauti wakati wa ibada zao kanisani bila ya kuwepo na tafsiri aina yoyote. Basi, tunajifunza kwamba kunena kwa lugha kuna matumizi mawili tofauti. Moja ni kuomba katika lugha, ambako Paulo anasema kufanywe kibinafsi. Matumizi hayo hayaambatani na tafsiri, kama Paulo alivyoandika, kwamba, “Roho yangu huomba, lakini akili yangu haina matunda” (1Wakor. 14:14). Ni kwamba Paulo hakujua kila wakati alikuwa anasema nini aliponena kwa lugha. Hakuelewa, wala haikuwepo tafsiri.

Ila pia kuna matumizi ya kunena kwa lugha ambayo ni kwa ajili ya kusanyiko, na hayo huambatana na karama ya tafsiri ya lugha. Hiyo hutokea wakati Roho Mtakatifu anapomjia mtu fulani kama apendavyo, akimpa karama hiyo. Mtu huyo atanena waziwazi, kisha inakuwepo tafsiri. Ila, Mungu hamtumii kila mtu hivyo. Ndiyo sababu Paulo aliandika kwamba si wote wanenao kwa lugha. Si wote wanaotumiwana Mungu katika kile kipawa kitolewacho mara moja cha lugha, kama ambavyo Mungu hamtumii kila mtu katika karama ya tafsiri za lugha. Hiyo tu ndiyo njia rahisi ya kufafanua swali la Paulo – “Kwani ni wote wanenao kwa lugha?” – na yanayofundishwa na Maandiko kwa ujumla.

Mimi naweza kunena kwa lugha wakati wowote nitakao, kama na Paulo pia. Basi, hatuwezi kusema kwamba kila tunaponena kwa lugha, ni “kama Roho apendavyo tu.” Hapana – ni kama sisi tupendavyo. Kwa hiyo, tunachofanya kila tunapotamani si karama ya kunena kwa lugha itokeayo “kama Roho apendavyo tu.” Tena, Paulo – kama mimi – alinena kwa lugha kibinafsi pasipo kuelewa alichokuwa anasema. Basi, hiyo si karama ya lugha ambayo aliandika habari zake katika 1Wakorintho, aliyosema kwamba lazima kila mara iambatane na karama ya tafsiri ya lugha.

Ni mara chache sana nimenena kwa lugha katika kusanyiko. Ni wakati nilipojisikia kwamba Roho Mtakatifu amenishukia ili nifanye hivyo, japo ningeweza (kama Wakorintho walivyokuwa wanafanya) kuomba kwa lugha kwa sauti wakati wowote niliotaka nikiwa kanisani bila ya kuwepo tafsiri. Ninapohisi Roho Mtakatifu akinijilia kwa nguvu na karama hiyo, kila mara imekuwepo tafsiri ambayo ilileta kujengwa kwa mwili wa Kristo wakati huo.

Tunapohitimisha sehemu hii, ni vizuri kutafsiri Biblia kwa umoja. Wale wanaosema kwamba si waamini wote wanaopaswa kunena kwa lugha kwa sababu ya swali la Paulo katika 1Wakorinto 12:30, wanapuuza maandiko mengine mengi sana yasiyokubaliana na tafsiri yao. Kwa sababu ya kosa lao, wanakosa baraka kubwa sana kutoka kwa Mungu.

Mhubiri Aliyependwa Na Yesu

Sura Ya Tisa

 

Labda utashangaa kujua kwamba Yesu alimpenda sana mhubiri fulani. Pengine utashangaa zaidi kujua kwamba mhubiri huyo aliyependwa na Yesu hakuwa Mluteri, wala Mmethodisti, wala Mpentekoste, wala Mwanglikana au hata Mpresbiteri. Alikuwa Mbatisti! Tunamfahamu sana kama Yohana Mbatizaji! Umemkumbuka? Yesu alisema hivi juu yake:

Amin nawaambia, miongoni mwa watu waliozaliwa na mwanamke hajawahi kutokea aliye mkuu kuliko Yohana Mbatizaji (Mathayo 11:11a, TLR).

Kwa kuwa watu wote “wanazaliwa na mwanamke”, hii ilikuwa namna nyingine ya kusema kwamba Yesu alimhesabu Yohana Mbatizaji kuwa mtu mkuu katika watu waliowahi kuishi. Sababu ya Yesu kufikiri hivyo si dhahiri, ila ni halali kufikiri kwamba Yesu alimhesabu Yohana kuwa mtu mkuu sana kwa sababu ya sifa zake kiroho. Kama ndivyo, ni busara hata sisi tujifunze na kuiga sifa hizo za kiroho. Nimepata kama sifa saba za kiroho katika maisha ya Yohana Mbatizaji zinazostahili kupongezwa. Japo huduma ya Yohana ni mfano wa huduma ya mwinjilisti zaidi, hizo sifa zote saba za kiroho zinafaa kwa mtumishi yeyote wa Injili. Hebu tutazame ya kwanza katika hizo saba.

Sifa Ya Kwanza Ya Yohana

Na huu ndio ushuhuda wake Yohana, Wayahudi walipotuma kwake makuhani na Walawi kutoka Yerusalemu ili wamwulize, “Wewe u nani?” Naye alikiri, wala hakukana. Alikiri kwamba, “Mimi siye Kristo”. Wakamwuliza, “Ni nini basi? U Eliya wewe?” Akasema, “Mimi siye.” “Wewe u nabii yule?” Akajibu, “La.” Basi wakamwambia, “U nani? Tuwape majibu wale waliotupeleka. Wanenaje juu ya nafsi yako?” Akasema, “Mimi ni sauti ya mtu aliaye nyikani, ‘Inyosheni njia ya Bwana!’, kama vile alivyonena nabii Isaya” (Yohana 1:19-23).

Yohana alijua wito wake, na aliutimiza kwa bidii. Ni muhimu sana kwa watumishi kujua mwito wao na kuutimiza kwa bidii. Kama wewe ni mwinjilisti, usijaribu kuwa mchungaji. Kama ni mwalimu, usijaribu kuwa nabii. Utachanganyikiwa bure na kuchoka.

Utaujuaje wito wako? Kwanza: Kwa kumtafuta Bwana, yule aliyekuita. Pili: Kwa kutazama vipawa vyako. Kama Mungu amekuita uwe mwinjilisti, atakuwezesha kufanya kazi hiyo. Na tatu: Kwa uthibitisho wa watu wengine ambao wataona karama uliy nayo.

Ukisha hakikisha mwito wako, utimize kwa bidii na moyo wako wote, wala usiruhusu kizuizi chochote kukupinga. Kuna wengi wanaokaa tu wakisubiri Mungu afanye kitu ambacho Yeye anatazamia wao wafanye. Nuhu hakusubiri Mungu ajenge safina!

Ni vizuri kujua kwamba huduma ni KAZI. Fahamu pia kwamba Shetani atajaribu kukuzuia usitimize wito wako, lakini huna budi kumpinga na kusonga mbele kwa imani. Hata ingawa Maandiko hayatuambii, fahamu kwamba ipo siku ambapo Yohana alianza kuhubiri katika eneo la Yordani. Bila shaka watu waliokwenda kumsikiliza kwa mara ya kwanza walikuwa si wengi kama wale wa baadaye. Bila shaka watu walimdhihaki na kumcheka, na si ajabu alipata mateso kiasi fulani. Lakini hakuacha. Lengo lake kuu lilikuwa kumpendeza Mungu wake aliyekuwa amemwita kufanya huduma hiyo. Mwishoni alifanikiwa.

Sifa ya kwanza ya kiroho aliyokuwa nayo Yohana ambayo inafaa tuiige ni hii: Yohana alijua wito wake, na aliutimiza kwa bidii.

Sifa Ya Pili Ya Yohana

Siku zile aliondokea Yohana Mbatizaj akihubiri katika nyika ya Uyahudi na kusema, ‘Tubuni! Kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia’ (Mathayo 3:1, 2).

Kwa kweli, Yesu alipendezwa na kukubaliana na huo ujumbe rahisi wa Yohana, maana ulifanana na ule ule aliohubiri Yeye Mwenyewe popote alipokwenda – ona Mathayo 4:17). Yohana aliwaita watu watubu – yaani, wageuke na kuacha maisha ya dhambi, na wageukie maisha ya haki. Alijua kwamba mahusiano na Mungu huanza kwa toba, na kwamba wale wasiotubu watatupwa jehanamu.

Yohana hakutaja kamwe upendo wa Mungu. Hiyo ni tofauti na wainjilisti wengi wa siku hizi. Wala hakuzungumza juu ya “mahitaji” ya watu kama njia ya kuwavuta wao waombe sala isiyokuwa na maana ya “kumpokea Yesu” ili waingie katika kitu kinachoitwa “uzima tele”. Hakuwafanya watu kuamini kwamba walikuwa watu wazuri na ambao Mungu alitaka kuwapeleka mbinguni, mradi watambue kwamba wokovu wao si wa matendo. Aliwaona kama Mungu alivyowaona – waasi walio katika hatari ya kukabiliana na matokeo ya milele kwa ajili ya dhambi zao. Aliwaonya kwa uzito kabisa juu ya ghadhabu itakayokuja. Alihakikisha kwamba wameelewa vizuri kwamba, kama wasingebadilisha mioyo yao na matendo yao, wamepotea.

Basi, sifa ya pili ambayo Yohana alikuwa nayo, inayofaa kuigwa na kila mtumishi anayefanya watu kuwa wanafunzi ni hii: Yohana alitangaza kwamba toba ndiyo hatua ya kwanza katika mahusiano na Mungu.

Sifa Ya Tatu Ya Yohana

Naye Yohana mwenyewe alikuwa na vazi lake la singa za ngamia, na mshipi wa ngozi kiunoni mwake, na chakula chake kilikuwa nzige na asali ya mwitu (Mathayo 3:4).

Hakika Yohana hakufanana na ile picha ya siku hizi ya “mhubiri wa mafanikio”. Wahubiri hawa wasingemruhusu mtu kama Yohana asimame madhabahuni pao kwa sababu mavazi yake hayakuonyesha kufanikiwa. Lakini, Yohana alikuwa mtu wa Mungu kweli, ambaye hakuwa na hamu ya kufuatilia hazina za duniani au kuwafanya watu wamwone na kumsifu kwa sababu ya kuonekana kwake. Yeye alijua kwamba Mungu hutazama moyo. Aliishi maisha rahisi tu, na mtindo wake wa maisha haukumkwaza yeyote, maana waliona nia yake si fedha. Hii ni tofauti sana na jinsi walivyo watumishi wengi sana wa kisasa duniani kote, wenye kutumia Injili kwa ajili ya kujipatia mapato binafsi. Na, kwa sababu wanamwakilisha Kristo kwa njia isiyofaa, wanaharibu sana Injili Yake.

Sifa ya tatu ya Yohana iliyofanya awe mhubiri aliyependwa sana na Yesu ni hii: Yohana aliishi maisha rahisi.

Sifa Ya Nne Ya Yohana

Basi, [Yohana] aliwaambia makutano ya wale waliomwendea ili awabatize, “Enyi wazao wa nyoka! Ni nani aliyewaonya ninyi kuikimbia hasira itakayokuja? Basi, toeni matunda yapatanayo na toba. Wala msianze kusema mioyoni mwenu, ‘Tunaye baba, ndiye Ibrahimu.’ Kwa maana nawaambia ya kwamba katika mawe haya Mungu aweza kumwinulia Ibrahimu watoto” (Luka 3:7-8).

Huduma ya Yohana ilipoanza kugusa watu wengi, inaonekana wazi kwamba hakubadilisha ujumbe wake ulingane na matakwa ya watu, au uwapendeze watu. Yawezekana alianza kuwa na mashaka kuhusu nia za watu alipoona kwamba kubatizwa kumependwa na wengi. Hata waandishi na Mafarisayo walikuwa wanakwenda Yordani (ona Mathayo 3:7). Aliogopa kwamba watu wengi walikuwa wanafuata mkumbo tu. Basi, alifanya kila alichoweza ili kuwazuia wasijidanganye, akiondoa vitu vyote vilivyokuwa tegemezi kwa udanganyifu wao. Hakutaka yeyote afikiri kwamba tendo la kubatizwa lilimwokoa, au kwamba ukiri tu wa toba ungemfanya mtu asiende jehanamu. Alionya kwamba toba ya kweli huleta matunda ya utii.

Tena, kwa sababu Wayahudi wengi walijihesabu kwamba wameokoka kwa sababu ya kuwa uzao wa Ibrahimu, Yohana aliweka wazi uongo wa matumaini hayo.

Sifa ya nne ya Yohana ni hii: Aliwapenda watu kabisa kiasi cha kuwaambia ukweli. Kamwe asingemhakikishia mtu ambaye hajatubu na asiye mtakatifu kwamba alikuwa anakwenda mbinguni.

Sifa Ya Tano Ya Yohana

Yohana asingekubali kuwabatiza watu wasio-onekana kutubu, ili asizidishe kujidanganya kwao. Aliwabatiza watu “huku wakiziungama dhambi zao” (Mathayo 3:6). Aliwaonya hivi wale waliomjia:

Na shoka limekwisha kuwekwa penye mashina ya miti. Basi, kila mti usiozaa matunda mazuri hukatwa na kutupwa motoni. … Ambaye pepeto lake li mkononi mwake, naye atausafisha sana uwanda wake na kuikusanya ngano yake ghalani. Bali, makapi atayateketeza kwa moto usiozimika (Mathayo 3:10, 12).

Yohana hakuogopa kusema kweli kuhusu jehanamu, kitu ambacho mara nyingi huepukwa na wahubiri wanaojaribu kujipatia sifa na kupendwa badala ya kutafuta kuwaleta watu waingie katika ufalme wa Mungu. Wala Yohana hakushindwa kutangaza kweli kuu ile tuliyoiona katika Mahubiri ya Mlimani ya Kristo – kwamba, ni watakatifu tu ndiyo wenye kurithi ufalme wa Mungu. Wasiozaa matunda mema watatupwa motoni.

Kama Yohana angekuwa hai leo, bila shaka angelaumiwa na Wakristo wengi wanaodai kwamba ni Wakristo. Wangemwita “mhubiri wa jehanamu tu” au “nabii mwenye kuzungumzia mambo mabaya tu.” Pengine wangesema ni mhubiri “asiyewajali watafutaji” au hata pengine wangemwita “mhubiri aliye kinyume”, “mwenye kuhukumu watu”, “mwenye kubana watu na sheria” au “mwenye kujihesabia haki mwenyewe”. Pamoja na hayo yote, alikuwa mhubiri aliyependwa sana na Yesu. Sifa yake ya tano ni hii: Yohana alihubiri kuhusu jehanamu, na aliweka wazi ni watu aina gani wanaokwenda huko. Luka anasema, ujumbe wa Yohana ni “Injili” (Luka 3:18). Ajabu hiyo!

Sifa Ya Sita Ya Yohana

Ingawa Yohana alitumiwa sana na Mungu na kuwa maarufu sana na kupendwa na watu, alijua yeye si kitu kulinganishwa na Yesu. Basi, kila wakati alimtukuza Bwana wake, kama ifuatavyo:

Kweli mimi nawabatiza kwa maji kwa ajili ya toba, bali yeye ajaye nyuma yangu ana nguvu kuliko mimi, wala sistahili hata kuvichukua viatu vyake. Yeye atawabatiza kwa Roho Mtakatifu na kwa moto (Mathayo 3:11).

Kujitathmini kwa Yohana ni tofauti kabisa na kiburi ambacho mara nyingi kinaonyeshwa na “watumishi” wa siku zetu. Magazeti yao ya rangi yenye kueleza kuhusu huduma zao yana picha zao kwenye kila ukurasa, na Yesu hatajwi sana. Wanatamba kwenye majukwaa ya makanisa yao kama tausi, wakijisifu mbele ya wafuasi wao. Hawaguswi wala hawafikiwi, na wamejaa umuhimu wao wenyewe. Wengine hata wanamwamuru Mungu na malaika! Lakini, Yohana alijihesabu kuwa hastahili hata kuvua viatu vya Yesu, kitu ambacho kingehesabiwa kuwa tendo la mtumwa wa hali ya chini kabisa. Alikataa wakati Yesu alipomwendea ili kubatizwa, na mara alipogundua kwamba Yesu ndiye Kristo, alianza mara moja kuwaelekeza watu Kwake, akimtangaza kwamba ndiye “Mwanakondoo wa Mungu, achukuaye dhambi za ulimwengu” (Yohana 1:29). Kauli mbiu yake Yohana ikawa hii: “Yeye hana budi kuzidi, bali mimi kupungua” (Yohana 3:30).

Hiyo ilikuwa sifa ya sita ya Yohana iliyomfanya kuwa mhubiri aliyependwa sana na Yesu: Yohana alijinyenyekeza mwenyewe na kumtukuza Yesu. Hakuwa na haja ya kujitukuza mwenyewe.

Sifa Ya Saba Ya Yohana

Mara nyingi, wahubiri wa siku hizi wanazungumza lugha ya jumla ili wasimkwaze yeyote. Ni rahisi sana kuhubiri na kusema hivi: “Mungu anataka sisi tufanye yaliyo sawa!” Wakristo wa kweli na wa uongo pia watasema “Amina!” kwa mahubiri kama hayo. Wahubiri wengi pia wanaona ni kitu rahisi kabisa kurudia rudia kutaja dhambi zile zenye kuaibisha za dunia, wakiacha kutaja dhambi hizo hizo katika kanisa. Kw amfano: Wanaweza kulalamika sana dhidi ya kuangalia picha chafu za ngono, lakini hawathubutu kutaja matendo ya washirika wao ya kutazama mikanda ya video na DVD za ngono. Hofu ya mwanadamu imewanasa.

Yohana yeye hakusita kuhubiri kinaga-naga. Luka anatuambia hivi:

Makutano wakamwuliza, ‘Tufanye nini basi?’ Akawajibu, ‘Mwenye kanzu mbili na ampe asiye na kanzu, na mwenye vyakula na afanye vivyo hivyo’. Watoza ushuru nao wakaja kubatizwa. Wakamwuliza, ‘Mwalimu, tufanye nini sisi?’ Akawaambia, ‘Msitoze kitu zaidi kuliko mlivyoamriwa’. Askari nao wakamwuliza wakisema, ‘Sisi nasi tufanye nini?’ Akawaambia, ‘Msidhulumu mtu, wala msishtaki kwa uongo, tena mtosheke na mshahara wenu.’ (Luka 3:10-14).

Cha ajabu ni kwamba maagizo matano kati ya sita ambayo Yohana alitoa, yanahusu fedha au mali. Yohana hakuogopa kuhubiri juu ya uwakili kama unavyoambatana na Amri Iliyo Kuu, na amri ya pili. Wala Yohana hakusubiri miaka kadhaa mpaka wale “waamini” wapya walipokuwa tayari kupokea mada “nzito” kama hizo. Aliamini kwamba haiwezekani kumtumikia Mungu na mali, na basi, uwakili ulikuwa kitu muhimu sana kuanzia mwanzo.

Hayo yote yanaleta hoja nyingine moja. Yohana hakusema sana mambo madogo madogo, kama vile mavazi na mambo mengine ya utakatifu yanayoambatana na kuonekana kwa nje. Alishughulikia maswala “makuu katika Torati” (Mathayo 23:23, TLR). Alijua kwamba kilicho muhimu zaidi ni kuwapenda jirani zetu kama nafsi zetu na kuwatendea wengine kama tunavyotaka kutendewa. Maana yake ni kushirikiana chakula na mavazi na wale wasiokuwa navyo, kuwatendea wengine haki, na kuridhika au kutosheka na tulivyo navyo.

Hiyo ilikuwa sifa ya saba ambayo ilimfanya Yesu kumpenda Yohana: Hakuhubiri mambo ya jumla jumla tu, bali alitaja vitu halisi ambavyo watu wanapaswa kutenda ili kumpendeza Mungu, pamoja na vitu vinavyohusiana na uwakili. Tena, alikazia mambo yaliyokuwa muhimu zaidi.

Kumalizia

Huduma ya mchungaji au mwalimu inahusu mambo mengi na mapana zaidi kuliko ya Yohana. Yohana alikuwa anawahubiria wasio-okoka. Wachungaji na waalimu wanatakiwa kuwafundisha wale ambao wamekwisha tubu tayari. Mafundisho yao yamejengwa juu ya mambo ambayo Yesu aliwaambia wanafunzi Wake na yale yaliyoandikwa katika nyaraka za Agano Jipya.

Mara nyingi sisi tunashindwa kutambua wasikilizaji wetu vizuri, na inaonekana kwamba siku hizi wenye dhambi wanahubiriwa kana kwamba ni waongofu. Kwa kuwa watu wameketi ndani ya kanisa haimaanishi kwamba kazi yetu ni kuwahakikishia wokovu wao, hasa kama maisha yao hayana tofauti yoyote na wale waliomo duniani. Tunawahitaji sana akina “Yohana Mbatizaji” watakaohubiri kutoka madhabahu za kanisani. Je, utapokea changamoto hiyo? Je, utakubali kuwa mmoja kati ya wahubiri wanaopendwa sana na Yesu?

Kuzaliwa Upya

Sura Ya Kumi

Watu wanapotubu na kumwamini Bwana Yesu Kristo, wana”zaliwa mara ya pili”. Nini hasa maana ya kuzaliwa mara ya pili? Sura hii itatazama jambo hili.

Ili kuweza kuelewa maana ya kuzaliwa mara ya pili, inasaidia sana kuanza kwa kuelewa asili ya wanadamu. Maandiko yanatuambia kwamba sisi si viumbe wa kimwili tu, bali wa kiroho pia. Kwa mfano: Paulo aliandika hivi:

Mungu wa amani mwenyewe awatakase kabisa. Nafsi zenu na roho zenu na miili yenu mhifadhiwe mwe kamili, bila lawama, hadi wakati wa kuja kwake Bwana wetu Yesu Kristo (1Wathes. 5:23, maneno mepesi kukazia).

Kama Paulo alivyoonyesha, tunaweza kujihesabu kuwa viumbe wenye sehemu tatu: roho, nafsi na mwili. Maandiko hayafafanui sana hizo sehemu tatu, kwa hiyo, tunajitahidi sana kuzitofautisha kwa ufahamu wetu wa maneno yenyewe. Mara nyingi tunasema hivi: Mwili wetu ni umbo tulilo nalo – nyama, mifupa, damu na kadhalika. Nafsi yetu ni ufahamu wetu na uwezo wetu wa kujisikia – akili yetu. Roho yetu bila shaka ni ile hali yetu ya kiroho, au kama mtume Petro anavyoeleza, “utu wa ndani uliofichika” (1Petro 3:4, TLR).

Kwa sababu roho haionekani kwa macho ya kimwili, watu wasio-okoka wanakana kuwepo kwake. Lakini Biblia iko wazi kabisa kwamba wote sisi ni viumbe wa kiroho. Maandiko yanatuambia kwamba mtu anapokufa, ni mwili wake tu ndiyo unakoma kufanya kazi, lakini roho yake na nafsi vinaendelea kama kawaida. Wakati wa kufa, hivyo viwili vinatoka katika mwili (kwa pamoja) ili kwenda kuhukumiwa mbele za Mungu (ona Wabrania 9:27). Baada ya hukumu, vinakwenda mbinguni au jehanamu. Mwisho wa yote, kila roho na nafsi ya mtu itaungana na mwili wake wakati wa ufufuo.

Roho Ya Mwanadamu Ikifafanuliwa Zaidi

Katika 1Petro 3:4, Petro anazungumza juu ya roho kama “utu wa moyoni usioonekana” kuonyesha kwamba roho ni mtu. Paulo pia alizungumza juu ya roho kama “mtu wa ndani” kuonyesha imani yake kwamba roho ya mwanadamu si nguvu fulani au wazo tu, bali ni mtu. Anasema hivi:

Kwa hiyo hatulegei, bali, ijapokuwa utu wetu wa nje unachakaa, lakini utu wetu wa ndani unafanywa upya siku kwa siku (2Wakor. 4:16, maneno mepesi kukazia).

“Utu wa nje” bila shaka ni maelezo kuhusu mwili, na “utu wa ndani” ni maelezo kuhusu roho. Ni hivi: Japo mwili unazeeka, roho inafanywa upya kila siku.

Ona tena kwamba Paulo anataja mwili na roho kama watu. Basi, unapofikiria roho yako, usifikiri wingu fulani la kiroho. Ni afadhali ufikiri kuhusu mtu mwenye umbo linalofanana na lako. Kama mwili wako umezeeka, usidhani na roho yako imezeeka pia. Jaribu kufikiri jinsi ulivyokuwa ujanani mwako, kwa sababu, roho yako haijazeeka – iko kama ulivyokuwa ukiwa kijana! Inafanywa upya siku kwa siku.

Roho yako ndiyo sehemu yako inayozaliwa mara ya pili (kama umemwamini Bwana Yesu). Roho yako inaungana na Roho wa Mungu (ona 1Wakor. 6:17), na Yeye ndiye anayekuongoza unapomfuata Yesu (ona Warumi 10:14).

Biblia inafundisha kwamba Mungu pia ni roho (ona Yohana 4:24), na hata malaika, na mapepo pia. Wote wana maumbo na wote wapo katika ulimwengu wa roho. Ila, ulimwengu wa roho hauwezi kutambuliwa kwa hisia zetu za kimwili. Kujaribu kuwasiliana na ulimwengu wa roho kwa hisia zetu za kimwili ni sawa na kujaribu kushika mawimbi ya redio kwa mikono yetu. Hatuwezi kutambua kwa hisia zetu za kimwili kwamba mawimbi ya redio yanapita katika chumba, lakini hiyo haithibitishi kwamba hakuna mawimbi ya redio. Njia pekee ya kuyapata hayo mawili ni kuifungulia redio.

Hayo pia ni kweli kwa habari ya ulimwengu wa kiroho. Kwa kuwa ulimwengu wa kiroho hauwezi kutambuliwa na hisia za kimwili haimaanishi kwamba haupo. Upo, na watu wakijua au wasijue, ni sehemu ya ulimwengu wa kiroho kwa sababu ni viumbe wa kiroho. Ama wanahusiana na Mungu kiroho (kama wamezaliwa mara ya pili), au wanahusiana na Shetani kiroho (kama hawajatubu). Kuna watua mbao wamejifunza jinsi ya kuwasiliana na ulimwengu wa kiroho kwa njia ya roho zao, lakini wao wanawasiliana na ufalme wa Shetani – ufalme wa giza.

Miili Ya Milele

Tukiwa katika mada hii, hebu nitaje kitu kuhusu miili yetu. Ingawa hatimaye itakufa, hali yetu ya kufa kimwili si tendo la mwisho. Iko siku ambapo Mungu Mwenyewe atafufua kila mwili wa mwanadamu uliokufa. Yesu alisema hivi:

Msishangae kwa hili, maana saa inakuja, ambayo wote waliomo makaburini wataisikia sauti Yake, nao watatoka. Waliofanya matendo mema, watafufuliwa ufufuo wa uzima, na wale waliofanya matendo maovu, watafufuliwa ufufuo wa kuhukumiwa (Yohana 5:28, 29, TLR).

Mtume Yohana aliandika katika kitabu cha Ufunuo kwamba kufufuliwa kwa miili ya wasio haki kutatokea miaka elfu moja baada ya kufufuliwa kwa miili ya wenye haki.

Nao [yaani, watakatifu waliouawa wakati wa dhiki] wakawa hai, wakatawala pamoja na Kristo miaka elfu. Na hao wafu waliosalia hawakuwa hai, hata itimie ile miaka elfu. Huo ndio ufufuo wa kwanza.[1] Heri na mtakatifu ni yeye aliye na sehemu katika ufufuo wa kwanza … watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, nao watatawala pamoja naye hiyo miaka elfu (Ufunuo 20:4b-6).

Biblia pia inatuambia kwamba wakati Yesu atakaporudi kulichukua kanisa, miili yote ya watakatifu itafufuliwa na kuunganishwa na roho zao, watakapokuwa wanarudi kutoka mbinguni na Yesu, kuja duniani. Tunasoma hivi:

Maana, ikiwa twaamini ya kwamba Yesu alikufa akafufuka, vivyo hivyo na hao waliolala katika Yesu, Mungu atawaleta pamoja naye. Kwa kuwa twawaambieni haya kwa neno la Bwana, kwamba, sisi tulio hai, tutakaosalia hata wakati wa kuja kwake Bwana, hakika hatutawatangulia wao waliokwisha kulala mauti. Kwa sababu Bwana mwenyewe atashuka kutoka mbinguni pamoja na mwaliko … nao waliokufa katika Kristo [yaani, miili yao] watafufuliwa kwanza. Kisha sisi tulio hai, tuliosalia, tutanyakuliwa pamoja nao katika mawingu ili tumlaki Bwana hewani, na hivyo tutakuwa pamoja na Bwana milele (1Wathes. 4:14-17).

Mungu alimwumba mwanadamu wa kwanza kutoka katika mavumbi ya nchi, kwa hiyo, haitakuwa shida Kwake kuchukua mabaki au sehemu za mwili wa kila mmoja na kuumba tena miili binafsi kutoka katika vifaa vile vile.

Kwa habari ya kufufuka kwa miili yetu, Paulo aliandika hivi:

Kadhalika na kiyama ya watu. Hupandwa katika uharibifu; hufufuliwa katika kutokuharibika. Hupandwa katika aibu, hufufuliwa katika fahari. Hupandwa katika udhaifu; hufufuliwa katika nguvu. Hupandwa mwili wa asili; hufufuliwa mwili wa roho. … Ndugu zangu, nisemayo ni haya: Nyama na damu haziwezi kuurithi ufalme wa Mungu, wala uharibifu kurithi kutokuharibika. Angalieni, nawaambia ninyi siri – hatutalala sote [yaani, kufa], lakini sote tutabadilika, kwa dakika moja, kufumba na kufumbua, wakati wa parapanda ya mwisho. Maana parapanda Italia, na wafu watafufuliwa, wasiwe na uharibifu, nasi tutabadilika. Maana sharti huu uharibikao uvae kutokuharibika, nao huu wa kufa uvae kutokufa (1Wakor. 15:42-44a, 50-53).

Ona kwamba sifa kubwa ya miili yetu mipya ni kwamba itakuwa haifi na isiyoharibika. Haitazeeka, haitapata magonjwa, wala haitakufa! Miili yetu mipya itakuwa kama ule mwili mpya ambao Yesu alipokea baada ya kufufuka Kwake.

Kwa maama sisi wenyeji wetu uko mbinguni. Kutoka huko tena tunamtazamia Mwokozi, Bwana Yesu Kristo; atakayeubadili mwili wetu wa unyonge upate kufanana na mwili wake wa utukufu, kwa uweza ule ambao kwa huo aweza hata kuvitiisha vitu vyote viwe chini yake (Wafilipi 3:20, 21, maneno mepesi kukazia).

Hata mtume Yohana anathibitisha kweli hii ya kupendeza sana, hivi:

Wapenzi, sasa tu wana wa Mungu, wala haijadhihirika bado tutakavyokuwa. Lakini twajua ya kuwa atakapodhihirishwa tutafanana naye, kwa maana tutamwona kama alivyo (1Yohana 3:2, maneno mepesi kukazia).

Japo hili ni gumu kwa akili zetu kuelewa kabisa, tunaweza kuliamini na kufurahia yaliyo mbele![2]

Anayosema Yesu Kuhusu Kuzaliwa Upya

Kuna wakati fulani ambao Yesu alizungumza na kiongozi Myahudi aliyeitwa Nikodemu juu ya umuhimu wa kuzaliwa upya kwa roho ya mwanadamu, kwa tendo la Roho Mtakatifu.

Yesu akajibu, akamwambia [Nikodemu], ‘Amin amin nakuambia, Mtu asipozaliwa mara ya pili, hawezi kuuona ufalme wa Mungu.’ Nikodemu akamwambia, ‘Awezaje mtu kuzaliwa akiwa mzee? Aweza kuingia tumboni mwa mamaye mara ya pili akazaliwa?’ Yesu akajibu, ‘Amin amin nakuambia, Mtu asipozaliwa kwa maji na kwa Roho hawezi kuuingia ufalme wa Mungu. Kilichozaliwa kwa mwili ni mwili, na kilichozaliwa kwa Roho ni roho. Usistaajabu kwa kuwa nimekwambia, Hamna budi kuzaliwa mara ya pili’ (Yohana 3:3-7).

Mwanzoni, Nikodemu alidhani kwamba Yesu anazungumzia kuzaliwa kimwili mara ya pili alipomwambia kwamba lazima mtu azaliwe tena ili kuingia ufalme wa mbinguni. Yesu akaweka wazi kwamba alikuza anazungumza juu ya kuzaliwa upya kiroho. Yaani, roho ya mtu lazima izaliwe tena.

Sababu ya kuhitaji kuzaliwa upya kiroho ni kwamba, roho zetu zimeathiriwa na asili ovu ya dhambi. Hiyo asili ya dhambi mara nyingi inatajw akatika Biblia kwamba ni kifo. Ili tuweze kuelewa, tutaitaja asili hiyo ovu kwamba ni kifo cha kiroho ili tutofautishe kati yake na kifo cha kimwili (ambacho ni wakati mwili wa kawaida unapokoma kufanya kazi).

Kifo Cha Kiroho Kinafafanuliwa

Paulo anaeleza maana ya kufa kiroho katika Waefeso 2:1-3. Anasema hivi:

Nanyi mlikuwa wafu kwa sababu ya makosa na dhambi zenu, ambazo mliziendea zamani kwa kuifuata kawaida ya ulimwengu huu na kwa kumfuata mfalme wa uwezo wa anga, roho yule atendaye kazi sasa katika wana wa kuasi. Zamani sisi sote nasi tulienenda kati yao katika tamaa za miili yetu, tulipoyatimiza mapenzi ya mwili na ya nia, tukawa kwa tabia yetu watoto wa hasira kama na hao wengine (maneno mepesi kukazia).

Bila shaka Paulo alikuwa hazungumzii kifo cha kimwili kwa sababu alikuwa anawaandikia watu waliokuwa hai kimwili. Lakini akasema, hapo zamani walikuwa “wafu kwa sababu ya makosa na dhambi zao.” Dhambi hufungua mlango wa kifo cha kiroho (tazama Warumi 5:12). Kuwa wafu kiroho maana yake ni kuwa na asili ya dhambi rohoni mwako. Ona maneno ya Paulo kwamba, “kwa tabia” wakawa watoto wa hasira.

Tena, kufa kiroho maana yake kuwa na asili ya Shetani katika roho yako kwa namna fulani. Paulo alisema kwamba wale wote waliokufa kiroho wana roho ya “mkuu wa uwezo wa anga” ikitenda kazi ndani yao. Huyo “mkuu wa uwezo wa anga” ni Shetani (tazama Waefeso 6:12), na roho yake inatenda kazi ndani yao wote ambao hawajaokoka.

Yesu aliwaambia hivi Wayahudi waliokuwa hawajazaliwa mara ya pili:

Ninyi ni wa baba yenu Ibilisi, na tamaa za baba yenu ndizo mpendazo kuzitenda. Yeye alikuwa mwuaji tangu mwanzo, wala hakusimama katika kweli, kwa kuwa hamna hiyo kweli ndani yake. Asemapo uongo husema yaliyo yake mwenyewe, kwa sababu yeye ni mwongo na baba wa huo (Yohana 8:44).

Kwa upande wa kiroho, wale ambao hawajazaliwa tena si tu kwamba wana asili ya Shetani katika roho zao, bali Shetani ni baba yao wa kiroho pia. Basi, ni kawaida kwao kutenda kama shetani. Wao ni wauaji na waongo.

Si kwamba watu wote ambao hawajaokoka wamefanya mauaji, bali ni kwamba wanahamasishwa na chuki ile ile kama ya wauaji, nao wangeweza kuua kama wangefanikiwa. Kuhalalishwa utoaji mimba katika nchi nyingi ni uthibitisho wa kweli hiyo. Watu ambao hawajaokoka wataua hata watoto wao wenyewe, ambao bado hawajzaliwa!

Hii ndiyo sababu mtu lazima azaliwe tena kiroho. Inapotokea hivyo, hiyo asili ya dhambi na kishetani huondolewa katika roho yake, na nafasi yake huchukuliwa na asili ya Mungu takatifu. Roho Mtakatifu wa Mungu huja na kukaa ndani ya roho yake. Hawi “mfu kiroho” tena, bali anafanywa “hai kiroho”. Roho yake haiwi imekufa tena bali inakuwa hai kwa Mungu. Badala ya kuwa mtoto wa kiroho wa Shetani, anakuwa mtoto wa kiroho wa Mungu.

Matengenezo Si Kuzaliwa Upya

Kwa sababu watu ambao hawajaokoka wamekufa kiroho, hawawezi kuokolewa kwa matengenezo, hata kama watajaribu kiasi gani. Watu ambao hawajaokoka wanahitaji asili mpya, si matendo mapya ya nje tu. Unaweza kumchukua nguruwe, ukamsafisha vizuri akawa safi, ukampulizia hata manukato na kumfungia tai ya rangi nzuri tu shingoni mwake, lakini mwisho wa siku ulicho nacho ni nguruwe aliyesafishwa tu! Bado asili yake ni ile ile. Na hautapita muda mrefu kabla hajaanza kunuka vibaya tena na kulala kwenye matope tena.

Ndivyo ilivyo kwa watu washika dini sana ambao hawajawahi kuzaliwa tena. Wanaweza kuwa wasafi kwa nje, lakini ndani ni wachafu tu kama kawaida. Yesu alisema hivi kwa watu washika dini wa siku Zake:

Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnasafisha nje ya kikombe na chano, na ndani yake vimejaa unyang’anyi na kutokuwa na kiasi. Ewe Farisayo kipofu! Safisha kwanza ndani ya kikombe, ili nje yake nayo ipate kuwa safi! Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mmefanana na makaburi yaliyopakwa chokaa, nayo kwa nje yaonekana kuwa mazuri, bali ndani yamejaa mifupa ya wafu na uchafu wote. Vivyo hivyo ninyi nanyi: Kwa nje mwaonekana na watu kuwa wenye haki, bali ndani mmejaa unafiki na maasi! (Mathayo 23:25-28).

Maneno ya Yesu ni maelezo sahihi kabisa ya washika dini wote ambao hawajawahi kuzaliwa upya kwa njia ya Roho Mtakatifu. Kuzaliwa upya huwasafisha watu ndani, si nje tu.

Nini Kinachotokea Kwa Nafsi Wakati Roho Inapozaliwa Upya?

Roho ya mtu inapozaliwa upya, nafsi yake hapo mwanzoni inabakia kama ilivyokuwa (ingawa kwa akili zake anakuwa amefanya uamuzi wa kumfuata Yesu). Ila, Mungu anatazamia kwamba tufanye kitu na nafsi zetu mara tunapokuwa watoto Wake. Nafsi zetu (au nia) zinapaswa kufanywa upya kwa Neno la Mungu ili tuweze kufikiri kama Mungu anavyofikiri. Kwa kufanywa upya nia zetu, badiliko la kudumu la nje linafanyika maishani mwetu, na kutufanya tuzidi kufanana na Yesu.

Wala msiifuatishe namna ya dunia hii, bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu (Warumi 12:2, maneno mepesi kukazia).

Hata Yakobo naye aliandika kuhusu mfuatano huo wa mambo katika maisha ya mwamini, hivi:

Kwa hiyo wekeni mbali uchafu wote na ubaya uzidio, na kupokea kwa upole neno lile lililopandwa ndani, liwezalo kuziokoa nafsi zenu (Yakobo 1:21, TLR).

Ona kwamba Yakobo alikuwa anawaandikia Wakristo – watu ambao roho zao zilikuwa zimekwisha zaliwa upya. Ila, walihitaji nafsi zao kuokolewa, na hayo yangefanyika tu wakati anapopokea “neno lile lililopandwa ndani”. Hii ndiyo sababu waamini wapya wanatakiwa kufundishwa Neno la Mungu.

Mabaki Ya Asili Ya Kale

Baada ya kuzaliwa upya kwao, Wakristo wengi hugundua kwamba ni watu wenye asili mbili, na kujikuta wakikabiliana na kile kitu kinachoitwa na Paulo, vita kati ya “Roho na mwili”.

Kwa sababu mwili hutamani ukishindana na Roho, na Roho kushindana na mwili, kwa maana hizi zi mepungana, hata hamwezi kufanya mnayotaka (Wagalatia 5:17).

Mabaki ya ile asili ya kale ya dhambi, yanaitwa “mwili” na Paulo. Hizo asili mbili ndani yetu huleta shauku tofauti, ambazo, kama watu watakubaliana nazo, husababisha matendo tofauti na mitindo tofauti ya maisha. Ona tofauti anayoweka Paulo kati ya “matendo ya mwili” na “tunda la Roho” katika fungu lifuatalo:

Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya: Uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo. Katika hayo nawaambia mapema, kama nilvyokwisha kuwaambia ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu. Lakini tunda la Roho ni: Upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi. Juu ya mambo kama hayo hakuna sheria (Wagalatia 5:19-23).

Bila shaka inawezekana kwa Wakristo kukubaliana na mwili, vinginevyo Paulo asingewaonya kwamba kuzoea kuufuata mwili kutawafanya wasiweze kuurithi ufalme wa Mungu. Katika barua yake kwa Warumi, Paulo aliandika pia juu ya hizo asili mbili za kila Mkristo, na akaonya tena juu ya matokeo hayo hayo, kama watu watakubaliana na mwili. Anasema hivi:

Na Kristo akiwa ndani yenu, mwili wenu umekufa kwa habari ya dhambi, bali roho yenu iko hai kwa habari ya haki. … Basi ndugu, kama ni hivyo, wote tunawajibika, si kwa mwili kwamba tuishi kwa kufuata mambo ya mwili. Kwa maana, mkiishi kwa kufuata mambo ya mwili mwataka kufa, bali mkiyafisha matendo ya mwili kwa Roho, mtaishi. Kwa kuwa wote wanao-ongozwa na Roho wa Mungu ndio wana wa Mungu hao (Warumi 8:10, 12-14, TLR. Maneno mepesi kukazia).

Hilo ni onyo dhahiri kabisa kwa Wakristo kwamba, kuishi (yaani tabia ya kawaida, au mazoea) kulingana na mwili matokeoyake ni kifo. Bila shaka Paulo alikuwa anaonya juu ya kifo cha kiroho maana kila mtu hatimaye hufa kimwili – hata Wakristo wale wanao”yafisha matendo ya mwili”.

Mkristo anaweza kuangukia katika mojawapo ya dhambi ambazo Paulo aliorodhesha hapo kwa kitambo tu. Ila, mwamini anapofanya dhambi, atajisikia hukumu na pengine atatubu. Yeyote anayeungama dhambi yake na kumwomba Mungu amsamehe, atasafishwa (ona 1Yohana 1:9).

Mkristo anapotenda dhambi haimaansihi kwamba amevunja uhusiano wake na Mungu. Maana yake ni kwamba amevunja ushirika wake na Mungu. Yeye bado ni mtoto wa Mungu, lakini sasa ni mtoto asiyeti. Ikiwa mwamini hataungama dhambi yake na kutubu, anajiweka kwenye nafasi ya kuadhibiwa na Bwana.

Vita Yenyewe

Kama umejikuta unatamani kufanya mambo unayojua ni makosa, basi umeanza kukabiliana na “tamaa ya mwili”. Bila shaka umegundua pia kwamba unapojaribiwa na mwili kufanya kisicho sawa, kuna kitu ndani yako kinachopinga majaribu hayo. Hicho ni “tamaa ya Roho”. Na kama unajua jinsi kujisikia hatia kunavyokupata ukikubaliana na majaribu, basi unaifahamu sauti ya roho yako, tunayoiita “dhamiri” yetu.

Mungu alijua vizuri sana kwamba tamaa zetu za mwili zingetujaribu tufanye makosa. Lakini, hiyo si sababu inayoturuhusu kukubaliana na tamaa za mwili. Bado Mungu anatutazamia tutende kwa utii na utakatifu, na tushinde asili ya mwili.

Lakini nasema hivi: Enendeni katika Roho, nanyi hamtazitimiza tamaa za mwili (Wagalatia 5:16, TLR).

Hakuna mbinu ya kiuchawi ya kushinda mwili. Paulo alisema tu kwamba “tuenende katika Roho” nasi “hatutatimiza tamaa za mwili” (Wagalatia 5:16). Hakuna Mkristo mwenye uwezo zaidi ya mwenzake katika jambo hili. Kutembea katika Roho ni uamuzi ambao kila mmoja wetu lazima aufanye, na kujitolea kwetu kwa Bwana kunaweza kupimwa kwa kiwango cha kutojitolea kwetu kwa tamaa za mwili.

Paulo akaandika hivi tena:

Na hao walio wa Kristo Yesu wameusulubisha mwili pamoja na mawazo yake mabaya, na tamaa zake (Wagalatia 5:24).

Ona anachosema Paulo: Wale walio wa Kristo wameusulubisha mwili (anatumia lugha ya wakati uliopita). Hayo yalitokea wakati tulipotubu na kumwamini Bwana Yesu Kristo. Hapo, tulisulubisha ile asili ya dhambi, tukaamua kumtii Mungu na kupingana na dhambi. Sasa, si swala la kusulubisha mwili tena, bali kudumisha kule kusulubiwa.

Si rahisi kuendelea kuusulubisha mwili, lakini ni kitu kinachowezekana. Kama tutatenda kulingana na kuongozwa kwa utu wa ndani badala ya kukubaliana na misukumo ya mwili, tutaonyesha maisha ya Kristo na kuenenda katika utakatifu mbele Zake.

Asili Ya Roho Zetu Zilizoumbwa Tena

Kuna neno moja lenye kueleza vizuri zaidi asili ya roho zetu zilizoumbwa tena. Neno hilo ni Kristo. Kwa njia ya Roho Mtakatifu ambaye ana asili ile ile ya Yesu, sisi ndani yetu tuna asili ya Yesu. Paulo aliandika hivi: “Si mimi ninayeishi tena, bali Kristo anaishi ndani yangu” (Wagalatia 2:20, TLR).

Kwa sababu tuna uwezo Wake na asili Yake ndani yetu, tunao uwezo wa ajabu sana wa kuishi kama Kristo. Hatuhitaji upendo zaidi, au uvumilivu, au kiasi – ndani yetu tunaye Mtu mwenye upendo sana, mwenye uvumilivu sana, mwenye kiasi sana – anakaa ndani yetu! Tunachohitaji kufanya ni kumruhusu Yeye kuishi kwa kututumia sisi.

Ila, wote tuna adui mmoja mkubwa ambaye anapambana na asili ya Yesu, akiizuia isijidhihirishe kupitia kwetu, naye ni mwili wetu. Ndiyo maana Paulo alisema lazima kuusulubisha mwili wetu. Ni wajibu wetu kufanya kitu juu ya mwili wetu, na ni kupoteza wakati kumwomba Mungu afanye chochote kuhusu mwili. Hata Paulo alikuwa na matatizo na asili yake ya kimwili, lakini aliwajibika na kuushinda. Anasema hivi:

Ninautesa mwili wangu na kuufanya mtumwa, ili, baada ya kuwahubiri wengine, mimi mwenyewe nisije nikakataliwa (1Wakor. 9:27, TLR).

Hata wewe itabidi kuufanya mwili wako kuwa mtumwa wa roho yako, kama unataka kuenenda kwa utakatifu mbele za Bwana. Na, inawezekana!


[1] Kwa sababu Yohana anasema huu ndiyo “ufufuo wa kwanza”, hayo yanatufanya tuamini kwamba hakuna ufufuo mwingine kabla ya huo. Na kwa sababu unatokea wakati wa kumalizika kwa kipindi cha dhiki ya dunia nzima wakati Yesu anaporudi, ni kinyume na lile wazo la kuwepo kwa unyakuo kabla ya dhiki, maana tunajua kwamba utakuwepo ufufuo wa wote wakati Yesu anapotoka mbinguni kulinyakua kanisa kulingana na 1Wathes. 4:13-17. Tutajifunza zaidi katika sura iliyoko mbele iitwayo UNYAKUO WA KANISA NA NYAKATI ZA MWISHO.

[2] Ukitaka kujifunza zaidi kuhusu mada ya ufufuo, tazama Danieli 12:1-2; Yohana 11:23-26; Matendo 24:14-15; 1Wakor. 15:1-57.

Jinsi Ya Kutafsiri Maandiko

Sura Ya Saba

Paulo alimwandikia hivi Timoteo:

Jitunze nafsi yako, na mafundisho yako. Dumu katika mambo hayo; maana kwa kufanya hivyo utajiokoa nafsi yako na wale wakusikiao pia (1Timo. 4:16. Maneno mepesi kukazia).

Kila mtumishi anatakiwa kutilia maanani ushauri huu, akiwa makini sana kuhusu yeye mwenyewe kwanza – yaani, kuhakikisha kwamba yeye ni mfano wa utauwa kwa wengine.

Cha pili – awe makini sana kuhusu mafundisho yake, kwa sababu wokovu wake wa milele na wa wanaomsikiliza unategemea anachofundisha, kama Paulo alivyoandika katika mstari huo hapo juu.[1] Mtumishi akifuata mafundisho ya uongo, au akipuuza kuwaambia watu ukweli, matokeo ni hasara ya milele kwake na kwa wengine.

Ila – hakuna kujitetea kwa mtumishi anayefanya wengine kuwa wanafunzi, kama atafundisha uongo, maana Mungu amempa yeye Roho Mtakatifu na Neno Lake ili kumwongoza katika kweli. Watumishi wenye makusudi mabaya mara nyingi hurudia kama kasuku mafundisho yanayopendwa na watu, yenye kutolewa na waalimu wengine. Wao hawajifunzi Neno ili wapate kitu cha kutoa, na inakuwa rahisi kwao kupotoka katika mafundisho yao na imani zao. Ulinzi kinyume cha hayo ni mtumishi kusafisha moyo wake, akihakikisha kwamba kusudi lake moyoni ni (1) kumpendeza Mungu, na (2) kuwasaidia watu wawe tayari kusimama mbele za Yesu, badala ya kutaka kutajirika kibinafsi, au kuwa na uwezo au kuwa maarufu. Tena, lazima ajifunze kwa bidii sana Neno la Mungu ili awe na ufahamu kamili na wenye usahihi. Paulo alimwandikia Timoteo tena, akasema hivi:

Jitahidi kujionyesha kuwa umekubaliwa na Mungu, mtenda kazi asiye na sababu ya kutahayari, ukitumia kwa halali neno la kweli (2Timo. 2:15).

Kusoma, kujifunza na kutafakari Neno la Mungu iwe ni kawaida kwa mtumishi kufanya kila wakati. Roho Mtakatifu atamsaidia kuelewa vizuri zaidi Neno la Mungu atakapojifunza kwa bidii. Hiyo itahakikisha kulitumia “kwa halali neno la kweli”. Tatizo moja kubwa katika kanisa siku hizi ni kwamba watumishi wanafasiri vibaya Neno la Mungu, na wanapotosha watu wanaowafundisha. Hii ni hatari sana. Yakobo alionya hivi:

Ndugu zangu, msiwe waalimu wengi, mkijua ya kuwa mtapata hukumu kubwa zaidi (Yakobo 3:1).

Basi, ni muhimu kwamba mtumishi anayefanya wengine kuwa wanafunzi ajue jinsi ya kufasiri sawasawa Neno la Mungu, huku lengo lake likiwa kuelewa ipasavyo maandiko yoyote na kuyafafanua ili watu wapate maana yake halisi.

Kufasiri sawasawa Neno la Mungu hufanywa sawa tu na kufasiri sawasawa maneno ya mtu. Tukitaka kuelewa vizuri maana iliyokusudiwa ya mwandishi yeyote au msemaji tunayemsikiliza, inabidi tufuate sheria fulani za ufasiri, ambazo msingi wake ni akili tu ya kawaida. Katika sura hii, tutatazama kanuni tatu muhimu za kufasiri Biblia ipasavyo. Ni hizi zifuatazo: (1) Soma na akili timamu, (2) Soma ukizingatia mantiki, na (3) Soma na moyo ulio wazi.

Kanuni ya kwanza: Soma na akili timamu. Elewa uliyosoma kama yalivyoandikwa isipokuwa kama ni dhahiri kwamba yalikusudiwa kueleweka kama mfano.

Biblia ni kama maandiko mengine. Imejaa lugha za mifano. Ukisoma sehemu kama hizo, zielewe hivyo hivyo.

Mlinganisho huonyesha jinsi vitu viwili ambavyo ni tofauti kabisa, vinavyofanana. Katika Maandiko utakutana na hili mara nyingi sana. Mfano mmoja ni maneno ya Kristo wakati wa Chakula cha Mwisho na wanafunzi Wake.

Nao walipokuwa wakila, Yesu alitwaa mkate, akabariki, akaumega, akawapa wanafunzi wake akasema, ‘Twaeni, mle; huu ndio mwili wangu’. Akakitwaa kikombe, akashukuru, akawapa akisema, ‘Nyweni nyote katika hiki; kwa maana hii ndiyo damu yangu ya agano, imwagikayo kwa ajili ya wengi kwa ondoleo la dhambi’ (Mathayo 26:26-28).

Je, Yesu kweli alimaanisha kwamba mkate aliowapa wanafunzi Wake ulikuwa mwili Wake halisi na kwamba ile divai waliyokunywa ilikuwa damu Yake halisi? Kufikiri kidogo tu kutaonyesha kwamba Sivyo. Maandiko yanasema wazi kwamba Yesu aliwapa mkate na divai, na hayasemi kwamba vitu hivyo vilibadilika wakati wowote na kuwa nyama na damu halisi. Hata Petro na Yohana hawasemi hivyo katika nyaraka zao wakati wowote, na wao walikuwepo kwenye Chakula hicho. Tena, haiwezekani kwamba wanafunzi wangekubali kujihusisha na ulaji wa nyama na damu ya mwanadamu!

Kuna wanaotoa hoja hivi: “Lakini, Yesu alisema kwamba mkate na divai ni mwili Wake na damu Yake. Mimi nitaamini alichosema Yesu!”

Sawa. Kuna wakati ambapo Yesu pia alisema ni mlango (Yohana 10:9). Je, alifanyika mlango halisi, wenye komeo na bawabu na kitasa? Wakati mwingine Yesu alisema Yeye ni mzabibu, na sisi ni matawi (Yohana 15:5). Je, Yesu alifanyika mzabibu halisi? Je, sisi tumefanyika matawi halisi ya mzabibu? Wakati mwingine Yesu akasema ni nuru ya ulimwengu na chakula kilichoshuka kutoka mbinguni (ona Yohana 9:5; 6:41). Je, Yesu ndiye mwangaza wa jua siku hizi na boflo ya mkate?

Basi – hizo zote ni lugha za mfano ambazo ni mlinganisho wa vitu viwili ambavyo ni tofauti kabisa, vyenye kufanana kwa kiasi fulani. Kwa namna fulani, Yesu ni kama mlango na mzabibu. Maneno ya Yesu wakati wa Chakula cha Mwisho ni mifano pia. Divai ilikuwa kama damu Yake (kwa kiasi fulani). Mkate ulikuwa kama mwili Wake (kwa kiasi fulani).

Mifano Ya Kristo

Mifano ya Kristo ni fungu lingine. Hiyo hufundisha masomo ya kiroho pia kwa kulinganisha vitu viwili visivyofanana. Ila, yenyewe ina neno umefanana na, au ni kama. Ni muhimu sana tukumbuke hilo tunapoifafanua, vinginevyo tutafanya kosa la kutafuta maana katika kila kitu kidogo kinachotajwa katika mfano. Mifano hufikia mwisho wa kufanana na tofauti zinaanza. Kwa mfano: Nikimwambia mke wangu hivi: “Macho yako ni kama vidimbwi vya maji” maana yake ni kwamba macho yake yanapendeza, yanavutia, na yana kina. Simaanishi kwamba kuna samaki ndani yake nao huogelea humo, wala kwamba ndege hutua hapo, wala kwamba wakati wa majira ya barafu yanaganda!

Hebu tutazame mifano mitatu ya Yesu, tukianza na Mfano wa Juya.

Tena ufalme wa mbinguni umefanana na juya, lililotupwa baharini, likakusanya samaki wa kila namna. Hata lilipojaa, walilivuta pwani wakaketi, wakakusanya walio wema vyomboni, bali walio wabaya wakawatupa. Ndivyo itakavyokuwa katika mwisho wa dunia; malaika watatokea, watawatenga waovu mbali na wenye haki na kuwatupa katika tanuru ya moto; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno (Mathayo 13:47-50).

Sasa swali – Je, ufalme wa mbinguni na juya ni kitu kimoja? Hapana kamwe! Vitu hivyo viwili vinatofautiana sana, lakini vinafanana kidogo. Kama ambavyo samaki wanapimwa na kutenganishwa katika makundi mawili – wanaotakiwa na wasiotakiwa – wanapotoka kwenye juya, ndivyo itakavyokuwa katika ufalme wa Mungu. Siku moja, waovu na wenye haki – ambao kwa sasa wanaishi pamoja wote – watatenganishwa. Lakini hapo ndipo mwisho wa kufanana. Samaki huogelea; wanadamu wanatembea. Wavuvi wanatenganisha samaki. Malaika watawatenganisha waovu na wenye haki. Samaki wanapimwa utamu wao baada ya kupikwa. Watu watapimwa kumtii Mungu au kutokumtii. Samaki wazuri wanawekwa katika vyombo, na wale wabaya wanatupiliwa mbali. Wenye haki wataurithi ufalme wa Mungu na waovu watatupwa jehanamu.

Mfano huu ni mzuri wa kuonyesha jinsi ambavyo kila mlinganisho usivyofaa kabisa kueleza kitu kwa sababu hatimaye vitu vile vinavyolinganishwa hufikia mahali pa kutofautiana. Hatupaswi kwenda zaidi ya kusudi la msemaji, yaani kudhani kwamba tofauti zote ndiyo kufanana. Kwa mfano: Wote tunajua kwamba “samaki wazuri” huishia kupikwa kwa moto, na “samaki wabaya” hurudi majini. Yesu hakutaja hayo, maana yangekuwa kinyume cha kusudi Lake.

Mfano huu haufundishi mkakati wa “uinjilisti kwa juya” – kwamba tujaribu kumkokota kila mmoja kanisani – mwema na mbaya – akitaka asitake! Mfano huu haufundishi kwamba ufuoni mwa bahari ndipo mahali panapofaa kufanyia uinjilisti. Mfano huu hauthibitishi kwamba Unyakuo wa kanisa utatokea mwisho wa kipindi cha dhiki kuu. Wala mfano huu haufundishi kwamba wokovu wetu ni chaguo la Mungu kwa kuwa samaki waliochaguliwa katika mfano hawakuhusika kwa njia yoyote na kuchaguliwa kwao. Usilazimishe maana isiyostahili katika mifano ya Yesu!

Kuwa Tayari

Angalia mfano mwingine maarufu sana wa Yesu – Mfano wa Wanawali Kumi.

Ndipo ufalme wa mbinguni utakapofanana na wanawali kumi waliotwaa taa zao, wakatoka kwenda kumlaki bwana arusi. Watano wao walikuwa wapumbavu, na watano wenye busara. Wale waliokuwa wapumbavu walizitwaa taa zao, wasitwae na mafuta pamoja nao; bali wale wenye busara walitwaa mafuta katika vyombo vyao pamoja na taa zao. Hata bwana arusi alipokawia, wote wakasinzia wakalala usingizi. Lakini usiku wa manane pakawa na kelele, ‘Haya, bwana arusi; tokeni mwende kumlaki’. Mara wakaondoka wanawali wale wote, wakazitengeneza taa zao. Wale wapumbavu wakawaambia wenye busara, ‘Tupeni mafuta yenu kidogo; maana taa zetu zinazimika.’ Lakini wale wenye busara wakawajibu wakisema, ‘Sivyo, hayatatutosha sisi na ninyi; afadhali shikeni njia mwende kwa wauzao, mkajinunulie’. Na hao walipokuwa wakienda kununua, bwana arusi akaja, nao waliokuwa tayari wakaingia pamoja naye arusini; mlango ukafungwa. Halafu wakaja na wale wanawali wengine wakasema, ‘Bwana, Bwana, utufungulie’. Akajibu akasema, ‘Amin nawaambia, siwajui ninyi’. Basi kesheni, kwa sababu hamwijui siku wala saa (Mathayo 25:1-13).

Je, somo kuu la mfano huu ni nini? Linapatikana katika maneno ya mwisho: Kaeni katika hali ya kusubiri kurudi kwa Bwana, maana anaweza kuchelewa kuliko inavyotazamia.

Kama nilivyokwisha sema huko nyuma, Yesu aliwaambia wanafunzi Wake wa karibu sana mfano huu (ona Mathayo 24:3; Marko 13:3), waliokuwa wanamfuata kwa uaminifu sana wakati huo. Basi – kinachosemwa wazi kabisa katika mfano huu ni kwamba iliwezekana kwa Petro, Yakobo, Yohana na Andrea kutokuwa tayari wakati Yesu atakaporudi. Hii ndiyo sababu alikuwa anawaonya. Basi, mfano huu unafundisha kwamba upo uwezekano kwa wale walio tayari sasa kwa ajili ya kurudi kwa Kristo kutokuwa tayari wakati atakaporudi. Wanawali wote kumi walikuwa tayari kimsingi, lakini watano wakawa hawako tayari. Kama bwana arusi angefika mapema zaidi, wote kumi wangeingia katika karamu ya arusi.

Lakini, nini maana ya kuwepo kwa wanawali watano wapumbavu na watano wenye busara? Je, maana yake ni kwamba katika waamini wote, nusu tu ndiyo watakuwa tayari wakati Kristo atakaporudi? Hapana.

Nini maana ya mafuta? Je, ni mfano wa Roho Mtakatifu? Hapana. Je, ni udhihirisho kwetu kwamba wale tu waliobatizwa na Roho Mtakatifu ndiyo watakaoingia mbinguni? Hapana.

Je, kurudi kwa bwana arusi usiku wa manane kunaonyesha kwamba Yesu atarudi usiku wa manane? Hapana.

Mbona bwana arusi hakuwaita wale wanawali wenye busara ili wawatambue wenzao wapumbavu? Kama angefanya hivyo, ingeharibu hoja nzima ya mfano, maana wale wapumbavu hatimaye wangeingia arusini.

Labda tunaweza kusema kwamba, sawa na jinsi wale wanawali wapumbavu waliyvokosa taa na wakalala, ndivyo na waamini wapumbavu wanavyoanza kutembea katika giza la kiroho na kujikuta wamelala kiroho pia. Mwishowe, wanajifikisha mahali pa kuhukumiwa. Pengine arusi katika mfano huu inaweza kufananishwa na karamu ya arusi ya Mwanakondoo hapo baadaye – ila, hapo ndipo tunapoweza kufika bila ya kuanza kulazimisha maana nyingine katika mfano huu.

Kuzaa Matunda

Tafsiri mbovu kuliko zote niliyowahi kusikia ya mfano mmoja wa Kristo ni ile iliyotolewa na mhubiri mmoja, kuhusu Mfano wa Ngano na Magugu. Hebu kwanza tusome mfano wenyewe.

Akawatolea mfano mwingie akisema, “Ufalme wa mbinguni umefanana na mtu aliyepanda mbegu njema katika konde lake; lakini watu walipolala, akaja adui yake akapanda magugu katikati ya ngano, akaenda zake. Baadaye majani ya ngano yalipomea na kuzaa, yakaonekana na magugu. Watumwa wa mwenye nyumba wakaenda wakamwambia, ‘Bwana, hukupanda mbegu njema katika konde lako? Limepata wapi basi magugu?’ Akawaambia, ‘Adui ndiye aliyetenda hivi’. Watumwa wakamwambia, ‘Basi, wataka twende tukayakusanye?’ Akasema, ‘La, msije mkakusanya magugu, na kuzing’oa ngano pamoja nayo. Viacheni vyote vikue hata wakati wa mavuno; na wakati wa mavuno nitawaambia wavunao, Yakusanyeni kwanza magugu, myafunge matita matita mkayachome; bali ngano ikusanyeni ghalani mwangu’.” (Mathayo 13:24-30).

Sasa, yule mhubiri akafafanua hivi:

Ni kweli kwamba ngano na magugu vinapochipua vinafanana. Hakuna awezaye kueleza kwamba hii ni ngano au haya ni magugu. Ndivyo ilivyo katika dunia na katika kanisa. Hakuna awezaye kueleza Wakristo wa kweli ni akina nani, na wasioamini n akina nani. Hawatambulikani kwa maisha yao, kwa sababu Wakristo wengi si watii kwa Kristo, sawa tu na wasioamini. Mungu tu ndiye ajuaye mioyo yao, Naye atawachambua wakati wa mwisho.

Shida ni kwamba – wazo la Mfano wa Ngano na Magugu si hilo! Ukitazama kwa makini utaona kwamba mfano unafundisha kwamba waamini ni rahisi kuwatofautisha na wasioamini. Angalia – watumwa walitambua kwamba magugu yamepandwa wakati ngano ilipoanza kuzaa (angalia ms. 26). Magugu hayazai matunda yoyote, na hiyo ndiyo njia rahisi ya kuyatambua. Mimi naona kuna fundisho kubwa kwa Yesu kuamua kwamba magugu yasiyozaa yawe mfano wa waovu watakaousanywa mwisho wa wakati na kutupwa jehanamu.

Hoja kuu za mfano huu ni dhahiri kabisa: Waliookoka kweli huzaa matunda; wasiookoka hawazai matunda. Japo Mungu hawahukumu waovu sasa hivi wanapoishi miongoni mwa waliookoka, siku moja atawatenganisha kutoka kwa wenye haki na kuwatupa jehanamu.

Halafu – Yesu Mwenyewe alitoa maana ya mfano huu, hivyo hakuna haja ya mtu kutafuta maana nyingine kuliko aliyotoa.

Azipandaye zile mbegu njema ni Mwana wa Adamu; lile konde ni ulimwengu; zile mbegu njema ni wana wa ufalme; na yale magugu ni wana wa yule mwovu; yule adui aliyeyapanda ni Ibilisi; mavuno ni mwisho wa dunia; na wale wavunao ni malaika. Basi, kama vile magugu yakusanywavyo na kuchomwa motoni; ndivyo itakavyokuwa katika mwisho wa dunia. Mwana wa Adamu atawatuma malaika zake, nao watakusanya kutoka katika ufalme wake machukizo yote na hao watendao maasi, na kuwatupa katika tanuru ya moto, ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno. Ndipo wenye haki watakapong’aa kama jua katika ufalme wa Baba yao. Mwenye masikio na asikie (Mathayo 13:36-43).

Kuzidisha Maana

Lugha nyingine inayotumiwa sana katika Biblia ni ile ya kuzidisha maana. Haya ni maneno yenye kuzidisha maana kwa makusudi ili kutilia mkazo kitu. Kwa mfano: Wakati mama anapomwambia mtoto wake hivi: “Nimekuita mara mia uje kula”, hapo maneno ya kuzidisha maana yametumiwa. Si kwamba ameitwa mara mia moja. Hebu tuone maneno ya Yesu katika Biblia yenye kuonyesha jambo hili.

Na mkono wako wa kuume ukikukosesha, ukate uutupe mbali nawe; kwa maana yakufaa kiungo chako kimoja kipotee wala mwili wako mzima usitupwe katika jehanamu (Mathayo 5:30).

Kama Yesu alimaanisha kwamba kila mmoja wetu anayetenda dhambi kwa njia fulani akitumia mkono wa kuume aukate, basi wote tungekuwa hatuna mikono ya kuume! Ila ni hivi: Tatizo la dhambi halimo katika mikono yetu. Basi, maana hasa ya Yesu ilikuwa kutufundisha kwamba dhambi inaweza kutupeleka jehanamu, na njia ya kuepuka dhambi ni kuondoa majaribu na vitu vile vinavyoweza kutufanya tujikwae na kuanguka.

Kumfananisha Mungu na Mwanadamu

Aina ya tatu ya lugha inayopatikana katika Maandiko ni kumfananisha Mungu na mwanadamu. Yaani, Mungu anapewa tabia au sifa za kibinadamu ili kutusaidia kumwelewa zaidi. Kwa mfano: Tunasoma hivi katika Mwanzo 11:5 –

BWANA akashuka ili auone mji na mnara waliokuwa wakiujenga wanadamu.

Hiyo ni lugha ya mfano kwa sababu, haiwezekani kwamba Mungu mwenye kujua yote alifanya safari kutoka mbinguni kwenda Babeli ili kuchunguza walichokuwa wanajenga wanadamu!

Wataalamu wengi wa Biblia wanahesabu kila tamko lenye kueleza viungo vya mwili wa Mungu kama vile mikono Yake, pua, macho na nywele kuwa ni lugha ya mfano. Wanasema haiwezekani Mungu Mwenyezi kuwa na viungo kama wanadamu.

Mimi sikubaliani nao kwa sababu kadhaa. Kwanza: Kwa sababu Maandiko yanasema wazi kabisa kwamba sisi tumeumbwa kwa mfano wa Mungu na sura Yake.

Mungu akasema, ‘Na tumfanye mtu kwa mfano wetu, kwa sura yetu’ (Mwanzo 1:26. Maneno mepesi kukazia).

Kuna wanaosema kwamba tumeumbwa kwa mfano wa Mungu na sura Yake kwa sababu tunajitambua, tunawajibika kiadili, tuna uwezo wa kufikiri na kadhalika. Sawa, lakini tusome maneno yanayofanana sana na Mwanzo 1:26. Haya yanapatikana sura kadhaa baadaye.

Adamu alipoishi miaka mia na thelathini, alizaa mwana kwa sura yake, kwa mfano wake, akamwita jina lake Seti (Mwanzo 5:3. Maneno mepesi kukazia).

Bila shaka maana yake ilikuwa hii: Seti alifanana kabisa na baba yake, kimwili. Kama hivyo ndivyo katika Mwanzo 5:3, bila shaka usemi huo unamaanisha hivyo hivyo katika Mwanzo 1:26. Tafsiri sahihi ya Maandiko na akili timamu zinasema hivyo.

Tena, tuna maelezo fulani kuhusu Mungu yatolewayo na waandishi wa Biblia waliomwona. Kwa mfano: Musa na wazee sabini na tatu wa Israeli walimwona Mungu!

Ndipo akakwea juu, Musa na Haruni na Nadabu na Abihu, na watu sabini miongoni mwa wazee wa Israeli; wakamwona Mungu wa Israeli; chini ya miguu yake palikuwa na kama sakafu iliyofanyizwa kwa yakuti samawi, kama zile mbingu zenyewe kwa usafi wake. Naye hakuweka mkono wake juu ya hao wakuu wa wana wa Israeli; nao wakamwona Mungu, wakala na kunywa (Kutoka 24:9-11).

Je, ungemwuliza Musa kama Mungu ana mikono na miguu, angesemaje?[2]

Nabii Danieli pia alipata maono ya Mungu Baba pamoja na Mungu Mwana.

Nikatazama hata viti vya enzi vikawekwa, na mmoja aliye mzee wa siku [Mungu Baba] ameketi; mavazi yake yalikuwa meupe kama theluji, na nywele za kichwa chake kama sufu safi; kiti chake cha enzi kilikuwa miali ya moto, na gurudumu zake moto uwakao. Mto kama wa moto ukatoka ukapita mbele zake; maelfu elfu wakamtumikia, na elfu kumi mara elfu kumi wakasimama mbele zake; hukumu ikawekwa, na vitabu vikafunuliwa … Nikaona katika njozi za usiku, na tazama, mmoja aliye mfano wa mwanadamu [Mungu Mwana] akaja pamoja na mawingu ya mbingu akamkaribia huyo mzee wa siku, wakamleta karibu naye. Naye akapewa mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa kabila zote na taifa zote na lugha zote wamtumikie; mamlaka yake ni mamlaka ya milele, ambayo hayatapita kamwe, na ufalme wake ni ufalme usioweza kuangamizwa (Danieli 7:9-10, 13-14).

Kama ungemwuliza Danieli ikiwa Mungu ana nywele nyeupe na umbo la kumwezesha kuketi kwenye kiti cha enzi, angejibuje?

Basi, mimi ninaamini kwamba Mungu Baba ana umbo lenye utukufu sana linalofanana na umbo la mwanadamu, japo Yeye hana mwili wa nyama na damu – ni roho (ona Yohana 4:24).

Sasa – Utajuaje mafungu ya Maandiko yanayotakiwa kufasiriwa kama yalivyo, na yapi yafasiriwe kwamba ni mifano? Hilo ni rahisi tu kwa yeyote anayeweza kufikiri vizuri. Wewe tafsiri kila kitu kama kilivyo, isipokuwa kama kinaeleweka vingine. Kwa mfano: Vitabu vya manabii katika Agano la Kale pamoja na kitabu cha Ufunuo cha Agano Jipya vimejaa lugha ya mifano. Kuna ambayo imefafanuliwa, na mingine haijafafanuliwa. Lakini lugha za mifano zinazohusika si ngumu kutambua.

Kanuni ya pili: Soma ukizingatia mantiki. Kila fungu lazima litafsiriwe kulingana na yatokanayo katika mafungu jirani, na Biblia nzima. Mantiki ya kihistoria na kitamaduni lazima pia izingatiwe kila inapowezekana.

Huenda ikawa kusoma Maandiko bila ya kujali mantiki yake na kwamba Biblia nzima inasema nini juu ya hicho, ndiyo sababu kubwa ya Maandiko kutafsiriwa vibaya.

Inawezekana kuifanya Biblia iseme chochote unachotaka iseme kwa kutenganisha maandiko na mantiki yake. Kwa mfano: Una habari kwamba Biblia inasema Mungu hayupo? Tunasoma hivi katika Zaburi ya 14, “Hakuna Mungu” (ms. 1). Lakini sasa, tukitaka kutafsiri maneno hayo kwa usahihi, lazima tuyasome katika mantiki yake. Ni hivi: “Mpumbavu amesema moyoni mwake, ‘Hakuna Mungu’.” (Zaburi 14:1. Maneno mepesi kukazia). Unaona? Mstari umekuwa na maana tofauti kabisa!

Mfano mwingine: Nilisikia mhubiri mmoja akihubiri juu ya Hitaji la Wakristo kubatizwa ‘katika moto’. Alianza ujumbe wake kwa kusoma maneno ya Yohana Mbatizaji katika Mathayo 3:11, kama ifuatavyo: “Kweli, mimi nawabatiza kwa maji kwa ajili ya toba, lakini yeye ajaye nyuma yangu ana nguvu kuliko mimi. Sistahili hata kuvua viatu vyake. Huyo atawabatiza kwa Roho Mtakatifu na kwa moto” (TLR).

Kutokana na mstari huo mmoja tu, alitengeneza ujumbe. Ninakumbuka akisema hivi: “Haitoshi kwamba umebatizwa na Roho Mtakatifu! Yesu anataka akubatize kwa moto pia, sawa na jinsi Yohana Mbatizaji alivyotamka!” Basi akaendela kueleza kwamba tukiisha “kubatizwa kwa moto” tutajaa shauku na ari ya kumtumikia Mungu. Hatimaye akaita watu wafike mbele, wale waliotaka “kubatizwa kwa moto”.

Kibaya ni hiki: Mhubiri huyo alifanya kosa la kawaida kabisa – la kuondoa mstari katika mantiki yake.

Kwani Yohana Mbatizaji alimaanisha nini aliposema Yesu angewabatiza watu kwa moto? Ili tupate jibu, tunachohitaji ni kusoma mistari miwili kabla ya mstari huo, na mstari mmoja baada ya mstari huo. Hebu tuanze na mistari miwili kabla. Yohana alisema hivi:

Msije mkadhani kwamba mtajiambia wenyewe, ‘Sisi ni wa uzao wa Ibrahimu’ kwa sababu nawaambia hivi: Mungu anaweza kumwinulia Ibrahimu watoto kutoka katika mawe haya. Tena, shoka limekwisha wekwa kwenye mashina ya miti. Basi, kila mti usiozaa matunda mazuri hukatwa na kutupwa motoni (Mathayo 3:9-10, TLR. Maneno mepesi kukazia).

Kwanza: Tunajifunza kwamba idadi fulani ya wasikilizaji wa Yohana siku hiyo

walikuwa Wayahudi, waliodhani kwamba wokovu wao ulitokana na ukoo wao. Hivyo, mahubiri ya Yohana yalikuwa uinjilisti.

Pili: Tunajifunza kwamba Yohana alikuwa anaonya kwamba watu wasio-okoka wako katika hatari ya kutupwa katika moto. Ni sahihi kufikiri kwamba “moto” anaosema Yohana katika mstari wa 10 ndiyo huo huo aliosema habari zake katika mstari wa 11.

Hayo yanakuwa wazi zaidi tukisoma mstari wa 12.

“Na pepeto Lake liko mkononi Mwake, naye atausafisha vizuri uwanda Wake wa kupuria nafaka. Ataikusanya ngano Yake ghalani, lakini makapi atayachoma kwa moto usiozimika” (Mathayo 3:12, TLR. Maneno mepesi kukazia).

Katika mstari wa 10 na 12, moto unaotajwa na Yohana ni ule wa jehanamu. Katika mstari wa 12 anataja kwa lugha ya mfano kwamba Yesu atagawanya watu katika makundi mawili – ngano, ambayo ataikusanya “ghalani”, na makapi, ambayo atayachoma “kwa moto usiozimika”.

Kutokana na mistari inayotangulia, bila shaka Yohana katika mstari wa 11 alimaanisha kwamba Yesu angewabatiza watu na Roho Mtakatifu kama ni waamini, au kwa moto, kama si waamini. Kwa kuwa ni hivyo, haipaswi mtu awahubirie Wakristo kwamba wanahitaji kubatizwa kwa moto!

Tukiachana na mantiki hiyo ya mistari husika, tutazame pia Agano Jipya lote. Je, kuna mfano wowote katika Matendo ya Mitume, mahali ambapo Wakristo wanatajwa kwamba walibatizwa “kwa moto”? Hapana. Kinachokaribia ni maelezo ya Luka kuhusu siku ya Pentekoste, wakati wanafunzi walipobatizwa kwa Roho Mtakatifu na ndimi za moto zikaonekana kwa muda juu ya vichwa vyao. Lakini Luka hakusema kwamba huo ulikuwa ni “ubatizo kwa moto”. Zaidi ya hayo – je, tunaweza kupata fundisho au ushauri wowote katika nyaraka za mitume kwamba Wakristo wabatizwe “kwa moto”? Hapana. Basi, ni salama kabisa kusema kwamba hakuna Mkristo anayetakiwa kutafuta ubatizo wa moto.

Injili Ya Uongo Iliyotoka Katika Maandiko

Mara nyingi, Injili yenyewe inatafsiriwa vibaya na wahubiri na waalimu ambao, kwa sababu wanashindwa kujali mantiki, wanatafsiri vibaya Maandiko. Mafundisho ya uongo kuhusu neema ya Mungu ni mengi sana kwa sababu hiyo.

Kwa mfano: Maneno ya Paulo kuhusu wokovu kupatikana kwa neema na si matendo, yapatikanayo katika Waefeso 2:8 yametumiwa vibaya kukuza injili ya uongo, na ni kwa sababu mantiki imepuuzwa. Paulo aliandika hivi:

Mmeokolea kwa neema kwa njia ya imani. Wala hiyo haitokani na ninyi wenyewe – ni zawadi ya Mungu. Si kwa sababu ya matendo, mtu yeyote asije akajisifu (Waefeso 2:8-9, TLR).

Wengi hutilia mkazo zaidi maneno ya Paulo kuhusu wokovu kuwa wa neema, kuwa zawadi, na si kwa ajili ya matendo. Kutokana na hilo, wanatoa fundisho kwamba wokovu na utakatifu havina uhusiano, kitu ambacho ni kinyume na ushahidi wa maandiko chungu nzima. Wengine hufikia hata mahali pa kusema kwamba hata toba si kitu cha lazima kwa wokovu kupatikana. Huo ni mfano mmoja mkubwa jinsi Maandiko yanavyotafsiriwa isivyo, kwa kupuuza mantiki.

Kwanza: Hebu tufikiri fungu lenyewe zima linasema nini. Paulo hasemi kwamba tumeokolewa kwa neema. Anasema tumeokolewa kwa neema kwa njia ya imani. Imani ni sehemu muhimu sana ya wokovu kama neema. Maandiko yanasema kwamba imani pasipo matendo haifai – imekufa – na haiwezi kuokoa (angalia Yakobo 2:14-26). Kwa hiyo, Paulo hafundishi kwamba utakatifu hauna maana kwa wokovu. Anachosema ni kwamba, juhudi zetu hazituokoi – msingi wa wokovu wetu ni neema ya Mungu. Yaani – tusingeweza kuokoka bila neema ya Mungu, lakini pia, ni wakati tunapoitikia neema ya Mungu kwa imani ndipo wokovu unapotokea katika maisha yetu. Matokeo ya wokovu kila mara ni utii, ambalo ni tunda la imani halisi. Tukitazama mantiki – mstari unaofuata tu – jambo hilo linathibitishwa. Paulo anasema hivi:

Kwa maana sisi tu kazi ya mikono Yake. Tumeumbwa katika Kristo Yesu tufanye matendo mema, ambayo Mungu aliyeandaa kabla, kwamba tuenende katika hayo (Waefeso 2:10, TLR).

Sababu ya kuzaliwa upya kwa njia ya Roho Mtakatifu, ya kuwa viumbe vipya ndani ya Kristo, ni ili tuweze kuenenda katika matendo mema ya utii. Kwa hiyo, ‘mchoro’ wa wokovu anaoeleza Paulo ungefanana hivi:

Neema + Imani = Wokovu + Utii

Yaani – neema ukijumlisha na imani matokeo ni wokovu pamoja na utii. Neema ya Mungu inapoitikiwa kwa imani, matokeo kila wakati ni wokovu na matendo mema.

Lakini, wale waliopasua maneno ya Paulo kutoka mantiki yake, wameunda kitu chao, kinachofanana hivi:

Neema + Imani – Utii = Wokovu

Yaani – neema ukijumlisha na imani bila utii husababisha wokovu. Kulingana na Biblia, huo ni uzushi – mafundisho potofu.

Tukisoma kidogo tu mantiki ya maneno ya Paulo, tutagunduapia kwamba hali halisi huko Efeso ilikuwa sawa na sehemu zingine alizohubiri Paulo. Yaani: Wayahudi walikuwa wanawafundisha waongofu wapya wa Paulo wasiokuwa Wayahudi kwamba iliwabidi kutahiriwa na kushika baadhi ya sheria za kidini za Torati ya Musa kama walitaka kuokoka. Basi, kutokana na mantiki hiyo ya tohara na matendo ya kidini, Paulo aliandika juu ya “matendo” yasiyotuokoa (ona Waefeso 2:11-22).

Tukisoma zaidi kidogo na kupata mantiki ya barua ya Paulo nzima kwa Waefeso, tutaona waziwazi kabisa kwamba Paulo aliamini utakatifu ni lazima kwa wokovu.

Lakini uasherati usitajwe kwenu kamwe, wala uchafu wowote wa kutamani, kama iwastahilivyo watakatifu; wala aibu wala maneno ya upuzi wala ubishi; hayo hayapendezi. Bali afadhali kushukuru. Maana neno hili mnalijua hakika, ya kwamba hakuna mwasherati wala mchafu wala mwenye tamaa, ndiye mwabudu sanamu, aliye na urithi katika ufalme wa Kristo na Mungu. Mtu asiwadangaye kwa maneno yasiyo na maana; kwa kuwa kwa sababu ya hayo hasira ya Mungu huwajia wana wa uasi (Waefeso 5:3-6. Maneno mepesi kukazia).

Kama Paulo aliamini kwamba neema ya Mungu mwishowe ingemwokoa mtu ambaye ni mchafu na asiyetubu, au mwenye tamaa, asingeandika maneno hayo. Maana aliyokusudia Paulo kwa maneno yake katika Waefeso 2:8-9 inaweza kueleweka vizuri tu katika mantiki yabarua yake nzima kwa Waefeso.

Vurugu Ya Galatia

Maneno ya Paulo katika barua yake kwa Wagalatia nayo yametafsiriwa hivyo – nje ya mantiki yake. Matokeo ni kupotoka kwa Injili, jambo ambalo Paulo alitarajia kulisahihisha kwa barua yake kwa Wagalatia.

Kiini cha barua nzima ya Paulo kwa Wagalatia ni: “Wokovu kwa imani, si kwa matendo ya Torati”. Lakini je, Paulo alikusudia kwamba wasomaji wake wafikie uamuzi kuwa utakatifu si kitu cha lazima ili mtu aingie katika ufalme wa Mungu? Hapana kamwe!

Kwanza: Tunaona kwamba kwa mara nyingine tena Paulo alikuwa anapambana na Wayahudi walikuja Galatia na kuwafundisha waongofu wapya kwamba wasingewokoka kama wasingetahiriwa na kuishika Torati ya Musa. Paulo anataja swala la tohara mara kadha katika barua yake, maana hilo linaonekana kuwa ndiyo mkazo mkuu kwa Wayahudi washika sheria (tazama 2:3, 7-9, 12; 5:2-3, 6, 11; 6:12-13, 15). Paulo hakusumbuliwa na waamini Wagalatia kuwa watii mno kwa amri za Kristo. Yeye alisumbuliwa na ukweli kwamba walikuwa hawamwamini Kristo kwa ajili ya wokovu wao, badala yake, wanaweka imani yao kwenye tohara na juhudi zao dhaifu sana za kuishika Sheria ya Musa.

Tunapotafakari mantiki nzima ya barua ya Paulo kwa Wagalatia, tunaona akiandika hivi katika sura ya 5:

Lakini mkiongozwa na Roho, hampo chini ya sheria. Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya: uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo. Katika hayo nawaambia mapema kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu (Wagalatia 5:18-21. Maneno mepesi kukazia).

Kama Paulo alitaka Wagalatia wajue kwamba wanaweza kupuuza utakatifu na bado waingie mbinguni, asingeandika maneno aliyoandika. Ujumbe wake si kwamba wasiokuwa watakatifu wanaweza kwenda mbinguni. Ujumbe wake ni kwamba wale wanaopuuza neema ya Mungu na kafara ya Kristo kwa kujaribu kujipatia wokovu wao kwa tohara na kushika Torati ya Musa hawawezi kuokolewa. Tohara haileti wokovu. Ni imani katika Yesu inayosababisha wokovu wenye kuwabadilisha waamini na kuwa viumbe vipya, vitakatifu.

Kwa sababu kutahiriwa si kitu wala kutokutahiriwa, bali kiumbe kipya (Wagalatia 6:15).

Yote hayo tena huonyesha jinsi ilivyo muhimu kujali mantiki wakati unapofasiri Maandiko. Njia ya pekee ya Injili kupotoshwa kwa kutumia Neno la Mungu ni kupuuza mantiki. Kinachotushangaza tu ni mioyo ya hao “watumishi” ambao wanafanya hivyo kwa ujasiri kabisa huku wakijua – yaani, makusudi.

Kwa mfano: Niliwahi kumsikia mhubiri mmoja akitangaza kwamba hatupaswi kutaja ghadhabu ya Mungu tunapohubiri Injili kwa sababu Biblia inasema hivi: “…wema wa Mungu wakuvuta upate kutubu” (Warumi 2:4b). Basi, kulingana na huyo ndugu, njia inayofaa ya kutangaza Injili ni kusema habari za upendo na wema wa Mungu tu. Hayo yangewavuta watu watubu.

Lakini, unaposoma mantiki ya mstari huo ambao mhubiri aliutaja – yaani sura ya pili ya kitabu cha Warumi – tunagundua kwamba unazungukwa na Maandiko kuhusu hukumu ya Mungu na hasira Yake takatifu! Mantiki yake inaonyesha kwamba hakuna uwezekano kuwa Paulo alikusudia kusema hayo aliyosema huyo mhubiri. Hebu ona.

Nasi twajua ya kuwa hukumu ya Mungu ni ya kweli juu yao wafanyao hayo. Wewe binadamu, uwahukumuye wale wafanyao hayo na kutenda yayo hayo mwenyewe, je! Wadhani ya kwamba utajiepusha na hukumu ya Mungu? Au waudharau wingi wa wema wake na ustahimili wake na uvumilivu wake, usijue ya kuwa wema wa Mungu wakuvuta upate kutubu? Bali kwa kadiri ya ugumu wako, na kwa moyo wako usio na toba, wajiwekea akiba ya hasira kwa siku ile ya hasira na ufunuo wa hukumu ya haki ya Mungu, atakayemlipa kila mtu kwa kadiri ya matendo yake; wale ambao kwa saburi katika kutenda mema wanatafuta utukufu na heshima na kutokuharibika, watapewa uzima wa milele; na wale wenye fitina, wasioitii kweli, bali wakubalio dhuluma, watapata hasira na ghadhabu; dhiki na shida juu ya kila nafsi ya mwanadamu atendaye uovu, Myahudi kwanza na Myunani pia (Warumi 2:2-9. Maneno mepesi kukazia).

Paulo anapotaja wema wa Mungu anasema juu ya wema ambao Mungu anaonyesha kwa kuchelewesha ghadhabu Yake! Sasa, inashangaza jinsi mtumishi anavyoweza kusema kitu cha kijinga namna hiyo, huku akijua Biblia nzima inavyosema juu ya hilo, na kwamba imejaa mifano tele ya wahubiri waliowaonya hadharani kabisa wenye dhambi kwamba watubu.

Jinsi Maandiko Yanavyokubaliana

Kwa kuwa Biblia imevuviwa na Mtu mmoja, ujumbe wake unakubaliana tangu mwanzo hadi mwisho. Hii ndiyo sababu tunaweza kuamini mantiki kutusaidia kutafsiri maana aliyokusudia Mungu katika fungu lolote. Mungu hawezi kusema kitu katika mstari mmoja kinachopingana na mstari mwingine, na ikionekana amefanya hivyo, hatuna budi kuendelea kujifunza mpaka tafsiri ya mistari hiyo miwili ikubaliane. Kwa mfano: Katika sehemu kadha za Mahubiri ya Yesu Mlimani, inaonekana kana kwamba anapinga na hata kurekebisha sheria ya kiadili ya Agano la Kale. Hebu tazama hii:

Mlisikia kwamba walisema hivi: ‘Jicho kwa jicho, na jino kwa jino’. Lakini mimi nawaambia, msishindane na mtu mwovu, bali mtu akikupiga kofi shavu la kuume, mgeuzie upande wa pili pia (Mathayo 5:38-39, TLR).

Yesu anatamka maneno ya Torati ya Musa, kisha anasema kitu kinacho-onekana kupinga sheria ile aliyoitamka. Tutafsiri alichosema namna gani? Je, Mungu amebadilisha mawazo kuhusu swala la maadili? Je, kulipiza kisasi kulikubalika katika agano la kale lakini hakukubaliki katika agano jipya? Kitakachotusaidia ni mantiki tu.

Yesu alikuwa anazungumza na wanafunzi Wake (ona Mathayo 5:1-2), watu ambao walichojua kuhusu Neno la Mungu ni mambo waliyofundishwa na waandishi na Mafarisayo katika masinagogi yao. Huko walisikia sheria ya Mungu ikitajw akwamba, “Jicho kwa jicho, na jino kwa jino.” Maana ya amri hiyo ilikuwa imegeuzwa sana na waandishi na Mafarisayo kwa sababu ya kupuuzia mantiki yake. Mungu hakutaka amri hiyo itafsiriwe kwamba ni sharti watu wajaribu kulipiza kisasi kila mara kwa makosa madogo. Katika Torati ya Musa Yeye alisema kisasi ni chake (ona Kumbu. 32:35), na kwamba watu Wake wawatendee mema adui zao (tazama Kutoka 23:4-5). Lakini waandishi na Mafarisayo walipuuza amri hizo na kutengeneza tafsiri yao wenyewe ya maneno ya Mungu ya “jicho kwa jicho”, iliyowapa wao haki inayofaa ya kujilipiza kisasi kibinafsi.[3] Walipuuza mantiki.

Agizo la Mungu kuhusu “jicho kwa jicho, na jino kwa jino” linapatikana katika mantiki ya amri Zake zenye kutoa haki inayostahili katika mahakama za Israeli (tazama Kutoka 21:22-24; Kumbu. 19:15-21). Kuwa na utaratibu wa mahakama ni ufunuo tosha wa jinsi Mungu asivyounga mkono kisasi cha mtu binafsi. Mahakimu wasio na upendeleo wanaotazama ushahidi husika wana uwezo zaidi wa kutoa haki kuliko watu binafsi ambao wamekosewa na wenye mtazamo wa kibinafsi. Mungua natazamia kwamba mahakama na mahakimu watatoa adhabu zinazostahili hatia, bila upendeleo. Ndiyo sababu ni “jicho kwa jicho, jino kwa jino”.

Basi, tunaweza kulinganisha maneno hayo ambayo mwanzoni yalionekana yanapingana. Yesu alikuwa anawasaidia wasikilizaji Wake waliokuwa wamefundishwa uongo maisha yao yote waelewe mapenzi ya Mungu ya kweli kwa ajili yao kuhusu kisasi cha binafsi. Hayo yalikuwa yamefunuliwa tayari katika Torati ya Musa, lakini yalipotoshwa na Mafairsayo. Hakuwa anakwenda kinyume na Torati alyompa Musa. Alikuwa anadhihirisha maana yake halisi – ile iliyokusudiwa.

Sasa hilo linatusaidia na sisi kuelewa vizuri kile ambacho Yesu anatazamia kutoka kwetu kuhusu kutokuelewana kunakoweza kusababisha twende mahakamani. Mungu hakuwatazamia Waisraeli kupuuzia kila kosa walilotendewa na Waisraeli wenzao. Ingekuwa hivyo asingeweka utaratibu wa mahakama. Vivyo hivyo, Mungu hatazamii Wakristo kupuuzia kila kosa wanalotendewa na waamini wanzao (au wasioamini basi). Agano Jipya linapendekeza kwamba Wakristo wasioweza kuelewana wapate msaada wa kupatanishwa na waamini wenzao (ona 1Wakorintho 6:1-6). Wala hakuna kosa kwa Mkristo kumpeleka asiyeamini mahakamani, kwa habari ya kutokuelewana kwa hali ya juu. Mfano ni kama kutolewa jicho au jino! Makosa madogo ni kama vile kupigwa kofi shavuni, au kunyang’anywa kitu kidogo (kama vile shati lako), au kulazimishwa kwenda maili moja. Mungu anataka watu Wake wamwige Yeye na kuonyesha neema isiyo ya kawaida kwa wenye dhambi na waovu wasiofikiri.

Wamekuwepo waamini wenye nia njema tu ambao, kwa kudhani kwamba wanamtii Yesu, wanakataa kuwashtaki wale ambao wameshikwa wakiwaibia. Walifikiri kwamba wanageuza “shavu la pili – kumbe wanamwezesha mwizi kuiba tena, wakimfundisha kwamba hakuna adhabu kwa kosa kama hilo. Wakristo wa namna hiyo hawaenendi kwa kuwapenda wengine ambao wataibiwa mali na mwizi huyo huyo! Mungu anataka wezi wapate haki na kutubu. Lakini, mtu anapokukosea kwa njia ndogo kama kukupiga kofi, usimpeleke mahakamani au kumpiga kofi na wewe. Mwonyeshe rehema na upendo.

Kutafsiri Ya Kale Kwa Kutumia Mpya

Hatupaswi kutafsiri maandiko ya Agano Jipya kwa mwanga wa Agano la Kale tu, bali kila wakati tutafsiri maandiko ya Agano la Kale kwa mwanga wa Agano Jipya. Kwa mfano: Waamini wazuri tu wamesoma zile sheria za chakula za Musa, na wakafikia uamuzi kwamba Wakristo wanatakiwa kula chakula kulingana na sheria hizo. Kama wangesoma mistari miwili tu katika Agano Jipya wangegundua kwamba sheria za Musa kuhusu vyakula haziwahusu walioko chini ya Agano Jipya.

[Yesu] Akawaambia, ‘Hivi hata ninyi hamna akili? Hamfahamu ya kwamba kila kitu kilicho nje ya mtu, kikimwingia, hakiwezi kumtia unajisi kwa sababu hakimwingii moyoni ila tumboni tu, kisha chatoka kwenda chooni?’ (Kwa kusema hivi alivitakasa vyakula vyote) (Marko 7:18-19).

Basi Roho anena waziwazi ya kwamba nyakati za mwisho wengine watajitenga na imani, wakisikiliza roho zidanganyazo na mafundisho ya mashetani; kwa unafiki wa watu wasemao uongo, wakichomwa moto dhamiri zao wenyewe, wakiwazuia watu wasioe, na kuwaamuru wajiepushe na vyakula ambavyo Mungu aliviumba vipokewe kwa shukrani na walio na imani wenye kuijua hiyo kweli. Kwa maana kila kiumbe cha Mungu ni kizuri, wala hakuna cha kukataliwa kama kikipokewa kwa shukrani; kwa kuwa kimetakaswa kwa neno la Mungu na kwa kuomba (1Timo. 4:1-5).

Chini ya agano jipya, hatutawaliwi na Torati ya Musa bali Torati ya Kristo (tazama 1Wakorintho 9:20-21). Ingawa Yesu aliunga mkono maadili ya Torati ya Musa (na kuyaingiza katika Torati ya Kristo), hakufundisha kwamba Wakristo ni lazima washike sheria za Musa kwa habari ya vyakula. Hata mitume hawakufundisha hivyo.

Ni wazi lakini kwamba Wakristo wa kwanza – ambao wote walikuwa Wayahudi walio-ongoka – waliendelea kufuata sheria za vyakula za agano la kale kwa sababu ya desturi zao (ona Matendo 10:9-14). Na watu wa Mataifa walipoanza kumwamini Yesu, wale Wayahudi Wakristo wa mwanzo waliwaambia wafuate sheria za vyakula za Musa kwa kiasi fulani kwa sababu tu ya kuwajali Wayahudi jirani ambao wangekwazwa (ona Matendo 15:1-21). Kwa hiyo, hakuna kosa lolote kwa Wakristo kufuata sheria za vyakula za Musa mradi tu wasizitumaini kwamba zitawaokoa au kuwapa haki fulani.

Baadhi ya Wakristo wa kwanza walishawishika pia kwamba ni kosa kula nyama au vyakula vilivyotolewa sadaka kwa sanamu. Paulo aliwashauri waamini waliokuwa na mawazo tofauti (kama yeye) wafuate kanuni ya upendo kwa ndugu zao wenye “imani dhaifu (tazama Warumi 14:1). Alishauri wasifanye chochote kitakachowakwaza dhamiri zao. Kama mtu ataacha kula vyakula kwa sababu ya kumwamini Mungu (hata kama imani yake haina msingi), anatakiwa kupongezwa kwa msimamo wake badala ya kulaumiwa kwa kutokuelewa kwake. Vivyo hivyo – wale wanaojiepusha na vyakula fulani kwa sababu ya imani zao binafsi wasiwahukumu wale wasiojiepusha. Wote wawili waenende kwa upendo, maana hilo linaagizwa na Mungu (tazama Warumi 14:1-23).

Vyovyote vile – Kwa sababu Biblia ni ufunuo unaoendelea, tunapaswa kutafsiri ufunuo wa zamani (yaani, Agano la Kale) kwa mwanga wa ufunuo mpya zaidi (yaani, Agano Jipya). Hakuna ufunuo wowote wa Mungu ambao unapingana – siku zote unasaidiana na kukubaliana.

Mantiki Ya Kitamaduni na Kihistoria

Kila inapowezekana, tunatakiwa kujali mantiki ya kitamaduni na kihistoria ya maandiko tunayojifunza. Kujua kitu juu ya mila, jiografia na historia ya fungu husika mara nyingi husaidia kupata mtazamo ambao tungeukosa. Hapo tunahitaji msaada kutoka vitabu vingine. Biblia nzuri ya kujifunzia (siku hizi zipo!) itakuwa na msaada katika eneo hili.

Ifuatayo ni mfano michache kuhusu jinsi habari za kihistoria au utamaduni zinavyoweza kutusaidia tusichanganyikiwe tunaposoma Biblia.

1) Wakati mwingine katika Maandiko tunasoma kuhusu watu kupanda darini (au orofani) – tazama Matendo 10:9 – au kutoboa dari (tazama Marko 2:4). Itasaidia tukijua kwamba kwa kawaida huko Israeli nyumba zilikuwa na mapaa yaliyonyooka, na kwamba pembeni mwa kila nyumba kulikuwa na ngazi za kupandia huko darini. Tusipojua hilo tutafikiri juu ya mtu katika Biblia akihangaika kuparamia bati la msonge huku akipata shida mahali pa kujishikilia!

2) Tunasoma katika Marko 11:12-14 kwamba Yesu aliulaani mtini kwa sababu haukuwa na tini, japo “hakikuwa kipindi cha tini”. Inasaidia tukijua kwamba kwa kawaida miti ya mtini huwa na tini chache hata kama si wakati wake. Basi, Yesu hakukosea kuwa na matazamio aliyokuwa nayo.

3) Tunasoma katika Luka 7:37-48 kuhusu mwanamke aliyeingia nyumbani mwa Farisayo, mahali Yesu alipokuwa akila chakula. Maandiko yanasema alisimama nyuma ya Yesu akilia, kisha akaanza kulowesha miguu ya Yesu kwa machozi yake, kuipangusa na nywele zake, na kuibusu na kuipaka marhamu. Itatushangaza kwamba iliwezekanaje hayo yote kufanikiwa huku Yesu ameketi mezani anakula chakula. Je, aliingia chini ya meza? Alifanikiwaje kuiepuka miguu ya wale walaji wengine wote?

Jibu ni kwamba katika siku zile, kawaida ilikuwa kula chakula ukiwa umejilaza chini kwa ubavu mmoja karibu na meza fupi. Mkono mmoja ulitumiwa kujitegemeza na mwingine kujilisha. Yesu akiwa hivyo, aliweza kuabudiwa na kutendewa yote hayo na yule mwanamke.

Hii pia inatusaidia kuelewa jinsi Yohana alivyoweza kuegama kifuani pa Yesu wakati wa Chakula cha Mwisho, na kumwuliza swali. Yohana alikuwa amejilaza kwa ubavu, mgongo wake ukimkabili Yesu. Basi ilikuwa rahisi tu kwake kuegama kifuani pa Yesu na kumwuliza swali bila kumsumbua mtu mwingine (ona Yohana 13:23-25). Ile picha maarufu ya Chakula cha Mwisho iliyochorwa na Da Vinci, ambapo Yesu na wanafunzi wake wameketi mezani – sita upande huu na sita upande huu – inaonyesha kutoelewa Biblia kwa mchoraji huyo. Hapo alihitaji kuelezwa kidogo mantiki ya kihistoria!

Swali La Kawaida Kuhusu Mavazi

Swali moja ninaloulizwa na wachungaji duniani kote mara nyingi ni hili: “Je, ni sawa kwa wanawake Wakristo kuvaa suruali, na huku Biblia inakataza wanawake kuvaa mavazi ya wanaume?”

Hili ni swali zuri tunaloweza kujibu tukitumia kanuni nzuri tu za kutafsiri, pamoja na kutazama mantiki ya kitamaduni.

Hebu kwanza tutazame zuio la Biblia juu ya wanawake kuvaa mavazi ya wanaume (na kinyume chake pia).

Mwanamke asivae mavazi ya mwanamume, na mwanamume asivae mavazi ya mwanamke, maana yeyote afanyaye mambo hayo ni chukizo kwa BWANA Mungu wako (Kumbu. 22:5, TLR).

Tunapaswa kuanza kwa kuuliza hivi: “Kusudi la Mungu kutoa amri hii lilikuwa nini?” Je, lengo Lake lilikuwa kuwazuia wanawake kuvaa suruali?

Hapana – hilo haliwezi kuwa kusudi Lake kwa sababu wakati huo wanaume wa Israeli hawakuwa wanavaa suruali. Suruali hazikuhesabiwa kuwa mavazi ya kiume au ya kike, wala ya mtu yeyote. Ukweli ni kwamba, mavazi yaliyovaliwa siku za Biblia yalifanana sana na mavazi ya kike ya siku hizi! Hiyo ni habari kidogo tu ya kihistoria na kitamaduni, inayotusaidia kutafsiri vizuri kile ambacho Mungu anasema.

Sasa – kusudi la Mungu lilikuwa nini?

Tunasoma kwamba yeyote aliyevaa mavazi yasiyo ya jinsia yake alikuwa chukizo kwa BWANA. Hilo ni jambo zito. Je, kama mwanamume akichukua kitambaa cha mwanamke akakivaa kichwani kwa nukta tatu anakuwa chukizo kwa Mungu? Hapana, si hivyo.

Inaonekana kwamba, kitu alichokuwa anapinga Mungu ni watu kuvaa makusudi ili waonekane kuwa ni wa jinsia nyingine na huku si hivyo. Mbona mtu atake kufanya hivyo? Pengine ni kwa sababu alitazamia kumshawishi mwingine wa jinsia ile kimapenzi – ufuska. Kama ni hivyo, bila shaka tunaanza kuelewa jinsi tendo hilo linavyoweza kuwa chukizo kwa Mungu.

Basi, haiwezekani mtu kuamua kwamba ni makosa kwa wanawake kuvaa suruali kutokana na maneno ya Kumbukumbu 22:5, isipokuwa kama atavaa ili kujifanya mwanamume, kwa lengo la kuwashawishi wanaume kimapenzi. Akivaa na aendelee kuonekana kama mwnaamke, hafanyi dhambi kwa kuvaa suruali.

Ila, Maandiko yanafundisha kwamba wanawake wavae mavazi ya staha (ona 1Timo. 2:9). Basi, suruali zenye kubana sana kiasi cha kuonyesha umbo hazifai. Hata magauni na sketi na blauzi za namna hiyo hazifai, kwa sababu zinaweza kusababisha wanaume kutamani. Mavazi mengi yanayovaliwa na wanawake hadharani katika nchi za Magharibi (na hata Afrika!) hayafai kabisa, na ni yale yanayovaliwa na makahaba katika nchi zingine. Hakuna mwanamke Mkristo anayetakiwa kuvaa mavazi hadharani yenye kuonyesha mwili, au kwa lengo la “kuvutia”.

Mawazo Mengine Machache

Inanishangaza kwamba sijawahi kuulizwa swali la wanawake kuvaa suruali na wachungaji huko Uchina. Pengine ni kwa sababu wanawake wengi wa Uchina wamekuwa wakivaa suruali kwa muda mrefu. Nimeulizwa swali hili na wachungaji katika nchi ambazo wanawake wengi hawavai suruali. Hapo tunaona mwingiliano wa utamaduni.

Pia inanishangaza kwamba sijawahi kuulizwa swali kama hilo na watumishi wanawake katika nchi ya Myanmar, ambako kimila wanaume huvaa vazi linalofanana na sketi liitwalo longgi. Ni kwamba mavazi ya kike na ya kiume hutofautiana kutoka mila hadi nyingine, hivyo tunapaswa kuwa waangalifu tusilazimishe utamaduni wetu kuingia katika Biblia.

Mwisho: Nashangaa ni kwa nini wanaume wengi wasiotaka wanawake wavae suruali kwa sababu ya Kumbukumbu 22:5 hawaoni sababu ya kujipima wenyewe na Walawi 19:27. Tunasoma hivi:

Msinyoe denge pembe za vichwani, wala msiharibu pembe za ndevu zenu.

Inawezekanaje wanaume – kinyume kabisa cha Walawi 19:27 – wanyoe kabisa ndevu walizopewa na Mungu, zenye kuwatofautisha na wanawake, kisha wawahukumu wanawake wanaovaa suruali kwamba wanajaribu kufanana na wanaume? Hapo kuna unafiki kiasi fulani!

Labda maelezo kidogo ya kihistoria yatasaidia kuelewa kusudi la Mungu katika Walawi 19:27. Kuharibu pembe za ndevu ulikuwa utaratibu wa kidini wa kipagani katika kuabudu sanamu. Mungu hakutaka watu wake waonekane kuwa wamejitoa kwa miungu ya kipagani.

Nani Anayezungumza?

Kila mara tutazame nani anazungumza katika maandiko, maana hilo litatusaidia kutafsiri fungu hilo vizuri. Japo kila kilichomo katika Biblia kimevuviwa kuwemo, si kila kitu kilichomo katika Biblia ni Neno la Mungu lililovuviwa. Nini maana yangu?

Katika mafungu mengi ya Maandiko, maneno ya watu ambayo hayajavuviwa yameandikwa. Kwa hiyo, hatupaswi kufikiri kwamba kila kitu kilichosemwa na watu kilichoandikwa katika Biblia kimevuviwa na Mungu.

Kwa mfano: Watu wengi hukosea kwa kutumia maneno ya Ayubu na rafiki zake kana kwamba ni maneno yaliyovuviwa ya Mungu. Kuna sababu mbili kubwa zenye kuonyesha kwamba ni kosa. Kwanza: Ayubu na rafiki zake walibishana kwa sura thelathini na nne. Hawakukubaliana. Basi, si kila walichosema kinachoweza kuhesabiwa kuwa Neno la Mungu lililovuviwa kwa sababu Mungu hajipingi Mwenyewe.

Pili: Mwishoni mwa kitabu cha Ayubu, Mungu mwenyewe anazungumza, naye anamkemea Ayubu na rafiki zake kwa kusema mambo ambayo hayakuwa sahihi (ona Ayubu 38 hadi 42).

Tunapaswa kuwa makini tunaposoma Agano Jipya pia. Mara kadhaa Paulo anasema wazi kwamba baadhi ya mafungu aliyoandika ni mawazo yake au maoni yake binafsi (ona 1Wakorintho 7:12, 25-26, 40).

Nani Anasemeshwa?

Hatupaswi tu kuuliza nani anayezungumza katika fungu lolote la Biblia. Tunapaswa pia kuona nani anaambiwa kinachosemwa. Tusipofanya hivyo, tutatafsiri vibaya kitu – kwamba kinatuhusu – kumbe si hivyo. Au tunaweza kutafsiri kwamba kitu hakituhusu, kinachotuhusu.

Mfano: Wengi hudai hii ahadi ipatikanayo katika Zaburi mojawapo, wakiamini ni yao.

Atakupa haja za moyo wako (Zaburi 37:4).

Lakini je, ahadi hiyo ni kwa kila aisomaye au ajuaye habari zake? Hapana! Tukisoma mantiki, tutaona kwamba inawahusu watu fulani tu, watakaotimiza masharti matano.

Umtumaini BWANA, ukatende mema, ukae katika nchi, upendezwe na uaminifu. Jifurahishe katika BWANA, naye atakupa haja za moyo wako (Zaburi 37:3-4, TLR).

Ni muhimu sana tujue nani anaambiwa maneno husika. Ona mfano mwingine.

Petro akaanza kumwambia [Yesu], ‘Tazama, sisi tumeacha vyote tukakufuata wewe’. Yesu akasema, ‘Amin nawaambieni, hakuna mtu aliyeacha nyumba, au ndugu waume au ndugu wake, au mama au baba au watoto, au mashamba kwa ajili yangu, na kwa ajili ya Injili, ila atapewa mara mia sasa wakati huu, nyumba na ndugu waume na ndugu wake na mama na watoto na mashamba, pamoja na udhia; na katika ulimwengu ujao uzima wa milele’ (Marko 10:28-30).

Ni kawaida sana mahali pengine kudai hiyo “mara mia” wakati mtu anapotoa kumsaidia mtu anayehubiri Injili. Lakini, hiyo ahadi ni kwa watu wa namna hiyo? Hapana. Imetolewa kwa watu wanaoacha familia zao, mashamba yao au hata nyumba zao ili kuhubiri Injili, kama alivyofanya Petro aliyemwuliza Yesu swali hilo. Alitaka kujua thawabu yake na wanafunzi wengine ingekuwa nini.

Cha kushangaza ni kwamba, wale wenye kuhubiri juu ya kurudishiwa mara mia hukazia sana nyumba na mashamba. Hawataji sana kuhusu watoto na udhia, ambavyo pia vimetajwa! Yesu hakumaanisha kwamba watakaoacha nyumba zao watapata nyumba mia moja badala yake. Aliahidi tu kwamba watu wakiacha familia zao na nyumba zao, wanafamilia wao wapya kiroho watawakaribisha majumbani mwao kukaa. Wanafunzi wa kweli hawajali sana kuhusu kumiliki vitu maana hawana chochote chao – wao ni mawakili tu wa vitu vya Mungu.

Mfano Wa Mwisho

Watu wanaposoma mahubiri ya Yesu ya pale “Mlima wa Mizeituni” katika Mathayo 24 na 25, kuna wanaodhani kwamba alikuwa anazungumza na wasiookoka, na kwamba hayo aliyosema hapo hayawahusu. Hayo ni makosa. Wanasoma Mfano wa Mtumishi Asiyekuwa Mwaminifu na Wanawali Kumi kana kwamba ni mambo wanayoambiwa wasioamini. Lakini kama nilivyokwisha sema huko nyuma, waliokuwa wanaambiwa ni wanafunzi waliokuwa karibu sana na Yesu (tazama Mathayo 24:3; Marko 13:3). Basi, kama Petro, Yakobo, Yohana na Andrea walihitaji kuonywa juu ya uwezekano wa kutokuwa tayari Yesu akirudi, sisi pia tunahitaji kuonywa juu ya hilo. Maonyo ya Yesu katika mafundisho Yake pale Mlima wa Mizeituni yanamhusu kila mwamini – hata wale wasiodhani yanawahusu kwa sababu ya kushindwa kujua waliokuwa wanaambiwa.

Kanuni ya tatu: Soma na moyo ulio wazi. Usilazimishe imani na mafundisho yako kwenye fungu la Maandiko. Ukisoma kitu kinachopingana na imani yako, usijaribu kuibadili Biblia. Badilisha unachoamini.

Kila mmoja wetu husoma Maandiko akiwa na mtazamo au msimamo fulani tayari. Kwa sababu hiyo, mara nyingi ni vigumu sana kwetu kusoma Biblia kwa moyo ulio wazi na wa dhati. Tunaishia kulazimisha imani zetu kwenye Maandiko, badala ya kuruhusu Biblia iumbe imani au itikadi au mafundisho yetu. Mara nyingine hata tunatafuta Maandiko yatakayounga mkono itikadi zetu, na kupuuza yale yenye kupingana nazo.

Angalia mfano huu niliokutana nao hivi karibuni, wenye kuonyesha jinsi unavyoweza kulazimisha itikadi yako iingie kwenye mstari. Mwalimu mmoja alianza kwa kusoma maneno maarufu sana ya Yesu – Mathayo 11:28-29.

Njooni kwangu ninyi nyote mliochoka, na wenye kulemewa, nami nitawapumzisha. Ivaeni nira yangu mjifunze kwangu, maana mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo, nanyi mtapata raha nafsini mwenu (TLR).

Kisha mwalimu akaendelea kwa kufafanua kwamba Yesu alikuwa anatoa mapumziko aina mbili. Pumziko la kwanza (kwa maoni yake) ni la wokovu, katika 11:28, na la pili ni la uanafunzi katika 11:29. Pumziko la kwanza linapatikana kwa kumjia Yesu, na la pili linapatikana kwa kujitoa Kwake awe Bwana, au, kujitia nira Yake.

Lakini – hiyo ndiyo maana aliyokusudia Yesu? Hapana. Huko ni kulazimisha maana kwenye andiko ambayo haipo wala haidhaniwi. Yesu hakusema anatoa mapumziko aina mbili. Alikuwa anatoa pumziko moja kwa wale waliochoka na wenye kulemewa, na njia pekee ya kupata pumziko hilo ni kwa kuvaa nira ya Yesu – yaani, kujinyenyekeza Kwake. Hiyo ndiyo maana ya Yesu.

Mbona huyo mwalimu akatoa tafsiri hiyo? Kwa sababu maana halisi ya fungu hilo haikulingana na imani aliyo nayo yeye – kwamba kuna aina mbili za Wakristo waendao mbinguni – waamini, na wanafunzi. Hivyo hakutafsiri fungu hilo kwa moyo ulio wazi na ukweli.

Kama ambavyo tumeona huko nyuma katika mafungu mengi tu ya Maandiko tulipochambua itikadi hiyo, tafsiri ya mwalimu hiyo hailingani na mantiki ya mafundisho mengine ya Yesu. Hakuna popote katika Agano Jipya tunapojifunza kwamba kuna aina mbili za Wakristo wanaokwenda mbinguni – waamini na wanafunzi. Waamini wote wa kweli ni wanafunzi. Wasiokuwa wanafunzi si waamini. Uanafunzi ni tunda la imani ya kweli.

Basi, tujitahidi kusoma Biblia kwa mioyo iliyo wazi, iliyo safi. Tukifanya hivyo, tutampenda Kristo zaidi, na kumtii.


[1] Ni dhahiri kwamba Paulo hakuamini juu ya usalama wa wokovu milele bila masharti. Ingekuwa hivyo, asingemwambia Timoteo – ambaye ameokoka – kwamba alihitaji kufanya kitu ili kuhakikisha wokovu wake.

[2] Wakati mwingine tena Musa alimwona Mungu ‘akipita’. Mungu aliweka mkono Wake kwa njia iliyomzuia Musa kuuona uso Wake. Tazama Kutoka 33:18-23.

[3] Na ijulikane pia kwamba Yesu alikwisha sema katika mahubiri Yake kwamba kama haki ya wasikilizaji Wake isingezidi ile ya waandishi na Mafarisayo, wasingeingia mbinguni (ona Mathayo 5:20). Kisha, Yesu aliendelea kuhubiri, akionyesha upungufu wa aina mbalimbali wa waandishi na Mafarisayo.

Mahubiri Ya Yesu Mlimani

Sura Ya Nane

 

Kwa sababu ya shauku yake ya kutaka kufanya watu kuwa wanafunzi na kuwafundisha kuyashika yote ambayo Kristo aliagiza, mtumishi anayefanya watu kuwa wanafunzi atavutiwa sana na Mahubiri ya Yesu pale Mlimani. Hakuna ujumbe mwingine mrefu wa Yesu ulioandikwa, nao umejaa maagizo au amri Zake. Mtumishi anayefanya watu kuwa wanafunzi atataka kutii mahubiri hayo na kuwafundisha wanafunzi wake kila kitu alichoamuru Yesu katika mahubiri hayo.

Kwa kuwa ni hivyo, nitakushirikisha ninayoelewa kuhusu mahubiri hayo, yapatikanayo katika Mathayo sura ya 5 hadi 7. Ninawatia moyo watumishi kuwafundisha wanafunzi wao Mahubiri ya Yesu ya Mlimani mstari kwa mstari. Natumaini kwamba niliyoandika yatasaidia kufanikisha jambo hilo.

Ufuatao ni ufupisho au muhtasari wa Mahubiri ya Yesu Mlimani, ili kutusaidia kuyaona kwa mtazamo wa jumla pamojana kuonyesha mada kuu.

I) Yesu akusanya wasikilizaji Wake (5:1-2)

II) Utangulizi (5:3-20)

A) Sifa na baraka za wenye heri (au waliobarikiwa) (5:3-12)

B) Wito wa kuendelea kuwa chumvi na nuru (5:13-16)

C) Uhusiano kati ya Torati na wafuasi wa Kristo (5:17-20)

III) Mahubiri Yenyewe: Kuwa na haki kuliko waandishi na Mafarisayo (5:21 – 7:12)

A) Pendaneni, si kama waandishi na Mafarisayo (5:21-26)

B) Usafi katika maadili ya kimwili. Msiwe kama waandishi na Mafarisayo (5:27-32)

C) Uwe mkweli, si kama waandishi na Mafarisayo (5:33-37)

D) Msilipe kisasi, kama wanavyofanya waandishi na Mafarisayo (5:38-42)

E) Msiwachukie adui zenu, kama wanavyofanya waandishi na Mafarisayo (5:43-48)

F) Tenda mema kwa nia njema, si kama waandishi na Mafarisayo (6:1-18)

1) Wape maskini kwa nia njema (6:2-4)

2) Omba kwa nia njema (6:5-6)

3) Maelezo kidogo kuhusu maombi na msamaha (6:7-15)

a) Mafundisho kuhusu maombi (6:7-13)

b) Umuhimu wa kusameheana (6:8-15)

4) Funga kwa nia njema (6:16-18)

G) Usitumikie fedha, kama waandishi na Mafarisayo (6:19-34)

H) Usitafute makosa madogo madogo kwa ndugu yako (7:1-5)

I) Usipoteze wakati kuwapa ukweli watu wasio na shukrani (7:6)

J) Himizo kuhusu kuomba (7:7-11)

IV) Hitimisho: Ufupisho wa Mahubiri Yenyewe

A) Maneno ya ufupisho (7:12)

B) Ushauri kuhusu kutii (7:13-14)

C) Jinsi ya kutambua manabii na waamini wa uongo (7:15-23)

D) Onyo la mwisho kuhusu kutokutii, na ufupisho (7:24-27)

Yesu Akusanya Wasikilizaji Wake

Naye alipowaona makutano alipanda mlimani; na baada ya kuketi, wanafunzi Wake walimjia. Naye, akifunua kinywa Chake alianza kuwafundisha (Mathayo 5:1-2, TLR).

Inaonekana kwamba Yesu alipunguza ukubwa wa wasikilizaji Wake kwa makusudi, maana aliondoka kuwaacha “makundi”, akapanda mlimani. Tunaambiwa “wanafunzi Wake wakamwendea,” kama ishara kwamba ni wale tu waliokuwa na njaa ya kumsikiliza ndiyo walikuwa radhi kupambana na kilima mpaka kufikia mahali alipopumzikia. Bila shaka walikuwa wengi maana katika 7:28 wanaitwa “makutano”.

Yesu akaanza mahubiri Yake akizungumza na wanafunzi Wake, na tangu mwanzo tunapata kidokezo kuhusu mada Yake kuu. Anawaambia wamebarikiwa (au wana heri) kama watakuwa na tabia fulani, kwa sababu tabia hizo ni za wanaokwenda mbinguni. Hiyo ndiyo mada itakayotawala mahubiri haya – Watakatifu tu ndiyo watakaorithi ufalme wa Mungu. Kiini hicho kinatawala sehemu ya mahubiri hayo yenye kuzungumza kuhusu “Heri”, katika 5:3-12.

Yesu aliorodhesha vitu mbalimbali vinavyoonyesha watu waliobarikiwa (au wenye heri), na akaahidi baraka nyingi mbalimbali kwao. Wasomaji wa juu juu mara nyingi hufkiri kwamba kila Mkristo anapaswa kujitafuta katika “Heri” mojawapo – moja tu. Ila – wasomaji waangalifu wanatambua kwamba Yesu hakuwa anapanga orodha ya waamini wa aina tofauti watakaopokea baraka mbalimbali, bali alizungumza juu ya waamini wote wa kweli watakaopokea baraka moja tu ya jumla katika siku za baadaye: kuurithi ufalme wa mbinguni. Hakuna njia nyingine inayofaa ya kutafsiri maneno yake, yafuatayo:

Heri walio maskini wa roho; maana ufalme wa mbinguni ni wao. Heri wenye huzuni; maana hao watafarijika. Heri wenye upole; maana hao watairithi nchi. Heri wenye njaa na kiu ya haki; maana hao watashibirishwa. Heri wenye rehema; maana hao watapata rehema. Heri wenye moyo safi; maana hao watamwona Mungu. Heri wapatanishi; maana hao wataitwa wana wa Mungu. Heri wenye kuudhiwa kwa ajili ya haki; maana ufalme wa mbinguni ni wao. Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu. Furahini na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni; kwa maana ndivyo walivyowaudhi manabii waliokuwa kabla yenu (Mathayo 5:3-12).

Baraka Zenyewe, Na Tabia

Kwanza, hebu tutazame zile baraka zote zilizoahidiwa. Yesu alisema hivi: Hao wenye heri – (1) wataurithi ufalme wa mbinguni, (2) watafarijiwa, (3) watairithi nchi, (4) watashibishwa, (5) watapata rehema, (6) watamwona Mungu, (7) wataitwa wana wa Mungu, na (8) wataurithi ufalme wa mbinguni (marudio ya namba 1).

Je, Yesu anataka tudhani kwamba ni walio maskini wa roho na ambao wameteswa kwa ajili ya haki ndiyo tu watakaorithi ufalme wa Mungu? Je, ni wale walio safi moyoni tu ndiyo watakaomwona Mungu, na ni wale wapatanishi tu ndiyo watakaoitwa watoto wa Mungu, lakini hakuna atakayerithi ufalme wa Mungu? Tukifikiri hivyo tutakuwa tunakosea. Basi, ni salama kusema kwamba zile baraka nyingi zilizoahidiwa ni baraka mbalimbali zilizomo katika baraka moja kuu – kuurithi ufalme wa Mungu.

Sasa, hebu tufikiri zile tabia mbalimbali ambazo Yesu alitaja: (1) maskini wa roho, (2) wenye huzuni, (3) wapole, (4) wenye njaa na kiu ya haki, (5) wenye rehema, (6) wenye moyo safi, (7) wapatanishi, na (8) wenye kushutumiwa na kuudhiwa.

Je, Yesu anataka tufikiri kwmaba mtu anaweza kuwa na moyo safi lakini akakosa rehema? Je, mtu anaweza kushutumiwa na kuudhiwa kwa ajili ya haki na asiwe mwenye njaa na kiu ya haki? Hapo tena tunasema haiwezekani. Zile tabia au sifa nyingi za walio na heri ni tabia mbalimbali ambazo, kwa pamoja – kwa kiwango fulani – zinapatikana katika wote wenye heri.

Ni dhahiri basi kwamba Maandiko hayo yanaeleza tabia au sifa za wafuasi wa kweli wa Yesu. Kwa kuorodhesha sifa hizo kwa wanafunzi Wake, aliwahakikishia kwamba wao wana heri na wameokoka, na ndiyo wangefurahia mbingu siku moja. Kwa wakati huo wanaweza wasijisikie kuwa ni heri kwa sababu ya mateso yao, na dunia inayowatazama inaweza ikawaona si heri, lakini machoni pa Mungu wao ni heri.

Ni hivi: Watu wasiolingana na maelezo ya Yesu si heri, na hawataurithi ufalme wa mbinguni. Kila mchungaji anayefanya watu kuwa wanafunzi anawajibika kuhakikisha kwamba watu katika kundi lake wanajua hayo.

Tabia Za Walio Heri

Hizo sifa au tabia nane za walio heri zinatakiwa kutafsiriwa kiasi fulani. Kwa mfano: Nini cha kujisifia ukiwa “maskini wa roho”? Mimi nadhani kwamba Yesu alikuwa anaeleza sifa ya kwanza muhimu ambayo mtu lazima awe nayo kama ataokolewa – lazima atambue umaskini wake kiroho. Mtu lazima kwanza aone kwamba anamhitaji Mwokozi ndipo aokolewe, na walikuwepo watu aina hiyo katika wasikilizaji wa Yesu waliokuwa ametambua hali yao mbaya. Kweli, wao walikuwa na heri, ukiwalinganisha na Israeli wenye kiburi, waliokuwa hawaona dhambi zao!

Hiyo sifa ya kwanza inaondoa hali yoyote ya kujitegemea au kujitosheleza, na wazo lolote kwamba mtu anastahili wokovu. Mtu mwenye heri kweli kweli ni yule anayetambua kwamba hana chochote cha kumpa Mungu, na kwamba haki yake binafsi ni sawa na “matambara machafu” (Isaya 64:6, TLR).

Yesu hakutaka mtu yeyote afikiri kwamba kwa juhudi zake mwenyewe anaweza kujipatia sifa za kuwa heri. Hapana. Watu wana heri – yaani, kubarikiwa na Mungu – kama watakuwa na tabia au sifa za wenye heri. Hayo yote yanatoka katika neema ya Mungu. Watu wenye heri ambao Yesu alizungumza juu yao walikuwa heri, si kwa sababu ya kilichokuwa kinawangojea mbinguni, bali kwa sababu ya kazi Mungu aliyokuwa amefanya katika maisha yao duniani. Ninapoona sifa za mwenye heri maishani mwangu zinatakiwa kunikumbusha juu ya kile ambacho Mungu amefanya ndani yangu kwa neema Yake, si kunikumbusha kile nilichofanya mimi.

Wenye Huzuni

Kama sifa ya kwanza kutajwa imetajwa kwa sababu ndiyo sifa ya kwanza inayotakiwa kwa wanaokwenda mbinguni, pengine ya pili nayo imetajwa ya pili kwa sababu maalum. “Heri wenye huzuni” (Mathayo 5:4). Je, Yesu alikuwa anazungumza kuhusu toba kutoka moyoni pamoja na kujisikia vibaya? Yawezekana. Maana, Maandiko yako wazi kabisa kwamba huzuni ya kiMungu huzaa toba ambayo ni ya lazima kwa wokovu (ona 2Wakor. 7:10). Yule mtoza ushuru aliyekuwa na huzuni, ambaye Yesu alimtaja katika mfano, ni mtu wa aina hiyo mwenye heri. Yeye aliinamisha kichwa chake Hekaluni kwa unyenyekevu sana, akipiga-piga kifua chake na kuomba rehema za Mungu. Farisayo jirani yake ambaye, alipoomba, alimkumbusha Mungu – tena kwa kiburi – kwamba yeye alitoa fungu la kumi na kufunga mara mbili kwa juma. Yule mtoza ushuru aliondoka hapo akiwa amesamehewa dhambi zake. Katika kisa hicho, mtoza ushuru alikuwa heri; Farisayo hakuwa (ona Luka 18:9-14). Mimi nadhani kwamba, katika wasikilizaji wa Yesu walikuwepo wengine ambao kwa kusukumwa na Roho Mtakatifu, walikuwa wana huzuni. Faraja ya Roho Mtakatifu ingewafikia!

Kama Yesu hakuwa anazungumza juu ya ile huzuni ya mwanzo, ya mwenye dhambi anayetubu na kumjia Kristo, basi pengine alikuwa anazungumza juu ya huzuni ambayo waamini wote huipata wanapokabiliana kila siku na dunia inayomwasi Mungu, anayewapenda. Paulo alieleza hilo kuwa “huzuni kubwa na uchungu usiokoma moyoni” (Warumi 9:2).

Wenye Upole

Sifa ya tatu – upole – inatajwa pia katika Maandiko kwamba ni tunda mojawapo la Roho (tazama Wagalatia 5:22-23). Upole si tabia itokanayo na mtu binafsi. Wale ambao wamepokea neema ya Mungu na Roho anakaa ndani yao wamebarikiwa pia kufanyika wapole. Siku moja watairithi nchi, maana ni wenye haki tu watakaoishi kwenye dunia mpya ambayo Mungu anaiumba. Wanaojiita Wakristo ambao ni wakali na wenye fujo wajiangalie. Wao si heri.

Njaa Na Kiu Ya Haki

Sifa ya nne – kuwa na njaa na kiu ya haki – hueleza ile shauku ya ndani, itokayo kwa Mungu, ambayo kila mtu aliyezaliwa mara ya pili anayo. Yeye anahuzunishwa na maovu yote duniani, na sehemu inayobaki ndani yake. Anachukia dhambi (ona Zaburi 97:10; 119:128, 163), na anapenda haki.

Mara nyingi tunaposoma neno haki katika Maandiko, tunatafsiri upesi kwamba ni “kuhesabiwa kuwa wenye haki na Kristo”. Lakini, neno hilo halimaanishi hivyo wakati wote. Mara nyingi maana yake ni: “Hali ya kuishi kwa haki kulingana na viwango vya Mungu”. Bila shaka hiyo ndiyo maana aliyokusudia Yesu hapa, maana hakuna sababu kwa Mkristo kuwa na njaa na kitu alicho nacho tayari. Wale waliozaliwa na Roho hutamani kuishi kwa haki, na uhakikisho ni kwamba “watashibishwa” (Mathayo 5:6). Ni hakika kwamba Mungu kwa neema Yake atakamilisha kazi aliyoianza ndani yao (ona Wafilipi 1:6).

Maneno ya Yesu hapa ni kama utabiri wa wakati wa dunia mpya – dunia ambayo “haki yakaa ndani yake” (2Petro 3:13). Hiyo haitakuwa na dhambi. Kila mtu atampenda Mungu kwa moyo wote na kumpenda jirani yake kama nafsi yake. Wale ambao sasa wana njaa na kiu ya haki watashibishwa wakati huo. Hatimaye, sala yetu ya dhati kabisa kutoka moyoni itajibiwa kikamilifu: “Mapenzi Yako yatimizwe hapa duniani, kama huko mbinguni” (Mathayo 6:10).

Wenye Rehema

Sifa ya tano – rehama – nayo inapatikana na kila mtu aliyezaliwa mara ya pili kwa sababu ya Mungu mwenye rehema kuishi ndani yake. Wale wasiokuwa na rehema hawana heri ya Mungu, nao wanadhihirisha kwamba si washiriki wa neema Yake. Mtume Yakobo anakubali – “Hukumu haitakuwa na rehema kwa asiyekuwa na rehema” (Yakobo 2:13, TLR). Unaonaje – mtu akisimama mbele za Mungu na kuhukumiwa pasipo rehema, ataingia mbinguni au jehanamu?[1] Nadhani jibu ni dhahiri kabisa.

Yesu alisimulia kisa fulani, cha mtumishi aliyepata rehema kutoka kwa bwana wake, ambaye hakuweza kumwonyesha mtumwa mwenzake rehema hata kidogo. Bwana wake alipogundua kilichokuwa kimetokea, alimpeleka “kwa watesaji mpaka atakapolipa kila alichokuwa anadaiwa” (Mathayo 18:34). Deni lake la zamani alilokuwa amesamehewa likarudi pale pale. Kisha Yesu akawaonya wanafunzi wake hivi: “Baba yangu wa mbinguni atafanya hivyo hivyo kwenu, kama ninyi hamtawasamehe ndugu zenu kutoka moyoni” (Mathayo 18:35). Kwa hiyo, kukataa kumsamehe ndugu au dada katika Kristo anayeomba msamaha husababisha dhambi zetu za zamani kurudishwa. Matokeo ni sisi kukabidhiwa kwa watesaji mpaka tulipe kitu ambacho hatuwezi kulipa. Na hapo si mbinguni. Narudia tena – wasio na rehema hawatapokea rehema kutoka kwa Mungu. Wao si heri.

Wenye Moyo Safi

Tabia au sifa ya sita ya wanaokwenda mbinguni ni usafi wa moyo. Tofauti na wengi wanaokiri Ukristo, wafuasi a kweli wa Kristo si watakatifu kwa nje tu. Mioyo yao imefanywa kuwa safi kwa neema ya Mungu. Wanampenda Mungu kweli kutoka ndani ya mioyo yao, na hali hiyo inaathiri tafakari zao na makusudi yao ya moyo. Yesu aliahidi kwamba watamwona Mungu.

Naomba niulize tena: Je, tuamini kwamba kuna waamini wa kweli Wakristo ambao si safi moyoni, na kwamba hawatamwona Mungu? Je, Mungu atawaambia, “Mnaweza kuingia mbinguni, lakini hamtaniona kamwe?” Hapana. Bila shaka, kila mwamini wa kweli aendaye mbinguni ana moyo safi.

Wapatanishi

Wapatanishi ndiyo wanaofuata. Wataitwa wana wa Mungu. Hapo tena ni kwamba Yesu anazungumza juu ya kila mfuasi wa kweli wa Kristo, maana kila amwaminiye Kristo ni mtoto wa Mungu (ona Wagalatia 3:26).

Wale waliozaliwa na Roho ni wapatanishi kwa namna tatu:

Kwanza – Wamefanya mapatano na Mungu, ambaye hapo kwanza alikuwa adui yao (ona Warumi 5:10).

Pili – Wanaishi kwa amani na watu wengine, kwa kiasi kinachowezekana. Si watu wenye tabia za vurugu na magomvi. Paulo aliandika kwamba wale wenye kutenda vurugu, fujo, wenye wivu, wenye ghadhabu, wenye mafarakano, wenye magomvi na kuleta mafarakano hawataurithi ufalme wa Mungu (ona Wagalatia 5:19-21). Waaini wa kweli watakwenda maili ya pili ili kuepuka ugomvi na kuhifadhi amani katika mahusiano yao. Hawadai kuwa na amani na Mungu na huku hawawapendi ndugu zao (ona Mathayo 5:23-24; 1Yohana 4:20).

Tatu – Kwa kuwaambia wengine Habari Njema (Injili), wafuasi wa kweli wa Kristo huwasaidia wengine nao kuwa na amani na Mungu, na wanadamu wenzao. Pengine Yakobo alikuwa anaunganisha hoja yake na Mahubiri ya Mlimani alipoandika hivi: “Na mbegu ile ambayo mazao yake ni haki, hupandwa katika amani na wale wafanyao amani” (Yakobo 3:8, TLR).

Wenye Kushutumiwa Na Kuudhiwa

Mwisho – Yesu alisema wale wanaoshutumiwa na kuteswa kwa ajili ya haki wana heri. Ni dhahiri kwamba alikuwa anazungumza na watu wenye kuishi maisha ya haki, si wale ambao wanafikiri tu kwamba haki ya Kristo imehesabiwa kwao. Watu wenye kutii amri za Kristo ndiyo wanaoshutumiwa au kuudhiwa na wasioamini. Hao wataurithi ufalme wa Mungu.

Sasa – Yesu alikuwa anazungumza juu ya kuudhiwa au shutuma za aina gani? Mateso kimwili? Kuteswa mpaka kufa? Hapana. Alichotaja hasa ni kutukanwa na kunenewa mabaya kwa ajili Yake. Hili tena linaonyesha kwamba wakati mtu anapokuwa Mkristo wa kweli, ni kitu kinachoonekana kwa wasioamini. Vinginevyo, wasioamini wasingejaribu kusema maovu kinyume chake. Je, ni wangapi wanaoitwa Wakristo wasioweza hata kutofautishwa na wasioamini kiasi cha kwamba wasioamini hawana la kusema vibaya juu yao? Ukweli ni kwamba hao si Wakristo wa kweli. Yesu alisema hivi: “Ole wenu ninyi watu wote watakapowasifu, kwa kuwa baba zao waliwatenda manabii wa uongo mambo kama hayo” (Luka 6:26). Watu wote wanapowasema vizuri, ni ishara kwamba wewe ni mwamini bandia. Dunia inawachukia Wakristo wa kweli (ona pia Yohana 15:18-21; Wagalatia 4:29; 2Timo. 3:12; 1Yohana 3:13-14).

Chumvi Na Nuru

Baada ya Yesu kuwahakikishia wanafunzi Wake watiifu kwamba walikuwa miongoni mwa waliobadilishwa na watu wenye heri, watakaourithi ufalme wa mbinguni, anatoa onyo. Yesu aliwapenda kweli kweli wanafunzi Wake halisi kiasi cha kuwaonya kwamba wangejiondoa katika fungu la wenye heri. Hii ni tofauti na wahubiri wengi wa siku hizi ambao wanawatia moyo tu mbuzi wa kiroho kwamba hawawezi kupoteza wokovu wanaodhani wanao.

Ninyi ni chumvi ya dunia. Lakini, chumvi ikiwa imeharibika itatiwa nini hata ikolee? Haifai tena kabisa ila kutupwa nje na kukanyagwa na watu. Ninyi ni nuru yaulimwengu. Mji hauwezi kusitirika ukiwa juu ya mlima. Wala watu hawawashi taa na kuiweka chini ya pichi, bali juu ya kiango, nayo yawaangaza wote waliomo nyumbani. Vivyo hivyo, nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni (Mathayo 5:13-16).

Ona kwamba Yesu hakuwashauri wanafunzi Wake kufanyika chumvi au kufanyika nuru. Alisema (kimfano) kwamba wao ni chumvi tayari, na akawashauri wadumu kuwa chumvi. Alisema (kimfano) kwamba wao ni nuru tayari, na akawashauri wasiache nuru yao isifichike bali iendelee kung’aa. Hiyo ni tofauti sana na yale mahubiri wanayoambiwa wanaojiita Wakristo, kwamba kuna haja kwao kufanyika chumvi na nuru. Kama watu si chumvi na nuru tayari, si wanafunzi wa Kristo hao. Hawako miongoni mwa walio na heri. Hawaendi mbinguni hao.

Katika siku za Yesu, chumvi ilitumiwa kimsingi kama kihifadhi nyama. Sisi kama wafuasi watiifu wa Kristo ndiyo tunaohifadhi dunia hii yenye dhambi isioze kabisa na kupotoka. Lakini, tukiwa kama dunia kwa tabia, kweli “hatufai kwa chochote” (ms. 13). Yesu aliwaonya walio heri kudumu kuwa chumvi, yaani, wahifadhi tabia zao za kipekee. Ni lazima wawe tofauti na dunia inayowazunguka, wasije wakapoteza ladha yao, wakastahili “kutupwa nje na kukanyagwa na watu.” Hili ni onyo mojawapo kati ya mengi ya wazi kabisa kuhusu kurudi nyuma, yapatikanayo katika Agano Jipya, lenye kuelekezwa kwa waamini wa kweli. Kama chumvi ni chumvi kweli, itakuwa na ladha ya chumvi. Vivyo hivyo, wafuasi wa Yesu hutenda kama wafuasi wa Yesu. Vinginevyo, wao si wafuasi wa Yesu hata kama waliwahi kuwa hapo zamani.

Pia, wafuasi wa kweli wa Kristo ni nuru ya dunia. Nuru hung’aa kila wakati. Kama haing’ai, hiyo si nuru. Kwa mfano huu, nuru inafananishwa na matendo yetu mema (ona Mathayo 5:16). Yesu hakuwa anawashauri wale wasio na matendo mema wafanye bidii wapate. Aliwashauri wale wenye matendo mema wasifiche wema wao kwa watu. Kwa kufanya hivyo, wangemtukuza Baba yao wa mbinguni kwa sababu kazi Yake ndani yao ndiyo asili ya wema wao. Hapo tunaona mlingano mzuri sana kati ya kazi ya Mungu ya neema na ushirikiano wetu sisi – pande zote mbili hizo zinahitajiana ili mtu awe mtakatifu.

Uhusiano Wa Torati Na Wafuasi Wa Kristo

Tumefikia mahali muhimu katika mafundisho haya. Ni sehemu ya msingi na yenye maana sana – ni kama utangulizi wa mengi ambayo Kristo atasema katika sehemu inayosalia ya mahubiri Yake.

Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii. La! Sikuja kutangua, bali kutimiliza. Kwa maana, amin nawaambia, mpaka mbingu na nchi zitakapoondoka, yodi moja wala nukta moja ya torati haitaondoka, hata yote yatimie. Basi mtu yeyote atakayevunja amri moja katika hizi zilizo ndogo na kuwafundisha watu hivyo, ataitwa mdogo kabisa katika ufalme wa mbinguni. Bali mtu atakayezitenda na kuzifundisha, huyo ataitwa mkubwa katika ufalme wa mbinguni. Maana nawaambia ya kwamba, haki yenu isipozidi hiyo haki ya waandishi na Mafarisayo, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni (Mathayo 5:17-20).

Ikiwa Yesu aliwaonya wasikilizaji Wake wasifikiri kwamba alikuwa anaitangua Torati au manabii, tunaweza kuamua kwamba bila shaka walikuwepo wachache katika kundi lililomsikiliza waliodhani hivyo. Kilichosababisha wafikiri hivyo hatukijui. Pengine ni kwa sababu Yesu aliwakemea vikali sana waandishi na Mafarisayo walioshika sana sheria.

Vyovyote vile ni kwamba, Yesu alitaka wanafunzi Wake watambue wazi wazi kosa la kufikiri hivyo. Yeye ndiye alivuvia Agano la Kale lote. Basi, asingeweza kutangua kila kitu alichosema kupitia kwa Musa na Manabii. Kinyume chake – angetimiliza Torati na Manabii, kama alivyosema.

Angetimilizaje Torati na Manabii? Kuna wanaofikiri kwamba Yesu alimaanisha kutimizwa kwa unabii uliomhusu Masiya. Ingawa kweli Yesu alitimiza (na bado atatimiza) kila unabii uliomhusu Masiya, hiyo haikuwa maana yake tu. Ni wazi kwamba mantiki ya mistari hiyo inaonyesha kwamba alikuwa anazungumza kuhusu yote yaliyoandikwa katika Torati na Manabii, mpaka “yodi ndogo kabisa” (ms. 18) ya Torati, na mpaka amri “iliyo ndogo kabisa” (ms. 19).

Kuna wengine wanaodhani kwmaba Yesu alimaanisha atatimiza Torati kwa kutimiza matakwa yake kwa niaba yetu, kwa maisha Yake ya kumtii Mungu na kifo Chake cha kujitoa (ona Warumi 8:4). Lakini ukitazama mantiki ya mistari husika, utaona kwamba hiyo haikuwa maana yake. Katika mistari inayofuata, yesu hasemi chochote kuhusu maisha Yake au kufa Kwake kwamba ni kitu kitakachotimiza Torati. Badala yake utaona kwamba katika mstari uliofuata alisema kwamba Torati itadumu mpaka “mbingu na nchi zitakapopita” na “kila kitu kitimizwe”. Hiyo inasema juu ya kipindi kirefu baada ya kifo Chake msalabani. Kisha akatangaza kwamba hali za moyo za watu kuhusu Torati zingeamua hata nafasi zao mbinguni (ms. 19), na kwamba watu lazima waitii Torati vizuri zaidi kuliko waandishi na Mafarisayo, la sivyo hawataingia mbinguni (ms. 20).

Basi, ni wazi kwamba, zaidi ya kutimiza tu unabii kuhusu Masiya na mifano yake ya Torati, pamoja na kutimiza matakwa ya Torati kwa niaba yetu, Yesu pia alikuwa anafikiri juu ya wasikilizaji Wake kuzishika amri za Torati na kufanya yaliyosemwa na Manabii. Kwa sehemu moja, Yesu angeitimiza Torati kwa kufunua kusudi la kweli la Mungu ndani yake, kwa kulifafanua na kuiunga mkono, na kukamilisha kilichokuwa kimepungua katika ufahamu wa wasikilizaje Wake.[2] Neno la Kiyunani linalotafsiriwa kutimiza katika mstari wa 17 ndilo linalotafsiriwa kukamilisha, kumaliza, kujaza na kutekeleza kikamilifu katika Agano Jipya. Hayo ndiyo Yesu aliyokuwa anataka kufanya, kama itakavyoonekana hapo baadaye.

Hapana. Yesu hakuja kutangua Torati wala Manabii. Alikuja kutimiliza – yaani – “kujazia.” Ninapofundisha fungu hili la Mahubiri ya Mlimani, mara nyingi ninawaonyesha watu bilauri ya maji ambayo iko nusu, ili kuwa mfano wa ufunuo wa Mungu aliotoa katika Torati na Manabii. Yesu hakuja kutangua Torati na Manabii (na ninaposema hivyo, ninajifanya kama anayetaka kumwaga yale maji). Kinyume chake, angetimiliza Torati na Manabii (na hapo, ninachukua chupa ya maji na kuijaza ile bilauri mpaka juu). Hilo huwasaidia watu kuelewa maana ya Yesu.

Umuhimu Wa Kushika Torati

Kuhusu kushika zile amri zipatikanazo katika Torati na Manabii, Yesu alisema mambo waziwazi kabisa. Aliwatazamia wanafunzi Wake kuziti. Zilikuwa za maana kama nini! Ukweli ni kwamba: Jinsi walivyothamini amri zile ingeamua nafasi yao mbinguni. “Basi, mtu yeyote atakayevunja amri moja katika hizi zilizo ndogo na kuwafundisha watu hivyo, ataitwa mdogo kabisa katika ufalme wa mbinguni. Bali mtu atakayezitenda na kuzifundisha, huyo ataitwa mkubwa katika ufalme wa mbinguni” (5:19).

Ndipo tunafikia mstari wa 20 sasa – “Maana nawaambia ya kwamba haki yenu isipozidi hiyo haki ya waandishi na Mafarisayo, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni.”

Ona kwamba hilo si wazo jipya, bali wazo la kumalizia mistari ile mingine yote iliyotangulia. Imeunganishwa na neno maana. Je, ni muhimu kiasi gani kuzishika amri? Ni muhimu sana. Mtu anapaswa azishike vizuri zaidi kuliko waandishi na Mafarisayo ili aweze kuingia katika ufalme wa mbinguni. Hapo tena tunamwona Yesu akibakia kwenye mada Yake kuu – Ni watakatifu tu watakaorithi ufalme wa Mungu.

Ili asipingane na Kristo, yule mtumishi mwenye kufanya watu kuwa wanafunzi hawezi kumhakikishia mtu yeyote kwamba wokovu wake uko salama kama haki yake haizidi ya waandishi na Mafarisayo.

Je, Yesu Alikuwa Anazungumzia Haki Ya Namna Gani?

Je, Yesu alipotamka kwamba haki yetu lazima izidi ile ya waandishi na Mafarisayo, hakumaanisha ule msimamo kisheria wa haki ambao tungehesabiwa baada ya wokovu kama zawadi? Hapana, na ni kwa sababu nzuri tu. Kwanza: Mantiki yenyewe hailingani na tafsiri hiyo. Kabla na baada ya kusema hivyo (na katika mahubiri yote), Yesu alikuwa anazungumza juu ya kushika amri – yaani, kuishi maisha ya haki. Tafsiri ya karibu kabisa ya maneno Yake ni kwamba lazima tuishi kwa haki zaidi ya waandishi na Mafarisayo. Na ni upuuzi kufikiri kwamba Yesu aliwabana waandishi na Mafarisayo washike kiwango ambacho hakutaka wanafunzi Wake washike. Itakuwa ni upuuzi kabisa kufikiri kwamba Yesu angewahukukumu waandhsi na Mafarisayo kwa ajili ya kufanya dhambi ambazo asingewahukumia wanafunzi Wake kwa kuwa waliomba “sala ya wokovu” tu.[3]

Tatizo letu ni kwamba hatutaki kukubali maana halisi ya mstari huo, kwa sababu tunaona ni kukazia ushikaji wa sheria. Lakini, tatizo letu hasa ni kwamba hatuelewi umoja ulioko kati ya haki inayohesabiwa na haki halisi ya vitendo. Mtume Yohana alielewa, na akaandika hivi: “Watoto wadogo! Mtu yeyote asiwadangaye. Yeye atendaye haki ni mwenye haki” (1Yohana 3:7, TLR). Tena, hatuelewi umoja ulipo kati ya kuzaliwa upya na haki halisi ya vitendo. Yohana alielewa, na anasema hivi: “Kila atendaye haki amezaliwa na Yeye” (1Yohana 2:29, TLR).

Yesu angeweza kuongezea maneno, katika yale aliyosema katika 5:20. Angeweza kusema hivi: “Mkitubu, na kuzaliwa mara ya pili kweli, na kupokea zawadi yangu ya haki kw anjia ya imani hai, haki yenu ya vitendo itazidi ile ya waandishi na Mafarisayo mtakaposhirikiana na nguvu za Roho Wangu, akaaye ndani yenu.”

Jinsi Ya Kuwa Mtakatifu Kuliko Waandishi Na Mafarisayo

Bila shaka swali linalojitokeza hapo kama itikio la maneno ya Yesu katika 5:20 ni hili: Hao waandishi na Mafarisayo walikuwa na haki kiasi gani? Jibu ni hili: Haikuwa Nyingi.

Wakati fulani Yesu aliwaita “makaburi yaliyopakwa chokaa ambayo kwa nje yanapendeza, lakini ndani yamejaa mifupa ya wafu, na uchafu wote” (Mathayo 23:27, TLR). Yaani, walionekana kuwa wenye haki kwa nje, lakini ndani walikuwa waovu. Walijitahidi sana kushika andiko la Torati, lakini walipuuzia maana yake, na mara nyingi walijihesabia haki kwa kupindisha au hata kubadili amri za Mungu.

Hili tatizo la ndani la waandishi na Mafarisayo ndilo Yesu alikazia zaidi katika sehemu inayosalia ya Mahubiri Yake pale Mlimani. Tunakuta kwamba alitaja baadhi ya amri zinazojulikana sana za Mungu, na baada ya kutaja kila moja, alionyesha tofauti kati ya kushika andiko na maana ya kila sheria. Kwa kufanya hivyo, alifunua tena na tena mafundisho ya uongo na unafiki wa waandishi na Mafarisayo, na kudhihirisha matazamio halisi ambayo Yeye alikuwa nayo kwa wanafunzi Wake.

Yesu alianza kila mfano kwa kusema hivi: “Mmesikia”. Alikuwa anazungumza na watu ambao hawakuwahi kusoma magombo ya Agano la Kale bali walisikia yakisomwa katika masinagogi na waandishi na Mafarisayo. Ni sawa kusema kwamba wasikilizaji Wake walikuwa wameketi chini ya mafundisho ya uongo maisha yao yote, wakisikiliza maelezo na mafafanuzi potofu ya waandishi na Mafarisayo kuhusu Neno la Mungu, na kuona jinsi walivyoishi maisha yasiyokuwa matakatifu.

Mafarisayo kuhusu Neno la Mungu, na kuona jinsi walivyoishi maisha yasiyokuwa matakatifu.

Mafarisayo kuhusu Neno la Mungu, na kuyaona maisha waliyoishi, ambayo hayakuwa matakatifu.

Pendaneni. Si Kama Waandishi Na Mafarisayo

Kwa kutumia amri ya sita kama kianzio, Yesu alianza kufundisha wanafunzi Wake matazamio ya Mungu kwao, na hapo hapo akifunua unafiki wa waandishi na Mafarisayo.

Mmesikia watu wa kale walivyoambiwa, ‘Usiue’, na mtu akiua, itampasa hukumu. Bali mimi nawaambieni, Kila amwoneaye ndugu yake hasira itampasa hukumu; na mtu akimfyolea ndugu yake itampasa baraza; na mtu akimwapiza, itampasa jehanamu ya moto (Mathayo 5:21-22).

Kwanza: Ona kwamba Yesu alikuwa anaonya kuhusu kitu kinachoweza kumsababisha mtu kwenda jehanamu. Hiyo ndiyo iliyokuwa mada Yake kuu – Watakatifu tu ndiyo watakaorithi ufalme wa Mungu.

Waandishi na Mafarisayo walihubiri na kukataza kuua, wakitumia amri ya sita, japo inaonekana wao walisema kuua kungemfikisha mtu mahakamani.

Yesu alitaka wanafunzi Wake wajue kitu ambacho ni kama waandishi na Mafarisayo hawakukitambua – yalikuwepo makosa mengine “madogo” ambayo yangemfikisha mtu mahakamani – mahakama ya Mungu. Kwa sababu ni muhimu sana sisi kwa sisi tupendane (ni amri ya pili iliyo kuu), tunapomkasirikia ndugu tunapaswa kujihesabu kwamba tayari tumepatikana na hatia katika mahakama ya Mungu. Kama tutaitamka hasira yetu kwa kusema maneno mabaya, kosa letu ni kubwa zaidi, na tunatakiwa kujihesabu kuwa na hatia katika mahakama ya juu sana ya Mungu. Na kama tutazidi hapo – na kumwaga chuki yetu dhidi ya ndugu kwa maneno mengine mabaya, tuna hatia mbele za Mungu ya kutosha kutupwa jehanamu![4] Hiyo si mchezo!

Uhusiano wetu na Mungu unapimwa na mahusiano yetu na ndugu zetu. Tukimchukia ndugu inadhihirisha kwamba hatuna uzima wa milele. Yohana aliandika hivi:

Kila amchukiaye ndugu yake ni mwuaji, nanyi mwajua kwamba hakuna mwuaji aliye na uzima wa milele ndani yake (1Yohana 3:15, TLR).

Mtu akisema, ‘Nampenda Mungu’ naye amchukia ndugu yake, ni mwongo huyo. Kwa maana, mtu asiyempenda ndugu yake ambaye amemwona, hawezi kumpenda Mungu ambaye hajamwona (1Yohana 4:20, TLR).

Ni muhimu sana tupendane, na kama Yesu alivyoamuru, tujitahidi kutafuta upatanisho wakati tunapokwazana (ona Mathayo 18:15-17). Yesu aliendelea hivi:

Basi, kama unatoa sadaka yako madhabahuni, na hapo ukumbuke kwamba ndugu yako ana jambo nawe, iache sadaka yako hapo mbele ya madhabahu uende zako. Patana kwanza na ndugu yako, kisha rudi na uitoe sadaka yako (Mathayo 5:23-24, TLR).

Maana ya hayo yote ni kwamba, kama mahusiano yetu na ndugu si mazuri, hata mahusiano yetu na Mungu si mazuri. Mafarisayo walikuwa na hatia ya kutilia mkazo vitu vilivyokuwa na umuhimu mdogo na kupuuzia vitu vilivyokuwa na umuhimu mkubwa, “wakichuja mbu na kumeza ngamia” kama Yesu alivyosema juu yao (Mathayo 23:23-24). Wao walikazia umuhimu wa kutoa zaka na sadaka, lakini walipuuza yaliyokuwa ya muhimu zaidi sana, yaani ile amri ya pili iliyo kuu ya kupendana. Ni unafiki ulioje, kuleta sadaka ambayo inadhanishia kuonyesha upendo wa mtu kwa Mungu, huku akihalifu ile amri kuu ya pili! Yesu alikuwa anaonya dhidi ya hayo. Kuhusu msimamo mkali wa mahakama ya Mungu, Yesu anaendelea kusema hivi:

Patana na mshitaki wako upesi wakati uwapo pamoja naye njiani; yule mshitaki asije akakupeleka kwa kadhi, na kadhi akakupeleka kwa askari, ukatupwa gerezani. Amin nakuambia, hutoki humo kamwe hata uishe kulipa senti ya mwisho (Mathayo 5:25-26).

Ni vizuri kuepuka kuingia mahakama ya Mungu kabisa kwa kuishi kwa amani na ndugu zetu kiasi inachowezekana. Kama ndugu au dada atatukasirikia, nasi kwa kujivuna tukatae kutafuta upatanisho “njiani kuelekea mahakamani”, yaani, katika safari yetu maishani kwenda kusimama mbele za Mungu, tutajutia jambo hilo. Alichosema Yesu hapa ni sawa na maonyo Yake kuhusu sisi kumwiga yule mtumwa ambaye hakumsamehe mwenzake katika Mathayo 18:23-35. Yule mtumwa aliyekuwa amesamehewa lakini yeye akakataa kusamehe alirudishiwa deni lake, akakabidhiwa kwa watesaji “mpaka atakapolipa yote aliyodaiwa” (Mathayo 18:34). Hapa, Yesu anaonya dhidi ya matokeo mabaya ya milele ya sisi kutowapenda ndugu zetu kama Mungu anavyotazamia.

Usafi Katika Maadili ya Kimwili. Msiwe Kama Waandhsi Na Mafarisayo

Amri ya saba ikatumiwa na Yesu kama mfano wa pili kuonyesha jinsi waandishi na Mafarisayo walivyoshika andiko la Torati huku wakipuuza maana yake. Yesu aliwatazamia wanafunzi Wake kuwa safi zaidi katika maadili ya kimwili kuliko waandishi na Mafarisayo.

Mmesikia kwamba imenenwa, Usizini. Lakini mimi nawaambia, Kila mtu atazamaye mwanamke kwa kumtamani amekwisha kuzini naye moyoni mwake. Jicho lako la kuume likikukosesha, ling’oe ulitupe mbali nawe. Kwa maana yakufaa kiungo chako kimoja kipotee wala mwili wako mzima usitupwe katika jehanamu. Na mkono wako wa kuume ukikukosesha, ukate uutupe mbali nawe. Kwa maana yakufaa kiungo chako kimoja kipotee wala mwili wako mzima usitupwe katika jehanamu (Mathayo 5:27-30).

Ona tena kwamba Yesu alikuwa bado kwenye mada Yake kuu – Watakatifu tu ndiyo watakaorithi ufalme wa Mungu. Alionya tena kuhusu jehanamu na kile kinachotakiwa kufanywa na mtu ili asiende huko.

Waandishi na Mafarisayo wasingeweza kuipuuza amri ya saba. Basi, waliitii kwa nje na kusalia waaminifu kwa wake zao. Lakini walikuwa wanafanya mapenzi na wanawake katika mawazo yao. Walipokuwa sokoni au barabarani, waliwavua nguo kimawazo wanawake waliokuwa wanawaona. Moyoni walikuwa wazinzi, na kwa njia hiyo walikuwa wanavunja maana ya amri ya saba. Je, ni wangapi siku hizi kanisani ambao hawana tofauti na hao?

Mungu alikusudia watu wawe safi kabisa kimaadili katika mahusiano ya kimwili. Ni wazi kwamba kama ni kosa kuwa na mahusiano kimapenzi na mke wa jirani yako, ni makosa pia kufikiri au kuwaza hayo hayo. Si kwamba Yesu aliongezea sheria kali zaidi kwenye ile iliyokuwepo katika Torati ya Musa. Amri ya kumi ilikuwa na maneno haya ya kukataza tamaa mbaya: “Usimtamani mke wa jirani yako” (Kutoka 20:17).

Je, kati ya wasikilizaji wa Yesu kuna aliyejisikia hatia? Bila shaka walikuwepo. Je, wafanye nini? Wangetubu mara moja, kama Yesu alivyoagiza. Wale wenye tamaa mbaya walitakiwa kuiacha – kwa gharama yoyote – maana, watu aina hiyo wanakwenda jehanamu.

Hakuna mtu mwenye akili timamu anayedhani kwamba Yesu alimaanisha kwamba watu wenye tamaa mbaya wang’oe jicho kweli au kukata mkono. Mtu mwenye tamaa anayeng’oa jicho anakuwa mwenye tamaa chongo tu! Yesu alikuwa anakazia tu umuhimu wa kutii maana ya amri ya saba – kwamba, umilele wa mtu ulitegemeana na jinsi anavyoitii.

Basi – akifuata mfano wa Kristo, mtumishi anayefanya watu kuwa wanafunzi atawashauri wanafunzi wake “kukatilia mbali” chochote kinachowafanya kujikwaa. Kama ni televisheni ya kulipia, iache kulipiwa. Kama ni ya kawaida, iondolewe. Kama ni gazeti linalolipiwa, liache kulipiwa. Kama ni mtandao, achana nao. Kama ni dirisha lisilofungwa, lifungwe. Hakuna hata kimoja katika vitu hivyo kinachostahili kumfanya mtu aende jehanamu milele, na kwa sababu mtumishi anayewafanya watu kuwa wanafunzi anawapenda kondoo wake, atawaambia ukweli na kuwaonya, sawa na jinsi Yesu alivyofanya.

Njia Nyingine Ya Kuzini

Mfano unaofuata wa Yesu unafanana na huo tuliomaliza. Pengine ndiyo sababu unatajwa sasa. Unatakiwa kuonekana kama ufafanuzi wa zaidi badala ya kuonekana kwamba ni mada mpya. Mada ni hii: “Kitu kingine Mafarisayo wafanyacho kinacholingana na uzinzi”.

Imenenwa pia, Mtu akimwacha mkewe na ampe hati ya talaka. Lakini mimi nawaambia, kila mtu amwachaye mkewe isipokuwa kwa habari ya uasherati, amfanya kuwa mzinzi; na mtu akimwoa yule aliyeachwa, azini (Mathayo 31-32).

Ufuatao ni mfano tu, jinsi waandishi na Mafarisayo walivyopindisha sheria ya Mungu ili kutosheleza maisha yao ya dhambi.

Hebu tujiundie Farisayo wa kufikirika, aliyeishi siku za Yesu. Kuna mwanamke mzuri tu anayemtamani sana, anayeishi ng’ambo ya barabara. Wanataniana kila wanapo-onana. Inaonekana huyo mwanamke amevutiwa naye, na tamaa ya Farisayo inazidi kuongezeka. Angependa kumwona akiwa hana nguo, naye humfikiria sana kila wakati, kimapenzi. Laiti ingewezekana akampata!

Lakini ana tatizo. Yeye ana ndoa, na dini yake inakataza uzinzi. Hataki kuivunja amri ya saba (ingawa amekwisha ivunja kila wakati anapotamani). Sasa, afanye nini?

Lipo jibu! Akiachana na mwenzake, anaweza kumwoa huyo mwanamke anayemtamani! Lakini, talaka inaruhusiwa? Farisayo mwenzake anamwambia, Ndiyo! Tena hata andiko lipo! Kumbukumbu 24:1 inasema kitu juu ya kumpa mke wako cheti cha talaka unapomwacha. Basi, talaka bila shaka ni halali kwa mazingira fulani! Sasa – ni mazingira gani hayo? Anasoma kwa makini maneno ya Mungu, kwamba:

Mtu akiisha kutwaa mke kwa kumwoa, asipopata kibali machoni mwake kwa kuwa ameona neno ovu kwake, na amwandikie hati ya kumwacha, akamtilie mkononi mwake na kumtoa katika nyumba yake (Kumbu. 24:1).

Loo! Kumbe inawezekana kumwacha mke wake akipata hitilafu kwake! Na amekwisha ipata! Havutii kama yule mwanamke anayekaa ng’ambo ya barabara! (Na huu si mfano usiowezekana. Kulingana na Rabbi Hillel, ambaye alikuwa na mafundisho kuhusu talaka yaliyopendwa sana katika siku za Yesu, mtu angeweza kumwacha mke wake kihalali kabisa kama angempata mwingine aliyekuwa wa kupendeza zaidi, maana tendo hilo lilimfanye mke wake “kutokuwa na kibali” machoni pake. Vile vile Rabbi Hillel alifundisha kwamba mwanamume angeweza kumwacha mke wake kama akizidisha chumvi katika chakula, au kama angezungumza na mwanamume mwingine, au kama asingezaa mtoto wa kiume).

Basi, Farisayo wetu mwenye tamaa anaachana na mke wake kihalali kabisa kwa kumpa hati ya talaka, na haraka sana anamwoa yule mwanamke anayemtamani. Tena, hayo yote yanafanyika bila yeye kujisikia hatia hata kidogo kwa sababu Torati ya Mungu imefuatwa!

Mtazamo Tofauti

Mungu anaona mambo kwa njia tofauti. Yeye hakutaja kwamba “kutokuwa na kibali” ni kitu gani katika Kumbukumbu 24:1. Wala haisemi kwamba sababu halali ya kuachana na mke ni nini. Maandiko hayo hayasemi chochote kuhusu wakati ambapo kuachana kunaruhusiwa au hakuruhusiwi. Hapo tunaambiwa tu juu ya katazo kuhusu mwanamke aliyeachwa mara mbili au mara moja, au hata aliyefiwa, kuolewa tena na mume wake wa kwanza. Kusema kwamba kuna hali ya “kutokuwa na kibali” mbele za Mungu, yenye kuhalalisha kuachana katika mistari hii ni kulazimisha maana nyingine kabisa.

Tena – mbele za Mungu, huyo mwanamume wa kufikirika ambaye nimesimulia habari zake hana tofauti na mzinzi. Amekwisha vunja ile amri ya saba. Tena ana hatia kuliko hata mzinzi wa kawaida, maana yeye ana kosa la uzinzi “mara mbili”. Utasema, kivipi? Kwanza: Amefanya uzinzi mwenyewe. Baadaye Yesu alisema hivi: “Kila mtu amwachaye mkewe, isipokuwa kwa sababu ya uasherati, akaoa mwanamke mwingine, anazini” (Mathayo 19:9, TLR).

Pili: Kwa sababu, huyo mkewe ambaye ameachika lazima atafute mwanamume mwingine ili aendelee kuishi. Machoni pa Mungu, huyo Farisayo amekwisha fanya kitendo kinacholingana na kumlazimisha mke wake kushirikiana kimwili na mwanamume mwingine. Basi, anakuwa na hatia kwa “uzinzi” wa huyo mwanamke.[5] Yesu alisema hivi: “Yeyote amwachaye mkewe, isipokuwa kwa habari ya uasherati, amfanya azini” (Mathayo 5:32, TLR. Maneno mepesi kukazia).

Yawezekana Yesu alikuwa anamhukumu hata huyo Farisayo wetu mwenye tamaa kwa kosa la “kuzini mara tatu” ikiwa maneno Yake yaliyofuata, kwamba “yeyote amwoaye mwanamke aliyeachwa azini” (Mathayo 5:32, TLR) yanamaanisha kwamba Mungu anamhesabia Farisayo huyo hatia kwa sababu ya “zinaa” ya mume mpya wa mke wake wa zamani. [6]

Hili lilikuwa jambo moto katika siku za Yesu, maana tunasoma mahali pengine Mafarisayo walipomwuliza hivi: “Je, ni halali kwa mtu kumwacha mkewe kwa sababu yoyote?” (Mathayo 19:3). Swali lao linadhihirisha mioyo yao. Bila shaka kuna waliotaka kuamini kwamba kuachana au talaka ni halali kwa sababu yoyote.

Ila, naomba niseme kwamba ni aibu sana kwa Wakristo kuchukua mistari hii kuhusu talaka, na kuitafsiri vibaya, kisha kuweka mizigo mizito juu ya watoto wa Mungu. Yesu hakuwa anazungumza juu ya Mkristo ambaye alikuwa na talaka wakati hajaokoka, na ambaye akiisha kumpata mwenzake mzuri tu anayempenda Kristo pia, wanaamua kuoana. Hiyo si uasherati. Kama Yesu alimaanisha hivyo, itabidi tubadilishe Injili maana haitoi nafasi ya msamaha kwa dhambi zote za wenye dhambi. Itabidi tangu sasa tuhubiri hivi: “Yesu alikufa kwa ajili yako, nawe ukitubu na kumwamini, utasamehewa dhambi zako zote. Lakini, kama umeachana na mwenzake, hakikisha kwamba huingii katika ndoa nyingine maana hapo utaishi katika uasherati, na Biblia inasema waasherati watakwenda jehanamu. Pia, kama umeachika na kuingia tena katika ndoa, unahitaji kufanya dhambi nyingine moja kabla ya kumjia Kristo – achana na mwenzako. La sivyo, utaendelea katika uasherati, na watu aina hiyo hawajaokoka.”[7] Je, hiyo ni injili?[8]

Uwe Mkweli. Si Kama Waandishi Na Mafarisayo

Mfano wa tatu wa Yesu kuhusu mwenendo usio wa haki na matumizi mabaya ya Maandiko ya waandishi na Mafarisayo unahusiana na amri ya Mungu kuhusu kusema ukweli. Waandishi na Mafarisayo walikuwa wabunifu sana kwa habari ya kudanganya. Tunajifunza kutoka Mathayo 23:16-22 kwamba wao hawakujihesabu kuwa na wajibu wa kutunza nadhiri zao kama wangeapa kwa hekalu, madhabahu au mbingu. Lakini, kama wangeapa kwa dhahabu ya hekalu, au sadaka iliyoko juu ya madhabahu, au kwa Mungu aliyeko mbinguni, basi walikuwa na wajibu wa kutunza nadhiri au viapo vyao! Hayo ni mawazo ya mtu mzima akifikiri kitoto kwamba ana haki ya kutosema ukweli mradi vidole vyake vimeshikana kwa nyuma. Yesu anatazamia wanafunzi Wake waseme ukweli.

Tena mmesikia watu wa kale walivyoambiwa, ‘Usiape uongo, ila mtimizie Bwana nyapo zako.’ Lakini mimi nawaambia, ‘Usiape kabisa; hat a kwa mbingu, kwa maana ndicho kiti cha enzi cha Mungu; wala kwa nchi, kwa maana ndiyo pa kuwekea miguu yake; wala kwa Yerusalemu, kwa maana ndio mji wa Mfalme mmuu. Wala usiape kwa kichwa chako, maana huwezi kufanya unywele mmoja kuwa mweupe au mweusi. Bali maneno yenu yawe Ndiyo, ndiyo; Siyo, siyo; kwa kuwa yazidiyo hayo yatoka kwa yule mwovu’ (Mathayo 5:33-37).

Amri ya Mungu kuhusu viapo na nadhiri haikusema chochote juuya kufanya kiapo kwa kuapa na kitu kingine. Mungu alikusudia watu Wake waseme kweli wakati wote. Basi, isingekuwepo haja ya kuapa kamwe.

Hakuna kosa kuapa, kwa sababu kiapo si kitu zaidi ya nadhiri au ahadi. Kwa kweli, viapo vya kumtii Mungu ni vizuri sana. Wokovu huanza kwa kiapo cha kumfuata Yesu. Lakini watu wanapotakiwa kuapa kwa kitu kingine ili kuwafanya wengine waamini wanachosema, ni ukiri wa moja kwa moja kwamba kwa kawaida wao husema uongo. Watu wanaosema kweli sikuzote hawana haja ya kuapa hata siku moja. Lakini makanisa mengi siku hizi yamejaa waongo, na watumishi mara nyingi ndio viongozi katika udanganyifu na hila.

Mtumishi anayefanya wengine kuwa wanafunzi huonyesha mfano wa kusema kweli na kuwafundisha wanafunzi wake kusema kweli sikuzote. Anajua Yohana alionya kwamba waongo wote watatupwa katika ziwa liwakalo moto na kibiriti (ona Ufunuo 21:8).

Msilipe Kisasi, Kama Wanavyofanya Waandishi Na Mafarisayo

Kinachofuata katika orodha ya malalamiko ya Yesu ni kupotoshwa kwa Kifarisayo kwa andiko maarufu sana katika Agano la Kale. Tumekwisha kutazama maandiko hayo katika sura kuhusu kutafsiri maandiko.

Mmesikia kwamba imenenwa, ‘Jicho kwa jicho, na jino kwa jino.’ Lakini mimi nawaambia, ‘Msishindane na mtu mwovu; lakini mtu akupigaye shavu la kuume mgeuzie na la pili. Na mtu atakaye kukushitaki na kuitwaa kanzu yako, mwachie na joho pia. Na mtu atakayekulazimisha mwendo wa maili moja, nenda naye mbili. Akuombaye mpe; naye atakaye kukopa kwako, usimpe kisogo’ (Mathayo 5:33-37).

Torati ya Musa ilitamka kwamba mahakama ikimpata mtu na hatia ya kumjeruhi mwingine, adhabu yake italingana na madhara aliyoleta. Kama alimtoa mtu jino, kwa haki na uhalali kabisa jino lake na yeye litang’olewa. Amri hii ilitolea ili kuhaikisha kwamba haki ingetendeka katika mashauri ya mahakamani kwa makosa makubwa. Mungu alianzisha utaratibu wa mahakama na mahakimu katika Torati ili kupinga uhalifu, kuhakikisha haki na kuzuia visasi. Na Mungu aliwaamuru mahakimu kutokuwa na upendeleo, na kuwa wenye haki katika hukumu zao. Walitakiwa kuhukumu “jicho kwa jicho na jino kwa jino”. Lakini, maneno hayo pamoja na amri hiyo hupatikana katika maandiko yanayohusiana na haki katika mahakama.

Lakini tena, waandishi na Mafarisayo walikuwa wamebadilisha amri yenyewe na kuifanya kuwa amri ya kulipiza kisasi kuwa wajibu mtakatifu. Walikuwa wamekubali kutokuwa na uvumilivu, wakitafuta kulipiza kisasi hata kwa makosa madogo madogo kabisa.

Mungu daima ametazamia viwango vya juu zaidi kutoka kwa watu Wake. Kisasi ni kitu alichokataza Yeye (ona Kumbu. 32:35). Agano la Kale lilifundisha kwamba watu wa Mungu wanatakiwa kuwaonyesha adui zao wema (ona Kutoka 23:4, 5; Mithali 25:21-22). Yesu aliunga mkono kweli hii kwa kuwaambia wanafunzi Wake wageuze shavu la pili na kwenda maili nyingine zaidi katika kushughulika na watu waovu. Tunapokosewa, Mungu anataka tuwe na rehema, tukilipa jema kwa ovu tulilotendewa.

Lakini je! Yesu anatazamia kwamba tutawaachia watu watutumie vibaya tu, wakiharibu maisha yetu kama wapendavyo? Je, ni makosa kumpeleka asiyeamini mahakamani na kutafuta haki kwa uovu tunaotendewa? Hapana. Yesu hakuwa anazungumza juu ya kupata haki tunayuostahili kwa makosa makubwa mahakamani. Alikuwa anazungumzia juu ya kutafuta kulipa kisasi kwa mambo madogo madogo.Ona kwamba Yesu hakusema tutoe shingo yetu ili tunyongwe na mtu ambaye ametuchoma kisu mgongoni. Hakusema tutoe nyumba kwa mtu anayetaka gari. Alichokuwa anatuambia ni jinsi ya kuonyesha uvumilivu na rehema kwa kiwango cha juu sana, tunapokutana na vikwazo vidogo vidogo kila siku, na zile changamoto za kawaida zinazotokana na kushughulika kwetu na watu wenye kujipenda, au ubinafsi. Anataka tuwe wakarimu kuliko watu wenye ubinafsi wanavyotazamia. Waandishi na Mafarisayo hawakukaribia kufikia kiwango hicho.

Mbona Wakristo wengi wanakwazika kirahisi? Mbona ni wepesi sana kukasirishwa na vikwazo vidogo ambavyo ni vidogo mara kumi kuliko kupigwa kofi? Je, hao watu wameokoka kweli? Mtumishi anayefanya watu kuwa wanafunzi huonyesha mfano wa kumgeuzia mtu shavu la pili, naye anawafundisha wanafunzi wake kufanya hivyo hivyo.

Msiwachukie Adui Zenu, Kama Wanavyofanya Waandishi Na Mafarisayo

Kwa kumalizia, Yesu anaorodhesha amri nyingine iliyotolewa na Mungu ambayo waandishi na Mafarisayo waliibadili ili kutosheleza mioyo yao yenye chuki.

Mmesikia kwamba imenenwa, ‘Umpende jirani yako na umchukie adui yako’. Lakini mimi nawaambia, ‘Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni. Maana Yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshe amvua wenye haki na wasio haki. Maana, mkiwapenda wanaowapenda ninyi mwapata thawabu gani? Hata watoza ushuru, je! Nao hawafanyi yayo hayo? Tena mkiwaamkia ndugu zenu tu, mnatenda tendo gani la ziada? Hata watu wa mataifa, je! Nao hawafanyi kama hayo? Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu’ (Mathayo 5:43-48).

Katika Agano la Kale Mungua likuwa amesema hivi: “Mpende jirani yako kama unavyojipenda mwenyewe” (Walawi 19:18, TLR). Waandishi na Mafarisayo wakatafsiri jirani kuw ani wale watu waliowapenda tu. Kila mwingine yeyote alikuwa adui, na kwa kuwa Mungu alisema kuwapenda jirani zetu tu, bila shaka ni sawa kuwachukia adui zetu. Lakini, kulingana na mafundisho ya Yesu, Mungu hakuwa amekusudia hayo.

Yesu baadaye angefundisha katika habari za Msamaria Mwema kwamba, tunatakiwa kumhesabu kila mtu kuwa jirani yetu.[9] Mungu anataka tumpende kila mtu, mpaka adui zetu. Hicho ndicho kiwango cha Mungu kwa ajili ya watoto Wake – na ni kiwango ambacho Yeye Mwenyewe anakitumia. Anatuma jua na mvua kwa ajili ya kuotesha mimea, kwa watu wote – wema na wabaya. Tunatakiwa kufuata mfano Wake, tukonyesha wema kwa watu wasiostahili. Tunapofanya hivyo, inaonyesha kwamba sisi ni “wana wa Baba [yetu] aliye mbinguni” (Mathayo 5:45). Watu waliozaliwa upya kweli kweli hutenda kama Baba yao.

Upendo ambao Mungu anatazamia tuuonyeshe kwa adui zetu si hisia au kukubaliana na uovu wao. Mungu hatutaki tuendelee kujisikia vizuri juu ya wale wanaotupinga. Hatuambii tuseme kisichokuwa kweli – kwamba adui zetu ni watu wazuri sana. Lakini, anatazamia kwamba tutawahurumia na kuchukua hatua ya makusudi kuonyesha jambo hilo – haidhuru hata kwa kuwasalimu tu na kuwaombea.

Ona tena kwamba Yesu anatilia mkazo mada Yake kuu – Ni watakatifu tu watakaorithi ufalme wa Mungu. Aliwaambia wanafunzi wake kwamba, kama watawapenda wale wawapendao tu, hawana tofauti na wapagani na watoza ushuru – aina mbili za watu ambao kila Myahudi alikubali kwamba wanakwenda jehanamu. Ilikuwa ni njia nyingine ya kusema kwamba watu wanaowapenda wale wanaowapenda tu wanakwenda jehanamu.

Tenda Mema Kwa Nia Njema, Si Kama Waandishi Na Mafarisayo

Yesu hatazamii wafuasi Wake kuwa watakatifu tu. Anawatazamia wawe watakatifu kwa sababu sahihi. Inawezekana kabisa kutii amri za Mungu na bado usimpendeze ikiwa utii wa mtu unatokana na nia mbaya. Yesu aliwahukumu waandishi na Mafarisayo kwa sababu walitenda matendo yao mema yote ili wasifiwe na watu (ona Mathayo 23:5). Yesu anatazamia wanafunzi Wake wawe tofauti.

Angalieni msifanye wema wenu machoni pa watu kusudi mtazamwe na wao; kwa maana mkifanya kama hayo, hampati thawabu kwa Baba yenu aliye mbinguni. Basi wewe utoapo sadaka, usipige panda mbele yako kama wanafiki wafanyavyo katika masinagogi na njiani, ili watukuzwe na watu. Amin nawaambieni, Wamekwisha kupata thawabu yao. Bali wewe utoapo sadaka, hata mkono wako wa kushoto usijue ufanyalo mkono wako wa kuume. Sadaka yako iwe kwa siri; na Baba yako aonaye sirini atakujazi (Mathayo 6:1-4).

Yesu alitazamia kwamba wafuasi Wake watawapa maskini sadaka. Torati iliagiza hivyo (Kutoka 23:11; Walawi 19:10; 23:22; 25:35; Kumbu. 15:7-11), lakini waandishi na Mafarisayo walifanya hivyo huku tarumbeta zikipigwa, bila shaka ili kuwaita masini waje kupokea sadaka zao za ukarimu. Pamoja na hayo, ni Wakristo wangapi wanaotoa chochote kwa maskini? Hawajawahi kufikia hata mahali pa kuchunguza tu nia yao ya kutoa sadaka. Kama ubinafsi uliwasukuma waandishi na Mafarisayo kutangaza kutoa kwao, ni kitu gani kinachowasukuma Wakristo kupuuza matatizo ya maskini? Kwa hali hiyo, haki yao inazidi ile ya waandishi na Mafarisayo?

Kama Paulo atakavyorudia katika 1Wakorintho 3:10-15, tunaweza kufanya mema kwa nia mbaya. Kama nia yetu si safi, matendo yetu mema hayatapata thawabu. Paulo aliandika kwamba inawezekana hata kuhubiri Injili kwa nia isiyo safi (ona Wafilipi 1:15-17). Kulingana na maneno ya Yesu, njia nzuri yakuhakikisha kwamba utoaji wetu ni kwa nia safi ni kutoa kwa siri kiasi iwezekanavyo – bila ya kuruhusu mkono wa kushoto kujua kinachofanywa na mkono wa kuume. Mtumishi anayefanya watu kuwa wanafunzi huwafundisha wanafunzi wake kuwapa vitu maskini (kama wanaweza), naye anatenda kama mahubiri yake, kimya kimya tu.

Kufunga Na Kuomba Kwa Sababu Zilizo Sahihi

Yesu pia alitazamia kwamba wafuasi Wake wataomba na kufunga, na kwamba wangefanya mambo hayo ili kumpendeza Baba yao, si ili kuonekana na watu. Vinginevyo wasingekuwa tofauti na wale waandishi na Mafarisayo wanaokwenda jehanamu, waliokuwa wanafunga na kuomba ili wasifiwe na watu. Hiyo ni thawabu ya muda sana. Yesu aliwashauri hivi wafuasi Wake:

Tena msalipo, msiwe kama wanafiki. Kwa maana wao wapenda kusali hali wamesimama katika masinagogi na katika pembe za njia ili waonekane na watu. Amin nawaambia, Wamekwisha kupata thawabu yao. Bali wewe usalipo ingia katika chumba chako cha ndani, na ukiisha kufunga mlango wako, usali mbele za Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi.

Tena mfungapo msiwe kama wanafiki wenye uso wa kukunjamana; maana hujiumbua nyuso zao ili waonekane na watu kuwa wanafunga. Amin nawaambia, wamekwisha kupata thawabu yao. Bali wewe ufungapo jipake mafuta kichwani, unawe uso; ili usionekane na watu kuwa unafunga, ila na Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi (Mathayo 6:5-6, 16-18).

Je, ni Wakristo wangapi wenye kuishi maisha yasiyo na maombi, na ambao hata hawajawahi kufunga?[10] Sasa, haki yao inalinganishwaje na ile ya waandishi na Mafarisayo, waliofanya yote mawili – japo ni kwa sababu mbaya?

Machache Kuhusu Maombi Na Msamaha

Akiendelea na somo la maombi, Yesu alifoa mafundisho ya ziada kwa wanafunzi Wake kuhusu jinsi wanavyotakiwa kuomba. Yesu anataka sisi tuombe kwa njia ambayo haimtukani Baba Yake kwa kukana yale aliyofunua juu Yake Mwenyewe. Kwa mfano: Kwa kuwa Mungu anajua tunachohitaji kabla ya kumwomba (maana anafahamu mambo yote), hakuna sababu ya kurudia-rudia maneno tunapoomba.

Nanyi mkiwa katika kusali, msipayuke-payuke kama watu wa mataifa; maana wao hudhani ya kuwa watasikiwa kwa sababu ya maneno yao kuwa mengi. Basi msifanane na hao; maana Baba yenu anajua mnayohitaji kabla ninyi hamjamwomba (Mathayo 6:7-8).

Kweli – maombi yetu hudhihirisha jinsi tunavyomjua Mungu vizuri. Wale wanaomjua kama alivyojidhihirisha katika Neno Lake huomba ili mapenzi Yake Yeye yafanyike, na Yeye atukuzwe. Shauku yao kuu ni kuwa watakatifu – wenye kumpendeza Yeye kabisa. Hili linaonekana katika sala ya Yesu ya mfano, ambayo sisi tunaiita Sala ya Bwana. Imo katika sehemu inayofuata ya mafundisho ya Yesu kwa wanafunzi Wake. Inadhihirisha matazamio Yake kwa habari ya mambo tunayotanguliza, na upendo wetu.[11]

Basi ninyi salini hivi: ‘Baba yetu uliye mbinguni, Jina lako litukuzwe. Ufalme wako uje, Mapenzi yako yatimizwe hapa duniani kama huko mbinguni. Utupe leo riziki yetu’ (Mathayo 6:9-11).

Basi, inatakiwa wajibu wa kwanza kabisa wa wanafunzi wa Kristo uwe jina la Mungu kutukuzwa – kwamba liheshimiwe, listahiwe na kutakatifuzwa.

Wale wanaoomba kwamba jina la Mungu litakaswe wanatakiwa kuwa watakatifu wao wenyewe – watu wenye kulitakasa jina la Mungu. Vinginevyo ni unafiki tu. Kwa hiyo, sala hii huonyesha shauku tuliyo nayo kwamba wengine wajinyenyekeze mbele za Mungu kama ambavyo sisi tumekwisha fanya.

Ombi la pili katika sala hiyo mfano linafanana: “Ufalme wako uje”. Wazo la ufalme linamaanisha kuwepo kwa Mfalme mwenye kutawala ufalme Wake. Mfuasi Mkristo anatamani kumwona Mfalme wake – yule anayetawala maisha yake – atawale dunia nzima. Laiti kila mmoja angepiga goti lake kwa Mfalme Yesu – katika imani tiifu!

Ombi la tatu katika sala hiyo linarudia la kwanza na la pili, hivi:

Mapenzi yako yatendeke hapa duniani kama huko mbinguni”. Hapa tena – tunawezaje kuomba kwa dhati sala kama hiyo bila sisi wenyewe kuwa tumekubali kukaa chini ya mapenzi ya Mungu maishani mwetu? Mwanafunzi wa kweli huwa na shauku kwamba mapenzi ya Mungu yafanyike duniani kama yafanyikavyo huko mbinguni – kikamilifu na kabisa.

Yanayotakiwa kuwa muhimu zaidi kwetu kuliko hata chakula – “riziki yetu” – ni jina la Mungu litakaswe, mapenzi Yake yafanyike, na ufalme Wake uje. Hili ombi la nne linawekwa la nne kwa kusudi. Hata kwa mtazamo huo tu inaonyesha mpangilio unaofaa wa mambo muhimu maishani mwetu, na hakuna dalili ya uchoyo au ubinafsi hapa. Wanafunzi wa Kristo wanamtumikia Mungu, sio mali. Lengo lao si kujiwekea hazina duniani.

Hebu niongeze pia kwamba ombi hili la nne linaonyesha kwamba sala hii mfano inapaswa kuombwa kila siku – mwanzo wa kila siku.

Sala Mfano Inaendelea

Je, wanafunzi wa Kristo hutenda dhambi? Wakati mwingine wanatenda, maana Yesu aliwafundisha kuomba msamaha wa dhambi zao.

“Utusamehe deni zetu kama sisi nasi tuwasamehevyo wadeni wetu. Na usitutie majaribuni, lakini utuokoe na yule mwovu. [Kwa kuwa ufalme ni wako, na nguvu, na utukufu, hata milele. Amina.] Kwa maana mkiwasamehe watu makosa yao, na Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi. Bali msipowasamehe watu makosa yao, wala Baba yenu hatawasamehe ninyi makosa yenu” (Mathayo 6:12-15).

Wanafunzi wa Yesu hutambua kwamba kutokutii kwao humkwaza Mungu, na wanapotenda dhambi, wanajisikia aibu. Wanataka doa hilo liondolewe, na Baba yao wa mbinguni, kwa neema sana, yuko tayari kuwasamehe. Lakini lazima waombe msamaha, ambalo ndilo ombi la tano lipatikanalo katika Sala ya Bwana.

Ila – kusamehewa kwao kunategemea sana wao kuwasamehe wengine. Kwa sababu wamesamehewa vingi, wanawajibika kumsamehe kila mtu anayewaomba msamaha (na kumpenda na kutafuta upatanisho na wale wasioomba msamaha). Wakikataa kusamehe, Mungu hatawasamehe.

Ombi la sita na la mwisho pia linaonyesha shauku ya mwanafunzi wa kweli kuwa mtaka tifu: “Na usitutie majaribuni, lakini utuokoe na yule mwovu [au, ‘maovuni’].” Mwanafunzi wa kweli ana shauku na utakatifu kiasi cha kwamba anamwomba Mungu asimwongoze katika hali anayoweza kujaribiwa, asije akashindwa. Tena, anamwomba Mungu amwokoe na maovu yoyote yanayoweza kumnasa. Hakika hii ni sala kubwa sana ya kuomba mwanzoni mwa kila siku, kabla hatujaingia katika dunia yenye maovu na majaribu. Na hakika tunaweza kumtazamia Mungu kujibu sala hii aliyotuambia tuiombe!

Wale wamjuao Mungu wanaelewa ni kwa nini maombi yote sita katika sala hii yanafaa. Sababu inafunuliwa katika mstari wa mwisho wa sala: “Kwa kuwa [au kwa sababu] ufalme ni wako, na nguvu, na utukufu, hata milele” (Mathayo 6:13). Mungu ni Mfalme mkuu anayetawala ufalme Wake ambao ndani yake sisi ni watumishi. Yeye ndiye mwenye nguvu zote, na hakuna anayethubutu kupingana na mapenzi Yake. Utukufu wote ni Wake milele. Anastahili watu wamtii.

Je, somo kubwa katika Sala ya Bwana ni nini? Utakatifu. Wanafunzi wa Kristo wanatamani jina la Mungu litukuzwe, utawala Wake uimarishwe duniani kote, na mapenzi Yake yafanyike kikamilifu kila mahali. Hii ni muhimu sana kwao kuliko hata riziki yao ya kila siku. Wanataka kumpendeza, na wanaposhindwa, wanataka msamaha Wake. Kama watu waliosamehewa, wanawasamehe wengine. Wanatamani kuwa watakatifu kabisa mpaka wanataka kuepuka majaribu kwa sababu majaribu huongeza nafasi zao za kutenda dhambi. Mtumishi anayefanya watu kuwa wanafunzi hufundisha mambo hayo kwa wanafunzi wake.

Mwanafunzi Na Vitu Alivyo Navyo

Somo linalofuata katika Mahubiri ya Mlimani linaweza kuwakorofisha Wakristo ambao lengo lao kubwa maishani ni kuzidi kujipatia vitu.

Msijiwekee hazina duniani, nondo na kutu viharibupo na wevi huvunja na kuiba; bali jiwekeeni hazina mbinguni, kusikoharibika kitu kwa nondo wala kutu, wala wevi hawavunji wala hawaibi. Kwa kuwa hazina yako ilipo ndipo utakapokuwapo na moyo wako. Taa ya mwili ni jicho. Basi jicho lako likiwa safi, mwili wako wote utakuwa na nuru. Lakini jicho lako likiwa bovu, mwili wako wote utakuwa na giza. Basi, ile nuru iliyomo ndani yako ikiwa giza; si giza hilo! Hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili. Kwa maana atamchukia huyu na kumpenda huyu, ama atashikamana na huyu na kumdharau huyu. Hamwezi kumtumikia Mungu na mali (Mathayo 6:19-24).

Yesu aliagiza kwamba tusijiwekee hazina hapa duniani. Sasa – “hazina” ni kitu gani? Hazina halisi huwekwa katika masanduku ya hazina, na kuhifadhiwa mahali. Hazitumiki kwa kitu chochote kinachofaa. Yesu alifafanua hizo kuwa ni vitu vinavyovutia kutu, nondo na wezi. Yaani ni kusema kwamba “si vya muhimu”. Nondo hula vilivyo ndani kabisa ya makabati yetu – hawali vile tunavyotumia kila siku. Kutu hula vtu tusivyotumia sana. Katika nchi zilizoendelea sana, kwa kawaida wevi huiba vitu ambavyo watu hawavihitaji sana: picha, lulu, vitu vya thamani, na kitu kinachoweza kuuzwa haraka.

Wanafunzi wa kweli wamekwisha “toa mali zao zote” (ona Luka 14:33). Wao ni wasimamizi tu wa fedha za Mungu. Basi, kila uamuzi wa kutumia fedha ni wa kiroho. Tunachofanya na fedha yetu huonyesha nani anayetawala maisha yetu. Tunapokusanya “hazina” na kwa njia hiyo kulundika fedha na kununua visivyo muhimu, tunadhihirisha kwamba Yesu si anayetawala maishani mwetu. Maana, kama angekuw andiye mtawala, tungefanya vitu bora zaidi na zile fedha alizotukabidhi.

Hivyo vitu bora zaidi ni kama nini? Yesu anatuagiza tujiwekee hazina mbinguni. Inawezekanaje kufanya hivyo? Anatuambia katika Injili ya Luka: “Viuzeni mlivyo navyo mtoe sadaka. Jifanyieni mifuko isiyochakaa, akiba isiyopungua katika mbingu, mahali pasipokaribia mwivi, wala nondo haharibu” (Luka 12:33).

Kwa kutoa fedha kuwasaidia maskini na kueneza Injili, tunajiwekea hazina mbinguni. Yesu anatuambia tuchukue kile kitakachopungua thamani mpaka kufikia kutokuwa nayo, tukitie katika kitu kingine ambacho hakipotezi thamani kamwe. Hayo ndiyo afanyayo mtumishi anayefanya watu kuwa wanafunzi, naye anawafundisha wanafunzi wake kufanya hivyo hivyo.

Jicho Bovu

Je, Yesu alimaanisha nini alipozungumza juu ya watu wenye macho mazuri ambao miili yao imejaa nuru, na watu wenye macho mabovu, ambao miili yao imejaa giza? Bila shaka maneno Yake yalihusu mambo ya fedha na vitu, kwa sababu kabla ya kusema hayo alikuwa anazungumzia vitu hivyo, na baada ya kusema hivyo alizungumzia vitu hivyo.

Neno la Kiyunani lililotafsiriwa “bovu” katika 6:23 ndiyo limetafsiriwa “ovu” katika Mathayo 20:15. Hapo tunasoma kuhusu mwajiri aliyemwambia mfanya kazi wake hivi: “Je, jicho lako limekuwa ovu kwa kuwa mimi ni mkarimu?” (TLR) Ni wazi kwamba jicho haliwezi kuwa ovu. Sasa – “jicho ovu (au bovu)” maana yake mtu mwenye choyo. Hii inatusaidia sisi kuelewa vizuri zaidi maana ya Kristo katika Mathayo 6:22-23.

Mtu mwenye jicho safi ni mfano wa yule mwenye moyo safi, anayeruhusu mwangaza wa kweli kuingia ndani yake. Basi, anamtumikia Mungu na kujiwekea hazina – si duniani – bali mbinguni, mahali ambapo moyo wake upo. Mtu mwenye jicho bovu hufungia nje mwanza wa kweli usiingie, kwa sababu yeye hudhani tayari ana ukweli. Basi amejaa giza, akiaini uongo. Anajiwekea hazina duniani mahali moyo wake ulipo. Yeye anaamini kwamba kusudi la maisha yake ni kujitosheleza. Fedha ni mungu wake. Haendi mbinguni.

Nini maana ya fedha kuwa mungu wako? Maana yake ni kwamba fedha ina nafasi ambayo Mungu anapaswa kuwa nayo maishani mwako. Fedha inatawala maisha yako. Ndiyo inayochukua nguvu zako, mawazo yako na muda wako. Ndiyo chanzo kikuu cha furaha yako. Unazipenda.[12] Ndiyo maana Paulo alifananisha tamaa (au choyo) na kuabudu sanamu, akisema kwamba hakuna yeyote mwenye tamaa atakayeurithi ufalme wa Mungu (ona Waefeso 5:5; Wakolosai 3:5-6).

Mungu na fedha hutaka kutawala maisha yetu, na Yesu alisema hatuwezi kuwatumikia wote wawili. Hapo tena tunaona Yesu alibakia kwenye somo Lake kuu – Ni watakatifu tu watakaorithi ufalme wa Mungu. Aliweka wazi kabisa kwamba watu waliojaa giza, ambao mungu wao ni fedha, ambao mioyo yao ipo duniani na wenye kujiwekea hazina za kidunia hawako kwenye ile njia nyembamba iongozayo watu kwenda uzimani.

Maskini Mwenye Kutamani

Kutaka sana kupata vitu si kosa wakati vitu hivyo ni vya anasa. Mtu anaweza kukosea na kuwaza sana kuhusu vitu hata kama hivyo vitu ni mahitaji ya msingi. Yesu aliendelea kufundisha hivi:

Kwa sababu hiyo nawaambieni, Msisumbukie maisha yenu, mle nini au mnywe nini; wala miili yenu, mvae nini. Maisha je! Si zaidi ya chakula na mwili zaidi ya mavazi? Waangalieni ndege wa angani ya kwamba hawapandi wala hawavuni wala hawakusanyi ghalani; na Baba yenu wa mbinguni huwalisha hao. Ninyi je! Si bora kupita hao? Ni yupi kwenu ambaye akijisumbua aweza kujiongeza kimo chake hata mkono mmoja? Na mavazi ya nini kuyasumbukia? Fikirini maua ya mashamba jinsi yameavyo; hayafanyi kazi wala hayasokoti, nami nawaambia ya kwamba hata Sulemani katika fahari yake yote hakuvikwa vizuri kama mojawapo la hayo. Basi, ikiwa Mungu huyavika hivi majani ya kondeni, yaliyopo leo na kesho hutupwa kalibuni, je! Hatazidi sana kuwavika ninyi, enyi wa imani hapa? Msisumbuke basi mkisema, Tule nini? Au Tunywe nini? Au Tuvae nini? Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta. Kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa. Basi msisumbukie ya kesho; kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe. Yatosha kwa siku maovu yake (Mathayo 6:25-34).

Wasomaji wengi wa kitabu hiki hawataweza kujilinganisha hata kidogo na watu ambao Yesu alikuwa anazungumza nao. Je, wewe ulipata wasiwasi lini mara ya mwisho kuhusu chakula, kinywaji au mavazi?

Maneno ya Yesu kwa hakika yanatuhusu sisi wote. Ikiwa ni makosa kuwaza sana na kuchukuliwa na upatikanaji wa mambo muhimu maishani, vipi kuhusu yasiyokuwa muhimu? Yesu anawatazamia wanafunzi Wake kuhusika zaidi na kutafuta mambo mawili: Ufalme Wake na haki Yake. Mkristo anaposhindwa kutoa zaka – fungu la kumi – (na hiyo ni amri ya agano la kale) lakini aweze kujipatia vitu vingi tu visivyo muhimu, je, anaishi kulingana na kanuni ya Kristo ya kutafuta kwanza ufalme na haki Yake? Jibu ni wazi kabisa!

Usiwe Mtafuta Makosa

Maagizo ya Yesu yanayofuata kwa wafuasi Wake yanahusu dhambi za kuhukumu na kutafuta makosa kwa wengine.

Msihukumu msije mkahukumiwa ninyi. Kwa kuwa hukumu ile mhukumuyo ndiyo mtakayohukumiwa; na kipimo kila mpimiacho ndicho mtakachopimiwa. Basi, mbona wakitazama kibanzi kilicho ndani ya jicho la ndugu yako, na boriti iliyo ndani ya jicho lako mwenyewe huiangalii? Au utamwambiaje nduguyo, Niache nikitoe kibanzi katika jicho lako; na kumbe! Mna boriti ndani ya jicho lako mwenyewe? Mnafiki wewe. Itoe kwanza ile boriti katika jicho lako mwenyewe; ndipo utakapoona vema kukitoa kile kibanzi katika jicho la ndugu yako (Mathayo 7:1-5).

Ingawa Yesu hakuwashtaki waandishi na Mafarisayo moja kwa moja au vinginevyo katika fungu hili, wao walikuwa na hatia ya dhambi hii. Walimkosoa Yeye!

Je, Yesu alimaanisha nini hasa katika onyo hili la kuwahukumu wengine?

Kwanza: Hebu tufikiri hakumaanisha nini. Yeye hakumaanisha kwamba tusiwe wenye uwezo wa kupambanua na kufanya maamuzi ya msingi kuhusu tabia za watu kwa kuwatazama matendo. Hilo ni wazi kabisa. Mara tu baada ya sehemu hii, Yesu aliwaagiza wanafunzi Wake wasitupe lulu zao mbele ya nguruwe na wasiwape mbwa kilicho kitakatifu (ona 7:6). Bila shaka alikuwa anazungumza kwa mifano juu ya watu fulani, akiwaita nguruwe na mbwa – watu ambao hawakuthamini thamani ya vitu vitakatifu – “lulu” – walivyokuwa wanapewa. Bila shaka hawajaokoka hao. Kwa kweli ni lazima kupima kama watu ni nguruwe na mbwa ikiwa tutatii agizo hili.

Tena, Yesu akawaambia wafuasi Wake baadaye kidogo jinsi ya kupima waalimu wa uongo – “mbwa mwitu waliovaa mavazi ya kondoo” (7:15) – kwa kukagua matunda yao. Basi, ni dhahiri kwamba ili tuweze kutii maagizo ya Yesu lazima tutazame jinsi watu wanavyoishi na kutoa hukumu.

Paulo vile vile aliwaambia waamini Wakorintho hivi:

Lakini mambo yalivyo, naliwaandikia kwamba msichangamane na mtu aitwaye ndugu akiwa ni mzinzi au mwenye kutamani au mwenye kuabudu sanamu au mtukanaji au mlevi au mnyang’anyi; mtu wa namna hii msikubali hata kula naye (1Wakor. 5:11).

Ili kutii agizo hili inatakiwa tuchunguze maisha ya watu na kufanya maamuzi juu yao – kuhukumu – kutokana na kile tunachokiona.

Hata mtume Yohana pia alituambia tunaweza kutambua kirahisi tu nani ni wa Mungu na nani ni wa Shetani. Kwa kutazama maisha ya watu, ni dhahiri kwetu nani ameokoka na nani hajaokoka (ona 1Yohana 3:10).

Kama mambo ni hayo, Kristo hasemi kwamba ni dhambi kutambua tabia za watu kwa kuyatazama maisha yao na kuhukumu kama wao ni wa Mungu au wa Shetani. Sasa, alimaanisha nini basi?

Hebu gundua kwamba Yesu alikuwa anazungumza juu ya kutafuta makosa madogo – vibanzi katika ndugu – tafadhali ona kwamba Yesu anatumia neno ndugu mara tatu katika fungu hili. Yesu hakuwa anatuonya dhidi ya kuwahukumu watu kwamba ni wasioamini kwa kutazama makmosa yao makubwa sana (kama tutakavyoona punde tu katika mahubiri haya). Kinyume chake – haya ni mafundisho kuhusu jinsi Wakristo wanavyopaswa kuwatendea Wakristo wengine. Hawapaswi kuwa watafutaji makosa madogo madogo miongoni mwao – hasa kama wao wenyewe hawaoni makosa yao makubwa sana. Ikifikia hapo wanakuwa wanafiki. Yesu aliwahi kuwaambia watu wengine waliokuwa wanafiki, hivi: “Yeyote asiyekuwa na dhambi miongoni mwenu, na awe wa kwanza kutupa jiwe” (Yohana 8:7, TLR).

Mtume Yakobo, ambaye barua yake inafanana na Mahubiri ya Mlimani sehemu sehemu, aliandika hivi, “Ndugu! Msinung’unikiane msije mkahukumiwa. Angalieni, mwamuzi amesimama mbele ya milango” (Yakobo 5:9). Pengine hili nalo litatusaidia kuelewa kidogo kuhusu kitu Yesu alichokuwa anaonya – kutafuta makosa katika waaminio kisha kutangaza tulichopata – kunung’unikiana. Hii ni dhambi moja kubwa sana katika kanisa, na wale wenye hatia ya dhambi hiyo wanajiweka katika nafasi hatari sana ya kuhukumiwa. Tunapomsema mwamini mwenzsetu, tukionyesha makosa yake kwa wengine, tunahalifu Amri Kuu, kwa sababu sisi hatupendi watu waseme ubaya wetu wakati hatupo.

Tunaweza kwa upendo kabisa kumwendea mwamini ambaye ana tatizo, lakini wakati tunapoweza kufanya hivyo bila ya unafiki, tukiwa na uhakika kwamba hatuna hatia (au hatia zaidi) ya dhambi hiyo hiyo kama mtu tunayembana. Ila, ni kupoteza wakati kabisa kufanya hivyo na asiyeamini, na hicho ndicho kisemwacho katika mstari unaofuata. Yesu alisema hivi:

Msiwape mbwa kilicho kitakatifu wala msitupe lulu zenu mbele ya nguruwe, wasije wakazikanyaga chini ya miguu yao, wakageuka na kuwararua (Mathayo 7:6).

Vivyo hivyo kuna mithali inayosema hivi: “Usimkaripie mwenye dharau asije akakuchukia. Mkaripie mwenye hekima, naye atakupenda” (Mithali 9:8). Mahali pengine Yesu aliwaambia wanafunzi Wake kukung’uta mavumbi ya miguu yao kama kulalamika kinyume cha wanaokataa injili yao. “Mbwa” wakiisha tambuliwa kwa kutokufurahia na kupenda kweli, Mungu hataki watumishi Wake wapoteze muda wao kujaribu kuwafikia, huku kuna wengine ambao hawajapata nafasi hata moja.

Himizo Kuomba

Hatimaye tunafikia sehemu ya mwisho ya mahubiri ya Yesu. Inaanza kwa ahadi za kutia moyo sana kuhusu maombi, kama ifuatavyo:

Ombeni nanyi mtapewa; tafuteni nanyi mtaona; bisheni nanyi mtafunguliwa. Kwa maana kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa. Au kuna mtu yupi kwenu ambaye, mwanamwe akimwomba mkate atampa jiwe? Au akiomba samaki atampa nyoka? Basi ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Si zaidi sana Baba yenu aliye mbinguni atawapa mema wao wamwombao? (Mathayo 7:7-11).

Msomaji mmoja anaweza kusema, “Aha! Nimepata sehemu ya Mahubiri ya Mlimani ambayo hayahusiani na utakatifu.”

Inategemeana na tunachokomba, na kwamba tunabisha na kutafuta nini katika sala. Kama wenye kuwa na “njaa na kiu ya haki”, tunatamani kutii yote ambayo Yesu ameamuru katika mahubiri Yake, na hiyo shauku inaonekana katika sala zetu. Ukweli ni kwamba ile sala mfano ambayo Yesu amefundisha hapo nyuma katika Mahubiri haya ni onyesho la shauku kwamba mapenzi ya Mungu yafanyike, na utakatifu upatikane.

Tena, tafsiri ya Luka ya ahadi hizo hizo za sala tunazotazama humalizika kwa maneno yafuatayo: “Basi ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Baba aliye mbinguni hatazidi sana kuwapa Roho Mtakatifu hao wamwombao?” (Luka 11:13). Yesu hakuwa anafikiria vituv ya starehe alipotuahidi “mema”. Katika akili Yake, Roho Mtakatifu ni “kipawa chema” kwa sababu hutufanya sisi kuwa watakatifu na kutusaidia kueneza Injili inayowafanya wengine kuwa watakatifu pia. Na watakatifu ndiyo wanaokwenda mbinguni.

Zawadi zingine nzuri ni chochote kilicho katika mapenzi ya Mungu. Ni wazi kwamba Mungu anashughulika zaidi na mapenzi Yake na ufalme Wake. Basi na sisi tutazamie kwamba sala zetu kuhusu chochote kitakachoongeza faida yetu katika ufalme wa Mungu zitajibiwa kila wakati.

Maneno Ya Kuhitimisha

Sasa tunafikia mstari ambao unapaswa kuhesabiwa kuwa ni hitimisho la kila kitu ambacho Yesu amesema kufikia hapa. Waandishi wengi wa mafafanuzi ya Biblia hushindwa kuona hilo, lakini ni muhimu sisi tusikosee. Mstari huu ni wa kumalizia maana unaanza kwa neno hili: Basi. Kwa hali hiyo umeunganika na mafundisho yaliyopita, na swali ni hili: Je, ni muhtasari kiasi gani wa yale ambayo Yesu amesema? Hebu tuusome na kufikiri kidogo juu yake.

Basi, yoyote mtakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo; maana hiyo ndiyo Torati na Manabii (Mathayo 7:12).

Maneno hayo hayawezi kuwa muhtasari wa ile mistari michache inayosema kuhusu maombi. Ingekuwa hivyo, haileti maana yoyote.

Kumbuka kwamba mapema kabisa katika mahubiri yake, Yesu alikuwa ameonya kuhusu kosa la kudhani kwamba amekuja kuitangua Torati na Manabii (ona Mathayo 5:17). Kuanzia hapo na kuendelea, mpaka mstari huu tunaotazama sasa, hakufanya kitu kingine isipokuwa kuunga mkono na kufafanua amri za Mungu katika Agano la Kale. Kwa hiyo sasa anahitimisha kila kitu kilichoagizwa – yote yaliyotoka katika Torati na Manabii – “Basi, yoyote mtakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo; maana hiyo ndiyo Torati na Manabii” (7:12). Maneno “Torati na Manabii” huunganisha kila kitu alichosema Yesu kati ya Mathayo 5:17 na 7:12.

Sasa, anapoanza kuhitimisha mahubiri Yake, anakariri tena fundisho Lake kuu – Ni watakatifu tu ndiyo watakaorithi ufalme wa Mungu.

Ingieni kwa kupitia mlango ulio mwembamba. Maana mlango ni mpana na njia ni pana iendayo upotevuni, nao ni wengi waingiao kwa mlango huo. Bali mlango ni mwembamba na njia imesonga iendayo uzimani, nao waionao ni wachache (Mathayo 7:13-14).

Bila shaka huo mlango mwembamba na njia endayo uzimani ambayo wachache wanaiona, ni mfano wa wokovu. Ule mlango mpana na njia pana iendayo upotevuni ambayo ndiyo inafuatwa na wengi, ni mfano wa kupotea. Kama kila kitu alichosema Yesu kabla ya maneno haya kinamaanisha chochote – kama mahubiri haya yanakwenda kwa mpangilio unaofaa – kama Yesu alikuwa msemaji fundi mwenye ufahamu kuhusu kuwasiliana na watu, basi tafsiri halisi kabisa ni kwamba njia nyembamba ni njia ya kumfuata Yesu na kutii mafundisho Yake. Ile pana ni kinyume chake. Je, ni Wakristo wangapi walio kwenye njia hiyo nyembamba yenye kuelezwa katika mahubiri haya? Mtumishi anayefanya wengine kuwa wanafunzi yuko kwenye ile njia nyembamba, naye anawaongoza wanafunzi wake kuipitia.

Inawashangaza Wakristo wengine kwamba Yesu hakusema chochote kuhusu imani au kumwamini katika mahubiri haya ambayo kwa sehemu kubwa sana alizungumzia juu ya wokovu na kupotea. Kwa wale wanaoelewa kiungo kilichoko kati ya kuamini na mwenendo, mahubiri haya hayana matatizo yoyote. Watu wanaomtii Yesu huonyesha imani yao kwa matendo yao. Wale wasiomtii hawaamini kwamba ni Mwana wa Mungu. Wokovu wetu si onyesho tu la neema ya Mungu kwetu, bali hata lile badiliko lililotokea maishani mwetu ni onyesho pia. Kihalisi ni kwamba utakatifu wetu ni utakatifu Wake.

Jinsi Ya Kutambua Viongozi Waongo Wa Dini

Yesu alipoendelea kumalizia mahubiri Yake, alitoa onyo kwa wanafunzi Wake kuhusu manabii wa uongo ambao wanawaongoza wasioweza kuwatambua kuelekea upotevuni kwa njia ile pana. Hao si wa Mungu kweli, lakini wamejigeuza na kuonekana hivyo. Waalimu wote wa uongo na viongozi wa aina hiyo wako katika fungu hili. Wanawezaje kutambuliwa?

Jihadharini na manabii wa uongo, watu wanaowajia wamevaa mavazi ya kondoo walakini kwa ndani ni mbwa-mwitu wakali. Mtawatambua kwa matunda yao. Je! Watu huchuma zabibu katika miiba, au tini katika mibaruti? Vivyo hivyo kila mti mwema huzaa matunda mazuri; na mti mwovu huzaa matunda mabaya. Mti mwema hauwezi kuzaa matunda mabaya, wala mti mwovu kuzaa matunda mazuri. Kila mti usiozaa tunda zuri hukatwa ukatupwa motoni. Ndiposa kwa matunda yao mtawatambua. Si kila aniambiaye ‘Bwana, Bwana’ atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni. Wengi wataniambia siku ile, ‘Bwana, Bwana, hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya miujiza mingi?’ Ndipo nitawaambia dhahiri, ‘Sikuwajua ninyi kamwe; ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu’ (Mathayo 7:15-23).

Yesu alionyesha waziwazi kwamba waalimu wa uongo ni wadanganyifu sana. Wanaonekana kwa nje kuwa ni halisi. Wanaweza kumwita Yesu Bwana wao, wakatabiri, wakatoa pepo na kutenda miujiza. Lakini yale “mavazi ya kondoo” huficha “mbwa mwitu wakali”. Wao si kondoo wa kweli. Itajulikanaje kwamba ni wa kweli au wa uongo? Tabia yao ya kweli inaweza kutambulika kwa kuchunguza “matunda” yao.

Nini matunda anayozungumzia Yesu? Bila shaka si matunda ya miujiza. Ila, ni matunda ya kutii yote ambayto Yesu alifundisha. Wale walio kondoo wa kweli hufanya mapenzi ya Baba. Wale walio wa uongo ni “watenda maovu” (7:23). Wajibu wetu basi ni kulinganisha maisha yao na yale ambayo Yesu alifundisha na kuamuru.

Siku hizi waalimu wa uongo ni wengi sana makanisani, na hilo lisitushangaze kwa sababu Yesu na Paulo walituonya kwamba, kadiri mwisho unavyokaribia, tutazamie hivyo (ona Mathayo 24:11; 2Timo. 4:3-4). Manabii wa uongo walio wengi siku hizi ni wale wanaofundisha kwamba mbinguni wataingia wasiokuwa watakatifu. Hao wanawajibika kwa kupotea kwa mamilioni ya watu. John Wesley – mhubiri maarufu wa siku za nyuma – aliandika hivi juu yao:

Kitu hiki ni kibaya sana! – wakati wawakilishi wa Mungu wanapofanyika watendaji wa Shet ani! – wakati wale ambao wameagizwa kuwafundisha watu njia ya kufika mbinguni wanapowafundisha njia ya kwenda jehanamu … Kama mtu akiuliza, “Nani amewahi kufanya hviyo?” … Ninajibu hivi: Watu elfu kumi, wenye hekima na wanaoheshimiwa sana. Naam, wale wote, wa dhehebu lolote lile, wanaowatia moyo watu wenye kiburi, wenye kuchukulia mambo kirahisi-rahisi tu, wenye tamaa, wanaopenda dunia, wanaopenda starehe, wasiotenda haki au wema, watu rahisi kudanganyika, wasiojali, wasiodhuru chochote, wasiofaa, wasiokuwa tayari kuteseka kwa ajili ya haki, kwamba hao watakwenda mbinguni. Hao ni manabii wa uongo wa hali ya juu sana. Hao ni wasaliti wa Mungu na mwanadamu … Daima wanawaongoza watu kuelekea katika nchi za giza; na watakapowafuata hao maskini waliowapoteza, “kuzimu chini itataharuki ili kuwapokea!”[13]

Maneno hayo aliyasema katika kufafanua juu ya waalimu wa uongo ambao Yesu alionya juu yake katika Mathayo 7:15-23.

Ona tena kwamba Yesu alisema wazi kabisa – kinyume na tunavyoambiwa na waalimu wengi wa uongo siku hizi – wale wasiozaa matunda mema watatupwa jehanamu (7:19). Tena, hilo si kwa ajili ya waalimu na manabii tu, bali ni kwa wote. Yesu alisema hivi: “Si kila mtu aniitaye ‘Bwana, Bwana’ atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni wale watendao mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni” (Mathayo 7:21, TLR). Kinachohusu manabii kinawahusu wote. Hiyo ndiyo mada kuu ya Yesu – Walio watakatifu tu ndiyo wataurithi ufalme wa Mungu. Watu wasiomtii Yesu wanakwenda jehanamu.

Ona pia jinsi Yesu anavyounganisha hali ya mtu ndani na jinsi alivyo nje. Miti “mizuri” huzaa matunda mazuri. Miti “mibaya” haiwezi kuzaa matunda mazuri. Chanzo cha matunda mazuri yanayoonekana kwa nje ni ile asili ya mtu. Mungu kwa neema Yake amebadilisha asili ya watu ambao wamemwamini Yesu kweli.[14]

Onyo La Mwisho Na Hitimisho

Yesu alimalizia mahubiri Yake kwa onyo la mwisho pamoja na hitimisho kwa njia ya mfano. Kama unavyotazamia, ni mfano kuhusu kweli kuu aliyozungumzia – Watakatifu ndiyo watakaorithi ufalme wa Mungu.

Basi kila asikiaye hayo maneno yangu na kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye akili aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba. Mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile isianguke; kwa maana misingi yake imewekwa juu ya mwamba. Na kila asikiaye hayo maneno yangu asiyafanye atafananishwa na mtu mpumbavu aliyejenga nyumba yake juu ya mchanga. Mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, ikaanguka; nalo anguko lake likawa kubwa (Mathayo 7:24-27).

Mfano wa mwisho wa Yesu sio ufunguo wa “mafanikio maishani” kama wengine wanavyosema. Mantiki inaonyesha kwamba hakuwa anatoa ushauri kuhusu jinsi ya kufanikiwa kifedha katika nyakati ngumu kwa kuwa na imani katika ahadi Zake. Huu ni muhtasari wa yote ambayo yesu alisema katika Mahubiri Yake ya Mlimani. Wale wanaofanya anayosema ni wenye hekima na watadumu. Hawahitaji kuogopa hasira ya Mungu itakapokuja. Wasiomtii ni wapumbavu nao watateseka sana. Watalipa gharama ya “adhabu ya kuangamizwa milele” (2Wathes. 1:9).

Jibu La Swali

Je, haiwezekani kwamba Mahubiri ya Yesu Mlimani yalikuwa ni kwa ajili ya wafuasi Wake tu, walioishi kabla ya kifo na kufufuka Kwake? Si wao walikuwa chini ya Torati kama njia ya muda tu ya wokovu, na baada ya Yesu kufa kwa ajili ya dhambi zao ndipo waliokolewa kwa imani na kutangua kweli kuu inayotawala mahubiri haya?

Wazo hilo ni baya sana. Hakuna yeyote aliyewahi kuokolewa kwa matendo yake. Kila wakati imekuwa ni kwa imani – kabla na katika kipindi cha agano la kale. Paulo anatoa hoja katika Warumi 4 kwamba Ibrahimu (kabla ya agano la kale) na Daudi (wakati wa agano la kale) walihesabiw ahaki kwa imani, si kwa matendo.

Tena, ilikuwa ni vigumu kwa yeyote katika wasikilizaji wa Yesu kuokolewa kwa matendo, maana wote walikuwa wametenda dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu (ona Warumi 3:23). Neema ya Mungu tu ndiyo ingewaokoa, na imani tu ndiyo ingepokea neema hiyo ya Mungu.

Kwa bahati mbaya sana – wengi katika kanisa siku hizi wanaona amri za Yesu kuwa hazina kusudi lingine isipokuwa kutufanya tujisikie hatia ili tuone jinsi isivyowezekana kupata wokovu kwa matendo. Kwa kuwa sasa “tumepata ujumbe” na kuokolewa kwa imani, tunaweza kupuuza amri Zake. Ila, kama tunataka wengine “waokolewe” basi tuzifuate. Tuzichomoe na kuwaonyesha watu jinsi walivyo na dhambi, ili waokolewe kwa “imani” isiyo na matendo.

Pamoja na hayo, Yesu hakuwaambia wanafunzi Wake hivi: “Enendeni ulimwenguni mwote mkawafanye watu kuwa wanafunzi, na mhakikishe kwamba, wakiisha tambua hatia yao na kuokolewa kwa imani, amri zangu zimemaliza kusudi lake katika maisha yao.” Badala yake alisema hivi: “Enendeni mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi … na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi” (Mathayo 28:19-20. Maneno mepesi kukazia). Watumishi wanaofanya watu kuwa wanafunzi wanafanya hayo hayo.


[1] Cha kuvutia ni kwamba, mstari unaofuata katika kitabu cha Yakobo unasema hivi: “Ndugu zangu, inafaa nini mtu akisema anayo imani, pasipo matendo? Je, imani hiyo yaweza kumwokoa?” (Yakobo 2:14).

[2] Hii ingekuwa kweli kwa habari ya kinachoitwa “sehemu za kuabudu katika Torati” pamoja na zile sehemu za “kiadili za Torati”, japo sehemu kubwa ya maelezo Yake kamili kuhusu Yeye kutimiza ile sehemu ya Torati ya kuabudu ingetolewa na Roho Wake Mtakatifu kwa mitume, baada ya kufufuka Kwake. Sasa tunaelewa ni kwanini hakuna haja ya kutoa dhabihu ya wanyama katika agano jipya. Ni kwa sababu Yesu alikuwa Mwanakondoo wa Mungu. Wala hatufuati zile sheria za vyakula zha agano la zamani kwa sababu Yesu alisema vyakula vyote vimetakaswa (ona Marko 7:19). Hatuna haja ya kuombewa na kuhani mkuu mwanadamu kwa sababu sasa Yesu ni Kuhani wetu Mkuu, n.k. Lakini – tofauti na sheria za kuabudu – hakuna sehemu yoyote ya sheria za maadili iliyobadilishwa na chochote alichosema au kutenda Bw2ana Yesu, kabla au baada ya kufa na kufufuka Kwake. Badala yake, Yesu alifafanua na kuunga mkono sheria ya Mungu ya maadili, kama walivyofanya wanafunzi kwa uvuvio wa Roho, baada ya kufufuka Kwake. Sehemu za maadili katika Torati ya Musa ziko kwa ukamilifu kabisa katika Sheria ya Kristo – sheria ya agano jipya. Kumbuka pia kwamba Yesu alikuwa anazungumza na Wayahudi waliokuwa chini ya Torati ya Musa. Basi maneno Yake katika Mathayo 5:17-20 yanapaswa kutafsiriwa katika mwangaza wa mafunuo Yake yanayoendelea yapatikanayo katika Agano Jipya.

[3] Tena, kama Yesu alikuwa anazungumza juu ya ile haki ya kisheria tunayohesabiwa na kuipokea kama zawadi kwa sababu ya kumwamini, mbona hakusema hivyo? Mbona akasema kitu ambacho kingekuwa rahisi kueleweka vibaya na wale watu waliokuwa wanamsikiliza, wasiosoma, ambao wasingeweza hata kukisia tu kwamba alikuwa anazungumza juu ya kuhesabiwa haki?

[4] Hilo linahusika katika mahusiano yetu na ndugu na dada zetu katika Kristo. Yesu aliwaita viongozi fulani wa kidini wapumbavu (tazama Mathayo 23:17), na utaona Maandiko mengine yakifanya hivyo kwa ujumla (ona Mithali 1:7; 13:20).

 

[5] Mungu hamhesabii hatia akiolewa tena, maana alinaswa katika dhambi ya mumewe. Maneno ya Yesu hayana maana yoyote kama hataolewa, maana kwa hali hiyo hawezi kuhesabiwa kuwa mzinzi.

[6] Hapa tena ni kwamba, Mungu hamhesabii hatia ya uasherati yule mume mpya. Yeye anafanya kitu cha kiungwana, kumwoa na kumtunza mwanamke aliyeachwa. Lakini, kama mwanamume atamtia mwanamke moyo amwache mume wake ili waoane, hapo ana hatia ya uzinzi, na yawezekana hiyo ndiyo maana ya maneno ya Yesu hapa.

[7] Kuna mazingira mengine ambayo lazima yashughulikiwe. Kwa mfano: Mwanamke aliyeokoka anayeachwa na mume wake asiyeokoka hana hatia ya uasherati kama ataolewa na mwanamume aliyeokoka.

[8] Huko mbele katika sura nyingine kuhusu talaka na ndoa tena, ninashughulikia swala hili kwa upana zaidi.

[9] Myahudi mmoja aliyekuwa mwalimu wa Torati alimwuliza Yesu swali hili: “Jirani yangu ni nani?” ili kujihesabia haki. Naomba ujue kwamba alikuwa anajua jibu sahihi. Bwana Yesu alimjibu kwa kusimulia habari ya Msamaria, mtu kutoka kabila lililochukiwa sana na Wayahudi, aliyejionyesha kuwa jirani kwa Myahudi aliyekuwa ametendewa vibaya. Jisomee Luka 10:25-37.

[10] Katika kitabu hiki huko mbele kuna sura nzima kuhusu hilo somo la kufunga.

[11] Kwa bahati mbaya, kuna wengine wanaosema haya si maombi yanayopaswa kutumiwa na Wakristo kwa sababu si “katika jina la Yesu”. Tukishika hoja hiyo, itabidi tuseme pia kwamba sala nyingi za mitume zinazopatikana katika Matendo na nyaraka mbalimbali hazikuwa “za Kikristo”.

[12] Wakati mwingine tena Yesu alisema haiwezekani kumtumikia Mungu na mali. Luka anatuambia hivi: “Basi Mafarisayo, ambao wenyewe ni wapenda fedha, waliyasikia hayo yote, wakamdhihaki” (Luka 16:14). Basi – hapa tena katika Mahubiri ya Mlimani, Yesu alikuwa anafunua wazi kawaida na mafundisho ya Mafarisayo.

[13] Hayo yametoka katika kitabu cha John Wesley kiitwacho The Works of John Wesley (Baker: Grand Rapids, 1996). Kimechapishwa upya kutoka toleo la 1872 la Wesleyan Methodist Book Room, London. Ukurasa wa 441, 416.

 

[14] Sitaacha kusema hapa kuhusu msemo wa kawaida watu wanaotumia, wanapojaribu kutetea dhambi ndani ya wengine. Wansema hivi: “Hatujui yaliyomo moyoni mwake.” Kinyume cha maneno hayo, Yesu anasema hapa kwamba mambo ya nje hudhihirisha mambo ya ndani. Mahali pengine alisema hivi: “Kinywa hunena yaujazayo moyo” (Mathayo 12:34). Mtu anapozungumza maneno ya chuki, inaonyesha chuki imejaa moyoni mwake. Yesu pia alituambia hivi: “Kutoka ndani – moyoni mwa mtu – hutokea mawazo maovu, uasherati, wizi, mauaji, uzinzi, tamaa na uovu, pamoja na udanganyifu, ashiki, wivu, matukano, kiburi na upumbavu” (Marko 7:21-22). Mtu anapozini, tunajua kilicho moyoni mwake: ni uzinzi.

 

Kukua Kwa Kanisa

Sura Ya Tano

 

Kumbe wewe ni mchungaji na ungependa kanisa lako likue. Hiyo ni shauku ya kawaida kabisa kwa wachungaji. Lakini – kwa nini unataka kanisa lako likue? Sababu ya kweli ndani ya moyo wako ni nini?

Je, unataka kanisa likue ili ujisikie umefanikiwa? Je, unataka uheshimiwe na kuwa na ushawishi mkubwa? Je, unataka kuwa na mamlaka juu ya watu? Je, unatazamia kutajirika? Hizo zote ni sababu mbaya za kutaka kanisa lako likue.

Ukitaka kanisa lako likue ili Mungu atukuzwe kadiri watu wengi wanavyobadilishwa maishani kwa Roho Mtakatifu, basi hiyo ni sababu nzuri ya kutamani kukua kwa kanisa.

Inawezekana kujidanganya – kufikiri kwamba makusudi yetu ni safi na huku ni ya kimwili kabisa, tena ya kibinafsi.

Tunawezaje kujua ukweli wa makusudi yetu? Tunawezaje kujua kama kweli tunataka kujenga ufalme wa Mungu au kujenga ufalme wetu binafsi tu?

Njia moja ni kwa kufuatilia jinsi tunavyoitikia mafanikio ya wachungaji wengine. Kama tunafikiri makusudi yetu ni safi, kama tunafikiri kwamba kweli tunataka ufalme wa Mungu na kanisa Lake likue, lakini tukigundua wivu mioyoni mwetu tunaposikia juu ya kukua kwa makanisa mengine, hiyo inadhihirisha kwamba makusudi yetu si safi. Huonyesha kwamba kweli hatujali sana kukua kwa kanisa, bali tunajali kuhusu kukua kwa kanisa letu. Mbona iwe hivyo? Kwa sababu makusudi yetu yana kiasi fulani cha ubinafsi.

Pia tunaweza kukagua makusudi yetu kwa kupima itikio letu la ndani tunaposikia kwamba kanisa jipya limeanzishwa katika eneo letu. Tukijisikia kutishika, hiyo ni ishara kwamba tunajali zaidi kuhusu ufalme wetu kuliko ufalme wa Mungu.

Hata wachungaji wa makanisa makubwa au yanayokua wanaweza kukagua makusudi yao hivyo hivyo. Wanaweza kujiuliza maswali kama haya: “Je, ningekubali kuanzisha makanisa mapya kwa kuwatuma na kuwaachilia kabisa viongozi muhimu na watu wa kanisani kwangu, na kwa njia hiyo kupunguza idadi ya washirika wangu?” Mchungaji anayepinga sana wazo hilo bila shaka anajenga kanisa lake kwa ajili ya utukufu wake. (Kwa upande wa pili, mchungaji mwenye kanisa kubwa anaweza kuanzisha makanisa mapya kwa ajili ya utukufu wake pia, ili aweze kujigamba kuhusu idadi ya makanisa yaliyozaliwa na kanisa lake.) Swali lingine la kujiuliza ni hili: “Je, nina mahusiano na wachungaji wa makanisa madogo au nimejitenga nao, nikijiona kwamba niko juu kuliko wao?” Au hili: “Je, nitakuwa tayari kuwa mchungaji wa watu kumi na mbili hadi ishirini katika kanisa la nyumbani, au hiyo itaniathiri katika ubinafsi wangu?”[1]

Kikundi Cha Kukua Kwa Kanisa

Katika maduka ya vitabu vya Kikristo Marekani, Kanada na hata Afrika, utakuta sehemu moja nzima imejaa vitabu kuhusu ukuaji wa kanisa. Hivi vitabu na yaliyomo ndani yake vimeenea duniani kote. Wachungaji wana njaa ya kujifunza jinsi ya kuongeza wahudhuriaji katika makanisa yao, na mara nyingi ni wepesi kupokea ushauri wa wachungaji wa Kimarekani wenye makanisa makubwa, wanaodhaniwa kuwa wamefanikiwa kwa sababu ya ukubwa wa majengo yao na wingi wa watu wanaoabudu kwenye ibada zao siku za Jumapili.

Ila, wale wenye utambuzi kidogo hutambua kwamba ukubwa wa wahudhuriaji na jengo si alama ya ubora wa huduma ya kufanya watu kuwa wanafunzi. Makanisa mengine ya Marekani yamekua kwa sababu ya mafundisho yenye kuvutia, ambayo ni upotoshaji wa kweli za KiBiblia. Nimezungumza na wachungaji duniani kote ambao wameshtushwa kujua kwamba wachungaji wengi wa Kimarekani wanaamini na kuhubiri kwamba mtu akiisha okoka tu, hawezi kupoteza wokovu wake hata akiamini nini au akiishi vipi. Pia, wachungaji wengi wa Kimarekani huhubiri Injili iliyotiwa maji kuhusu neema isiyo na gharama, wakiwaongoza watu kudhani kwamba wanaweza kuingia mbinguni pasipo utakatifu. Kuna wengi pia wanaohubiri Injili ya mafanikio, wakichochea roho ya tamaa katika watu ambao dini ni njia ya kujipatia hazina zaidi za kujiwekea hapa duniani. Hao ni wachungaji ambao mbinu zao za ukuaji wa kanisa hazifai kuigwa.

Nimesoma kwa upana sana vitabu juu ya mada ya ukuaji wa kanisa, nami nashindwa kutoa uamuzi juu ya vitabu hivyo. Vingi vina mbinu na ushauri ambao kwa kiwango fulani ni wa KiBiblia, na hivyo vinafaa kusomwa. Lakini karibu vyote vina misingi kwenye taratibu za makanisa jengo – taratibu zenye umri wa miaka elfu na mia saba hivi – badala ya utaratibu wa KiBiblia. Basi, lengo lake si kuujenga mwili wa Kristo kwa kuwaongeza wanafunzi na wenye kufanya watu kuwa wanafunzi, bali ni kujenga makanisa jengo ya kipekee, ambayo kila mara yatahitaji majengo makubwa zaidi, watumishi wenye taaluma za hali ya juu pamoja na mipango aina hiyo, na mtiririko wa uongozi kama wa shirika badala ya familia.

Kuna mbinu za kisasa za ukuaji wa kanisa ambazo zinatosha ushauri kwamba, kwa ajili tu ya kupata washirika wengi, ibada ziwe za kuvutia kwa ajili ya watu wasiotaka kumfuata Yesu. Zinashauri kwamba kuwe na mahubiri mafupi, yasiyokuwa na maneno ya kuudhi, na ibada tulivu, na mambo mengi ya kijamii, na fedha zisitajwe, na kadhalika. Hii haisababishi kuzaa wanafunzi wanaojikana na kutii amri zote za Kristo. Husababisha watu wanaojiita Wakristo, wasioweza kutofautishwa na dunia, na ambao wanaelekea jehanamu kupitia barabara ile pana. Hiyo si mbinu ya Mungu ya kuwaleta watu Kwake bali ni ya Shetani ya kuliteka kanisa. Huo si “ukuaji wa kanisa” bali ni “ukuaji wa dunia”.

Mpango Wenye Kumjali Mtafutaji

Mbinu yenye kupendwa sana ya ukuaji wa kanisa huko Marekani huitwa mpango “wenye kumjali mtafutaji”. Katika mbinu hii, ibada za Jumapili asubuhi huandaliwa ili (1) Wakristo wajisikie huru kuwakaribisha rafiki zao ambao hawajaokoka, na (2) wasio-okoka wasikie Injili inayotumia maneno yasiyokwaza, wanayoweza kuyaelewa. Halafu, ibada za katikati na vikundi vidogo huwa maalum kwa ajili ya kuwafanya waamini kuwa wanafunzi.

Kwa kutumia mbinu hiyo, makanisa mengi sana yamekuwa makubwa. Katika makanisa ya Kimarekani, makanisa aina hii yanakuwa na uwezo mkubwa wa kufanya uinjilisti na kuwafanya watu kuwa wanafunzi, mradi kila mtu aingizwe katika kikundi kidogo (sivyo ilivyo lakini!) na kufundishwa. Pia, kama Injili haichujwi (na mara nyingi inachujwa, maana, Injili ya kweli inakwaza viburi vya watu). Basi, makanisa yenye mbinu hii ya kumjali mtafutaji yameweka mikakati fulani ya kuwafikia wasio-okoka, kitu ambacho makanisa mengine hayajafanya.

Ila sasa – mpango huo wa kumjali mtafutaji unafananaje na mfano wa KiBiblia wa ukuaji wa kanisa?

Katika kitabu cha Matendo utaona kwamba mitume na wainjilisti walioitwa na Mungu walihubiri Injili hadharani na nyumba hadi nyumba, na huduma zao ziliambatana na ishra na maajabu yaliyowavutia wasioamini. Waliotubu na kumwamini Bwana Yesu walidumu katika fundisho la mitume, na walikutana kila mara katika nyumba na kujifunza Neno la Mungu, kutumia karama za kiroho, kushiriki Meza ya Bwana, kuomba pamoja na kadhalika. Hayo yote yalikuwa chini ya uongozi wa wazee au wachungaji au waangalizi. Waalimu na manabii walioitwa na Mungu walitembea katika makanisa. Kila mmoja alimwambia jirani na rafiki yake Injili. Hayakuwepo majengo ya kujengwa ambayo yangepunguza kasi ya kukua kwa kanisa na kuiba rasilmali za ufalme wa Mungu ambazo zingesaidia kueneza Injili na kuwafanya watu kuwa wanafunzi. Viongozi walifundishwa haraka wakiwa kazini badala ya kutumwa waende vyuo vya Biblia. Hayo yote yalisababisha kukua haraka kwa kanisa katika kipindi fulani, mpaka watu wote katika eneo fulani waliokuwa tayari kupokea Neno walifikiwa.

Ukilinganisha na mpango wa makanisa yenye kumjali mtafutaji, tofauti ni kwamba huu hauna ishara na maajabu. Basi, hauna jinsi ya KiMungu ya kujitangaza, kuvutia na kushawishi. Hutegemea sana njia za kawaida za kujitangaza na kujiuza ili kuwavutia watu wafike kwenye jengo ili wasikie ujumbe. Ujuzi wa mhubiri kuzungumza na uwezo wake kushawishi ndiyo njia pekee za kuwafanya watu wavutwe. Hiyo ni tofauti sana na mbinu za Paulo, aliyeandika hivi: “Ujumbe wangu na mahubiri yangu havikuwa kwa maneno ya kushawishi yenye hekima, bali katika maonyesho ya Roho na nguvu, ili imani yetu isijengwe juu ya hekima ya wanadamu, bali juu ya nguvu za Mungu” (1Wakor. 2:4, 5 – TLR).

Tofauti Zingine

Mpango wa kumjali mtafutaji kwa kawaida hauna mitume na wainjilisti, kwa sababu kinara wa mpango huo ni mchungaji. Swali: Je, kuwaondoa mitume na wainjilisti kwenye nafasi zao za kushuhudia, na kuwapa wachungaji wajibu hizo ni njia nzuri ya kusaidia ukuaji wa kanisa?[2]

Mchungaji mwenye kumjali mtafutaji huhubiri mara moja kwa juma katika ibada ya Jumapili ambayo Wakristo wanatiwa moyo kuwaleta watua mbao hawajaokoka. Kwa hiyo – kimsingi – Injili inasikiwa mara moja tu kwa juma, na wale rafiki wasio-okoka wa washirika. Hao watu lazima wakubali kuja kanisa, nao ni lazima wakaribishwe na washirika ambao nao wamekubali kuwakaribisha kanisani. Katika mfano wa KiBiblia, mitume na wainjilisti hutangaza Injili daima hadharani na nyumba hadi nyumba, na waamini wote huwashirikisha Injili rafiki zao na jirani zao. Kama ni kuuliza – kwa habari ya mifumo hiyo miwili, ni upi unaofikisha Injili kwa wengi wasio-okoka?

Mpango wa kumjali mtafutaji unahitaji jengo linaloweza kukubalika – yaani, ambalo waamini hawalionei aibu na wanaweza kuwakaribisha rafiki zao wasio-okoka. Pia, liwe jengo ambalo hao wasio-okoka hawatapata shida kwenda huko. Hali hiyo daima inadai fedha nyingi tu. Kabla ya Injili “kuenezwa”, lazima jengo linalofaa lipatikane au lijengwe. Kwa habari ya Marekani, jengo hilo lazima liwe mahali pazuri, katika maeneo ya kitajiri. Lakini mfano wa KiBiblia hauhitaji jengo maalum, mahali maalum wala fedha. Kuenea kwa Injili hakufungwi na idadi ya watu wanaoweza kuingia katika jengo fulani siku za Jumapili.

Tofauti Zingine Tena

Ukilinganisha baadhi ya makanisa yenye kumjali mtafutaji na mfano wa KiBiblia, utaona tofauti zingine tena.

Mitume na wainjilisti katika kitabu cha Matendo waliwataka watu watubu, wamwamini Bwana Yesu na kubatizwa mara moja. Wakati wa kuokoka kwao, watu walitazamia kuwa wanafunzi wa Kristo, wenye kutimiza masharti yaliyotolewa na Yesu kuhusu uanafunzi, kama yanavyotajwa katika Luka 14:26-33 na Yohana 8:31-32. Walianza kumpenda Yesu kuliko vyote, kuishi katika Neno Lake, kujitwika misalaba yao na kuachilia mbali haki zote za kumiliki chochote. Wakawa mawakili wapya wa vitu ambavyo kuanzia wakati huo vilikuwa mali ya Mungu.

Mara nyingi, Injili yenye kuhubiriwa katika makanisa yenye kumjali mtafutaji ni tofauti. Wenye dhambi huambiwa jinsi Mungu anavyowapenda, jinsi anavyoweza kukutana nao katika mahitaji yao wanayosikia, na jinsi wanavyoweza kuokolewa kwa “kumkubali Yesu kama Mwokozi”. Baada ya kuomba sala fupi “ya wokovu”, na bila kuambiwa chochote juu ya kuhesabu gharama ya uanafunzi, mara nyingi wanahakikishiwa kwamba wameokoka kabisa na wanashawishiwa kujiunga na darasa ambalo ndani yake wanaweza kuanza kukua ndani ya Kristo. Wakijiunga na darasa hilo (maana wengi huwa hawarudi kanisani), mara nyingi wanapitia utaratibu wa kujifunza na kujua zaidi mafundisho ya kanisa hilo badala ya kufundishwa jinsi ya kuwa watiifu zaidi kwa amri za Kristo. Kilele cha mpango huo wa “uanafunzi” ni wakati mwamini anapoanza kutoa zaka ya mapato yake kanisani (ili kugharimia ujenzi wa kanisa na mishahara ya watumishi ambao si wa KiBiblia – uwakili mbaya tu maana unasaidia vitu vingi ambavyo havijaamriwa na Mungu, na kuacha kusaidia vile ambavyo Mungu ameamuru). Halafu anaongozwa kuamini kwamba amegundua “huduma yake” anapoanza kufanya shughuli fulani katika kanisa, isiyotajwa na Maandiko.

Hebu fikiri kidogo: Ingekuwaje kama serikali yenu – kwa kujali kwamba watu wanaojiunga na jeshi si wengi – ingeamua “kumjali mtafutaji”? Tudhanie kuwa watatoa ahadi kwa wote wanaotaka kujiunga nao, kwamba hakuna chochote kinachotazamiwa kutoka kwao – watalipwa mishahara yao kama zawadi, bila kufanyia kazi, bila kustahili. Wawaambie kwamba wanaweza kuamka saa yoyote wanayotaka asubuhi. Wakipenda kufanya kwata, sawa, lakini wakitaka kutazama televisheni ni sawa pia. Vita ikitokea, wako huru kuamua kama wanataka kwenda kupigana au kwenda kuogelea. Kungekuwa na matokeo gani?

Bila shaka jeshi lingejaa watu! Lakini, lisingekuwa jeshi tena maana lisingefaa kwa kazi yake. Na ndivyo yalivyo makanisa yenye kumjali mtafutaji. Kushusha viwango huongeza mahudhurio ya Jumapii, lakini hupunguza uanafunzi na utii. Makanisa yenye kumjali mtafutaji yatakayojaribu “kuhubiri Injili” siku za Jumapili na “kufanya uanafunzi” katika ibada za katikati ya juma yatagundua kwamba yana shida baada ya kuwaambia watu kwamba ni wanafunzi wa Yesu tu ndiyo wanaokwenda mbinguni. Watu wataanza kujisikia kwamba huwa wanadanganywa Jumapili asubuhi. Basi, makanisa aina hiyo lazima yawadanganye watu katika ibada za katikati ya juma pia, kwa kuwaambia kwamba uanafunzi na utii ni vitu vya hiari – si masharti kwa watu wanaokwenda mbinguni.[3]

Naelewa vizuri sana kwamba kuna makanisa jengo yenye kuchanganya baadhi ya mambo ya KiBiblia, na makanisa mengine hayafanyi hata kidogo. Pamoja na hayo – ukweli ni kwamba mfano wa KiBiblia ndiyo unaofaa zaidi katika kuongeza idadi ya wanafunzi na ya wenye kufanya wengine kuwa wanafunzi.

Sasa – mbona mfano wa KiBiblia haufuatwi siku hizi? Hoja zinazotolewa kujitetea hazina mwisho, lakini, sababu ya kutofuata mfano wa KiBiblia ni mapokeo, kutokuamini na kutokutii. Wengi wanasema kwamba mfano wa KiBiblia hauwezekani katika dunia yetu ya kisasa. Lakini – kwa mfano – kulipuka kwa ukuaji wa kanisa huko Uchina katika miaka 50 iliyopita ni kwa sababu waamini walifuata huo mfano wa KiBiblia! Je, Mungu huko Uchina yuko tofauti na mahali pengine?

Hayo yote ni ili kusema hivi: Wachungaji ambao si WaMarekani wajihadhari na mbinu za ukuaji kanisa za KiMarekani, zinazoenezwa duniani kote. Mtafanikiwa zaidi mkiwa na nia ya kutimiza lengo la Kristo la kufanya watu kuwa wanafunzi, kama mtafuta mfano wa KiBiblia wa ukuaji wa kanisa.

Hatima

Mimi nimegundua pia kwamba wengi wanaotetea na kufundisha mbinu za kisasa za ukuaji wa kanisa hawajui jinsi mchungaji wa kawaida duniani alivyo. Idadi kubwa ya wachungaji duniani huchunga makundi yenye watu wasiozidi mia moja. Wachungaji wengi kati ya hao huvunjika moyo baada ya kujaribu mbinu za ukuaji wa kanisa ambazo hazifanyi kazi, au zinazokwama kwa sababu ambazo wao hawahusiki nazo. Hakuna aliye tayari kukubali kwamba kuna mambo kadhaa yaliyo nje ya uwezo wa wachungaji, yenye kuzuia ukuaji wa makanisa yao. Hebu tutazame baadhi ya mambo hayo.

Kwanza kabisa: Ukuaji wa kanisa hutawaliwa na idadi ya wakazi wa mahali kanisa lilipo. Ni dhahiri kwamba makanisa mengi yenye majengo makubwa yanapatikana katika maeneo ya miji yenye watu wengi sana. Mara nyingi miji hiyo itakuwa na mamilioni ya wakazi – na washirika hupatikana humo. Lakini, kama idadi tu ndiyo kipimo cha mafanikio, basi kanisa linapaswa kupimwa – si kwa ukubwa wake – bali kwa idadi ya wakazi wa mahali pale walioko kanisani. Kwa msingi huo utagundua kwamba makanisa mengine yenye watu kumi yamefanikiwa zaidi ya makanisa mengine yenye watu elfu kumi. Kanisa lenye washirika kumi katika kijiji chenye watu hamsini limefanikiwa sana kuliko kanisa lenye watu elfu kumi katika mji wenye watu milioni tano. (Lakini – wachungaji hao wenye watu kumi hawatakaribishwa hata siku moja kusema kitu kwenye kongamano la ukuaji wa kanisa!)

Kizuizi Cha Pili Kwa Ukuaji Wa Kanisa

Pili: Kukua kwa kanisa hutawaliwa kwa kiwango cha kuenezwa Injili kati ya watu walio tayari kupokea kunakofanywa na makanisa yote katika eneo husika. Ni hivi: Kila wakati, kuna idadi fulani tu ya watu katika eneo ambao mioyo yao iko wazi kwa Injili. Hao wakiisha fikiwa wote, hakuna kanisa litakalokua – labda kama watu wengine ambao ni washirika tayari watahamia kanisa lingine. (Hivyo ndivyo makanisa mengi makubwa yalivyokua – kwa gharama ya makanisa mengine katika mikoa au majimbo yao.)

Ni kweli kwamba kila Mkristo wa sasa hakuwa mpokeaji wa Injili wakati fulani, ila kwa ushawishi wa Roho Mtakatifu aliweza kupokea. Basi, inawezekana kabisa kwamba wale watu ambao kwa wakati huu hawapokei, watapokea wakati fulani. Hilo litakapotokea, makanisa yanaweza kukua. Kile ambacho mara nyingi tunakiita “uamsho” hutokea wakati wengi wasiokuwa tayari kupokea Injili mara huipokea. Ila tusisahau kwamba hata mtu mmoja anapopokea Injili ni uamsho pia, japo mdogo. Kila uamsho mkubwa huanza kwa mtu mmoja kuwa msikivu na kupokea. Basi mchungaji – usidharau siku za mianzo midogo.

Yesu aliwatuma wanafunzi Wake kuhubiri Injili katika miji aliyojua haitapokea – ambapo hakuna hata mtu mmoja angetubu (tazama Luka 9:5). Lakini bado Yesu aliwatuma wakahubiri huko. Je, hao wanafunzi hawakufanikiwa? Hatuwezi kusema hivyo, japo hawakupata washirika (na kanisa halikukua). Walifanikiwa kwa sababu walimtii Yesu.

Vivyo hivyo Yesu bado anatuma wachungaji waende vijijini, mijini na katika viunga vya miji – mahali anapojua kwamba idadi ndogo tu ya watu ndiyo itakayopokea Injili. Hao wachungaji wanaohudumia makundi yao madogo kwa uaminifu wamefanikiwa mbele za Mungu, japo wanaweza kuonekana wameshindwa machoni pa ‘wataalamu’ wengine wa kukua kwa kanisa.

Wachungaji wote katika kila eneo wanapaswa watiwe moyo na ukweli kwamba, kwa sababu ya rehema za Mungu zilizo nyingi, na katika kujibu maombezi ya watu Wake, yuko kazini ili kuwafanya watu wasiopokea waweze kupokea. Anajitahidi kuwashawishi wasio-okoka kwa dhamiri zao, uumbaji Wake, mazingira, huku Zake za muda, ushuhuda hai wa kanisa Lake, kuhubiriwa kwa Injili na kujisikia hatia kunakoletwa na Roho Mtakatifu. Hivyo mchungaji – jipe moyo. Endelea kutii, kuomba na kuhubiri. Kabla ya kila uamsho mkubwa kwanza huwepo haja kubwa ya uamsho. Na siku zote yupo mtu ambaye anaota kuhusu uamsho. Endelea kuota!

Kizuizi Cha Tatu Kwa Ukuaji Wa Kanisa

Kitu cha tatu kinachozuia ukuaji wa makanisa ni uwezo wa mchungaji. Wachungaji wengi hawana ule ujuzi unaotakiwa kusimamia kusanyiko kubwa, na si kosa lao. Ni kwamba hawana karama za usimamizi, utawala au kuhubiri na kufundisha, zinazotakiwa kwa ajili ya kusanyiko kubwa. Ni dhahiri basi kwamba wachungaji kama hao hawajaitwa na Mungu kuchunga makanisa makubwa, nao watakosea sana wakijaribu kuchunga kanisa linalozidi wastani – liwe kanisa jengo au la nyumbani.

Hivi karibuni tu nilisoma kitabu kinachopendwa sana kuhusu uongozi, kilichoandikwa na mchungaji mmoja kiongozi wa kanisa moja kubwa sana Marekani. Niliposoma ushauri wake kwa wachungaji wa kisasa, uliojaa kurasa zenye kueleza ujuzi wake, niliwaza hivi: “Hasemi chochote hapa juu ya jinsi ya kuwa mchungaji – anatuambia jinsi ya kuwa mkurugenzi mkuu wa shirika kubwa.” Na mchungaji kiongozi wa kanisa kubwa la KiMarekani hakuna uchaguzi mwingine. Anahitaji kundi kubwa la wasaidizi, na kuwasimamia hao ni kazi ya wakati wote. Mwandishi wa kitabu nilichosoma alikuwa na ujuzi wa kutosha kuwa mkurugenzi mkuu wa shirika kubwa la kidunia. (Katika kitabu chake alinukuu maneno ya mabingwa wa kushauri kuhusu usimamizi, akitoa ushauri wao kwa wachungaji wenzake watakaosoma kitabu hicho.) Lakini wasomaji wake wengi – kama si wote – hawana ujuzi huo wa uongozi na utawala kama alio nayo yeye.

Katika kitabu hicho hicho, mwandishi alieleza wazi jinsi ambavyo mara kadhaa katika kujenga kundi lake kubwa, alifanya makosa yaliyokuwa hatari sana – makosa ambayo yangemgharimu familia yake au kuendelea kwake kufanya huduma baadaye. Kwa neema ya Mungu akapona. Lakini, mambo aliyopitia yalinikumbusha mifano mingi ya wachungaji kama yeye ambao, wakifukuzia mafanikio ya aina hiyo, walifanya makosa hayo hayo na kuharibikiwa kabisa. Wengine – kwa sababu ya kujikita makanisani mwao – walipoteza watoto wao au kuharibu ndoa zao. Wengine walipata matatizo kiakili au walimalizika kihuduma. Wengine walichanganyikiwa kiasi cha kufikia kuacha huduma moja kwa moja. Wengine walipona – hivyo tu. Wanaendelea na maisha lakini katika hali ya wasiwasi mkubwa, wakijiuliza ikiwa dhabihu waliyotoa – isiyokuwa ya kawaida – ilistahili yote waliyopata.

Niliposoma kitabu hicho, nilizidi kuona hekima ya kanisa la kwanza, ambalo halikuwa na mfumo unaofanana na makanisa ya siku hizi. Hakuna mchungaji aliyewajibika kusimamia kundi lililozidi watu ishirini na tano au zaidi. Kama nilivyosema katika sura iliyotangulia – wachungaji wengi wanaofikiri kwamba makanisa yao ni madogo wanapaswa kutazama upya huduma zao kulingana na Maandiko. Kama wana watu hamsini, pengine makanisa yao ni makubwa sana. Ikiwa wana viongozi wenye uwezo, ni vizuri waombe kisha wafikiri kugawa kanisa hilo liwe makanisa matatu ya nyumbani, wauze jengo lao, na wawe na lengo la kuwafanya watu kuwa wanafunzi na kuujenga ufalme wa Mungu kwa njia ya Mungu.

Kama hili litaonekana la tofauti sana, basi waanze kuwafanya wanafunzi watakaokuwa viongozi wa baadaye, au waanzishe vikundi vidogo, au kama wanavyo tayari, wavifungue vingine ili kuwa makanisa huru ya nyumbani, waone kitakachotokea.

Mbinu Zingine Za Kisasa Za Ukuaji Wa Kanisa

Zipo mbinu zingine zinazopigiwa debe siku hizi kwamba ni za muhimu sana kwa ajili ya kukua kwa kanisa, zaidi ya mpango ule wa kanisa lenye kumjali mtafutaji. Nyingi katika mbinu hizo si za KiBiblia, nazo zinaangukia katika swala la “vita vya kiroho”. Hutangazwa kwa maneno kama: “kuvunja ngome”, au “maombi ya mapambano” au wakati mwingine, “uchoraji ramani wa kiroho”.

Katika sura ya baadaye tutazama mambo hayo ya vita vya kiroho. Pengine tujiulize – kwa kifupi – kwa nini mambo hayo ambayo hayakujulikana kabisa na mitume yahesabiwe kuwa ya lazima sana kwa ajili ya kukua kwa kanisa siku hizi.

Nyingi ya hizo mbinu mpya za kukua kwa kanisa ni matokeo ya ujuzi wa wachungaji wachache wanaosema hivi: “Mimi nilifanya hivi na vile, na kanisa langu likakua. Na wewe ukifanya hivyo hivyo, kanisa lako litakua pia.” Ukweli ni kwamba, kukua kwa kanisa hilo hakukutokana na hayo mambo ya ajabu waliyofanya, japo wao walidhani hivyo. Hii huthibitika mara kwa mara wakati wachungaji wengine wanapofuata mafundisho hayo ya kipekee na kufanya mambo yale yale. Makanisa yao hayakui hata kidogo.

Mchungaji wa kukua kwa kanisa anaweza kusikika akisema hivi: “Tulipoanza kuwapigia kelele mapepo walio juu ya mji wetu, uamsho ulitokea kanisani kwetu. Wewe pia inabidi uwapigie kelele hao mapepo ukitaka uamsho uje kanisani mwako.”

Lakini – mbona kumekuwa na uamsho mzuri tu duniani kote katika miaka elfu mbili iliyopita ya historia ya Ukristo bila ya kuwepo kwa yeyote aliyewapigia kelele mapepo juu ya miji? Hiyo inaonyesha kwamba, hata ingawa mchungaji yule alidhani uamsho ulitokana na kupigia mapepo kelele, haikuwa hivyo. Sana sana ni kwamba watu katika mji wake walianza kuwa wasikivu kwa Injili – labda kwa sababu ya maombi ya mshikamano kanisani, naye akawepo kuhubiri Injili watu walipoanza kupokea. Mara nyingi sana, kukua kwa kanisa ni matokeo ya kuwa mahali panapotakiwa kwa wakati unaotakiwa. (Na Roho Mtakatifu hutusaidia kuwepo mahali panapotakiwa kwa nyakati zinazotakiwa.)

Kama kupigia kelele mapepo katika mji kulileta uamsho kanisani kwa mchungaji fulani, mbona baada ya kipindi fulani uamsho ulipungua kisha ukakoma, kama inavyokuwa? Ikiwa ufunguo ni kuwapigia kelele mapepo, basi ni kwamba tukiendelea tu kupiga kelele hizo kila mtu mjini humo atamfuata Kristo. Lakini haiwi hivyo.

Ukweli utadhihirika tukifikiri kidogo. Njia ya pekee ya KiBiblia ya kanisa kukua ni maombi, mahubiri, kufundisha, kufanya watu kuwa wanafunzi, msaada wa Roho Mtakatifu, na kadhalika. Na hata hizo njia za KiBiblia hazihakikishi ukuaji wa kanisa kwa sababu Mungu amewaumba watu kuwa viumbe wenye uchaguzi na hiari. Wanaweza kuamua kutubu au kutotubu. Inawezekana kusema kwamba hata Yesu alishindwa katika swala la ukuaji wa kanisa nyakati fulani wakati miji aliyoitembelea ilipokataa kupokea ujumbe wake na kutubu.

Hayo yote maana yake ni hii: Tunahitaji kutumia njia za KiBiblia ili kulijenga kanisa. Kingine chochote ni kupoteza muda. Kuna kazi ambazo ni mbao, majani na manyasi ambazo siku moja zitachomwa na moto na kutopata thawabu (1Wakor. 3:12-15).

Mwisho: Lengo lisiwe kuongezeka idadi tu, bali kuwafanya watu kuwa wanafunzi. Kama kanisa linakua tunapofanya watu kuwa wanafunzi, basi Mungu asifiwe!

Yaliyomo | Sura Iliyopita | Sura Ifuatayo | Mwanzo wa Ukurasa | Pa Kuanzia


[1] Faida nyingine ya kanisa la nyumbani ni hii: wachungaji hawashindani ili kuwa na washirika wengi kwa sababu zisizofaa, maana ukubwa wa kanisa unatawaliwa na ukubwa wa nyumba.

[2] Hii ndiyo sababu kubwa ya siku za leo kuwa na wainjilisti wengi, waalimu, manabii na hata mitume wakifanya kazi ya uchungaji. Huduma nyingi zitokazo kwa Mungu hazipewi nafasi yake – au nafasi kabisa – katika mfumo wa kanisa wa kisasa. Hiyo hupelekea watumishi wengi ambao si wachungaji kuchunga makanisa. Hilo huibia kanisa baraka kubwa ambazo zingepatikana kwa mwili wa Kristo katika mfumo wa KiBiblia. Imefikia mahali ambapo kila mtu ameamua kujenga ufalme wake kwa habari ya kuwa na kanisa, bila kujali wito wake halisi. Kwa kuwa wachungaji wanadaiwa kuwa na haki ya zaka za “watu wao”, na kwa kuwa sehemu kubwa ya hizo inaingia kwenye ujenzi na utunzaji wa majengo, watumishi ambao si wachungaji huingia kwenye kuchunga makanisa ili wapate fedha za kufanya huduma waliyoitiwa.

 

[3] Kumbuka kwamba masharti aliyo-orodhesha Yesu kwa wanafunzi Wake wa kweli katika Luka 14:26-33 hayakusemwa kwa watu waliokuwa waamini tayari, kana kwamba anawapa uchaguzi wa kupiga hatua ya pili katika safari yao ya kiroho. Alikuwa anazungumza na makundi ya watu. Hatua ya pekee ya kwanza aliyotoa Yesu ni mtu kuwa mwanafunzi Wake, ambayo si kitu kingine, ni wokovu. Hayo ni tofauti kabisa na mambo yanayofundishwa katika makanisa yenye kumjali mtafutaji.

 

Huduma Ya Kufundisha

Sura Ya Sita

 

Katika sura hii tutatazama sehemu nyingi za huduma ya kufundisha. Kufundisha ni wajibu wa mitume, manabii, wainjilisti,[1] wachungaji/wazee/waangalizi, waalimu (ndiyo kabisa!), na kwa kiwango fulani, wafuasi wote wa Kristo. Maana sisi sote tunatakiwa kuwa katika kufanya watu kuwa wanafunzi, tukiwafundisha wanafunzi wetu kutii yote aliyoagiza Kristo.[2]

Kama nilivyokwisha kazia hapo nyuma, mchungaji – au mtumishi – anayefanya watu kuwa wanafunzi kwanza hufundisha kwa mfano wa maisha yake, kisha kwa maneno. Anahubiri anachokitenda. Mtume Paulo ambaye alifaulu sana katika kufanya watu kuwa wanafunzi, aliandika hivi:

Niigeni mimi, kama na mimi ninavyomwiga Kristo (1Wakor. 11:1 – TLR).

Hilo linapaswa kuwa lengo la kila mtumishi – kuweza kusema ukweli kwa wale anaowaongoza: “Fanyeni kama mimi. Mkitaka kujua jinsi mfuasi wa Kristo anavyoishi, nitazameni mimi.”

Nikitazama nyuma, nakumbuka nikiwaambia washirika wangu zamani: “Msinifuate mimi … mfuateni Kristo!” Japo halikuniingia wakati huo, nilichofanya ni kukiri kwamba mimi sikuwa mfano mzuri wa kufuata. Ukweli ni kwamba, nilikuwa nakiri kwamba sikuwa namfuata Kristo inavyotakiwa, kisha ninawaambia wengine wote kufanya kitu ambacho mimi sikuwa nakifanya! Hiyo ilikuwa tofauti kabisa na jinsi Paulo alivyosema. Ni hivi: Kama hatuwezi kuwaambia watu watuige kwa sababu na sisi tunamwiga Kristo, hatupaswi kuwa katika huduma. Kwa sababu, watu huwatumia watumishi kama mifano ya kuiga katika maisha yao. Kanisa ni onyesho la viongozi wake.

Kufundisha Umoja Kwa Njia Ya Mfano

Hebu tuonyeshe kanuni hii ya kufundisha kwa njia ya mfano kuhusu mada moja muhimu sana: umoja. Wachungaji wote au wazee au waangalizi wanatamani kwamba makundi wanayoyaongoza yawe na umoja. Wanachukia migawanyiko katika makundi yao. Wanajua kwamba migawanyiko inamchukiza Bwana. Yesu alituamuru tupendane sisi kwa sisi kama Yeye alivyotupenda (ona Yohana 13:34-35). Kupendana kwetu sisi kwa sisi ndicho kinachotujulisha kuwa wanafunzi Wake kwa dunia inayotutazama. Kwa kuwa ni hivyo, viongozi wengi wa makundi huwashauri kondoo wao kupendana, na kutafuta sana umoja.

Lakini – kama watumishi tunaopaswa kufundisha kwanza kwa mfano wetu wenyewe, sisi mara nyingi tunapungua sana katika mafundisho yetu kuhusu upendo na umoja, kwa jinsi tunavyoishi. Kwa mfano: Wakati sisi tunapo-onyesha kutokuwa na upendo na umoja na wachungaji wengine, tunapeleka ujumbe ambao ni kinyume cha kile tunachohubiri kwa washirika wetu. Tunawatazamia wafanye kitu ambacho sisi hatufanyi.

Ukweli ni kwamba: Maneno muhimu sana ambayo Yesu alizungumza kuhusu umoja, aliyasema kwa viongozi juu ya mahusiano yao na viongozi wengine. Mfano: Wakati wa Chakula cha Mwisho baada ya kuwanawisha wanafunzi Wake miguu, Yesu aliwaambia hivi:

Mnaniita Mwalimu na Bwana. Ni sawa, maana ndivyo nilivyo. Kama mimi, Bwana na Mwalimu, nimewasafisha miguu yenu, ninyi pia mnatakiwa kusafishana miguu. Maana nimewapa mfano ili mfanye kama nilivyowafanyia (Yohana 13:13-15. TLR) [Hebu jionee mwenyewe: Yesu alifundisha kwa mfano.]

Mara nyingi wachungaji hutumia mstari huo kuwafundisha watu wao juu ya kupendana. Ni sawa kabisa. Ila, maneno ya fungu hili yalitolewa kwa viongozi – wale mitume kumi na mbili. Yesu alijua kwamba kanisa Lake la baadaye lisingekuwa na matumaini ya kufanikiwa katika utume wake kama viongozi wake wangekuwa wamegawanyika, au kama wangeshindana wao kwa wao. Basi akaweka wazi kabisa kwamba anatazamia viongozi Wake wahudumiane kwa unyenyekevu.

Kulingana na utamaduni wa siku alizokuwa hapa duniani, Yesu alionyesha unyenyekevu katika huduma kwa kufanya kazi ya chini sana iliyofanywa na mtumishi wa nyumbani – kunawisha watu miguu. Kama angetembelea utamaduni mwingine katika wakati tofauti kihistoria, pengine angechimba vyoo au kusafisha mapipa ya takataka ya wanafunzi Wake. Je, ni wangapi katika viongozi Wake wa kisasa walio tayari kuonyesha aina hiyo ya upendo na unyenyekevu kwa wenzao?

Baada ya muda usiozidi saa moja, Yesu alirudia kutilia mkazo ujumbe huo muhimu sana. Dakika chache tu baada ya kuwanawisha miguu yao, Yesu aliwaambia hivi viongozi Wake wa kanisa la baadaye:

Nawapa amri mpya kwamba mpendane. Kama mimi nilivyowapenda ninyi, ninyi nanyi pendaneni. Kwa hilo, watu wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkipendana (Yohana 13:34-35. TLR).

Hayo maneno kweli yanawafaa wanafunzi wote wa Kristo, lakini yalizungumzwa hasa kwa viongozi kwa habari ya mahusiano yao na viongozi wenzao.

Dakika chache baadaye, Yesu akasema tena, hivi:

Amri yangu ni hii, kwamba mpendane ninyi kwa ninyi, kama ambavyo mimi nimewapenda. Hakuna mwenye upendo mkuu kuliko huu, kwamba mtu atoe uhai wake kwa ajili ya rafiki zake (Yohana 15:12-13. TLR).

Ona tena kwamba Yesu alikuwa anazungumza na viongozi.

Baada ya nukta chache alisema hivi tena:

Ninawaamuru hivi: pendaneni ninyi kwa ninyi (Yohana 15:17).

Dakika chache baadaye, wanafunzi wa Yesu wakamsikia akiwaombea.

Mimi siko tena duniani, ila wao wapo, nami nakuja kwako. Baba Mtakatifu, walinde katika jina Lako, jina lile ulilonipa, ili wawe na umoja, kama sisi tulivyo (Yohana 17:11, TLR. Maneno mepesi kukazia).

Mwishowe, nukta chache tu baadaye alipoendelea na maombi Yake, wanafunzi walimsikia Yesu akisema hivi:

Siombi kwa ajili ya hawa tu, bali hata kwa ajili ya watakaoniamini

kupitia neno lao. Kwamba wote wawe na umoja; kama ambavyo Wewe Baba, ulivyo ndani Yangu, nami ndani Yako, na wao wawe ndani Yetu, ili dunia ipate kuamini kwamba ulinituma. Na utukufu ule ulionipa, nimewapa wao, ili wawe na umoja, kama sisi tulivyo. Mimi ndani yao, na Wewe ndani Yangu, wapate kukamilishwa katika umoja, ili dunia ijue kwamba ulinituma, na kwamba unawapenda, kama ulivyonipenda mimi (Yohana 17:20-23. TLR – maneno mepesi kukazia).

Basi – katika kipindi kisichozidi saa moja, Yesu mara sita alikazia kwa viongozi Wake wa baadaye umuhimu wa wao kuwa na umoja na kuonyesha umoja wao kwa kupendana na kuhudumiana kwa unyenyekevu sana. Bila shaka jambo hili lilikuwa la muhimu sana kwa Yesu. Umoja wao ulikuwa kitu cha msingi katika dunia kumwamini Yeye.

Tunaendeleaje Mpaka Sasa?

Kwa bahati mbaya sana – tunapotazamia makundi yetu yaungane kwa upendo – wengi wetu tunashindana na kutumia njia ambazo si halali kuyakuza makanisa yetu kwa gharama ya mengine. Wengi wetu tunaepuka kushirikiana na wachungaji wowote ambao mafundisho yao ni tofauti na yetu. Hata tunatangaza kutokuwa na umoja kwetu kwa njia ya vibao tunavyoweka mbele ya makanisa yetu ili dunia ivione, tukipeleka ujumbe huu kwa kila mtu: “Sisi si kama wale Wakristo wengine katika makanisa mengine”. (Na tumefaulu sana kuelimisha dunia kuhusu kutokuwa na umoja kwetu, maana wasioamini wengi wanajua Ukristo ni dini iliyogawanyika sana.)

Kwa kifupi ni hivi: hatutendi tunayohubiri, na mifano ya maisha yetu huwafundisha watu wetu mengi kuliko mahubiri yetu ya umoja. Ni upumbavu kufikiri kwamba Wakristo wa kawaida wataungana na kupendana wakati viongozi wao wanafanya kinyume.

Ufumbuzi wa pekee ni toba. Lazima tutubu kwa kuwa mifano mibaya mbele ya waamini na mbele ya dunia. Lazima tuondoe kuta zinazotugawa na tuanze kupendana kama Yesu alivyoagiza.

Maana yake ni kwamba – kwanza kabisa: Tukutane na wachungaji wengine na watumishi ambao wanafuata mafundisho tofauti na yetu. Hapa sisemi tuwe na ushirika na wachungaji ambao hawajaokoka, ambao hawana juhudi yoyote katika kumtii Yesu, au ambao wanafanya huduma kwa faida zao binafsi. Hao ni mbwa mwitu waliovaa ngozi ya kondoo, na Yesu alituambia jinsi ya kuwagundua. Wanajulikana kwa matunda yao.

Ila ninazungumza juu ya wachungaji na watumishi wanaojitahidi kushika amri za Yesu – ndugu na dada kweli katika Kristo. Kama wewe ni mchungaji, unatakiwa kujitoa kuwapenda wachungaji wengine, na kuonyesha upendo huo kwa njia za vitendo mbele ya kundi lako. Njia moja ni kwa kuanza kuwaendea wachungaji wengine katika eneo lako na kuwaomba msamaha kwa kutowapenda kama inavyotakiwa. Tendo hilo litavunja kuta. Kisha, jitoe kukutana nao mara kwa mara ili kula chakula pamoja, kutiana moyo, kushauriana na kuomba pamoja. Hayo yatakapotokea, itawezekana hata kuzungumza na kujadili kwa upendo yale mafundisho yanayowatenganisha, na hatimaye kutafuta kuwa na umoja – mwe mmekubaliana au bado juu ya kila mtakachozungumza. Maisha yangu na huduma vilitajirishwa sana nilipokuwa tayari kuwasikiliza wachungaji waliokuwa na itikadi tofauti na kambi yetu. Kwa kujifungia nilikuwa nakosa baraka nyingi sana kwa miaka mingi sana.

Unaweza pia kuonyesha upendo wako na umoja kwa kuwakaribisha wachungaji wengine waje kuhubiri kanisani kwako au katika makanisa ya nyumbani, au mnaweza kuunganisha ibada na hayo makanisa, mkafanya ibada ya pamoja.

Unaweza pia kubadilisha jina la kanisa lako ili lisitangazie dunia kwamba huna umoja na wengine katika mwili wa Kristo. Unaweza kutoka katika dhehebu lako au shirika unalohusiana nalo na ukajitambulisha na mwili wa Kristo tu, kwa njia hiyo kutuma ujumbe kwa kila mtu kwamba unaamini kwamba Yesu anajenga kanisa moja tu, sio makanisa mengi tofauti yasiyoweza kushirikiana.

Najua hilo linasikika kuwa gumu. Lakini, kwa nini ufanye kitu chochote kuendeleza yale ambayo Yesu hakukusudia? Mbona kujihusisha na kitu chochote kinachomchukiza? Hakuna madhehebu wala miungano maalum inayotajwa katika Maandiko. Wakorintho walipogawanyika juu ya waalimu waliowapenda, Paulo aliwakemea sana, akisema migawanyiko yao ilidhihirisha kwamba wao ni watu wa kimwili na ni wachanga kiroho (ona 1Wakor. 3:1-7). Je, migawanyiko yetu sisi inadhihirisha kitu kingine tofauti na hicho?

Chochote kinachotutenganisha kiepukwe. Makanisa ya nyumbani yanatakiwa kujiepusha kujipa majina au kujiunga na mashirika yoyote yenye majina. Katika Maandiko, makanisa yalijulikana kwa nyumba waliyokutania. Muungano wa makanisa mahali ulijulikana kwa miji yaliyokuwemo. Yote yalijihesabu kuwa sehemu ya kanisa moja tu – Mwili wa Kristo.

Kuna Mfalme mmoja tu na ufalme mmoja tu. Yeyote ajiinuaye ili waamini au makanisa yajitambulishe naye anajenga ufalme wake mwenyewe ndani ya ufalme wa Mungu. Ni afadhali awe tayari kusimama mbele za Mfalme anayesema hivi: “Sitampa mwingine utukufu wangu” (Isaya 48:11).

Hayo yote ni ili tuseme hivi: Watumishi wanatakiwa kuonyesha mfano mzuri wa kumtii Kristo mbele ya watu wote, kwa sababu watu watafuata mfano wao. Jinsi wanavyoishi mbele ya wengine ndiyo njia kuu yenye ushawishi ya kufundisha. Paulo aliwaandikia hivi waamini wa Filipi:-

Ndugu, jiungeni katika kufuata mfano wangu, na mwatazame kwa makini wale wanaoenenda kulingana na mfano mlioona kwetu (Wafilipi 3:17 – TLR. Maneno mepesi kukazia).

Cha Kufundisha

Mtumishi mwenye kufanya wengine kuwa wanafunzi ana lengo, sawa tu na Paulo. Lengo hilo ni “kumfikisha kila mmoja akiwa mkamilifu katika Kristo” (Wakolosai 1:28b). Basi, yeye naye, sawa na Paulo, ata”mwonya kila mtu na kumfundisha kwa hekima yote” (Wakolosai 1:28a – TLR. Maneno mepesi kukazia). Ona kwamba Paulo hakufundisha ili kuwaelimisha watu tu au kuwastarehesha.

Mtumishi mwenye kufanya wengine kuwa wanafunzi anaweza kusema na Paulo:- “Lengo la mafundisho yetu ni upendo utokao katika moyo wa kweli, na dhamiri safi, na imani ya dhati” (1Timo. 1:5 – TLR). Yaani, anachotaka ni kusababisha hali ya kufanana kweli na Kristo, na utakatifu katika maisha ya watu anaowahudumia. Ndiyo sababu anawafundisha waamini kuzitii amri zote za Kristo. Anafundisha ukweli, akiwashauri wasikilizaji wake kutafuta “kwa bidii amani na watu wote, na utakaso [au utakatifu] ambao bila huo hakuna mtu atakayemwona Bwana” (Waebrania 12:14 – TLR).

Mtumishi mwenye kufanya watu kuwa wanafunzi anajua kwamba Yesu aliwaagiza wanafunzi Wake wawafundishe wanafunzi wao kutii yote, wala si sehemu tu ya maagizo Yake (tazama Mathayo 28:19-20). Anataka kuhakikisha kwamba hataacha kufundisha chochote kilichoagizwa na Kristo, kwa hiyo, anafundisha Injili na Nyaraka zote mstari kwa mstari, mara kwa mara. Maagizo ya Yesu yameandikwa humo na kutilia mkazo pia.

Mafundisho hayo ya kufafanua pia huhakikisha kwamba yatakuwa na mlingano. Tunapofundisha jumbe zenye kulenga mada fulani tu, inakuwa rahisi kujali mada zinazopendwa na watu na kupuuza zile zisizopendwa sana. Mwalimu anayefundisha mstari kwa mstari hatafundisha juu ya pendo la Mungu tu, bali pia juu ya adhabu na hasira Yake. Hatafundisha tu juu ya baraka za kuwa Mkristo, bali pia juu ya wajibu au majukumu ya Mkristo. Hatatilia mkazo mambo madogo na kupuuza mambo ya muhimu zaidi. (Hilo ndilo kosa walilofanya Mafarisayo, kulingana na Yesu – ona Mathayo 23:23-24).

Kushinda Hofu Za Mafundisho Ya Kufafanua

Wachungaji wengi wanaogopa kufundisha mstari kwa mstari kwa sababu kuna mengi wasiyoelewa katika Maandiko, na hawataki washirika wao wajue kwamba hawajui! Hayo ni majivuno. Hakuna mtu yeyote duniani anayeelewa kikamilifu kabisa kila kitu katika Maandiko. Hata Petro alisema kwamba baadhi ya mambo aliyoandika Paulo yalikuwa magumu kuelewa (ona 2Petro 3:16).

Mchungaji anayefundisha mstari kwa mstari anapofikia mstari au fungu la Maandiko ambalo haelewi, anatakiwa kuwaambia washirika wake kwamba haelewi sehemu inayofuata, na kuiacha. Pia anaweza kuwaomba washirika wamwombee ili Roho Mtakatifu amsaidie kuelewa. Unyenyekevu wake utakuwa mfano mzuri mbele ya kundi lake, na kuwa ujumbe kamili kabisa.

Mchungaji au mzee au mwangalizi wa kanisa la nyumbani ana ziada nyingine ya kufundisha kundi dogo katika mazingira yasiyo rasmi, kwa sababu maswali yanaweza kuulizwa wakati wa mafundisho yake. Hili pia hutoa nafasi ya uwezekano wa Roho Mtakatifu kuwapa wengine katika kikundi hicho ufahamu kuhusu maandiko yanayochunguzwa. Matokeo ni kwamba kila mtu anaweza kujifunza kwa uzuri zaidi.

Mahali pazuri pa kuanza kufundisha amri za Kristo ni kwenye Mahubiri Yake aliyotoa mlimani, katika Mathayo sura ya 5 hadi ya 7. Yesu alitoa amri nyingi sana hapo, na aliwasaidia wafuasi Wake Wayahudi kuelewa vizuri zile sheria zilizotolewa kwa njia ya Musa. Baadaye katika kitabu hiki nitafundisha kutoka Mahubiri ya Mlimani mstari kwa mstari ili uone inavyoweza kuwa.

Kuandaa Mahubiri

Hakuna ushahidi wowote katika Agano Jipya kwamba mchungaji yeyote, au mzee, au mwangalizi aliandaa mahubiri au hotuba ya kila juma, ikiwa na mada zilizoandaliwa vizuri na vielelezo au mifano iliyoandikwa kwa muhtasari, kama ilivyo kawaida ya watumishi wengi wa kisasa. Nadhani hatuwezi kufikiria Yesu akifanya hivyo! Katika kanisa la kwanza, mafundisho yalifanyika kimatendo na kila mmoja alihusika, kwa kufuata mtindo wa Kiyahudi badala ya kuwa mihadhara au hotuba, kama ilivyokuwa desturi ya Wayunani na Warumi. Desturi hii ilikuja kuingizwa katika kanisa mwishoni, lilipokuja kuwa kama lilivyo leo. Ikiwa Yesu aliwaambia wanafunzi Wake wasitayarishe jinsi watakavyojitetea wakiitwa mahakamani, akiahidi kwamba Roho Mtakatifu angewapa pale pale maneno ya kusema ambayo yasingekuwa rahisi kupingwa, ni vizuri tutazamie kwamba Mungu ataweza kuwasaidia wachungaji katika mikutano ya kanisa kwa kiwango fulani!

Hii si kusema kwamba watumishi wasijiandae wenyewe kwa kuomba na kujisomea. Paulo alimshauri Timoteo hivi:

Jitahidi kujionyesha kuwa umekubaliwa na Mungu kama mtendakazi asiyehitaji kuaibika, anayetumia sawasawa neno la kweli (2Timo. 2:15 – TLR).

Watumishi wanaofuata mashauri ya Paulo kwamba “Neno la Kristo likae kwa wingi ndani yenu” (Wakolosai 3:16 – TLR) watajawa na Neno la Mungu kiasi cha kwamba wataweza kulifundisha kutokana na “kufurika” kwao. Basi mchungaji mpendwa: Cha muhimu ni kwamba, zama ndani ya Biblia. Ukijua vizuri mada yako, na ukiwa na moto juu ya mada yako, hakuna matayarisho mengine unayohitaji ili uweze kuwasilisha kweli ya Mungu kwa wasikilizaji wako. Tena, kama unafundisha mstari kwa mstari, unaweza kutumia mstari unaofuata kama muhtasari wako. Basi, maandalizi yako yawe ni kutafakari kwa hali ya maombi mistari ile utakayofundisha juu yake. Kama wewe ni mchungaji wa kanisa la nyumbani, ile hali ya kushirikiana katika kufundisha itapunguza sana hitaji la kuwa na muhtasari wa mahubiri.

Mtumishi mwenye imani kwamba Mungu atamsaidia wakati anapofundisha, atazawadiwa msaada wa Mungu. Basi, usijiamini wewe sana, wala matayarisho yako au vidokezo ulivyuoandika. Mtumaini Mungu zaidi. Kadri utakavyopata imani na kujiamini, punguza vidokezo unavyoandaa mpaka uweze kufundisha ukitumia vidokezo kidogo au bila muhtasari wenye vidokezo kabisa.

Mwenye kujifikiria mbele ya wengine ndiye atakayetegemea vidokezo alivyoandaa kwa sababu anaogopa kufanya makosa mbele ya watu. Anahitaji kujua kwamba hofu yake inatokana na kutojiamini, na kiburi. Afadhali asijali jinsi anavyo-onekana machoni pa watu, ajali zaidi jinsi yeye na wasikilizaji wake wanavyoonekana mbele za Mungu. Hakuna hotuba iliyoandaliwa inayhoweza kuwagusa wasikilizaji kama mafundisho toka moyoni, yenye upako wa Roho Mtakatifu. Hebu fikiri jinsi ambavyo mawasiliano yangekwamishwa kama kila mtu angetumia vidokezo vilivyoandikwa katika mazungumzo yake yote! Kuzungumza kungekoma! Mtindo wa mazungumzo yasiyoandaliwa husikika kuwa kweli kuliko mhadhara ulioandaliwa. Kufundisha si kuigiza. Ni kutoa ukweli. Wote tunajua wakati tunaposikiliza hotuba, na inapokuwa hivyo, tunajua jinsi ya kufunga “mawazo” yetu tusisikie chochote.

Mawazo Mengine Manne

(1) Watumishi wengine ni kama kasuku. Wao hupata vitu vya kuhubiri kutoka kwenye vitabu vilivyoandikwa na wengine. Wanapoteza baraka kubwa sana ya kufundishwa na Roho Mtakatifu, na kuna uwezekano mkubwa sana kwao kuendeleza makosa ya waandishi wanaowanakili.

(2) Wachungaji wengi huiga mitindo ya kuhubiri na kufundisha ya watu wengine – ya kimapokeo. Kwa mfano: Inaaminika kwamba mahubiri yamevuviwa kama yatakuwa kwa haraka na kwa sauti kubwa. Basi, wahudhuriaji wanaketi kusikiliza mahubiri ambayo ni kelele tupu tangu mwanzo hadi mwisho. Ukweli ni kwamba watu huacha kusikiliza kelele zisizo na maana, kama wanavyofanya wakati mtu anapozungumza kwa sauti moja tu isiyobadilika. Sauti yenye kubadilika-badilika inavutia zadi. Tena, mahubiri huwa ya sauti kubwa kidogo kwa sababu ni kama mawaidha, ila mafundisho hufanywa kwa sauti kama ya kuzungumza maana ni kama ushauri.

(3) Nimeona wasikilizaji mahubiri wengi sana katika makanisa mengi sana, nami sijaacha kushangaa jinsi ambavyo wahubiri wengi na waalimu wasivyoweza kuona ishara nyingi kwamba wasikilizaji wao wamechoka na hawasikilizi. Mchungaji, ni hivi: Watu wanao-onekana wamechoka ni kweli wamechoka! Wale wasiokutazama ni kwamba hawaskilizi. Watu ambao hawasikilizi hawapati msaada hata kidogo. Kama watu wenye kumaanisha wamechoshwa na hawasikilizi, unahitaji kurekebisha mahubiri yako. Toa mifano zaidi. Eleza visa vyenye maana na msaada kwao. Tunga mithali. Rahisisha mambo. Fundisha Neno la Mungu kutoka moyoni. Maanisha unachosema. Usiige mtu. Badilisha sauti yako. Jaribu kuwatazama watu wengi iwezekanavyo machoni. Simulia kisa chako kwa maigizo. Tumia mikono. Usisimame mahali pamoja – tembea tembea. Usizungumze kwa muda mrefu. Kama kundi ni dogo, ruhusu watu waulize maswali kwa wakati unaofaa.

(4) Wazo kwamba kila mahubiri yanatakiwa kuwa na mambo makuu matatu ni la kibinadamu. Lengo ni kuwafanya watu kuwa wanafunzi, siyo kufuata nadharia za kisasa za kutayarisha mahubiri. Yesu alisema hivi: “Lisha kondoo wangu”. Hakusema: “Babaisha kondoo wangu”.

Wa Kufundishwa

Anapofuata mfano wa Yesu, mtumishi mwenye kufanya watu kuwa wanafunzi huchagua atakayefundishwa. Pengine litakushangaza hilo, lakini ndiyo ukweli. Mara nyingi Yesu alizungumza na makundi ya watu kwa mifano, na alikuwa na sababu ya kufanya hivyo. Hakutaka kila mtu aelewe alichokuwa anasema. Maandiko yanaweka hilo wazi, kama ifuatavyo:

Wakaja wanafunzi wakamwambia, Kwa nini wasema nao kwa mifano? Akajibu akawaambia, Ninyi mmejaliwa kuzijua siri za ufalme wa mbinguni, bali wao hawakujaliwa. Kwa maana yeyote mwenye kitu atapewa, naye atazidishiwa tele; lakini yeyote asiye na kitu, hata kile alicho nacho atanyang’anywa. Kwa sababu hii nasema nao kwa mifano; kwa kuwa wakitazama hawaoni, na wakisikia hawasikii, wala kuelewa (Mathayo 13:10-13).

Fursa au nafasi ya kuelewa mifano ya Kristo ilitolewa kwa wale tu waliokuwa wametubu na kuamua kumfuata. Wale waliopuuza nafasi ya kutubu na kupinga mapenzi ya Mungu kwa ajili ya maisha yao, walikataliwa na Mungu na kupingwa Naye pia. Mungu huwapinga wenye kiburi, bali huwapa neema wanyenyekevu (ona 1Petro 5:5).

Vile vile Yesu aliwaagiza wafuasi wake hivi: “Msiwape mbwa kilicho kitakatifu, wala msitupe lulu zenu mbele ya nguruwe, wasije wakazikanyaga chini ya miguu yao, wakageuka na kuwararua” (Mathayo 7:6). Hapa, Yesu alizungumza kwa lugha ya mfano. Alimaanisha hivi: “Msitoe kitu cha thamani kwa watu wasiothamini thamani yake.” Nguruwe hawatambui kwamba lulu zina thamani. Vivyo hivyo, nguruwe wa kiroho hawatambui thamani ya Neno la Mungu wanapolisikia. Wangeamini kwamba wanasikia Neno la Mungu, wangelisikiliza kwa makini sana na kulitii.

Utajuaje mtu ni nguruwe kiroho? Wewe mtupie lulu moja uone atakachofanya. Akiipuuza, utajua kwamba yeye ni nguruwe kiroho. Akiitii, utajua kwamba si nguruwe kiroho.

Cha kusikitisha ni kwamba wachungaji wengi hufanya kile ambacho Yesu amewakataza kufanya. Wanaendelea kutupa lulu zao mbele ya nguruwe, wakiwafundisha watu ambao wanapinga au waliokataa Neno la Mungu. Watumishi hao wanapoteza muda wao waliopewa na Mungu. Wangepaswa kukung’uta mavumbi ya miguuni pao na kwenda mahali pengine zamani, kama Yesu alivyoagiza.

Kondoo, Mbuzi Na Nguruwe

Ukweli ni huu: Huwezi kumfanya mtu kuwa mwanafunzi ambaye hataki hivyo, yaani, mtu asiyetaka kumtii Yesu. Makanisa mengi yamejaa watu wa aina hiyo, watu ambao wana mila ya Kikristo. Wengi hufikiri kwamba wamezaliwa mara ya pili kwa sababu tu wamekubaliana na kweli fulani za kitheolojia kuhusu Yesu au Ukristo. Wao ni nguruwe na mbuzi – si kondoo. Lakini, wachungaji wengi hutumia asilimia 90 ya wakati wao wakijaribu kufurahisha hao nguruwe na mbuzi, huku wanapuuzia wale ambao wangeweza kuwasaidia kiroho na wanaotakiwa kuhudumiwa – yaani, kondoo wa kweli! Ewe mchungaji: Yesu anataka ulishe kondoo Zake, si mbuzi au nguruwe! (Ona Yohana 21:17)

Lakini sasa, utajuaje nani kondoo? Ni wale wanaokuja kanisani mapema, na kuondoka wa mwisho. Hao wana njaa ya kujifunza ukweli, kwa sababu Yesu ni Bwana wao, na wanataka kumpendeza. Wanakuja kanisani – si Jumapili tu – bali sikuzote kunapokuwa na mkutano. Wanajiunga na vikundi vidogo. Mara nyingi wanauliza maswali. Wana msisimko kuhusu Bwana. Wanatafuta nafasi za kutumika.

Mchungaji: Tumia muda wako mwingi kwa watu hawa. Hao ndiyo wanafunzi. Kuhusu mbuzi na kondoo wanaohudhuria kanisani kwako: Wewe hubiri Injili muda wote watakaoweza kuvumilia. Lakini ukihubiri Injili ya kweli, hawataweza kuvumilia kwa muda mrefu. Wtaondoka kanisani – au kama wana uwezo – watajaribu kukuondoa. Wakifanikiwa, kung’uta mavumbi miguuni pako unapo-ondoka. (Lakini: Katika kanisa la nyumbani, jambo hilo haliwezi kutokea, hasa kama kanisa lenyewe linakutania nyumbani mwako!)

Wainjilisti nao wasijisikie wajibu wa kuendelea kuhubiri Injili kwa watu wale wale ambao wameikataa mara kadhaa. Waache wafu wazike wafu wenzao (ona Luka 9:60). Wewe ni balozi wa Kristo, mwenye ujumbe wa maana sana kutoka kwa Mfalme wa wafalme! Nafasi yako ni ya juu sana katika ufalme wa Mungu, na wajibu wako ni mkubwa! Usipoteze wakati kumwambia mtu Injili mara mbili kabla wengine hawajasikia hata mara moja.

Basi: Kama utakuwa mtumishi mwenye kufanya watu kuwa wanafunzi, unatakiwa kuchagua sana wale utakaowafundisha, ili usipoteze wakati wako wa thamani sana kwa watu wasiotaka kumtii Yesu. Paulo alimwandikia Timotheo hivi:-

Mambo yale uliyosikia kutoka kwangu mbele ya mashahidi wengi, wewe wakabidhi watu waaminifu, watakaoweza kuwafundisha na wengine pia (2Timo. 2:2 – TLR. Maneno mepesi kukazia).

Kulifikia Lengo

Hebu fikiri kidogo juu ya kitu ambacho kisingetokea katika huduma ya Yesu, kinachotokea kila mara katika makanisa ya kisasa. Tufikiri kwamba, baada ya kufufuka Kwake, Yesu alibaki duniani na kuanzisha kanisa kama haya tuliyo nayo, na kulichunga kwa miaka thelathini. Hebu fikiri kwamba kila Jumapili aliwahubiria watu wale wale. Fikiri kwamba Petro, Yakobo na Yohana wanaketi kiti cha mbele katika mahubiri hayo, mahali ambapo wameketi kila Jumapili kwa miaka ishirini. Jaribu kupiga picha umwone Petro akimwinamia Yohana na kusema sikioni mwake, “Aa! Tumesikia mahubiri haya haya mara kumi.”

Tunajua kwamba ni kitu kisichowezekana, maana wote tunafahamu kwamba asingejiweka katika hali kama hiyo, wala kuwaweka mitume Wake. Yesu alikuja kufanya watu kuwa wanafunzi, kwa namna fulani na katika kipindi fulani. Kwa kipindi cha miaka mitatu, alimfundisha Petro, Yakobo na Yohana, na wengine pia. Hakufanya kwa kuwahubiria mara moja kila Jumapili katika jengo la kanisa. Alifanya kwa kuishi maisha Yake mbele yao, kwa kujibu maswali yao, na kwa kuwapa nafasi ya kutumika. Alimaliza kazi Yake akasonga mbele.

Sawa. Sasa, mbona sisi tunafanya kitu ambacho Yesu asingekifanya? Kwa nini tunajaribu kukamilisha kile ambacho Mungu anataka kwa kuwahubiria watu wale wale miaka na miaka? Tutakamilisha lini kazi yetu? Kwa nini wanafunzi wetu – baada ya miaka fulani – hawako tayari kutoka na kuwafanya wengine kuwa wanafunzi wao pia?

Ninachosema ni hiki: Kama tunafanya kazi zetu sawasawa, wakati utafika ambapo wanafunzi wetu watakua kiasi cha kutosha kutohitaji huduma yetu. Ikifikia hapo, waruhusiwe kwenda kufanya wengine kuwa wanafunzi. Tunatakiwa kulifikia lengo ambalo Mungu ameweka mbele yetu, na Yesu alituonyesha jinsi ya kulifikia. Katika kanisa la nyumbani linalokua, lipo hitaji la kudumu la kuwafanya watu kuwa wanafunzi, na kuzaa viongozi. Kanisa la nyumbani lenye afya halitaingia katika mzunguko wa mhubiri huyo huyo kuwahubiria watu hao hao kwa miaka na miaka.

Makusudi Sahihi Ya Moyo

Makusudi sahihi ya moyo ni muhimu sana katika kufanikiwa kufundisha kwa njia itakayopelekea watu kufanywa kuwa wanafunzi. Mtu anapokuwa katika huduma kwa sababu zisizofaa atafanya makosa. Hii ndiyo sababu ya msingi ya kuwepo na mafundisho mengi ya uongo na yasiyo na maana katika kanisa siku hizi. Wakati makusudi ya mtumishi ni kupata umaarufu, kufanikiwa machoni pa watu, au kujipatia fedha nyingi, anaelekea kwenye kushindwa mbele za Mungu. Cha kusikitisha ni kwamba anaweza kufanikiwa kufikia lengo lake la kupata umaarufu, kufanikiwa machoni pa watu, au kutengeneza fedha nyingi tu, lakini siku itafika ambapo makusudi yake mabaya yatafunuliwa mbele ya kiti cha hukumu cha Kristo, naye hatapata thawabu yoyote kwa ajili ya kazi yake. Kama ataruhusiwa kuingia katika ufalme wa mbinguni,[3] kila mtu atakayekuwepo atajua ukweli juu yake, maana kukosa thawabu kwake na nafasi yake ya chini katika ufalme vitadhihirisha hayo. Bila shaka kuna nafasi tofauti tofauti mbinguni. Yesu alionya hivi:-

Basi mtu yeyote atakayevunja amri moja katika hizi zilizo ndogo na kuwafundisha watu hivyo, ataitwa mdogo kabisa katika ufalme wa mbinguni; bali mtu atakayezitenda na kuzifundisha, huyo ataitwa mkubwa katika ufalme wa mbinguni (Mathayo 5:19).

Watumishi wale wanaotii na kufundisha amri za Kristo watateseka kidogo hapa duniani kwa sababu hiyo. Yesu aliahidi mateso kwa watakaomtii (ona Mathayo 5:10-12); Yohana 16:33). Hawataweza kufanikiwa duniani, au kuwa maarufu au kupata mali. Wanachopata ni thawabu za baadaye na sifa kutoka kwa Mungu. Je, wewe ungependa kipi? Paulo aliandika hivi kuhusu jambo hili:-

Basi Apolo ni nani? Na Paulo ni nani? Ni wahudumu ambao kwao mliamini; na kila mtu kama Bwana alivyompa. Mimi nilipanda, Apolo akatia maji; bali mwenye kukuza ni Mungu. Hivyo, apandaye si kitu, wala atiaye maji, bali Mungu akuzaye. Basi yeye apandaye na yeye atiaye maji ni wamoja, lakini kil amtu atapata thawabu yake mwenyewe sawasawa na taabu yake mwenyewe. Maana sisi tu wafanya kazi pamoja na Mungu; ninyi ni shamba la Mungu, ni jengo la Mungu.

Kwa kadiri ya neema ya Mungu niliyopewa, mimi, kama mkuu wa wajenzi mwenye hekima naliuweka msingi, na mtu mwingine anajenga juu yake. Lakini kila mtu na aangalie jinsi anavyojenga juu yake. Maana msingi mwingine hakuna mtu awezaye kuuweka, isipokuwa ni ule uliokwisha kuwekwa, yaani, Yesu Kristo. Lakini kama mtu akijenga juu ya msingi huo, dhahabu au fedha au mawe ya thamani, au miti au majani au manyasi, kazi ya kila mtu itakuwa dhahiri. Maana siku ile itaidhihirisha, kwa kuwa yafunuliwa katika moto; na ule moto wenyewe utaijaribu kazi ya kila mtu, ni ya namna gani. Kazi ya mtu aliyoijenga juu yake ikikaa, atapata thawabu. Kazi ya mtu ikiteketea, atapata hasara; ila yeye mwenyewe ataokolewa; lakini ni kama kwa moto (1Wakor. 3:5-15).

Paulo alijilinganisha na mjenzi bingwa mwenye kuweka msingi. Apolo ambaye ni mwalimu aliyekuja Korintho baada ya Paulo kuanzisha kanisa hapo analinganishwa na mtu ambaye anajenga juu ya msingi uliokwisha wekwa.

Ona kwamba Paulo na Apolo wangepata thawabu mwishowe, kutokana na sifa ya kazi yao, siyo wingi wa kazi yao (ona 3:13).

Kimfano ni kwamba Paulo na Apolo wangeweza kujenga jengo la Mungu kwa kutumia aina sita tofauti za vifaa – vitatu vya kawaida kabisa na ambavyo si ghali, tena vyepesi kuungua. Vitatu si vya kawaida sana, ni ghali sana, na haviungui kwa urahisi. Siku moja, vitu vyao vya kujengea vingepitia hukumu ya moto wa Mungu, na zile mbao, majani na manyasi vingeteketezwa kwa moto na kudhihirisha sifa yake isiyo ya thamani na ya muda sana. Lakini dhahabu, fedha na mawe ya thamani ambavyo ni mfano wakazi za thamani na za milele mbele za Mungu, vingeshinda kipimocha moto.

Tuwe na uhakika kabisa kwamba mafundisho yasiyo ya KiBiblia yatachomwa na kuteketea kabisa wakati wa hukumu mbele ya Kristo. Hata vitu vingine vyote vitakavyofanywa kwa nguvu, mbinu au hekima ya mwili, pamojana chochote kitakachofanywa kwa makusudi yasiyo mazuri. Yesu alionya kwamba chochote tunachoweza kufanya kitakachotokana na kutaka sifa ya watu hakitapata thawabu (tazama Mathayuo 6:1-6, 16-18). Matendo hayo ambayo si kitu yanaweza yasiwe dhahiri machoni pa watu wakati huu, lakini hakika yatadhihirishwa kwa wote siku za baadaye, kama alivyosema Paulo. Kibinafsi – kama matendo yangu ni miti, majani na manyasi – ningependa kujua sasa kuliko baadaye. Kwa sasa iko nafasi ya kutubu; wakati huo haitakuwepo!

Kukagua Makusudi Yetu

Ni rahisi sasa kujidanganya kwa habari ya makusudi yetu. Hata mimi nimewahi kudanganyika. Je, tutajuaje ikiwa makusudi yetu ni safi?

Njia iliyo bora zaidi ni kumwomba Mungu atufunulie ikiwa makusudi yetu ni mabaya, kisha kuendelea kufuatilia mawazo yetu na matendo yetu. Yesu alituambia tutende mema kama vile kuomba na kuwasaidia maskini kwa siri. Hiyo ni njia moja ya kujihakikishia kwamba tunatenda vema kwa sababu tunatafuta sifa ya Mungu badala ya sifa za watu. Kama tutamtii Mungu wakati watu wanapotuona tu, hiyo ni ishara kwamba kuna kitu kisicho sawa. Au – kama tutaepuka dhambi mbaya ambazo zitaharibu sifa yetu tukigunduliwa, hukmu tunajihusisha na dhambi ndogo ambazo hakuna mtu anayeweza kufahamu, hilo linaonyesha kwamba makusudi yetu si mazuri. Ikiwa kweli tunajaribu kumpendeza Mungu – anayejua kila wazo letu, neno na tendo – basi tutajitahidi kumtii kila wakati katika mambo makubwa na madogo, mambo yajulikanayo na yasiyojulikana kwa wengine.

Pia, kama makusidi yetu ni sahihi, hatutafuata mitindo ya ukuaji wa kanisa ambayo lengo lake ni kuongeza wahudhuriaji tu huku ikipuuza kuwafanya watu kuwa wanafunzi watakaotii maagizo yote ya Kristo.

Tutalifundisha Neno kamili la Mungu badala ya kulenga mada zinazopendwa tu, zenye kuwavutia watu wa kidunia, wasio wa kiroho.

Hatutalibadili Neno la Mungu au kufundisha Maandiko kwa njia yenye kuhalifu mantiki yake katika Biblia.

Hatutafuta majina makubwa au nafasi za heshima kwa ajili yetu wenyewe. Hatutatafuta kujulikana.

Hatutawahudumia matajiri tu (au wenye mali) na kujali maslahi yao.

Hatutajiwekea hazina duniani, bali tutaishi kwa hali ya kawaida na kutoa kiasi tunachoweza, na kuwa mfano wa uwakili mwema mbele ya kondoo wetu.

Tutajali zaidi Mungu anasema nini juu ya mahubiri yetu kuliko mawazo ya watu.

Vipi basi: Makusudi yako yakoje?

Fundisho Lenye Kuharibu Mpango Wa Kufanya Watu Kuwa Wanafunzi

Mtumishi mwenye kufanya watu kuwa wanafunzi hafundishi chochote kitakachopingana na lengo la kuwafanya watu kuwa wanafunzi. Hivyo, hasemi kitu chochote kitakachowafanya watu wajisikie vizuri kuacha kumtii Bwana Yesu. Haelezi juu ya neema ya Mungu kama ruhusa ya watu kufanya dhambi bila kuogopa hukumu. Yeye huelezea juu ya neema ya Mungu kwamba ni njia ya kutubu dhambi na kusaidia kuishi maisha ya ushindi. Kama tujuavyo, Maandiko yanasema kwamba ni washindaji tu ndiyo watakaourithi ufalme wa Mungu. Tazama Ufunuo 2:11; 3:5; 21:7.

Kwa bahati mbaya sana, kuna watumishi wa kisasa ambao wanashikilia mafundisho yasiyo ya KiBiblia, yenye kudhuru sana lengo la kuwafanya watu kuwa wanafunzi. Fundisho moja ambalo limekuwa maarufu sana Marekani ni lile la usalama wa milele usio na masharti, yaani, “ukiisha okoka, umeokoka milele”. Hili fundisho linasema kwamba watu waliozaliwa mara ya pili hawawezi kupoteza wokovu wao hata kama wataishi maisha ya aina gani. Kwa kuwa wokovu ni kwa neema, neema ile ile yenye kuwaokoa watu wenye kuomba sala ya kupokea wokovu, ndiyo itakayowadumisha. Wanasema kwamba wazo la namna nyingine ni sawa na kusema watu huokolewa kwa matendo yao.

Msimamo wa aina hiyo ni kikwazo kikubwa sana kwa utakatifu. Kwa kuwa kumtii Kristo si kitu cha lazima kwa mtu kuingia mbinguni, hakuwi na hamasa yoyote ya kumtii Yesu, hasa utii unapokuwa na gharama.

Kama nilivyokwisha kusema mapema, neema ambayo Mungu anawapa wanadamu haiwaondolei wajibu wa kumtii. Maandiko yanasema kwamba wokovu si kwa neema tu, bali pia kwa imani (tazama Waefeso 2:8). Neema na imani ni vya lazima ili wokovu upatikane. Imani ndiyo itikio sahihi kwa neema ya Mungu, na imani ya kweli sikuzote husababisha toba na kutii. Imani isiyo na matendo imekufa, haifai, na haiwezi kuokoa. Hayo ni maneno ya Yakobo (ona sura ya 2:14-26).

Hii ndiyo sababu Maandiko yanarudia kusema kwamba kuendelea katika wokovu hutegemea kuendelea katika imani na utii. Yapo Maandiko mengi sana yenye kuweka wazi jambo hilo. Mfano: Paulo anawaambia hivi waamini wa Kolosai:-

Na ninyi, mliokuwa hapo kwanza mmefarikishwa tena adui katika nia zenu kwa matendo yenu mabaya, amewapatanisha sasa katika mwili wa nyama yake, kwa kufa kwake, ili awalete ninyi mbele zake, watakatifu, wasio na mawaa wala lawama, mkidumu tu katika ile imani, hali mmewekwa juu ya msingi, mkawa imara; msipogeuzwa na kuliacha tumaini la Injili mliyosikia habari zake, iliyohubiriwa katika viumbe vyote vilivyo chini ya mbingu; ambayo mimi Paulo nalikuwa mhudumu wake (Wakolosai 1:21-23. Maneno mepesi kukazia).

Yaani – ni wazi mno. Anayeweza kukosa kuelewa maana ya Paulo au kuigeuza ni mwana-theolojia tu. Yesu atatuthibitisha bila lawama ikiwa tutaendelea katika imani. Kweli hiyo hiyo inarudiwa katika Warumi 11:13-24; 1Wakor. 15:1-2 na Waebrania 3:12-14; 10:38-39. Inatamkwa waziwazi hapo kwamba wokovu wa mwisho unategemeana na kudumu katika imani. Mafungu hayo yote ya Maandiko yanalo neno ikiwa au kama.

Umuhimu Wa Utakatifu

Je, mwamini anaweza kupoteza wokovu wa milele kwa kutenda dhambi? Jibu linapatikana katika Maandiko mengi sana, kama haya yafuatayo, yenye kuthibitisha kwamba wale watendao dhambi fulani fulani hawataurithi ufalme wa Mungu. Kama mwamini atarudia kutenda dhambi zile katika orodha zifuatazo za Paulo, basi anaweza kupoteza wokovu.

Au hamjui ya kuwa wadhalimu hawataurithi ufalme wa Mungu?Msidanganyike; waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti, wala wevi, wala watamanio, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi (1Wakor. 6:9-10. Maneno mepesi kukazia).

Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya: uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo kama hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu (Wagalatia 5:19-21. Maneno mepesi kukazia).

Maana neno hili mnalijua hakika ya kwamba hakuna mwasherati wala mchafu wala mwenye tamaa, ndiye mwabudu sanamu, aliye na urithi katika ufalme wa Kristo na Mungu. Mtu asiwadanganye kwa maneno yasiyo na maana; kwa kuwa kuwa sababu ya hayo hasira ya Mungu huwajia wana wa uasi (Waefeso 5:5, 6. Maneno mepesi kukazia).

Ona kwamba katika kila sehemu, Paulo alikuwa anawaandikia waamini, akiwaonya. Mara mbili aliwaonya wasidanganywe, kuonyesha kwamba alijali maana waamini wengine wangeweza kudhani kwamba mtu anaweza kutenda dhambi zilizotajwa na bado akaurithi ufalme wa Mungu.

Yesu aliwaonya wafuasi wake wa karibu sana – Petro, Yakobo, Yohana na Andrea – juu ya uwezekano wao kutupwa jehanamu kwa sababu yakutokuwa tayari kwa ajili ya kurudi Kwake. Ona kwamba wao ndiyo walioambiwa maneno yafuatayo (ktk Marko 13:1-4), sio kundi la wasioamini.

Kesheni basi; kwa maana hamjui ni siku ipi atakayokuja Bwana wenu. Lakini fahamuni neno hili: kama mwenye nyumba angaliijua ile zamu mwivi atakayokuja, angalikesha, wala asingaliicha nyumba yake kuvunjwa. Kwa sababu hiyo ninyi nanyi [Petro, Yakobo, Yohana na Andrea] jiwekeni tayari; kwa kuwa katika saa msiyodhani [ninyi akina Petro, Yakobo, Yohana na Andrea] Mwana wa Adamu yuaja.

Ni nani basi yule mtumwa mwaminifu mwenye akili, ambaye bwana wake alimweka juu ya nyumba yake, awape watu chakula kwa wakati wake? Heri mtumwa yule, ambaye bwana wake ajapo atamkuta akifanya hivyo. Amin, nawaambieni, atamweka juu ya vitu vyake vyote. Lakini mtumwa yule mbaya akisema moyoni mwake, Bwana wangu anakawia; akaanza kuwapiga wajoli wake na kula na kunywa pamoja na walevi; bwana wake mtumwa huyo atakuja siku asiyodhani, na saa asiyojua, atamkata vipande viwili, na kumweka fungu lake pamoja na wanafiki; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno (Mathayo 24:42-51. Maneno mepesi kukazia).

Fundisho la habari hii ni nini? Ni hili: “Petro, Yakobo, Yohana na Andrea – msiwe kama mtumwa asiyekuwa mwaminifu katika mfano huu.”[4]

Ili kutilia mkazo kile alichowaambia wanafunzi Wake wa karibu sana, Yesu aliendelea kutoa mfano wa Wasichana Wanawali Kumi. Hao wote walikuwa tayari kwa ajili ya kuja kwa bwana arusi, lakini watano wakawa hawakujiandaa vizuri, basi wakaikosa ile karamu. Yesu alimalizia mfano wake kwa maneno haya: “Basi kesheni [Petro, Yakobo, Yohana na Andrea]; kwa sababu hamwijui siku wala saa (Mathayo 25:13). Yaani, “Petro! Yakobo! Yohana! Andrea! Msiwe kama wale wanawali watano wapumbavu.” Ni hivi: Kama usingekuwepo uwezekano wa Petro, Yakobo, Yohana na Andrea kutokuwa tayari, Yesu asingekuwa na haja ya kuwaonya.

Ndipo Yesu akasimulia mara hiyo hiyo Mfano wa talanta. Ujumbe ulikuwa ni ule ule – “Msiwe kama yule mtumishi wa talanta moja, ambaye hakuwa na kitu cha kumwonyesha bwana wake kutokana na mali aliyokabidhiwa, wakati aliporudi.” Mwisho wa mfano huo, yule bwana alitamka hivi, “Mtupeni mbali katika giza la nje; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno” (Mathayo 25:30). Yesu aliweka wazi kabisa ujumbe Wake – hauwezi kuwa wazi kuliko hapo. Anayeweza kubadilisha maana ya ujumbe huo ni mwana-theolojia tu – ndiye haelewi! Ni hivi: Ilikuwepo hatari ya Petro, Yakobho, Yohana na Andrea kutupwa jehanamu mwishoni kama wasingekuwa watiifu wakati wa kurudi kwa Yesu. Sasa – kama uwezekano huo ulikuwepo kwa ajili ya Petro, Yakobo, Yohana na Andrea, ni kwamba upo hata kwetu wote. Kama alivyoahidi Yesu ni kwamba, wale tu watendao mapenzi ya Baba Yake ndiyo watakaoingia katika ufalme wa mbinguni (ona Mathayo 7:21). [5]

Wale wanaofundisha uongo kwamba ukiokoka unalindwa milele bila masharti yoyote ni wafanya kazi kinyume cha Kristo. Wanamsaidia Shetani, wakifundisha kinyume na yale aliyofundisha Yesu na mitume. Wao wanabatilisha kabisa agizo la Yesu kwamba watu wafanye wengine kuwa wanafunzi, watakaoitii yote aliyoamuru. Wanaiziba njia ile nyembamba iendayo mbinguni, na wanaipanua ile njia pana iendayo upotevuni.[6]

Fundisho Lingine La Kisasa Linalopingana Na Mpango Wa Kufanya Watu Kuwa Wanafunzi

Si mafundisho ya usalama wa wokovu wa milele bila masharti yoyote tu yanayowadanganya watu kufikiri kwamba utakatifu si muhimu kwa ajili ya wokovu. Upendo wa Mungu mara nyingi unaelezwa kwa njia yenye kubatilisha shughuli ya kuwafanya watu kuwa wanafunzi. Mara nyingi wahubiri watasikika wakisema hivi: “Mungu anakupenda bila masharti yoyote.” Watu hutafsiri maneno hayo kuwa yanamaanisha hivi: “Mungu ananikubali na kunipokea bila kujali kama ninamtii au simtii.” Lakini huo si ukweli.

Wahubiri wengi wa aina hiyo pia wanaamini kwamba Mungu huwatupa jehanamu watu ambao hawajaokoka. Ni sawa kabisa. Sasa hebu tufikiri kidogo juu ya hilo. Ni wazi kwamba Mungu hakubaliani na watu anaowatupa jehanamu. Sasa, inawezekanaje basi kwamba anawapenda tena? Je, watu wanaotupwa jehanamu wanapendwa na Mungu? Je, unadhani watakwambia kwamba Mungu anawapenda? Hapana. Je, Mungu atasema anawapenda? Hapana! Wanamchukiza, ndiyo sababu anawaadhibu jehanamu. Ni kwamba hakubaliani nao wala hawapendi.

Kama ni hivyo basi, ni kwamba upendo wa Mungu kwa watenda dhambi wa hapa duniani ni wa rehema ambao ni wa muda tu. Si upendo wenye kukubali mtu. Anawarehemu kwa kuchelewesha hukumu Yake na kuwapa nafasi ya kutubu. Yesu alikufa kwa ajili yao na kutengeneza njia ya wao kusamehewa. Kwa hali hiyo na njia hiyo tunaweza kusema Mungu anawapenda. Lakini hakubaliani na hali yao. Hajisikii upendo kwao kama baba anavyojisikia kwa mtoto wake. Maandiko yanatangaza hivi juu ya jambo hili: “Kama baba anavyowahurumia watoto wake, ndivyo na Bwana alivyo na huruma kwa wale wamchao” (Zaburi 103:13 – maneno mepesi kukazia). Basi, tunaweza kusema kwamba Mungu hana huruma ile ile kwa watu wasiomcha Yeye. Upendo wa Mungu kwa wenye dhambi unalingana na huruma ambayo hakimu anaweza kuonyesha kwa mwuaji anayehukumiwa kifungo cha maisha badala ya kunyongwa.

Hatusomi popote katika Matendo ya Mitume kwamba mhubiri alihubiri Injili na kusema kwa watu wasio-okoka kwamba Mungu anawapenda. Wahubiri wa KiBiblia mara nyingi walionya wasikilizaji wao kuhusu ghadhabu ya Mungu na kuwataka watubu, na kuwajulisha kwamba Mungu hakuwa anakubaliana na hali zao, na kwamba walikuwa hatarini, na kwamba walihitaji kufanya mabadiliko makubwa sana maishani mwao. Kama wangewaambia wasikilizaji wao kwamba Mungu aliwapenda (kama ambavyo wahubiri wengi wa siku hizi wanavyofanya), wangewapotosha wasikilizaji wao kufikiri kwamba hawako katika hatari aina yoyote, kwamba hawakuwa wanajikusanyia ghadhabu, na kwamba hawakuwa na haja ya kutubu.

Mungu Anavyowachukia Wenye Dhambi

Tofauti na jinsi inavyotangazwa siku hizi kwamba Mungu anawapenda wenye dhambi, Maandiko yanasema mara nyingi sana kwamba Mungu anachukia wenye dhambi.

Wajivunao hawatasimama mbele za macho yako; unawachukia wote watendao ubatili. Utawaharibu wasemao uongo; BWANA humzira mwuaji na mwenye hila (Zaburi 5:5-6. Maneno mepesi kukazia).

BWANA humjaribu mwenye haki; bali nafsi yake humchukia asiye haki, na mwenye kupenda udhalimu (Zaburi 11:5. Maneno mepesi kukazia).

Nimeiacha nyumba yangu, nimeutupa urithi wangu; nimemtia mpenzi wangu katika mikono ya adui zake. Urithi wangu umekuwa kwangu kama simba msituni; ameinua sauti yake juu yangu; kwa sababu hiyo nimemchukia (Yeremia 12:7-8. Maneno mepesi kukazia).

Uovu wao wote u katika Gilgali; maana huko naliwachukia; kwa sababu ya uovu wa matendo yao nitawafukuza watoke katika nyumba yangu; sitawapenda tena; wakuu wao wote ni waasi (Hosea 9:15. Maneno mepesi kukazia).

Angalia mistari yote hiyo – haisemi kwamba Mungu anachukia matendo ya watu tu. Inasema anawachukia hata watu wenyewe. Hii inaweka wazi ule usemi wa kisasa kwamba Mungu anampenda mwenye dhambi bali anachukia dhambi yake. Hatuwezi kumtengansiha mtu na kile anachofanya. Anachofanya hudhirisha alivyo. Kwa hiyo, Mungu anawachukia watu watendao dhambi, si dhambi tu watu wanazotenda. Kama Mungua nawakubali watu wanaofanya kile anachochukia, basi hana msimamo. Katika mahakama za kibinadamu watu hufikishwa mbele ya sheria kwa ajili ya makosa yao, nao wanapokea ijara inayostahili. Hatuchukii uhalifu na kuwakubali wanaoufanya.

Watu Ambao Mungu Anawazira

Maandiko yanafundisha kwamba Mungu anawachukia watu fulani. Pia, yanatangaza kwamba Mungu anawazira wenye dhambi wa aina fulani – yaani, ni chukizo Kwake. Angalia tena maandiko yafuatayo, uone kwamba hayasemi yanayotendwa na watu hao kuwa ni chukizo kwa Mungu, bali kwamba wao wenyewe ni chukizo kwa Mungu. Hayasemi kwamba Mungu anazira dhambi zao, bali kwamba Mungu anawazira wao.[7]

Mwanamke asivae mavazi yampasayo mwanamume, wala mwanamume asivae mavazi ya mwanamke; kwa maana kila afanyaye mambo hayo ni machukizo kwa BWANA, Mungu wako (Kumbu. 22:5. Maneno mepesi kukazia).

Kwa kuwa wote wayatendao mambo kama haya, wote watendao yasiyo haki, ni machukizo kwa BWANA, Mungu wako (Kumbu. 25:16. Maneno mepesi kukazia).

Nanyi mtakula nyama ya miili ya wana wenu, na nyama ya miili ya binti zenu mtaila. Nami nitapaharibu mahali penu palipoinuka, na kuziangusha sanamu zenu za jua, nami nitaitupa mizoga yenu juu ya mizoga ya sanamu zenu; na roho yangu itawachukia (Walawi 26:29-30. Maneno mepesi kukazia).

Wajivunao hawatasimama mbele za macho yako; unawachukia wote watendao ubatili. Utawaharibu wasemao uongo; BWANA humzira mwuaji na mwenye hila (Zaburi 5:5-6. Maneno mepesi kukazia).

Maana mtu mkaidi ni chukizo kwa BWANA, bali siri yake ni pamoja na wanyofu (Mithali 3:32. Maneno mepesi kukazia).

Wenye kuhalifu moyoni ni chukizo kwa BWANA; walio wakamilifu katika njia zao humpendeza (Mithali 11:20. Maneno mepesi kukazia).

Kila mwenye moyo wa kiburi ni chukizo kwa BWANA; hakika hatakosa adhabu (Mithali 16:5. Maneno mepesi kukazia).

Yeye asemaye kwamba asiye haki ana haki; naye asemay ekwamba mwenye haki hana haki; hao wote wawili ni chukizo kwa BWANA (Mithali 17:15. Maneno mepesi kukazia).

Sasa, tuowanisheje maandiko kama hayo na yale yanayosema kuhusu upendo wa Mungu kwa wenye dhambi? Inawezekanaje kusema kwamba Mungu anawachukia na kuwazira wenye dhambi, lakini tena anawapenda?

Lazima tutambue kwamba upendo haufanani. Kuna upendo ambao hauna masharti. Huo unaweza kuitwa “upendo wenye rehema”. Ni upendo unaosema hivi: “Nakupenda licha ya”. Unawapenda watu licha ya matendo yao. Upendo aina hiyo ndiyo Mungu anao kwa wenye dhambi.

Kinyume cha huo ni ule mwingine – upendo wa masharti. Huu unaweza kuitwa “upendo unaokubali”. Ni upendo unaopatikana kwa kazi au matendo. Ni upendo unaosema hivi: “Ninakupenda kwa sababu ya.”

Kuna wanaodhani kwamba upendo ukiwa wa masharti, si upendo. Au, wanaupuuzia, wakisema kwamba ni wa kibinafsi sana – kichoyo – tena, haulingani na upendo wa Mungu.

Lakini, ukweli ni kwamba Mungu ana upendo wa masharti, kama tutakavyoona hivi karibuni tu katika Maandiko. Basi, upendo unaokubali usipuuzwe. Upendo unaokubali ndiyo upendo wa msingi ambao Mungu anao kwa watoto Wake wa kweli. Tunatakiwa kutamani zaidi upendo unaokubali wa Mungu kuliko ule wa rehema.

Je, Upendo Unaokubali Ni Upendo Wa Hali Ya Chini?

Hebu jiulize swali hili: “Ningependa watu wanipende upendo aina gani – wa huruma au wa kukubali?” Nina hakika ungependa watu wakupende “kwa sababu ya,” badala ya kukupenda “licha ya”.

Je, ungefurahia kusikia mwenzako akisema hivi: “Sina sababu ya kukupenda, na hakuna chochote kwako kinachonihamasisha nionyeshe kukujali”? Au ungependa kusikia hivi: “Ninakupenda kwa sababu nyingi sana, maana kuna mambo mengi juu yako ninayofurahia”? Nadhani tungependa wenzetu watupende kwa upendo unaokubali. Huo ndio upendo wa msingi unaowavutia wenzi kuwa pamoja, na kuwafanya waendelee kuwa pamoja. Wakati kinapokosekana chochote ambacho mtu anakipenda kwa mwenzake, wakati upendo unaokubali unapomalizika, ndoa hazidumu. Zikidumu, ni kwa sababu ya upendo wa rehema, ambao unatokana na asili ya utauwa ya yule mwenye kuutoa upendo huo.

Basi, mambo ni hayo. Tunaona kwamba upendo unaokubali – au, wenye masharti, si upendo wa hali ya chini hata kidogo. Japo upendo wa kurehemu ndiyo unaosifika na unaopaswa kutolewa, upendo unaokubali ndiyo unaostahili kupatikana. Tena, ukweli kwamba upendo unaokubalika ndiyo upendo pekee ambao Baba alikuwa nao kwa Yesu, unaufanya uwe na nafasi yake ya kipekee na ya heshima. Mungu Baba hakuwahi kuwa na tone la upendo wa rehema kwa Yesu, kwa sababu hakukuwa na chochote kibaya ndani ya Kristo. Yesu alishuhudia mwenyewe, hivi:

Kwa sababu hii, Baba ananipenda, kwa kuwa nautoa uhai wangu, kisha naweza kuutwaa tena (Yohana 10:17 – TLR. Maneno mepesi kukazia).

Basi tunaona kwamba Baba alimpenda Yesu kwa sababu ya utii wake kukubali kufa. Upendo unaokubali unadai kila kitu kiwe sawa. Yesu alipata na kustahili upendo wa Baba Yake.

Pia, Yesu alitamka kwamba alikaa katika pendo la Baba Yake kwa kuzishika amri za Baba Yake.

Kama Baba alivyonipenda mimi, mimi nami nimewapenda ninyi. Kaeni katika pendo langu. Mkizishika amri zangu mtakaa katika pendo langu; kama mimi nilivyoshika amri za Baba yangu na kukaa katika pendo Lake (Yohana 15:9-10, TLR. Maneno mepesi kukazia).

Tena, kama tunavyoona katika mstari huu, tunatakiwa kufuata mfano wa Yesu na kukaa katika pendo Lake kwa kuzishika amri Zake. Anazungumza kuhusu upendo unaokubali katika fungu hili, na anatuambia kwamba tunaweza na tunapaswa kupata upendo Wake. Tena, kwamba tunaweza kujiondoa katika pendo Lake kwa kutokutii amri Zake. Tunadumu katika upendo Wake kama tutashika amri Zake tu. Kitu kama hicho hakifundishwi sana siku hizi, lakini kinapaswa kufundishwa, maana ndiyo aliyosema Yesu.

Yesu alithibitisha upendo unaokubali wa Mungu kwa wale tu wanaozishika amri Zake, hivi:

Kwa sababu Baba Mwenyewe anawapenda, kwa kuwa mmenipenda Mimi na kuamini kwamba nilitoka kwa Baba (Yohana 16:27, TLR. Maneno mepesi kukazia).

Yeye aliye na amri zangu na kuzishika ndiye anipendaye; naye anipendaye atapendwa na Baba yangu. Mimi pia nitampenda na kujidhihirisha kwake … Mtu yeyote akinipenda, atashika maneno Yangu; na Baba Yangu atampenda, nasi tutakuja kwake na kufanya makao yetu pamoja naye (Yohana 14:21, 23, TLR. Maneno mepesi kukazia).

Ona katika fungu la pili kwamba Yesu hakuwa anatoa ahadi kwa waamini wasiojitolea Kwake, kwamba, kama wangeanza kuyashika maneno Yake, angewakaribia kwa njia ya kipekee sana. Hapana! Yesu alikuwa anaahidi kwamba kama mtu yeyote angeanza kumpenda Yeye na kuyashika maneno Yake, basi Baba Yake angempenda mtu huyo, na wote wawili – Yeye na Baba – wangekuja kukaa katika mtu huyo, ambayo ni njia nyingine ya kusema kwamba amezaliwa mara ya pili. Kila mtu aliyezaliwa mara ya pili anaye Baba na Mwana ndani yake, kwa njia ya Roho Mtakatifu (tazama Warumi 8:9). Basi, hapo tena tunaona kwamba wale waliozaliwa upya kweli kweli ni wale wenye kutubu na kuanza kumtii Yesu, nao ndiyo watakaoweza kupata ule upendo unaokubali, wa Baba.

Bado Yesu anao ule upendo wa rehema kwa ajili ya watakaomwamini. Wanapoacha kumtii, Yeye yuko tayari kuwasamehe kama watakiri dhambi zao na kuwasamehe wengine.

Hitimisho

Kinachosemwa ni hiki: Mungu hawapendi watoto Wake watiifu kwa namna ile ile anayowapenda wenye dhambi. Anawapenda wenye dhambi kwa upendo wa rehema tu, na upendo huo ni wa muda, unaodumu mpaka wanapokufa. Wakati huo huo anapowapenda kwa upendo wa rehema, anawachukia kwa chuki itokanayo na kutokubali tabia na mwenendo wao. Hayo ndiyo mafundisho ya Maandiko.

Kwa upande mwingine ni kwamba, Mungu anawapenda watoto Wake zaidi kuliko wale ambao hawajazaliwa mara ya pili. Kimsingi, anawapenda kwa upendo unaokubali kwa sababu wametubu na wanajitahidi kutii amri Zake. Wanapokua katika utakatifu, sababu ya kuwapenda kwa upendo wa rehema zinapungua, na sababu za kuwapenda kwa upendo unaokubali zinaongezeka, na ndicho wanachotaka.

Vile vile tunachoona hapa ni kwamba jinsi wahubiri wengi wa kisasa na waalimu wanavyoonyesha upendo wa Mungu si sahihi. Kulingana na kinachosemwa na Maandiko, hebu tafakari kidogo semi hizi za kawaida kuhusu upendo wa Mungu.

1) Hakuna chochote unachoweza kufanya kitakachomfanya Mungu akupende zaidi au pungufu ya anavyokupenda sasa hivi.

2) Hakuna chochote unachoweza kufanya kitakachomfanya Mungu aache kukupenda.

3) Upendo wa Mungu hauna masharti.

4) Mungu anampenda kila mtu sawasawa.

5) Mungu anampenda mwenye dhambi, lakini anachukia dhambi yake.

6) Hakuna chochote unachoweza kufanya ili upate au kustahili upendo wa Mungu.

7) Upendo wa Mungu kwetu hautegemei tunavyotenda.

Hayo yote yaliyosemwa hapo juu yanaweza kukupotosha au ni uongo kabisa,

maana sehemu kubwa inakataa moja kwa moja upendo wa kukubali wa Mungu, na mengi yanaeleza vibaya upendo wa rehema wa Mungu.

Kuhusu la kwanza – Kuna kitu waamini wanachoweza kufanya kitakachomfanya Mungu awapende na kuwakubali zaidi: wawe watiifu zaidi. Na kuna kitu wanachoweza kufanya ili kumfanya Mungu asiwapende sana na kuwakubali: waache kutii. Kwa wenye dhambi, kuna kitu wanachoweza kufanya kitakachomfanya Mungu awapende zaidi: watubu. Kisha wangejipatia upendo wa kukubalika wa Mungu. Na kuna kitu wanachoweza kufanya kitakachomfanya Mungu asiwapende zaidi: kufa. Hapo watakuwa wamepoteza upendo wa pekee ambao Mungu alikuwa nao kwa ajili yao – yaani, upendo wa rehema.

Kuhusu la pili – Mkristo anaweza kupoteza upendo wa kukubalika na Mungu kwa kurudia dhambi – kujiweka katika nafasi ya kupokea upendo wa rehema tu wa Mungu. Tena, asiyeamini angeweza kufa, na hilo lingekomesha upendo wa rehema wa Mungu, ambao ndiyo pekee alikuwa nao kwa ajili yake.

Kuhusu la tatu – Upendo wa kukubalika wa Mungu ni wa masharti. Na hata upendo wa rehema wa Mungu ni wa masharti kwamba mtu awe hai kimwili. Baada ya kifo, upendo wa rehema wa Mungu unakoma. Basi, ni wa masharti kwa sababu ni wa muda tu.

Kuhusu la nne – Ni kweli kwamba Mungu hawapendi wote kwa kiwango kinachofanana, kwa sababu wote – wenye dhambi na watauwa – anawakubali au kuwakataa kwa kiwango fulani. Ni kweli kwamba upendo wa Mungu haufanani kwa wenye dhambi na watakatifu.

Kuhusu la tano – Mungu anawachukia wenye dhambi pamoja na dhambi zao. Ingekuwa afadhali kusema kwamba anawapenda wenye dhambi kwa upendo wa rehema na anachukia dhambi zao. Kwa habari ya upendo wa kukubali, anawachukia.

Kuhusu la sita – Mtu yeyote anaweza na anapaswa kupata upendo wa kukubalika na Mungu. Ila, hakuna awezaye kuupata upendo wa rehema, maana wenyewe hauna masharti.

Kuhusu la saba – Upendo wa rehema wa Mungu hautokani na matendo, bali ule wa kukubalika unategemea matendo.

Yote hayo ni kwa sababu hii: Mtumishi anayefanya watu kuwa wanafunzi anapaswa kueleza upendo wa Mungu kwa usahihi, kama unavyoelezwa katika Biblia, kwa sababu hataki mtu yeyote adanganywe. Ni watu ambao Mungu anawapenda kwa kuwakubali tu ndiyo watakaoingia mbinguni, na Mungu anawapenda na kuwaubali wale waliozaliwa mara ya pili, na wenye kumtii Yesu. Mtumishi anayefanya wengine kuwa wanafunzi kamwe asifundishe kitu kinachoweza kuwafanya watu waondoke kwenye utakatifu. Lengo lake ni sawa na lile la Mungu – kuwafanya wanafunzi watakaotii amri zote za Kristo.


[1] Mahubiri ya Injili yanayofanywa na wainjilisti yahesabiwe kuwa ni aina ya kufundisha. Wainjilisti wanatakiwa kutangaza Injili iliyo sahihi KiBiblia.

[2] Si waamini wote waliopewa wajibu wa kufundisha makundi ya watu, ila wote wana wajibu wa kufundisha mtu kwa mtu, wanapowafanya watu kuwa wanafunzi (taszama Mathayo 5:19; 28:19-20; Wakolosai 3:16; Waebrania 5:12).

[3] Nasema “kama” kwa sababu walio mbwa mwitu waliovaa mavazi ya kondoo ni “watumishi” wenye makusudi ya ubinafsi. Hao watatupwa jehanamu. Nadhani kinachowatenganisha na watumishi wa kweli wenye makusudi yasiyo sahihi ni kiwango cha kinachowasukuma.

[4] Cha kushangaza ni hiki: Kuna waalimu wengine wanaofundisha kwamba pale kwenye kilio na kusaga meno ni eneo fulani nje kidogo ya mbinguni. Wanasema kwamba hapo, waamini wasiokuwa waaminifu watapewa nafasi ya kuomboleza – kwa muda fulani – kupoteza thawabu kwao, mpaka Yesu atakapowafuta machozi, kisha awakaribishe mbinguni! Wanafundisha hivyo kwa sababu ya kushindwa kuepuka ukweli kwamba Yesu alikuwa anawaonya wanafunzi Wake wa karibu sana, na kwamba mtumwa asiyekuwa mwaminifu ni mwamini.

[5] Ieleweke kwamba Wakristo watendao dhambi moja hawapotezi wokovu wao saa hiyo hiyo. Wale wanaotubu dhambi zao wanasamehewa na Mungu (kama nao watawasamehe wenye kuwakosea). Wale wasiomwomba Mungu msamaha wanajiweka katika hatari ya kuadhibiwa na Mungu. Waamini wanaweza kupoteza wokovu wao kama wataifanya mioyo yao kuwa migumu, katika kipindi cha kuadhibiwa na Mungu.

[6] Kama bado kuna wasioamini kwamba Mkristo anaweza kupoteza wokovu wake, hebu watazame maandiko yote yafuatayo katika Agano Jipya: Mathayo 18:21-35; 24:4-5, 11-13, 23-26, 42-51; 25:1-30; Luka 8:11-15; 11:24-28; 12:42-46; Yohana 6:66-71; 8:31-32, 51; 15:1-6; Matendo 11:21-23; 14:21-22; Warumi 6:11-23; 8:12-14, 17; 11:20-22; 1Wakor. 9:23-27; 10:1-21; 11:29-32; 15:1-2; 2Wakor. 1:24; 11:2-4; 12:21 – 13:5; Wagalatia 5:1-4; 6:7-9; Wafilipi 2:12-16; 3:17 – 4:1; Wakolosai 1:21-23; 2:4-8, 18-19; 1Wathes. 3:1-8; 1Timo. 1:3-7, 18-20; 4:1-16; 5:5-6, 11-15; 6:9-12, 17-19, 20-21; 2Timo. 2:11-18; 3:13-15; Waebrania 2:1-3; 3:6-19; 4:1-16; 5:8-9; 6:4-9, 10-20; 10:19-39; 12:1-17, 25-29; Yakobo 1:12-16; 4:4-10; 5:19-20; 2Petro 1:5-11; 2:1-22; 3:16-17; 1Yohana 2:15-28; 5:16; 2Yohana 6-9; Yuda 20-21; Ufunuo 2:7, 10-11, 17-26; 3:4-5, 8-12, 14-22; 21:7-8; 22:18-19. Maandiko “ya kuthibitisha” yatolewayo na wale wenye kufundisha usalama wa milele wa wokovu bila masharti ni yenye kutilia mkazo uaminifu wa Mungu katika wokovu, na wala hayasemi chochote juu ya wajibu wa mwanadamu. Kwa hiyo, lazima yafasiriwe na kulingana na hayo maandiko mengi niliyoorodhesha hapo juu. Ahadi ya Mungu kwamba ni mwaminifu si uhakikisho kwamba na mwingine ni mwaminifu kama Yeye. Kumwahidi mke wangu kwamba sitamwacha, na kuitunza ahadi yangu, si uhakikisho kwamba yeye hataniacha!

[7] Hoja inaweza kutolewa kwamba maandiko hayo yote yenye kuonyesha chuki na Mungu kuwazira wenye dhambi yanatoka katika Agano la Kale. Ni sawa, lakini hali ya moyo ya Mungu kuhusu wenye dhambi haitofautiani katika Agano la Kale na katika Agano Jipya. Yesu alipokutana na mwanamke Mkanaani katika Mathayo 15:22-28 ni mfano mzuri katika Agano Jipya. Mwanzoni, Yesu alikataa hata kujibu kilio chake, akamwita mbwa. Imani yake isiyokata tamaa ilisababisha Yeye kumwonyesha rehema kiasi fulani. Hali ya moyo aliyokuwa nayo Yesu kuhusu waandishi na Mafarisayo haiwezi kuhesabiwa kwamba ilikuwa upendo wenye kuwakubali (ona Mathayo 23).

Makanisa Ya Nyumbani

Sura Ya Nne

 

Watu wanaposikia kwa mara ya kwanza kuhusu makanisa ya nyumbani, mara nyingi wanafanya makosa na kudhani kwamba tofauti pekee kati ya makanisa ya nyumbani na makanisa majengo ni ukubwa wake na uwezo wa kutoa “huduma”. Mara nyingi watu hudhania kwamba kanisa la nyumbani haliwezi kutoa huduma kwa kiwango kinachotolewa na makanisa jengo. Ila – kama mtu anafafanua “huduma” kwamba ni kile kinachochangia kuwafanya watu kuwa wanafunzi, kuwasaidia wawe kama Kristo na kuwawezesha wafanye huduma, basi makanisa jengo hayana cha zaidi. Kama nilivyo-onyesha hapo nyuma, yanaweza hata kulemewa. Ni kweli kwamba makanisa ya nyumbani hayawezi kutoa wingi wa shughuli zinazofanywa katika makanisa jengo, lakini yanaweza kuwa bora sana kwenye kutoa huduma ya kweli.

Watu wengine hukataa kwamba makanisa ya nyumbani si makanisa ya kweli kwa kuwa hayana majengo. Kama hao watu wangeishi wakati wowote katika zile karne tatu za kwanza za kanisa, wangekataa kila kanisa duniani. Yesu alitangaza hivi: “Mahali popote ambapo wawili au watatu wamekusanyika pamoja katika Jina langu, nipo katikati yao” (Mathayo 18:20). Yesu hakusema chochote kuhusu mahali pa waamini kukutanika. Na hata kama wapo waamini wawili tu, aliahidi kuwepo kama watakusanyika katika Jina Lake. Kitu ambacho wanafunzi wa Kristo hufanya mara nyingi katika mahoteli, wakila chakula pamoja na kushirikishana kweli, wakifundishana na kuonyana, hufanana zaidi na utaratibu wa Agano Jipya kwa habari ya kukusanyika kama kanisa, kuliko mambo yanayotokea katika majengo mengi ya kanisa siku za Jumapili asubuhi.

Katika sura iliyotangulia niliorodhesha baadhi ya faida ambazo makanisa ya nyumbani yanazo, ambayo makanisa jengo hayana. Ningependa kuanza sura hii kwa kutoa sababu zingine kadhaa kuonyesha ni kwa nini kanisa la nyumbani ni kitu cha KiBiblia kinachofaa sana kufanikisha lengo la kuwafanya watu kuwa wanafunzi. Lakini, nianze kwa kusema kwamba lengo langu si kushambulia makanisa jengo wala wachungaji wao. Kuna wachungaji wengi sana wenye majengo ambao ni wacha Mungu na wenye kumaanisha moyoni mwao, wanaofanya kila wanachoweza katika utaratibu wao kumpendeza Bwana. Mimi huwahudumia maelfu ya wachungaji wa aina hiyo kila mwaka, nami nawapenda sana na kuwafuahia. Ni watu wa maana sana duniani. Kwa kuwa ninajua ugumu wa kazi zao ndiyo sababu nataka kuleta hili jambo mbadala ambalo litawasaidia kuepukana na mateso kiasi fulani na kuwawezesha wafanikiwe na kufurahi pia. Utaratibu wa kanisa la nyumbani ni wa KiBiblia na wenye kutoa nafasi ya kufanikiwa kuwafanya watu kuwa wanafunzi, na kupanua ufalme wa Mungu. Sina shaka kwamba wachungaji wengi wenye majengo wangefurahi zaidi na kufanikiwa zaidi na kutosheka zaidi kama wangehudumu katika mfumo wa makanisa ya nyumbani.

Mimi mwenyewe nilikuwa mchungaji mwenye jengo kwa zaidi ya miaka ishirini, na nilijitahidi sana wakati huo kwa kile nilichojua. Lakini baada ya kutembelea makanisa mengi kwa miezi mingi sana siku za Jumapili ndipo nilipata picha ya kuhudhuria kanisa kama “mshirika”. Nilifunguliwa macho nami nikaanza kuelewa ni kwa nini watu wengi hawana hamu sana ya kuhudhuria ibada. Mimi – kama wengine wote – nikaanza kuketi kwa heshima na uungwana sana – nikisubiri ibada iishe. Ambaye hakuwa na shida ni mchungaji tu! Ibada ilipomalizika, nafasi ilikuwepo ya kushirikiana na wengine kama mmoja wao badala ya kuwa mtazamaji aliyechoka. Jambo hilo pamoja na mengine lilihusika kunifanya nianze kufikiri juu ya kitu kingine kilicho bora, nami nikaanza kufanya utafiti kuhusu kanisa la nyumbani. Nilishangaa kugundua kwamba kuna mamilioni ya makanisa aina hiyo duniani kote, na nikafikia uamuzi kwamba bila shaka makanisa yanayokutania majumbani yana kitu cha zaidi kuliko makanisa jengo.

Wachungaji wengi wanaosoma kitabu hiki hawana makanisa yanayokutania majumbani. Wao ni wachungaji wa makanisa jengo. Najua kwamba mengi niliyoandika yanaweza kuwa magumu kwao kukubali upesi, kwa sababu yanaonekana ni ya kitofauti sana. Lakini nawaomba wajipe muda wa kutosha kutafakari nitakachosema. Wala sitazamii kwamba watakubaliana na kila kitu kwa siku moja. Lakini, nimewaandikia wachungaji, nikisukumwa na upendo nilio nao kwao na makanisa yao.

Aina Pekee Ya Kanisa Katika Biblia

Cha kwanza: Makanisa yenye kukutanika kwenye majengo maalum hayajulikani katika Agano Jipya. Makanisa yenye kukutania majumbani yalikuwa ndiyo kawaida katika siku za kanisa la kwanza. Tazama Maandiko yafuatayo:

Naye alipotambua hilo, alikwenda moja kwa moja hadi nyumbani kwa Mariamu, mama yake Yohana aliyeitwa Marko pia, ambapo watu wengi walikuwa wamekusanyika pamoja, wakiomba (Matendo 12:12 – TLR. Maneno mepesi kukazia).

… Jinsi ambavyo sikujizuia kuwaambia chochote chenye faida na kuwafundisha hadharani [lakini si katika jengo la kanisa] na nyumba hadi nyumba … (Matendo 20:20 – TLR. Maneno mepesi kukazia).

Wasalimuni Priska na Akwila … pamoja na kanisa lililo nyumbani mwao (Warumi 16:3-5, TLR – maneno mepesi kukazia. Ona pia Warumi 16:14-15 ambapo yawezekana makanisa mengine mawili ya aina hiyo yanatajwa, huko Rumi).

Makanisa ya Asia yanawasalimu. Akwila na Priska wanawasalimu sana katika Bwana, pamoja na kanisa lililo nyumbani mwao (1Wakor. 16:19 – TLR. Maneno mepesi kukazia).

Wasalimuni ndugu walioko Laodikia, pamoja na Nimpa, na kanisa lililo nyumbani mwake (Wakolosai 4:15 – TLR. Maneno mepesi kukazia).

Na kwa dada yetu Afia, na Arkipo, mtenda kazi mwenzetu, na kwa kanisa lililo nyumbani mwako … (Filemoni mstari wa 2 – TLR. Maneno mepesi kukazia).

Imeelezwa kuwa sababu ya pekee ya kanisa la kwanza kutojenga majengo ni kwamba lilikuwa changa. Lakini huo uchanga ulidumu kwa muda mrefu sana basi, kulingana na historia ya Agano Jipya (na karne mbili baada ya hapo)! Kama kujenga majengo ni alama ya kukomaa kwa kanisa, basi kanisa la mitume tunalosoma habari zake katika kitabu cha Matendo hlikuwahi kukomaa kamwe.

Napendekeza kuwa sababu ya mtume hata mmoja kutojenga kanisa ni kwamba ingehesabiwa kuwa nje ya mapenzi ya Mungu, maana Yesu hakuacha mfano wa namna hiyo wala agizo. Aliweza kupata wanafunzi bila ya majengo maalum, na aliwaambia wanafunzi Wake wafanye watu kuwa wanafunzi. Wasingeona haja yoyote ya kuwa na jengo. Yesu alipowaambia wanafunzi Wake waende duniani kote na kuwafanya watu kuwa wanafunzi, wasingefikiri hivi: “Anachotaka Yesu tufanye ni kujenga majengo na kutoa mahubiri kwa watu humo, mara moja kwa juma”.

Tena, kujenga majengo maalum kungeweza kuhesabiwa kuwa ni kuhalifu amri ya Kristo ya kutojiwekea hazina duniani – yaani kupoteza fedha kwenye kitu ambacho hakikuwa cha lazima – na kuuibia ufalme wa Mungu rasilmali ambazo zingeweza kutumiwa kwenye huduma ya kubadilisha maisha.

Uwakili Wa Kikristo Wa Mali

Tunafikia faida ya pili ya makanisa yenye kukutania majumbani: aina hii ya kanisa hukuza uwakili mzuri wa rasilmali za washirika. Jambo hilo ni muhimu sana katika uanafunzi.[1] Hakuna fedha itakayopoelea kwenye majengo: ili kuyamiliki, kukodisha, kukarabati, kupanua, kufanya upya, kuyapasha joto wakati wa baridi kali au kuyapooza wakati wa joto kali. Basi – kile ambacho kingepotea kwa habari ya majengo kinaweza kutumiwa kuwalisha na kuwavika walio maskini, au kueneza Injili na kuwafanya watu kuwa wanafunzi, sawa na ilivyokuwa katika kitabu cha Matendo. Hebu fikiri mambo mazuri ambayo yangefanywa kwa ajili ya ufalme wa Mungu kama mabilioni ya shilingi yanayotumiwa kwa majengo ya kanisa yangetumiwa kueneza Injili na kuwahudumia maskini! Hata haifikiriki.

Tena, makanisa ya nyumbani yenye washirika wasiozidi ishirini yangeweza kusimamiwa hata na wazee au wachungaji au waangalizi “washona mahema” (yaani, wasiolipwa na kanisa). Hicho ni kitu kinachowezekana ikiwepo idadi kubwa ya waamini waliokomaa katika kanisa la nyumbani. Makanisa kama hayo yasingehitaji fedha nyingi kufanya kazi!

Biblia inafundisha kwamba wazee au wachungaji au waangalizi wanapaswa kulipwa kulingana na kazi yao, kwa hiyo wale wanaotumia muda wao wote kwenye huduma wanapaswa waishi kwa hiyo (ona 1Timo. 5:17, 18). Watu kumi wenye kazi za mshahara katika kanisa la nyumbani wanaotoa zaka wanaweza kumtunza mchungaji mmoja aishi maisha ya wastani. Watoa zaka watano katika kanisa la nyumbani wanaweza kumweka huru mchungaji atoe nusu ya jumla ya muda wake wote katika juma kufanya huduma.

Kwa kufuata mtindo wa makanisa ya nyumbani, fedha ambazo zingetumiwa kwa majengo zinakuwa huru kuwasaidia wachungaji. Basi, wachungaji wenye makanisa jengo wasifikiri kwamba kuongezeka kwa makanisa ya nyumbani ni tishio kw ausalama wao kikazi. Ni kwamba watu wengi zaidi wangeweza kufanikisha azma ambayo Mungu ametia katika mioyo yao kwamba wamtumikie katika huduma.[2] Hilo lingesaidia kufanikisha lengo la kufanya watu kuwa wanafunzi. Tena, kanisa la nyumbani lenye wafanyakazi ishirini lingeweza kutoa nusu nzima ya mapato yake kwa ajili ya umisheni na kuwasaidia maskini.[3]

Kama kanisa lenye jengo lingefanya kazi kwa kuwa na mtandao wa makanisa ya nyumbani, watu ambao wangepoteza ajira ni watumishi waandamizi – makatibu tawala na wengine wenye huduma maalum (mfano: watumishi wa watoto na vijana katika makanisa makubwa), ambao wangekataa kubadili huduma zisizokuwa na msingi KiBiblia ili wapate zenye msingi. Makanisa ya nyumbani hayana hajaya watumishi wa watoto na vijana kwa sababu wazazi wamepewa jukumu hilo katika Biblia. Kwa kawaida, watu katika makanisa ya nyumbani hujaribu kufuata Biblia kuliko kawaida za Ukristo wa kitamaduni. Vijana wa Kikristo ambao hawana wazazi Wakristo wanaweza kuingizwa katika makanisa ya nyumbani na kufanywa wanafunzi, sawa tu na inavyokuwa katika makanisa ya kawaida. Je, hamshangai kwamba katika Agano Jipya hawatajwi “wachungaji wa vijana” au “wa watoto”? Huduma hizo hazikuwepo kwa takriban miaka elfu moja na mia tisa hivi ya Ukristo. Mbona sasa zimekuwa za lazima, tena katika nchi za magharibi ambazo ni tajiri?[4]

Mwisho: Katika mataifa maskini, wachungaji mara nyingi hupata shida kukodisha au kuwa na majengo ya kanisa bila ya kusaidiwa na Wakristo wa nchi za Magharibi. Matokeo mabaya ya hali hii ni mengi, ila ukweli ni kwamba kwa miaka mia tatu, tatizo hilo halikuwepo katika Ukristo. Kama wewe ni mchungaji katika nchi inayoendelea, na kusanyiko lako haliwezi kujipatia jengo, huna haja ya kumpaka mafuta Mmarekani fulani aliyekutembelea ili ujipatie. Mungu amekwisha tatua tatizo lako tayari. Huna haja ya kuwa na jengo ili kufanikiwa katika kuwafanya watu kuwa wanafunzi. Fuata mpango wa Biblia tu.

Mwisho Wa Familia Zilizogawanyika

Kitu kingine ambacho makanisa yanayokutania nyumbani yanacho ni hiki: yanafanikiwa sana kuwafundisha watoto na vijana. Uongo mmoja mkubwa sana wenye kuenezwa na makanisa makubwa ya Marekani ni kwamba wanatoa huduma nzuri sana kwa watoto na vijana. Wanachoficha ni kwamba, idadi kubwa ya watoto wanaofurahia huduma zao kanisani hawarudi tena baada ya kuondoka nyuumbani. (Mwulize mchungaji yeyote wa vijana akupe takwimu – anazijua vizuri.

Tena, makanisa yenye wachungaji kwa ajili ya vijana na watoto huwaambia wazazi uongo wa kudumu, kwamba wao hawawezi au hawawajibiki kutoa mafunzo ya kiroho kwa watoto wao. “Tutashughulika na mafunzo ya kiroho ya watoto wako. Sisi ni wataalamu katika hilo.”

Jinsi utaratibu ulivyo husababisha kushindwa, kwa sababu hujenga mzunguko wa kuachilia mambo. Huanza na wazazi wanaotafuta makanisa ambayo watoto wao watayafurahia. Ikiwa wakati wa kurudi nyumbani Yohana atasema kwenye gari kwamba alifurahia kanisa hilo, wazazi wanafurahi sana kwa sababu wanaona kufurahia kanisa kwa Yohana ni sawa na yeye kupenda mambo ya kiroho. Mara nyingi wanakuwa wamekosea sana.

Wachungaji “viongozi” wanaotafuta mafanikio hutaka makanisa yao yakue. Basi, wale wachungaji wanaohusika na vijana au watoto huondoka kwenye vikao wakiwa wamebanwa kutengeneza mipango “ifaayo”, ambayo watoto wataipenda. (“Ifaayo” maana yake “yenye kuvutia”. Tena haimaanishi, “Waongoze watoto kutubu, kuamini na kutii amri za Yesu”.) Kama watoto watakubaliana na mipango hiyo, wazazi (ambao hawajui mengi) watarudi hapo (na fedha zao), na kanisa litakua.

Kufanikiwa kwa makundi ya vijana kanisani hupimwa kwa mahudhurio. Wachungaji wa vijana hujikuta wakifanya chochote wanachoweza ili kuwajaza, na mara nyingi hiyo inamaanisha kupunguza hali ya kweli ya kiroho. Mhurumie mchungaji wa vijana atakayesikia kwamba wazazi wananung’unika kwa mchungaji kiongozi kwamba vijana wao wanalalamika juu ya mahubiri anayotoa, ya hukumu na yenye kuwachosha.

Lakini, wachungaji wa vijana wanaweza kuwa baraka sana katika mwili wa Kristo wakiwa viongozi wa makanisa ya nyumbani. Kwa kawaida, wana ujuzi mkubwa tayari wa mahusiano, na wana shauku ya ujanani na nguvu tele. Wengi wao ni wachungaji wa vijana tu kwa sababu ndiyo hatua ya kwanza kwao kufikia ujuzi ule usio wa kawaida unaotakiwa kufaulu kama mchungaji kiongozi. Wengi wao wana uwezo wa kusimamia makanisa ya nyumbani. Walichokuwa wanafanya katika kundi la vijana kinakaribia utaratibu wa KiBiblia wa kanisa kuliko kilichokuwa kinaendelea katika kanisa kubwa! Hayo hayo yanaweza kusemwa juu ya wachungaji wa watoto, ambao si ajabu wako maili nyingi sana mbele ya wachungaji viongozi wengi, kwa habari ya kuweza kutumika katika makanisa ya nyumbani, ambayo kila mtu – pamoja na watoto, huketi kwenye mduara, na kushiriki kila kitu – mpaka hata chakula.

Kwa kawaida watoto na vijana hufanyika wanafunzi vizuri zaidi katika makanisa ya nyumbani, wanapo-ona jumuiya ya kweli ya Kikristo na kupata nafasi za kushiriki, kuuliza maswali na kuhusiana na watu wa umri tofauti – wote wakiwa kama familia moja ya Kikristo. Katika makanisa jengo wanachokiona ni maonyesho makubwa na “starehe” katika kujifunza, hawapati nafasi kubwa ya kujua jumuiya ya kweli, na mara nyingi wanaona unafiki. Kama shuleni, wanajifunza tu jinsi ya kuhusiana na watu wa umri wao.

Lakini katika kusanyiko lenye watu wa umri zote, vipi kuhusu watoto wanaolia au watoto wadogo ambao hawatulii?

Hao wafurahiwe tu, na hatua zifaazo zichukuliwe kuwashughulikia wanapoleta matatizo. Kwa mfano: Wanaweza kupelekwa chumba kingine kunyamazishwa na kushguhulikiwa huko – hata wakapewa kitu cha kufanya kama kuchora. Katika jumuiya ya kanisa la nyumbani, watoto wadogo na wa kawaida si tatizo linalopelekwa mahali pa kulelewa watoto, penye kusimamiwa na mtu wasiyemfahamu. Hapana – wanapendwa na kila mmoja katika familia hiyo kubwa. Mtoto anayeanza kulia katika kanisa jengo anasumbua ule mtiririko wa ibada na analeta aibu kwa wazazi wake, wanaoweza kuhisi jinsi watu wasiowajua wanavyowatazama kwa macho mabaya. Mtoto anayeanza kulia katika kanisa la nyumbani amezungukwa na watu wa familia yake, na hakuna anayejali sana ukumbusho kwamba kuna zawadi ndogo kutoka kwa Mungu katikati yao – mtu ambaye wote wamewahi kumkumbatia.

Wazazi ambao watoto wao hawana nidhamu wanaweza kufundishwa kwa upole na wazazi wengine kinachotakiwa. Waamini wanakuwa na mahusiano ya kweli na yenye kujali. Hawasengenyani kama ilivyo kawaida katika makanisa jengo. Wanajuana na wanapendana.

Wachungaji Wenye Furaha Na Heri

Baada ya kuchunga makanisa kwa miaka zaidi ya ishirini, na kuzungumza na wachungaji maelfu duniani kote, pamoja na kuwa na marafiki binafsi ambao ni wachungaji, nadhani ninaweza kusema kwamba najua kiasi fulani cha uzito wa kuchunga kanisa la kisasa. Kama kila mchungaji mwenye kanisa jengo, mimi nina ujuzi na “upande wa giza” kihuduma. Huduma inaweza kuwa na giza sana wakati mwingine. Pengine neno bora zaidi ni “katili”.

Mara nyingi, yale matazamio ambayo wachungaji wengi hukutana nayo husababisha misukumo ambayo wakati mwingine huharibu mahusiano katika familia zao wenyewe. Wachungaji huvunjika moyo kwa sababu nyingi sana. Inawabidi wawe wana-siasa, mahakimu, waajiri, wana-saikolojia, wakurugenzi wa shughuli, wajenzi, washauri wa ndoa, wasemaji bingwa hadharani, mameneja, wawezao kusoma mawazo na fikra za watu na wasimamizi. Mara nyingi wanajikuta katika mashindano makubwa sana na wachungaji wengine ili kupata kipande kikubwa zaidi cha mwili wa Kristo. Hawana muda wa kujiendeleza kibinafsi kwa habari ya kiroho. Wengi hujisikia kama wamenaswa katika kazi yao, halafu hawalipwi inavyostahili. Washirika wao ndiyo wateja wao na waajiri hapo hapo. Wakati mwingine hao waajiri na wateja hufanya maisha yao kuwa magumu sana.

Mchungaji wa kanisa la nyumbani ana maisha rahisi sana ukilinganisha na huyo tuliyetaja hapo juu. Kwanza: Kama ataishi maisha ambayo ni mfano wa mwanafunzi wa kweli na afundishe utii halisi kwa amri za Yesu, ni mbuzi wachache sana watakaotaka kuwa katika kundi hilo. Kule kukutania majumbani tu kunatosha kuwazuia mbuzi wengi wasifike. Kwa hiyo, ni kondoo ndiyo watakaokuwa wengi.

Pili: Anaweza kuwapenda na kuwafanya kondoo wake wote kuwa wanafunzi kibinafsi, kwa sababu anasimamia watu wazima kumi nambili hadi ishirini tu. Anaweza kufurahia kuwa karibu sana nao, maana anakuwa kama baba wa familia. Anaweza kuwapa wao muda wanaotaka. Ninakumbuka nilipokuwa mchungaji wa kanisa jengo, kwamba mara nyingi nilikuwa najisikia mpweke. Nisingeweza kuwa karibu na yeyote katika kusanyiko langu, wengine wasije wakanichukia kwa kutowaingiza katika kundi la marafiki wa karibu, au wasije kuwaonea wivu wale walio katika kundi hilo. Nilitamani sana kupata ukaribu wa kweli na waamini wengine, lakini sikuwa tayari kulipa hiyo gharama ya kupata marafiki wa kweli.

Katika familia yenye ukaribu kama kanisa la nyumbani, washirika wanasaidiana kumfanya mchungaji kuwajibika, maana yeye ni rafiki wa karibu – si mwigizaji aliyeko jukwaani.

Mchungaji wa kanisa la nyumbani anaweza kutumia muda mwingi tu kuzaa na kuwaendeleza viongozi kwa ajili ya makanisa ya nyumbani ya baadaye. Basi, wakati ukifika wa kuongezeka, viongozi tayari wapo. Halazimiki kuwatazama viongozi wake wazuri sana wa baadaye wakiondoa karama zao kanisani na kuzipeleka kwenye Shule ya Biblia mahali pengine.

Anaweza kuwa na muda wa kukuza huduma nyingine nje ya kusanyiko lake. Pengine anaweza kuhudumia gerezani, kwenye vituo vya utunzaji wazee au watoto, au anaweza kuhusika katika kushuhudia mtu mmoja mmoja kati ya wakimbizi au wafanya biashara. Kutegemana na ujuzi alio nao, anaweza kutumia muda wake mwingine kuanzisha makanisa mengine ya nyumbani, au kuwa kama msaada kwa wachungaji vijana wa makanisa ya nyumbani, ambao wamelelewa na kukua katika huduma yake.

Hajisikii msukumo wa kuwa mwigizaji wa Jumapili asubuhi. Hana haja ya kuandaa mahubiri yenye vipengele vitatu siku ya Jumamosi jioni, akitafakari jinsi anavyoweza kuwatosheleza watu wengi ambao wako katika viwango vingi tofauti vya kiroho.[5] Atafurahia kuona jinsi Roho Mtakatifu anavyomtumia kila mmoja kwenye makusanyiko hayo na kuwatia moyo watumie vipawa vyao. Anaweza asiwepo kwenye mikutano na kila kitu kiende sawa bila yeye.

Hana jengo la kumpoteza mawazo, wala watumishi wa kusimamia.

Hana sababu ya kushindana na wachungaji wengine.

Hakuna “bodi ya kanisa” ya kufanya maisha yake kuwa magumu, na ambayo hutumiwa kuingiza siasa za magomvi.

Ana nafasi ya kuwa kile alichoitwa na Mungu kuwa, sio kuwa kile ambacho Ukristo wa desturi unamlazimisha kuwa. Yeye si kama mwigizaji mkuu, au rais wa kampuni, au kitovu cha kila kitu. Yeye anafanya watu kuwa wanafunzi – ni mkamilishaji au mwezeshaji wa watakatifu.

Kondoo Wenye Furaha Na Heri

Kila kitu kuhusu makanisa ya nyumbani ya kweli na ya KiBiblia ndicho hutakiwa na waamini wa kweli na ndicho wanachofurahia.

Waamini wote wa kweli wanatafuta mahusiano ya kweli na waamini wengine, kwa sababu upendo wa Mungu umemiminwa mioyoni mwao. Mahusiano kama hayo ni sehemu ya makanisa ya nyumbani. Hicho ndicho kinaitwa ushirika katika Biblia – ile hali ya kweli ya kuwashirikisha ndugu na dada maisha yako. Makanisa ya nyumbani huzaa mazingira ambayo waamini wanaweza kutenda yale ambayo waamini wengine wanapaswa kutenda, kama inavyotajwa katika vifungu vingi ya Agano Jipya vyenye maneno haya: “ninyi kwa ninyi”. Katika mazingira ya kanisa la nyumbani, waamini wanaweza kuonyana, kutiana moyo, kujengana, kufarijiana, kufundishana, kuhudumianana kuombeana. Wanaweza kuhimizana katika upendo na kazi njema, wanaweza kuungamiana dhambi, wanaweza kuchukuliana mizigo, na kusemezana kwa zaburi, nyimbo na tenzi za rohoni. Wanaweza kuomboleza na waombolezao, na kufurahi na wenye kufurahi. Mambo hayo hayatokei sana katika mikutano ya Jumapili asubuhi ya makanisa jengo, mahali ambapo waamini huketi na kutazama tu. Kama nilivyowahi kuambiwa na mshirika mmoja wa kanisa la nyumbani: “Mtu anapokuwa mgonjwa katika kundi letu, sipeleki chakula nyumbani kwa mtu nisiyemjua kwa kuwa nilijiandikisha kutoa ‘huduma ya chakula’ – napeleka chakula kwa mtu ninayemjua na kumpenda”.

Waamini wa kweli wanafurahia ushirikiano na wengine. Kuketi tu bila ya kufanya chochote na kusikiliza mahubiri yasiyo na maana au yasiyokuwa na faida yoyote mwaka baada ya mwingine ni kama tusi kwa akili na ufahamu wa wasikilizaji. Wangependelea kupata nafasi ya kushiriki kwa kutoa mitazamo wanayopata kuhusu Mungu na Neno Lake. Makanisa ya nyumbani yanatoa nafasi hiyo. Kufuata mpango wa KiBiblia kuliko wa kitamaduni ni hivi: “Kila mmoja ana zaburi, ana fundisho, ana ufunuo, ana ujumbe katika lugha, ana tafsiri” (1Wakor. 14:26 – TLR). Katika makanisa ya nyumbani, hakuna anayepotelea katika kundi au kuachwa na tabaka za kikanisa.

Waamini wa kweli hutamani kutumiwa na Mungu katika huduma. Nafasi ipo kwa kila mmoja kutumiwa katika kanisa la nyumbani, tena wajibu zinagawanywa kwa wote, ili mmoja asije akamalizika kutokana na wingi wa shughuli, kama ilivyo kawaida katika makanisa jengo. Kwa kiwango cha chini kabisa ni kwamba, kila mmoja anaweza kuleta chakula cha kuchangia mlo wa pamoja – kile kinachoitwa na Maandiko “karamu ya upendo” (Yuda mstari wa 12). Kwa makanisa mengi ya nyumbani, mlo huo hufanana na Chakula cha Mwisho cha Bwana, ambacho kwa kweli kilikuwa ni sehemu ya mlo wa kawaida kabisa wa Pasaka. Meza ya Bwana si “kula vitafunio vitakatifu vya Mungu” – kama mtoto mmoja mdogo alivyoita ibada hiyo wakati nikiwa mchungaji mahali. Tendo la kula mkate mdogo na kunywa maji kidogo sana ya matunda katikati ya wageni katika ibada fupi tu ni tofauti kabisa na Biblia na makanisa ya nyumbani. Utakatifu wa Meza ya Bwana unaongezeka sana kama ni mlo wa pamoja kati ya wanafunzi wanaopendana.

Katika kanisa la nyumbani, ibada ni rahisi, ya dhati na yenye kuwashirikisha watu wote – sio onyesho. Waamini wa kweli hupenda kumwabudu Mungu katika roho na kweli.

Mlingano Katika Mafundisho, Na Kuchukuliana

Katika makusanyiko ya vikundi vidogo vya uwazi kanisani, mafundisho yote yanaweza kuchunguzwa na mtu yeyote anayeweza kusoma. Ndugu na dada wanaojuana na kupendana inawabidi wafikiri kwa heshima sana mawazo ambayo ni tofauti na yao, na hata kama kundi zima halitakubaliana, kinachowaunganisha pamoja ni upendo, sio mafundisho. Fundisho lolote linalofanywa na yeyote katika kundi – hata wazee, wachungaji na waangalizi – linapimwa kwa upendo na mtu yeyote, kwa sababu Mwalimu Mkuu yumo ndani ya kila mmoja (ona 1Yohana 2:27). Ukaguzi na vipimo vitokanavyo na mfano wa KiBiblia huepusha kupotoka kiitikadi.

Hiyo ni tofauti kabisa na jinsi makanisa jengo yalivyo, maana mafundisho hupangwa na kuthibitishwa tangu mwanzo, na hayatakiwi kupingwa. Basi, mafundisho mabaya hudumu sana, na kipimo cha kukubalika ni itikadi. Kwa sababu hiyo, hoja moja tu katika mahubiri inaweza kusababisha wasiokubaliana nayo wote waondoke mara moja na kwenda kutafuta “waamini wenye mawazo kama yao” mahalipengine. Wanajua hakuna haja hata ya kuzungumza na mchungaji kuhusu kutokubaliana kwao kiitikadi. Hata kama angeshawishiwa abadilishe msimamo wake, itabidi iwe ni kwa siri na wengi kanisani wasijue, pamoja na wale wa ngazi za juu katika dhehebu lake. Tofauti za itikadi katika makanisa jengo huzaa wachungaji ambao ni wanasiasa bingwa katika dunia, wasemaji wazuri wajuao kusema kitu kisichoeleweka kwa urahisi na wenye kuepuka chochote kinachoweza kuleta ubishi. Hilo huwafanya wote waamini kwamba mchungaji yuko upande wake.

Mwelekeo Wa Kisasa

Cha kushangaza ni kwamba makanisa mengi siku hizi yameanza kuunda vikundi vidogo vidogo, wakitambua thamani yake katika uanafunzi. Hata makanisa mengine yanazidisha: Yanaunda kiini chake kwenye vikundi vidogo, wakivihesabu hivyo kuwa sehemu ya maana zaidi katika huduma yao. “Mikutano mikubwa ya kusherehekea” inakuwa ya pili kwa umuhimu – vikundi vidogo ndivyo vyenye umuhimu wa kwanza (kinadharia).

Hizo ni hatua nzuri kuelekea kuzuri, na Mungu hubariki hatua hizo, maana baraka Zake zinalingana na jinsi tunavyolingana na mapenzi Yake. Kwa kweli, “makanisa vikundi” yana utaratibu mzuri zaidi kuliko yale mengine, na yanarahisisha ufuasi. Yapo katikati ya makanisa jengo na makanisa ya nyumbani, maana yanachukua vichache kutoka pande zote mbili.

Lakini je, makanisa jengo ya kisasa yenye vikundi vidogo yanalinganaje na makanisa ya zamani ya nyumbani, au ya kisasa? Zipo tofauti.

Mfano: Wakati mwingine – kwa bahati mbaya sana – vikundi vya makanisa jengo hutumiwa kuendeleza yale makosa ya kanisa jengo – hasa inapotokea kwamba kusudi halisi la kuanzisha huduma ya vikundi vidogo ni kujenga ufalme wa kanisa la mchungaji kiongozi. Anawatumia watu kwa malengo yake mwenyewe, na vikundi vidogo huingia katika mpango wa namna hiyo vizuri sana. Inapokuwa hivyo, viongozi wa vikundi vidogo huchaguliwa kutokana na uaminifu wao kwa kanisa, na hawapaswi kuwa wenye vipawa au wenye uwezo wa kuongoza, isije kutokea kwamba Shetani atajaza vichwa vyao wazo kwamba wanaweza kufaulu peke yao. Aina hiyo ya sera huzuia kufanikiwa kwa vikundi vidogo, na hatimaye huwafukuza walioitwa kweli kweli na viongozi wenye nia ya kuongoza. Wanaishia kwenye Vyuo vya Biblia, na kanisa linakosa vipawa vyao, nao wanakwenda mahali pa kufundishwa kwa mihadhara badala ya kufanywa wanafunzi wakiwa kazini.

Vikundi vidogo katika makanisa jengo mara nyingi huishia kwenye kuwa vikundi vya kushirikiana tu. Tendo la kufanya watu kuwa wanafunzi halitokei. Kwa kuwa watu wanatakiwa kulishwa kiroho Jumapili asubuhi, vikundi vidogo mara nyingi hutilia mkazo vitu vingine zaidi ya Neno la Mungu, maana hawataki marudio ya Jumapili asubuhi.

Vikundi vidogo katika makanisa jengo mara nyingi husimamiwa na mtumishi wa kanisa badala ya kuzaliwa kwa Roho Mtakatifu. Vinakuwa utaratibu mwingine tena katika taratibu nyingi za kanisa. Watu wanapangwa kulingana na umri, hali zao kijamii, wanakotoka, vitu wanavyopenda, ndoa au kutokuwa nayo, na hata maeneo wanakotoka. Mara nyingi mbuzi wanachanganywa na kondoo. Mipango hiyo yote ya kimwili haiwasaidii waamini kujifunza kupendana licha ya tofauti zao. Kumbuka kwamba wengi katika kanisa la kwanza walikuwa mchanganyiko – Wayahudi na watu wa Mataifa. Mara nyingi walikula chakula pamoja, kitu kilichokatazwa kabisa na mapokeo ya Kiyahudi. Bila shaka wakati huo ulikuwa wa kujifunza sana! Bila shaka nafasi zilipatikana za kuonyesha mwenendo wa upendo! Ulikuwa ushuhuda mkubwa kuhusu nguvu za Injili! Sasa basi – kwa nini tunafikiri tunapaswa kuwagawa watu katika vikundi vinavyowafaa ili vikundi vidogo vifanikiwe?

Makanisa jengo yenye vikundi vidogo bado yana lile onyesho (au igizo!) la Jumapili asubuhi – mahali ambapo watazamaji wanaketi kuona mabingwa wakifanya vitu vyao. Vikundi vidogo haviruhusiwi kukutana wakati kuna ibada “halisi” kanisani – na hilo huonyesha kwamba ibada za kanisani ndiyo muhimu. Kwa sababu hiyo, wengi – kama si wote – katika wahudhuriaji ibada za Jumapili asubuhi hawapendi kujiunga au kuhusika na vikundi vidogo hata wakitiwa moyo, maana wanaona ni kitu cha hiari. Wanatosheka kwamba wanahudhuria ibada ya muhimu zaidi ya juma. Kwa hiyo, vikundi vidogo vinaweza kutiliwa mkazo kwamba ni muhimu, lakini umuhimu wake si kama ibada ya Jumapili asubuhi. Basi – nafasi bora zaidi ya kuwa na ushirika wa kweli, na uanafunzi na kukua kiroho inapuuzwa na kuonyeshwa si kitu. Ujumbe mbaya unapelekwa, kwamba, ibada ya kanisani ndiyo mfalme.

Tofauti Zingine

Makanisa jengo yenye vikundi vidogo bado yana mipango kama shirika – kila mtu anajua nafasi yake katika mtiririko wa vyeo. Walioko juu wanaweza kujiita “viongozi watumishi” lakini mara nyingi wao ni kama wakurugenzi wenye wajibu wa kufanya maamuzi ya kikurugenzi. Kadiri kanisa linavyozidi kukua ndivyo mchungaji anavyokuwa mbali na kundi lake. Kama yeye ni mchungaji wa kweli, na apate nafasi ya kukwambia ukweli, atakwambia kwamba alikuwa na furaha alipokuwa na kundi dogo.

Vivyo hivyo, makanisa jengo yenye vikundi vidogo bado huweka ile tofauti kati ya wachungaji na washirika wa kawaida. Kwa kawaida, viongozi wa vikundi vidogo wako chini ya wale mabingwa wanaolipwa. Masomo ya Biblia kwa kawaida yanatayarishwa na hao mabingwa au yanapitishwa nao, kwa kuwa viongozi wa vikundi vidogo hawawezi kuaminiwa kuwa na mamlaka mengi sana. Vikundi vidogo haviruhusiwi kuwa na Meza yaBwana wala kubatiza. Kazi hizo ‘takatifu’ zimetengwa kwa ajili ya watu maalum wenye vyeo na vyeti. Wale wanaoitwa kuingia katika huduma lazima waende Vyuo vya Biblia ili wafaulu kufanya huduma ya “kweli”, wajiunge na kundi lile maalum.

Vikundi vidogo katika makanisa jengo mara nyingi ni kama nakala ya ibada za kanisa tu. Muda wake si zaidi ya dakika 60 hadi 90, na mtu mmoja mwenye karama huongoza ibada na mwingine mwenye karama hutoa fundisho lililokubalika. Hakuna nafasi hata kidogo kwa Roho kuwatumia wengine, au kugawa karama, au kukuza watumishi.

Mara nyingi watu hawajitoi kuwa waaminifu kwa vikundi vidogo. Wanafika inapowezekana, na vikundi vyenyewe mara nyingi hupangwa kuwa vya muda. Basi, undani wa jumuiya hiyo ni mdogo sana – si kama makanisa ya nyumbani.

Kwa kawaida, vikundi vidogo katika makanisa jengo hukutana katikati ya juma ili kutoingilia shughuli za mwisho wa juma kwa kuwa na mkutano mwingine wa kanisa. Basi – mkutano wa kikundi katikati ya juma unatawaliwa na muda – usizidi masaa mawili kwa wanaoweza kuhudhuria. Unawazuia wale wenye watoto wadogo au wanaokaa mbali.

Hata kama makanisa jengo yatahamasisha huduma ya vikundi vidogo, bado kuna swala la jengo – kupoteza fedha tena. Ni hivi: Kama utaratibu wa vikundi vidogo utaongeza watu kanisani, fedha zitazidi kupotezwa kwa habari ya ujenzi. Tena, vikundi vidogo katika makanisa jengo husababisha nyongeza ya mfanyakazi mmoja atakayelipwa – fedha zaidi kwa ajili ya mpango mwingine wa kanisa.

Labda kibaya zaidi ni hiki: Wachungaji wa makanisa jengo yenye vikundi vidogo mara nyingi wanakuwa na mipaka katika kufanya watu kuwa wanafunzi, wao binafsi. Wana shughuli nyingi sana kwa sababu ya wajibu zao nyingi kiasi cha kwamba hawana nafasi kabisa ya kufanya watu kuwa wanafunzi. Wakijaribu sana ni kuwafundisha wale viongozi wa vikundi vidogo, lakini hata hilo huwa ni mikutano ya mara moja kwa mwezi.

Hayo yote yamesemwa ili kusema hivi: Kwa maoni yangu mimi – makanisa ya nyumbani yana mafanikio zaidi katika kufanya watu kuwa wanafunzi, kuwaongeza na kuwasaidia wanafunzi kufanya wengine kuwa wanafunzi. Tena, ni mpango wa KiBiblia kabisa kuliko makanisa jengo. Ila natambua kwamba mawazo yangu hayawezi kubadilisha mapokeo ya kanisa yaliyodumu karne na karne. Basi nashauri kwamba wachungaji wa makanisa jengo wafanye kitu kuelekea kwenye kuyafanya makanisa yao yafanane na mpango wa KiBiblia wa kufanya watu kuwa wanafunzi.[6] Wanaweza kufikiria kuwafanya viongozi wa siku za baadaye kuwa wanafunzi, au kuanzisha huduma ya vikundi vidogo. Wanaweza kuwa na “Jumapili Ya Kanisa La Kwanza” ambapo kanisa litafungwa na kila mtu apate nafasi ya kushiriki chakula nyumbani, na kujaribu kukutana kama Wakristo wa kwanza walivyofanya kwa karne tatu.

Wachungaji wenye vikundi vidogo makanisani mwao wanaweza kufikiri jinsi ya kuruhusu vikundi vidogo hivyo kuwa makanisa ya nyumbani, waone kitakachotokea. Ikiwa vikundi vidogo vitakuwa na afya na kuongozwa na viongozi walioitwa na Mungu – wachungaji au wazee au waangalizi – havitashindwa kuendelea vyenyewe. Havihitaji kanisa mama. Mbona usiwaweke huru?[7] Fedha za washirika zinazoingia kwenye kanisa mama zinaweza kumtunza mchungaji wa kanisa la nyumbani.

Je, ninapounga mkono makanisa ya nyumbani maana yake ni kwamba hakuna chema kuhusu makanisa jengo? Hapana! Makanisa jengo yanastahili pongezi ikiwa yanazaa wanafunzi wanaomtii Kristo. Lakini, mara nyingi, taratibu zao na mipango yao huwa ni vizuizi badala ya msaada katika kufikia lengo ambalo Kristo ametuwekea, na huua wachungaji.

Nini Hutokea Katika Mkutano Wa Nyumbani?

Makanisa ya nyumbani hayatakiwi kufanana, na kuna nafasi ya tofauti nyingi tu. Kila kanisa la nyumbani lionyeshe utamaduni na maisha ya jamii husika. Hii ni sababu moja ya kufanikiwa sana kufanya uinjilisti kwa makanisa ya nyumbani, hasa katika nchi ambazo hazina utamaduni wa Kikristo. Washirika wa makanisa ya nyumbani hawawakaribishi jirani zao kuingia kwenye kanisa jengo ambalo ni tofauti kabisa na kitu walichozoea, mahali ambapo watahusika katika taratibu za kigeni kabisa kwao. Mambo hayo wakati mwingine ni vizuizi vikubwa kwa watu kuokoka. Badala yake, wanawakaribisha jirani zao kula chakula na rafiki zao.

Kitu kikubwa katika mkutano wa kanisa la nyumbani ni mlo wa pamoja. Kwa makanisa mengi ya nyumbani, mlo huo ni pamoja na Meza ya Bwana, au ndiyo Meza ya Bwana. Kila kanisa la nyumbani kipekee linaweza kuamua jinsi ya kusababisha umuhimu wa kiroho wa Meza ya Bwana ujulikane. Kama tulivyokwisha tangulia kusema, Meza ya Bwana ya kwanza ilianza kama mlo wa kawaida tu wa Pasaka, uliokuwa na maana kubwa kiroho. Kuwa na Meza ya Bwana kama sehemu ya mlo wa kawaida ndiyo utaratibu uliofuatwa wakati waamini wa kanisa la mwanzo walipokutana. Tunasoma hivi juu yao:-

Wakawa wakidumu katika fundisho la mitume, na katika ushirika, na katika kuumega mkate, na katika kusali … Na siku zote kwa moyo mmoja walidumu ndani ya hekalu, wakimega mkate nyumba kwa nyumba, na kushiriki chakula chao kwa furaha na kwa moyo mweupe (Matendo 2:42, 46. Maneno mepesi kukazia).

Wakristo wa kwanza walikuwa wanashika mikate mikubwa, wanaimega na kuila pamoja – kitu kilichokuwa kawaida katika utamaduni wao kwa habari ya mlo. Je, huko kumega mkate katika chakula kulikuwa na maana fulani ya kiroho kwa Wakristo wa kwanza? Biblia haiweki wazi. Lakini, William Barclay, mwalimu maarufu sana, anaandika hivi katika kitabu chake kiitwacho (tafsiri) Meza Ya Bwana – “Hakuna shaka kwamba Meza ya Bwana ilianza kama mlo wa kifamilia au mlo wa marafiki katika nyumba … Jambo la kula kijipande kidogo cha mkate na kunywa divai kidogo halihusiani hata kidogo na Meza ya Bwana kama ilivyokuwa mwanzo … Meza ya Bwana ilikuwa ni mlo katika nyumba ya marafiki.” Cha kushangaza ni kwamba kila msomi wa kisasa wa Biblia anakubaliana na Barclay, lakini kanisa bado linafuata desturi yake badala ya Neno la Mungu kwenye swala hili!

Yesu aliwaamuru wanafunzi Wake wawafundishe wanafunzi wao kuyashika yote aliyokuwa amewagiza. Basi, alipowaagiza kula mkate na kunywa divai pamoja kama kumbukumbu Yake, bila shaka waliwafundisha wanafunzi wao kufanya hivyo. Je, hayo yangefanyika kwenye mlo wa kawaida? Inaonekana hivyo, tunaposoma maneno ya Paulo kwa waamini Wakorintho.

Basi, mkutanikapo pamoja [wala hasemi juu ya kukutanika katika kanisa, maana wakati huo makanisa hayakuwepo] haiwezekani kula chakula cha Bwana; kwa maana kila mmoja hutangulia kutwaa chakula chake katika kule kula; hata huyu ana njaa, na huyu amelewa (1Wakor. 11:20-21. Maneno mepesi kukazia).

Maneno hayo yangewezaje kueleweka kama Paulo alikuwa anazungumzia Meza ya Bwana kama inavyoendeshwa katika makanisa ya kisasa? Je, umewahi kusikia juu ya tatizo la kula chakula chake kwanza, na mwingine kuwa na njaa huku mwingine amelewa kwa habari ya Meza ya Bwana katika ibada ya kanisa la kisasa? Maneno hayo yana maana ikiwa Meza ya Bwana ilikuwa inaunganishwa na mlo. Tazama anachoendelea kusema.

Je! Hamna nyumba za kulia na kunywea? Au mnalidharau kanisa la Mungu [na usisahau kwamba Paulo hakuwa anaandika juu ya jengo, bali kusanyiko la watu – yaani, kanisa la Mungu], na kuwatahayarisha hao wasio na kitu? Niwaambieni? Niwasifu? La! Siwasifu kwa ajili ya hayo (1Wakor. 11:22).

Jiulize: Watu wangeonaje aibu – wasio na kitu – kama kilichokuwa kinafanywa hakikuwa mlo wa kawaida? Paulo alikuwa anaonyesha kwamba baadhi ya waamini Wakorintho waliofika mapema kwenye mikutano yao walikula vyakula vyao bila ya kuwasubiri wengine. Walipofika wale ambao pengine ni maskini sana kiasi cha kutokuwa na kitu cha kuleta ili watu washiriki katika mlo wa pamoja walikuta chakula kimeliwa, kimekwisha. Hawakubaki na njaa tu, bali pia waliaibika kwa sababu ilionekana wazi kwamba hakuna walicholeta.

Mara tu baada ya hayo, Paulo aliandika zaidi kuhusu Meza ya Bwana, ambayo ni agizo alilopokea “kutoka kwa Bwana” (1Wakor. 11:23), naye akaeleza mambo yaliyofanyika wakati wa Meza ya Bwana mara ya kwanza (ona 1Wakor. 11:24-25). Kisha akawaonya Wakorintho wasishiriki Meza ya Bwana kwa njia isiyostahili, akisema kwamba wasipojihukumu wenyewe, watakula na kunywa hukumu juu yao wenyewe. Itakuwa udhaifu, magonjwa na hata kufa kabla ya wakati (ona 1Wakor. 11:26-32).

Kisha akamalizia hivi:

Kwa hiyo ndugu zangu, mkutanikapo mpate kula, ngojaneni; mtu akiwa na njaa, na ale nyumbani kwake; msipate kukutanika kwa hukumu (1Wakor. 11:33-34).

Ni hivi: Kosa lililokuwa linafanywa wakati wa Meza ya Bwana ni kutowajali na kuwafikiria waamini wengine. Paulo kwa mara nyingine tena akaonya kwamba wale waliokuwa wanakula chakula chao kwanza, kwenye tukio ambalo lilipaswa kuwa mlo wa pamoja walikuwa katika hatari ya kuhukumiwa (au kuadhibiwa) na Mungu. Ufumbuzi ulikuwa rahisi tu. Kama mtu alikuwa na njaa kiasi cha kutoweza kuwasubiri wengine, ale kitu nyumbani kwake kabla ya kuja kwenye mkutano. Na wale waliofika mapema wawasubiri wale watakaochelewa kufika kwenye mlo – ambao ulihusisha Meza ya Bwana, au ndiyo ulikuwa Meza ya Bwana.

Tukitazama fungu zima, Paulo anachosema kwa uwazi kabisa ni kwamba, kama kilichokuwa kinaliwa ni Meza ya Bwana, basi ingefanyika kwa njia ambayo ingempendeza Bwana – kuonyesha upendo na kujaliana.

Ni dhahiri kwamba kanisa la kwanza lilishiriki Meza ya Bwana kama sehemu ya chakula cha kawaida katika nyumba, bila ya kuwepo kwa usimamizi wa kichungaji. Mbona sisi hatufanyi hivyo?

Mkate Na Divai

Aina ya vinavyotumiwa katika Meza ya Bwana si muhimu sana. Kama ni lazima tujitahidi kufanya kama ilivyokuwa ile Meza ya Bwana ya kwanza kabisa, basi itabidi tujue mkate ule ulitengenezwa na nini, na zabibu zilizotoa divai ile ya kwanza zilikuwa za aina gani. (Kwa habari ya hilo: kuna viongozi wa kanisa katika karne za mwanzo waliosema kwamba mvinyo husika ulibidi utiwe maji mengi, la sivyo Meza ya Bwana ilikuwa inafanyika visivyo.)

Mkate na mvinyo vilikuwa vitu vya kawaida kabisa katika mlo wa Wayahudi zamani. Yesu alivipa umuhimu wa kipekee vitu viwili ambavyo vilikuwa vya kawaida kabisa – vyakula vilivyoliwa na kila mtu kila siku. Angetembelea utamaduni mwingine katika kipindi tofauti cha historia, bila shaka Meza ya Bwana ya kwanza ingekuwa na jibini na maziwa ya mbuzi, au mkate wa mchele na juis ya nanasi. Kwa hiyo – chakula chochote na kinywaji vinafaa kuwakilisha mwili Wake na damu Yake kwenye mlo wa kawaida wa wanafunzi Wake. Kitu muhimu ni ile maana yake kiroho. Tusije tukapuuza maana ya Sheria katika juhudi za kushika andiko!

Si lazima mlo wa kawaida uwe kama maombolezo ya msiba. Kama tulivyokwisha soma, Wakristo wa kwanza walikuwa “wakimega mkate nyumba kwa nyumba … wakila pamoja kwa furaha na udhati wa moyo” (Matendo 2:46 – TLR. Maneno mepesi kukazia). Ila, hali ya kumaanisha ni sawa wakati tunapofikia kwenye kukumbuka dhabihu ya Yesu na kula ule mkate na ile divai. Ni muhimu sana kujichunguza kabla ya kula Meza ya Bwana, kama inavyo-onyeshwa na maneno mazito ya Paulo ya kuwaonya waamini Wakorintho katika 1Wakor. 11:17-34. Uhalifu wowote kwa amri ya Kristo kupendana sisi kwa sisi ni kutaka adhabu kutoka kwa Mungu. Na matengano yote au hali ya kutopatana vitengenezwe kabla ya kushiriki. Kila mwamini ajichunguze mwenyewe na kutubu dhambi zozote, tendo ambalo ni sawa na “kujihukumu mwenyewe” kulingana na maneno ya Paulo.

Roho Hudhihirishwa Kupitia Mwili

Mlo wa watu wote unaweza kufanyika kabla au baada ya mkutano wenye ibada, mafundisho na ushirikishwaji wa karama za kiroho. Ni juu ya kila kanisa la nyumbani kuamua utaratibu wake, na taratibu zinaweza kutofautiana kutoka kusanyiko hadi kusanyiko la kanisa hilo moja la nyumbani.

Ni dhahiri kutokana na Maandiko kwamba mikutano ya kanisa la kwanza ilikuwa tofauti sana na ibada za siku hizi za makanisa jengo. Tunapewa katika 1Wakorintho sura ya 11 hadi 14 mambo mengi yaliyotokea wakati Wakristo wa kwanza walipokutanika, na hakuna sababu ya kufikiri kwamba mtindo huo hauwezekani siku hizi. Pia ni dhahiri kwamba yaliyotokea katika mikutano ya kanisa la kwanza kama yanavyoelezwa na Paulo yangeweza tu kutokea katika vikundi vidogo. Anayoeleza Paulo hayawezekani katika mkutano mkubwa.

Naomba niwe wa kwanza kukiri kwamba sielewi yote aliyoandika Paulo katika hizo sura nne za 1Wakorintho. Lakini inaonekana kwamba kitu muhimu sana katika mikutano hiyo ya 1Wakorintho 11 hadi 14 ni uwepo wa Roho Mtakatifu miongoni mwao, na madhihirisho Yake kupitia viungo vya mwili. Aliwapa watu binafsi karama kwa ajili ya kujengwa kwa mwili wote.

Paulo anaorodhesha karama kama tisa hivi za kiroho: unabii, lugha, tafsiri za lugha, neno la maarifa, neno la hekima, kupambanua roho, karama za kuponya, imani, na matendo ya miujiza. Hasemi kwamba karama zote hizo zilionekana katika kila mkutano, lakini anaonyesha uwezekano wa utendaji wa karama hizo zote, na anaonekana kuhitimisha kwa kutaja madhihirisho ya Roho yaliyokuwa ya kawaida katika 1Wakorintho 14:26.

Basi ndugu, matokeo ni nini? Mkutanikapo, kila mmoja ana zaburi, ana fundisho, ana ufunuo, ana lugha, ana tafsiri. Mambo yote na yafanywe kwa kusudi la kujenga (TLR).

Hebu tutazame hayo matano yote, yaliyokuwa madhihirisho ya kawaida ya Roho, na katika sura nyingine, tutazame kwa undani zaidi hizo karama tisa za Roho zinazotajwa katika 1Wakorintho 12:8-10.

Ya kwanza ni zaburi. Zaburi zitolewazo na Roho zinatajwa na Paulo katika barua mbili zingine za Paulo kwa makanisa, kuonyesha nafasi yake katika makusanyiko ya Kikristo.

Wala msilewe kwa mvinyo, maana si vizuri. Bali mjazwe na Roho, mkizungumza wenyewe kwa wenyewe katika zaburi na nyimbo na tenzi za rohoni, kwa kuimba na kumfanyia Bwana shangwe kwa moyo (Waefeso 5:18, 19 – TLR).

Ruhusuni Neno la Kristo likae kwa wingi ndani yenu, mkifundishana kwa hekima yote na kushauriana wenyewe kwa wenyewe kwa zaburi na nyimbo na tenzi za rohoni, na kumwimbia Mungu kwa shukrani mioyoni mwenu (Wakolosai 3:16 – TLR).

Tofauti kati ya zaburi, nyimbo na tenzi za rohoni haiko wazi sana, lakini wazo kuu ni kwamba vyote vina msingi katika maneno ya Kristo, vimevuviwa na Roho, na vinatakiwa kuimbwa na waamini ili kufundishana na kushauriana. Ni kweli kwamba nyimbo na pambio ambazo zimeimbwa na waamini katika kipindi chote kilichopita cha historia ya kanisa zinaangukia katika mojawapo ya vipengele hivyo. Kwa bahati mbaya, nyimbo nyingi za kisasa na pambio hazina undani KiBiblia, kuonyesha kwamba hazitokani na Roho, na kwa kuwa hazina kina, hazina thamani yoyote kwa kufundisha au kuwashauri waamini. Lakini, waamini wanaokutanika katika makanisa ya nyumbani wanapaswa kutazamia kwamba Roho atawavuvia watu binafsi, si kuongoza tu nyimbo maarufu za Kikristo za zamani na mpya, bali pia kuwapa nyimbo maalum washirika wengine zitakazoweza kutumiwa kwa ajili ya kufaidia wote. Ni kitu cha kipekee sana kwa makanisa kuwa na nyimbo zao wenyewe, zilizotolewa na Roho!

Kufundisha

Cha pili katika orodha ya Paulo ni kufundisha. Hili tena linaonyesha kwamba mtu yeyote anaweza kutoa fundisho lililovuviwa na Roho katika kusanyiko. Kila fundisho lilitakiwa kupimwa ili kuona kama lingalingana na mafundisho ya mitume (maana kila mmoja alidumu katika hayo: ona Matendo 2:42). Sisi pia tunapaswa kufanya hivyo hivyo siku hizi. Ila – ona kwamba hakuna mahali popote hapa au penginepo katika Agano Jipya, penye kuonyesha kwamba mtu yule yule alitoa mahubiri kila juma wakati makanisa yalipokutanika – na kuwa kinara katika kila mkutano!

Pale Yerusalemu kulikuwa na mikutano mikubwa ambayo waliofundisha ni mitume. Tunajua kwamba wazee walipewa majukumu ya kufundisha katika makanisa, na kwamba kuna watu wanaoitwa kufanya huduma ya kufundisha. Paulo alifundisha sana – hadharani na nyumba kwa nyumba (ona Matendo 20:20). Lakini, katika mikutano midogo ya waamini, Roho Mtakatifu anaweza kuwatumia wengine kufundisha ambao si mitume, wazee au waalimu.

Kwa habari ya kufundisha, sisi tunawazidi watu wa kanisa la kwanza kwa sababu tunaweza kuja na nakala binafsi za Biblia kwenye mikutano yetu. Kwa upande wa pili, yawezekana upatikanaji rahisi wa Biblia kwetu umetusababisha kutukuza mafundisho kuliko kumpenda Mungu kwa moyo wote, na kuwapenda jirani zetu kama tunavyojipenda wenyewe. Jambo hilo limetuibia uzima uliokusudiwa kutoka katika Neno la Mungu. Tumefundishwa mpaka tumekufa. Mafundisho mengi ya Biblia katika vikundi vidogo yamekuwa yenye kuchosha na yasiyofaa, sawa tu na mahubiri ya Jumapili asubuhi. Kipimo kizuri kuhusu mafundisho ya makanisa ya nyumbani ni hiki: Kama watoto wakubwa hawafichi kuchoka kwao, watu wazima wanaficha. Watoto ni kipimo kizuri sana cha ukweli wa hali halisi.

Ufunuo

Cha tatu kinachotajwa na Paulo ni “ufunuo”. Maana yake ni chochote kinachofunuliwa na Mungu kwa mtu fulani katika kundi. Kwa mfano: Paulo anataja jinsi ambavyo mtu asiyeamini anavyoweza kutembelea kusanyiko la Kikristo na “siri za moyo wake zikadhihirishwa” kwa karama ya unabii. Matokeo ni kwamba “atajisikia hatia” na “kutakiwa kujibu”, naye “ataanguka kifudifudi na kumwabudu Mungu, akisema, ‘Hakika Mungu yuko miongoni mwenu’.” (1Wakor. 14:24, 25 – TLR).

Hapa tena tunaona kwamba uwepo halisi wa Roho Mtakatifu ulikuwa kitu kilichotazamiwa katika mikusanyiko ya kanisa, na kwamba vitu visivyo vya kawaida vingetokea kwa sababu hiyo. Wakristo wa mwanzo waliamini kweli ahadi ya Yesu kwamba, “Popote walipokusanyika wawili au watatu katika jina langu, nipo katikati yao” (Mathayo 18:20 – TLR). Kama Yesu Mwenyewe alikuwepo katikati yao, miujiza ingetokea. Waliabudu kweli kweli “katika Roho wa Mungu” (Wafilipi 3:3).

Hata hivyo, unabii – ambao nitasema mengi juu yake hapo baadaye – unaweza kuwa na ufunuo juu ya mioyo ya watu. Lakini ufunuo unaweza kutolewa kuhusu vitu vingine na kwa njia nyingine, kama kupitia ndoto au maono (angalia Matendo 2:17).

Lugha Na Tafsiri

Cha nne ni kwamba Paulo aliunganisha karama mbili zinazofanya kazi pamoja – lugha na tafsiri za lugha. Huko Korintho, lugha zilikuwa nyingi na matumizi yake yalikuwa mabaya. Yaani – watu walinena kwa lugha wakati wa mikutano ya kanisa, na hapakuwa na tafsiri. Basi, hakuna aliyejua kinachosemwa. Tunaweza kujiuliza kwa nini Wakorintho walaumiwe, maana inaonekana kama ni kosa la Roho Mtakatifu kuwapa watu karama ya lugha bila ya kumpa yeyote karama ya kutafsiri. Lipo jibu zuri tu kwa swali hilo ambalo nitalitoa katika sura ya huko mbele. Lakini, Paulo hakukataza watu kunena kwa lugha (kama makanisa jengo mengi yanavyofanya). Yeye alichokataza ni watu kukatazwa kunena kwa lugha, na akasema, hilo ni agizo la Bwana (ona 1Wakor. 14:37-39)![8] Ilikuwa ni karama ambayo, kama ingetumiwa vizuri, ingejenga mwili wa Kristo na kuthibitisha uwepo wa Mungu usio wa kawaida miongoni mwao. Mungu alikuwa anazungumz akupitia watu, akiwakumbusha kweli Yake na mapenzi Yake.

Katika sura ya 14, Paulo anatetea ukuu wa unabii juu ya kunena kwa lugha bila tafsiri. Aliwatia moyo sana Wakorintho watamani kutabiri, na hii ni ishara kwamba karama za Roho zitafanya kazi miongoni mwa watu wanaozitamani. Tena, Paulo aliwashauri hivi waamini wa Thesalonike – “Msimzimishe Roho; msidharau matamko ya kinabii” (1Wathes. 5:19 – TLR). Hii inaonyesha kwamba waamini wanaweza “kuzima moto wa” Roho kwa kuwa na mtazamo usiofaa juu ya karama ya unabii. Bila shaka ndiyo sababu karama ya unabii haionekani sana miongoni mwa waamini siku hizi.

Jinsi Ya Kuanza

Makanisa ya nyumbani huzaliwa na Roho Mtakatifu kupitia huduma ya mwanzilishi wa makanisa ya nyumbani au mzee au mchungaji au mwangalizi mwenye kupewa maono na Mungu juu ya kanisa la nyumbani. Kumbuka kwamba mzee KiBiblia, au mwangalizi au mchungaji anaweza kuitwa “aliyekomaa” na makanisa jengo. Hakuna mwanzishaji wa makanisa ya nyumbani anayehitaji elimu maalum kuhusu huduma.

Baada ya maono hayo kutolewa na Roho Mtakatifu, anahitaji kumwomba Bwana kuhusu wengine wanaoweza kuungana naye. Bwana atamkutanisha na watu wenye maono yanayofanana, akithibitisha uongozi wake. Au anaweza kuongozwa kwa wasioamini walio tayari, anaoweza kuwaleta kwa Kristo na kuwafanya wanafunzi katika kanisa la nyumbani.

Wale wanaoanzisha kanisa la nyumbani watazamie kwamba itachukua muda kwa washirika kuzoeana na kujifunza kushirikiana na kutembea katika Roho Mtakatifu. Hali ya kila mshirika kuhusika, uongozi wa kitumishi KiBiblia, kuwawezesha wazee kutumika, uongozi wa Roho Mtakatifu na karama Zake, mlo wa pamoja, na hali ya kiroho ya kawaida tu ni vitu vigeni sana kwa watu waliozoea ibada za makanisani. Hivyo basi, kutumia neema na subira ni kitu cha busara sana wakati wa kuanza kanisa jipya la nyumbani. Mwanzo unaweza kuwa kama kikundi cha kujifunza Biblia nyumbani, huku mtu mmoja akiongoza kuabudu na mwingine akifundisha somo lililoandaliwa, kisha kumaliza kwa nafasi ya watu kuomba pamoja, kuwa na ushirika na kula pamoja. Lakini, kikundi kitakapojifunza zaidi mfumo wa KiBiblia kuhusu makanisa ya nyumbani, yule mzee au mchungaji au mwangalizi atalazimika kuwatia moyo washirika kujitahidi kupata kilicho bora toka kwa Mungu. Baada ya hapo, furahia safari yenyewe!

Mikutano ya makanisa ya nyumbani inaweza kuhama kutoka kwa mshirika mmoja hadi kwa mwingine kila juma, au mtu mmoja anaweza kutoa nyumba yake itumiwe kila juma. Makanisa mengine ya nyumbani huhamia nje kwenye viwanja vizuri mara moja moja, hali ya hewa ikiruhusu. Wala si lazima wakati wa kukutana uwe ni Jumapili asubuhi tu, bali wakati wowote unaowafaa washirika. Mwisho: Ni vizuri kuanza na idadi ndogo ya watu – wasizidi kumi na mbili.

Jinsi Ya Kufanya Mabadiliko

Bila shaka wachungaji wengi wanaosoma maneno haya wanafanya kazi katika taratibu za makanisa jengo, na yawezekana hata wewe ni mmoja wao. Kama nimegusa kitu katika maisha yako kinachotamani kanisa la aina niliyokuwa naeleza, basi bila shaka umeanza kujiuliza jinsi ya kufanya mabadiliko. Hebu nikutie moyo kwamba, usiwe na haraka. Anza kwa kufundisha kweli za Biblia tu, na kufanya chochote unachofanya wakati huu katika mfumo wako ili uzae wanafunzi wanaotii maagizo ya Yesu. Wanafunzi wa kweli watapenda kufanya mabadiliko wenyewe, wafuate mfumo wa kanisa la KiBiblia kama wanavyoufahamu. Mbuzi na watu wa kidini watapinga mabadiliko hayo kwa nguvu zote.

Pili: Jifunze Maandiko yanasema nini juu ya jambo hilo, ufundishe kusanyiko lako juu ya mfumo wa kanisa la nyumbani na baraka zake. Hatimaye waweza kufuta ibada zote za katikati ya juma au za Jumapili jioni ili uanzishe mikutano ya vikundi katika nyumba, itakayosimamiwa na waamini waliokomaa. Mtie moyo kila mmoja ahudhurie. Jitahidi kufananisha mikutano hiyo na ile ya KiBiblia kiasi inachowezekana. Kisha, toa nafasi kwa watu kuanza kufurahia baraka za vikundi vidogo.

Baada ya kila mmoja kuanza kufurahia mikutano hiyo ya nyumbani, unaweza kutangaza kwamba Jumapili fulani ya mwezi unaofuata itakuwa “Jumapili Ya Kanisa La Kwanza”. Na siku hiyo ni kwamba kanisa litafungwa na kila mtu atakwenda kwenye nyumba ili kukutanika, kama kanisa la kwanza lilivyofanya, na kula pamoja, kuwa na Meza ya Bwana, kuwa na ushirika, maombi, kuabudu, mafundisho ya pamoja na karama za kiroho. Mambo yakifaulu, unaweza kufanya hivyo Jumapili moja kwa mwezi, kisha mbili, kisha tatu. Mwishoni, utaruhusu kila kikundi kuwa kanisa huru la nyumbani, lenye uhuru wa kukua na kuongezeka, na labda kuwa na mkutano wa pamoja kila baada ya miezi kadha.

Mabadiliko hayo niliyoeleza yanaweza kuchukua kati ya mwaka mmoja hadi miwili.

Au kama unataka kwenda polepole, unaweza kuanzisha mkutano mmoja katika nyumba, na wachache kati ya washirika wako wenye kupenda, uwaongoze wenyewe. (Hapa tena narudia: makanisa ya nyumbani si lazima yakutane Jumapili asubuhi.) Unaweza kuwaambia kwamba ni kitu cha majaribio, na inaweza kuwa mafunzo kwa wote.

Mambo yakifaulu, chagua mwangalizi kisha ulifungue kundi hilo kuwa kanisa linalojitegemea ambalo litaungana na ibada ya Jumapili mara moja kwa mwezi. Hivyo kanisa hilo jipya bado litakuwa sehemu ya kanisa mama, na halitatazamwa vibaya na wale ambao wamebakia. Pia inaweza kuwashawishi wengine katika kanisa kufikiri kuhusu kujiunga na kanisa lingine la nyumbani linaloanzishwa na kanisa.

Kundi la kwanza likikua, omba kisha uligawe, ili makundi yote mawili yawe na viongozi wazuri na karama za kutosha katika washirika wao. Makundi hayo mawili yanaweza kukutanika pamoja katika ibada ya pamoja kwenye mahali watakapokubaliana – mara moja kwa mwezi au mara moja kila baada ya miezi mitatu.

Njia yoyote utakayoamua kufuata, hakikisha macho yako yanatazama lengo hata utakapovunjwa moyo – na haitakuwa kidogo. Makanisa ya nyumbani yana watu, na watu husababisha matatizo. Usikate tamaa.

Haitawezekana kila mmoja katika dhehebu lako akubali kufanya mabadiliko kama hayo. Basi itakubidi uamue ni wapi utaanza kibinafsi kujiingiza katika kuunda kanisa la nyumbani au kikundi cha makanisa ya nyumbani na kuachana na dhehebu. Siku hiyo itakuwa muhimu sana kwako!

Kanisa Lililo Sawa

Je, mchungaji wa kanisa la nyumbani anaweza kufanikiwa zaidi machoni pa Mungu kuliko mchungaji wa kanisa kubwa lenye jengo kubwa na maelfu ya watu wanaohudhuria kila Jumapili? Ndiyo, kama anaongeza wanafunzi wenye kumtii Yesu na wenye kufanya wengine kuwa wanafunzi. Kama anafuata mpango wa Yesu badala ya kukusanya mbuzi wa kiroho mara moja kwa juma kutazama onyesho na kusikiliza hotuba yenye kustarehesha, iliyo’takatifuzwa’ na mistari kadhaa isiyokuwa katika mantiki yake.

Mchungaji atakayeamua kufuata mpango wa kanisa la nyumbani hatakuwa na kusanyiko kubwa. Lakini, atakuwa na matunda yanayodumu, maana wanafunzi wake watafanya wengine kuwa wanafunzi. Wachungaji wengi wa makanisa “madogo” ya watu 40 au 50 wanaotaka zaidi, ni vizuri warekebishe kufikiri kwao. Tayari makanisa yao ni makubwa sana. Pengine waache kuombea majengo makubwa na waanze kuomba nani achaguliwe kuongoza makanisa mapya mawili ya nyumbani. (Angalizo: Tafadhali sana – hayo yatakapotokea, usitafute jina jipya kwa ajili ya dhehebu lako, na wewe mwenyewe usijiite ‘askofu’!)

Tunahitaji kufuta mawazo kwamba kikubwa ni bora inapofikia mambo ya kanisa. Kama ni kupima kwa kufuata misingi ya KiBiblia, sharika binafsi zenye watazamaji wasio na nidhamu wenye kukutania katika majengo maalum zingehesabiwa kuwa za ajabu sana. Kama mtume mmoja angetembelea makanisa jengo ya kisasa, wangejikuna vichwa!

Hoja Ya Mwisho

Mara nyingi imesemekana kwamba watu hawawezi kukubaliana na wazo la makanisa kukutania nyumbani katika dunia ya Magharibi, ambapo Ukristo umekwisha kuwa sehemu ya utamaduni. Hoja imetolewa kwamba ni lazima tubaki kama tulivyo.

Kwanza: Hiyo si kweli kwa sababu makanisa ya nyumbani yanazsidi kupata kasi katika nchi za Magharibi.

Pili: Tayari watu wanakutanika nyumbani – tena kwa furaha sana – kwa ajili ya sherehe, vyakula, ushirika, kujifunza Biblia na mikutano ya nyumba kwa nyumba. Kukubali wazo la kanisa kuwa nyumbani huhitaji badiliko kidogo tu la mawazo.

Tatu: Ni kweli kwamba watu wa dini – “mbuzi kiroho” – hawatakubali wazo la makanisa ya nyumbani. Hawatafanya chochote cha kuwaonyesha kuwa watu tofauti – “wa ajabu” – kwa jirani zao. Lakini wanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo watakubali jambo la makanisa ya nyumbani mara watakapoelewa msingi wake KiBiblia. Wanatambua upesi jinsi majengo ya kanisa yasivyohitajika katika kufanya watu kuwa wanafunzi. Ukitaka kujenga kanisa kubwa kwa “mbao, majani na manyasi” (1Wakor. 3:12), utahitaji jengo, lakini mwisho wa yote kila kitu kitaungua. Lakini ukitaka kuongeza wanafunzi na wenye kufanya watu kuwa wanafunzi, yaani kulijenga kanisa la Yesu Kristo kwa “dhahabu, fedha na mawe ya thamani,” basi huna haja ya kupoteza fedha na nguvu kwenye majengo.

Cha kusisimua ni kwamba, shirika la kienyeji la uinjilisti ambalo ni kubwa kuliko yote duniani liitwalo “kurudi Yerusalemu”, la makanisa ya nyumbani ya Uchina, limeweka mkakati halisi wa kuzifikia nchi za eneo lijulikanalo kama ‘Dirisha la 10/40’. Wamesema hivi: “Hatutamani kujenga jengo la kanisa popote! Hii inaruhusu Injili kuenea haraka. Viongozi wa kiserikali wanapata shida kufuatilia, na hutuwezesha kuingiza rasilmali yetu yote kwenye huduma ya Injili”.[9] Ni mfano wa KiBiblia, tena wa hekima kabisa. Unastahili kuigwa!


[1] Ona makala iitwayo (tafsiri) “Asemacho Yesu Kuhusu Fedha” katika sehemu iitwayo Mada Za KiBiblia kwenye mtandao huu: www.shepherdserve.org.

 

[2] Japo itaonekana ni kitu cha tofauti sana – sababu ya kweli ya kuhitajika majengo ni kukosekana kwa viongozi wa kusimamia makanisa madogo ya nyumbani, ambayo ni matokeo ya udhaifu katika kufanya wanafunzi. Je, yawezekana kwamba wachungaji wa makanisa jengo wana hatia ya kuwaibia huduma watu wengine walioitwa na Mungu kuwa wachungaji katika kusanyiko zao? Jibu ni ndiyo – wana hatia.

[3] Kiwango hicho (moja hadi kumi au ishirini) kisihesabike kuwa ni kikubwa sana, ukilinganisha na mpango wa Yesu kuwa na wanafunzi kumi na mbili, au jinsi Musa alivyoweka wakuu juu ya watu kumi (ona Kutoka 18:25). Wachungaji wengi wanasimamia watu wengi kuliko uwezo wao wa kuwafanya wanafunzi.

[4] Tunaweza pia kuhoji kwamba mbona hakuna wachungaji “viongozi”, “wenza” au “wasaidizi” katika Maandiko. Vyeo hivyo ambavyo vinaonekana kuwa vya lazima sana katika kanisa la kisasa kwa sababu ya muundo wake havikuwa na ulazima katika kanisa la kwanza kwa sababu ya muundo wake pia! Makanisa ya nyumbani yenye watu ishirini hayahitaji kuwa na mchungaji kiongozi, mchungaji mwenza na mchungaji msaidizi!

 

[5] Wachungaji wengi huwa hawafanikiwi kuwa wasemaji wazuri, japo wameitwa na Mungu na ni watumishi wanaojali sana wa Kristo. Je, ni ukatili kusema kwamba mahubiri mengi ya wachungaji yanachosha – au mara nyingi yanachosha? Lakini – wachungaji hao hao ambao wanachosha watu kwa maneno yao wakati wa mihadhara ni wazuri sana kuzungumza. Watu hawachoki mara nyingi wanapozungumza wao kwa wao. Hii ndiyo sababu ule mtindo wa kufundisha wenye kumshirikisha kila mmoja katika makanisa ya nyumbani unasisimua kila mara. Wakati huenda haraka vipindi hivyo, na huoni watu wakitazama saa kama inavyokuwa kwenye mahubiri. Wachungaji wa makanisa ya nyumbani hawana wasiwasi kwamba wanachokesha watu.

[6] Tafsiri ya wazimu ninayoipenda sana ni hii: Kurudia kufanya kitu kile kile, na kutazamia matokeo tofauti kila unapokifanya. Wachungaji wanaweza kufundisha juu ya wajibu wa kila mshirika kujihusisha katika kufanya watu kuwa wanafunzi kwa miaka mingi, lakini, wasipofanya kitu kubadilisha mifumo na taratibu, watu wataendelea kuja kanisani kuketi, kusikiliza na kurudi nyumbani. MCHUNGAJI: Ukiendelea kufanya kitu ambacho hakikubadilisha watu zamani, hakitabadilisha watu siku zijazo. Badilisha unachofanya!

 

[7] Lakini ukweli halisi ni huu: Sababu kubwa ya wazo kama hili kukataliwa na wachungaji wengi ni kwamba wanajenga falme zao wenyewe, si ufalme wa Mungu.

[8] Ninatambua kwamba kuna wale wanaosema kwamba madhihirisho yote yasiyo ya kawaida ya Roho Mtakatifu yalifanyika katika karne ya kwanza, na baada ya hapo inadaiwa yalikoma. Hivyo hatuna sababu ya kutafuta kile kilichokuwepo katika kanisa la kwanza, tena, kunena kwa lugha hakupo tena. Sina huruma na watu ambao ni kama Masadukayo wa kisasa. Kama mtu ambaye mara kadhaa amemsifu Mungu kwa Kijapani – kwa ushuhuda wa wenye kujua Kijapani walionisikia – na sijawahi kujifunza lugha hiyo, najua kwmaba karama hizo hazijaacha kutolewa na Roho Mtaka tifu. Pia nashangaa ni kwa nini Masadukayo hao wanakubali kwamba Roho Mtakatifu huita watu, huwaonyesha watu hatia, na kuwafanya upya wenye dhambi, halafu wanakataa kazi ya Roho baada ya miujiza hiyo. “Theolojia” ya aina hiyo ni matokeo ya kutokuamini kwa mwanadamu na kutokuti kwake, na haiungwi mkono na Maandiko, tena, iko kinyume kabisa na lengo la Kristo. Ni tendo la kutokumtii Kristo moja kwa moja kulingana na alichoandika Paulo katika 1Wakor. 14:37.

[9] Maneno ya Ndugu Yun katika kitabu chake kiitwacho (tafsiri) Kurudi Yerusalemu, ukurasa wa 58.

 

Kuanza Vizuri

Sura Ya Pili

 

Kibiblia, mwanafunzi ni mtu anayemwamini Bwana Yesu Kristo kwa dhati – mwenye kudumu katika Neno Lake na anayeendelea kuwekwa huru kutoka dhambini siku baada ya siku. Mwanafunzi ni mtu anayejifunza kutii amri zote za Kristo, naye anampenda Yesu kuliko familia yake, kuliko starehe na anasa zake, kuliko mali zake, naye huonyesha pendo hilo kwa jinsi anavyoishi. Wanafunzi wa kweli wa Yesu hupendana wao kwa wao na huonyesha pendo hilo katika matendo. Ni wenye kuzaa matunda.[1] Watu aina hiyo ndiyo Yesu anawataka.

Ni dhahiri kwamba wasiokuwa wanafunzi Wake hawawezi kumzalia wanafunzi. Basi kwanza kabisa inatubidi tuwe na uhakika kwamba sisi ni wanafunzi Wake, kabla ya kujaribu kuwafanya wengine kuwa wanafunzi Wake. Watumishi wengi wanapopimwa kwa ile tafsiri ya KiBiblia ya uanafunzi, wanapungua sana. Hakuna tumaini kwamba watumishi kama hao wanaweza kufanya wengine kuwa wanafunzi, nao wenyewe hawatajaribu. Wao wenyewe hawajajitoa vya kutosha kwa Yesu Kristo kuvumilia magumu yanayoambatana na tendo la kuwafanya watu kuwa wanafunzi.

Kuanzia hapa na kuendelea, nitahesabu kwamba watumishi watakaoendelea kusoma ni wanafunzi wa Bwana Yesu Kristo wao wenyewe, waliojitoa kabisa kutii amri Zake. Kama wewe hauko hivyo, hakuna maana kwako kuendelea kusoma mpaka utakapofanya uamuzi unaofaa wa kuwa mwanafunzi wa kweli. Wala usingoje zaidi! Sasa hivi piga magoti na utubu! Kwa neema Yake nyingi, Mungu atakusamehe na kukufanya kiumbe kipya ndani ya Kristo!

Kufafanua Uanafunzi Kwa Upya

Japo Yesu aliweka bayana kabisa kwamba mwanafunzi ni nani, wengi wameibadili tafsiri Yake na kuweka zao. Kwa mfano: Kwa wengine, neno mwanafunzi ni neno lisiloeleweka vizuri, lenye kumhusu yeyote anayekiri kwamba ni Mkristo. Kwao, neno mwanafunzi limeondolewa maana yake yote KiBiblia.

Wengine wanahesabu uanafunzi kuwa ni hatua ya hiari inayofuata katika kujitolea kwao waaini wanaokwenda mbinguni. Wanaamini kwamba mtu anaweza kuwa mwenda mbinguni anayemwamini Yesu, lakini asiwe mwanafunzi Wake! Kwa kuwa ni vigumu sana kupuuza yale masharti magumu ya Yesu kwa habari ya uanafunzi yaliyoandikwa katika Biblia, wanafundisha kwamba kuna Wakristo aina mbili – waaminio wenye kumwamini Yesu, na wanafunzi, ambao wanamwamini Yesu na wamejitolea Kwake. Basi inasemekanaga kwamba kuna waamini wengi lakini wanafunzi ni wachache, ila, wote wanakwenda mbinguni.

Fundisho hilo linaua agizo la Kristo kwamba tufanye watu kuwa wanafunzi, na tendo hilo humaliza kabisa juhudi za kufanya watu kuwa wanafunzi. Kama kuwa mwanafunzi maana yake ni kujikana na kupatikana hata na mambo magumu, na ikiwa kuwa mwanafunzi ni kitu cha hiari, watu wengi wataamua wasiwe wanafunzi, hasa kama wanafikiri kwamba watakaribishwa mbinguni kama wasiokuwa wanafunzi.

Sasa, yafuatayo ni maswali muhimu sana ambayo lazima tuulize. Je, Maandiko yanafundisha kwamba mtu anaweza kuwa mwamini aendaye mbinguni na asiwe mwanafunzi wa Yesu Kristo? Je, uanafunzi ni hatua ya hiari kwa waamini? Je, kuna aina mbili za Wakristo – waamini wasiojitoa, na wanafunzi waliojitoa?

Jibu kwa maswali yote hayo ni Hapana. Hakuna popote katika Agano Jipya penye kufundisha kwamba kuna aina mbili za Wakristo – waamini na wanafunzi. Kama utasoma kitabu cha Matendo ya Mitume, utaona mara nyingi sana neno wanafunzi, na wala hawatajwi kama waamini wa hali ya juu sana. Kila aliyemwamini Yesu alikuwa mwanafunzi.[2] Ukweli ni kwamba, “wanafunzi waliitwa Wakristo kwa mara ya kwanza huko Antiokia” (Matendo 11:26, TLR – maneno mepesi kukazia).

Cha kushangaza ni hiki: Neno la Kiyunani – mathetes – ambalo tafsiri yake ni mwanafunzi linapatikana mara 261 katika Agano Jipya, ambapo neno – pistos – linalotafsiriwa mwamini linapatikana mara tisa tu. Neno la Kiyunani – christianos – linalotafsiriwa Mkristo linapatikana mara tatu tu. Hayo yote yanapaswa kumfanya mtafutaji wa kweli kujua kwamba wote waliomwamini Yesu katika Kanisa la Mwanzo walihesabiwa kuwa wanafunzi Wake.

Maelezo Ya Yesu

Kwa kweli, Yesu hakufikiri kwamba kuwa mwanafunzi ni hatua ya pili tena ya hiari kwa waamini. Masharti Yake matatu ya uanafunzi tunayosoma katika Luka 14 hayakusemwa kwa waamini kama mwaliko wa kuingia katika kiwango cha juu zaidi cha kujitoa. Maneno Yake yalitolewa kwa kila mtu aliyekuwemo katika kusanyiko. Uanafunzi ni hatua ya kwanza katika mahusiano na Mungu. Tena tunasoma hivi katika Yohana 8:

Naye [Yesu] alipokuwa akisema hayo, wengi walimwamini. Basi Yesu akawaambia wale Wayahudi waliomwamini, “Ninyi mkikaa katika neno langu, mmekuwa wanafunzi wangu kweli kweli; tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru” (Yohana 8:30-32).

Hakuna atakayetoa hoja kinyume cha kweli iliyo dhahiri kabisa kwamba Yesu alikuwa anazungumza na waamini wapya kabisa, kuhusu kuwa wanafunzi Wake. Yesu hakuwaambia hao waamini wapya, “Hapo baadaye itabidi mfikiri juu ya kuchukua hatua ya pili – ya kujitoa – ili mwe wanafunzi Wangu.” Hapana. Yesu alizungumza na hao wanafunzi wapya kama aliyewatazamia kuwa ni wanafunzi tayari, kana kwamba maneno aaminiye na mwanafunzi yanafanana. Aliwaambia hao waamini wapya kwamba njia ya kuthibitisha wao ni wanafunzi Wake ni kukaa katika Neno Lake, kitu ambacho kingepelekea wao kuwekwa huru kutoka dhambi (ona 8:34-36).

Yesu alijua kwamba watu kukiri imani tu si uthibitisho kwamba kweli walikuwa wanaaini. Pia alijua kwamba wale waliokuwa wanaamini kweli kweli kwamba Yeye alikuwa Mwana wa Mungu wangetenda hivyo – mara moja wangekuwa wanafunzi Wake – wenye shauku ya kumtii na kumpendeza Yeye. Waamini aina hiyo – au wanafunzi – wangedumu katika Neno Lake, na kulifanya makao yao. Na, kadiri wanavyogundua mapenzi Yake kwa kujifunza amri Zake, wangeendelea kuwekwa huru kutoka dhambi siku baada ya siku.

Ndiyo sababu mara moja Yesu aliwapa changamoto wale waamini wapya, wajipime. Maneno yake – “mkiwa wanafunzi Wangu kweli kweli” – yanaonyesha kwamba aliamini kuwa kuna uwezekano wa kutokuwa wanafunzi wa kweli, bali wanafunzi wa kujisemea tu. Wangeweza kuwa wanajidanganya. Ila, kama wangefaulu kipimo cha Yesu ndipo wangekuwa na hakika kwamba wao ni wanafunzi Wake wa kweli. (Kutokana na kusoma mazungumzo yaliyoendelea katika Yohana 8:37-59, inaonekana Yesu alikuwa sawa alipotilia mashaka ukweli wao.)[3]

Mstari wetu mkuu – Mathayo 28:18 hadi 20 – unakanusha itikadi kwamba wanafunzi ni kundi tofauti la waamini wa hali ya juu waliojitoa kwa Mungu. Yesu alisema katika Agizo Lake Kuu kwamba wanafunzi wabatizwe. Taarifa za kitabu cha Matendo ya Mitume zinaonyesha kwamba mitume hawakusubiri mpaka hao waamini wapya walipopiga “hatua ya pili ya kujitoa kwa Kristo” ndipo wakawabatiza. Badala yake, mitume waliwabatiza waamini wote wapya mara tu baada ya kuongoka kwao. Wao waliamini kwamba waamini wapya wote walikuwa wanafunzi.

Katika swala hili basi, wale wenye kuamini kwamba wanafunzi ni waamini waliojitolea kwa Yesu kwa hali ya juu sana hawakubaliani katika mafundisho yao. Wengi wao humbatiza yeyote anayekiri kwamba anamwamini Yesu, wala hawangoji wafikie kiwango cha kujitolea cha “uanafunzi”. Ambapo, kama wangeamini kile wanachofundisha, wangewabatiza wale tu wanaofikia kiwango cha uanafunzi, ambao wasingekuwa wengi.

Pigo moja la mwisho kwa fundisho hili ovu. Kama wanafunzi ni tofauti na waamini, mbona Yohana aliandika kwamba kuwapenda ndugu ndiyo alama ya kuwatambulisha waamini waliozaliwa mara ya pili kweli kweli (1Yohana 3:14)? Mbona hata Yesu alisema kupendana kwa ndugu ndiyo alama yenye kuwatambulisha wanafunzi Wake wa kweli (Yohana 13:35)?

Mwanzo Wa Fundisho Hili La Uongo

Kama wazo la makundi mawili tofauti ya Wakristo – waamini na wanafunzi – halipatikani katika Maandiko, fundisho hilo linawezaje kutetewa mpaka lisimame? Jibu ni kwamba, fundisho hilo linaungwa mkono na fundisho lingine – la uongo – linalohusu wokovu. Fundisho hilo linadai kwamba masharti hayo mazito ya uanafunzi hayakubaliani na ukweli kwamba wokovu ni kwa neema. Kwa hoja hiyo, uamuzi unafikiwa kwamba masharti ya uanafunzi hayawezi kuwa masharti kwa ajili ya wokovu. Basi, bila shaka kuwa mwanafunzi ni hatua ya hiari ya kujitolea, kwa waamini waendao mbinguni wanao-okolewa kwa neema.

Kasoro kubwa ya nadharia hii ni kwamba kuna maandiko mengi sana yenye kupingana nayo. Kwa mfano: kuna kilicho wazi kuliko maneno ya Yesu alipokaribia kumalizia Mahubiri Yake Mlimani, baada ya kueleza amri nyingi? Angalia maneno haya.

“Si kila mtu aniambiaye, ‘Bwana, Bwana’, atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni” (Mathayo 7:21).

Ni wazi kwamba Yesu aliunganisha utii na wokovu – hapa, na sehemu nyingi nyingine. Sasa basi: tunawezaje kuoanisha mistari mingi ya Maandiko kama hayo na ukweli wa Biblia kwamba wokovu ni kwa neema? Rahisi sana. Mungu kwa neema Yake ya ajabu, anampa kila mtu nafasi kwa muda ya kutubu, kuamini na kuzaliwa upya, na kupewa nguvu za kuishi maisha ya utii kwa Roho Mtakatifu. Basi wokovu ni kwa neema. Bila neema ya Mungu, hakuna ambaye angeokoka, maana wote wametenda dhambi. Wenye dhambi hawawezi kustahili kupokea wokovu. Basi wanahitaji neema ya Mungu kuokolewa.

Ni hivi: Neema ya Mungu inadhihirishwa kwa njia nyingi sana kuhusu wokovu wetu. Inadhihirishwa kwa Yesu kufa msalabani, kwa Mungu kutuita kupitia Injili, kwa Yeye kutuvuta kwa Kristo, kwa Yeye kutuonyesha dhambi zetu, kwa Yeye kutupa nafasi ya kutubu, kwa Yeye kutuzaa upya na kutujaza kwa Roho Wake Mtakatifu, kwa Yeye kuvunja nguvu ya dhambi juu ya maisha yetu, kwa Yeye kutuwezesha kuishi maisha matakatifu, kwa Yeye kutuadhibu tunapotenda dhambi, na kadhalika. Hakuna baraka hata moja katika hizo ambayo tumeifanyia kazi. Tunaokolewa kwa neema kutoka mwanzo hadi mwisho.

Laini kulingana na Maandiko, wokovu si “kwa neema” tu, bali pia “kwa njia ya imani” kama tunavyosoma:- “Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani” (Waefeso 2:8a – maneno mepesi kukazia). Yote mawili yanahitajika, na yanategemeana. Watu wakitaka kuokoka, neema na imani ni muhimu. Mungu anatoa neema Yake, nasi tunaitikia kwa imani. Na imani ya kweli inasababisha kutii amri za Mungu. Kama Yakobo alivyoandika katika sura ya pili ya barua yake – imani pasipo matendo imekufa, haina faida, na haiwezi kuokoa – ona Yakobo 2:14-26).[4]

Ukweli ni kwamba neema ya Mungu haijawahi kumpa mtu yeyote kibali cha kutenda dhambi. Neema ya Mungu huwapa watu nafasi kwa muda ya kutubu na kuzaliwa tena. Baada ya kufa, hakuna nafasi tena ya kutubu na kuzaliwa upya, na neema ya Mungu haipatikani tena. Basi, neema Yake yenye kuokoa ni ya muda bila shaka.

Mwanamke Ambaye Yesu Alimwokoa Kwa Neema Kwa Njia Ya Imani

Mfano mkamilifu wa wokovu utolewao kwa neema kwa njia ya imani unapatikana katika habari za Yesu alipokutana na mwanamke aliyeshikwa katika tendo la uzinzi. Yesu alimwambia hivi: “Hata mimi sikuhukumu [hiyo ndiyo neema, kwa sababu alistahili hukumu]. Enenda zako; wala usitende dhambi tena” (Yohana 8:11 – maneno mepesi yameongezwa). Alistahili kufa – Yesu akamwachia. Lakini, alimruhusu aondoke akiwa na onyo: Kuanzia sasa usitende dhambi tena. Maneno hayo ndiyo Yesu anamwambia kila mtenda dhambi duniani – “Sikuhukumu sasa. Unastahili kufa na kuhukumiwa ukae milele jehanamu, lakini, ninakuonyesha neema Yangu. Ila, neema Yangu ina mwisho, kwa hiyo, tubu. Acha kutend adhambi sasa, kabla neema Yangu haijafika mwisho na ukajikuta umesimama mbele ya kiti Changu cha hukumu kama mwenye dhambi aliye na hatia.”

Sasa – Hebu tudhanie kwamba yule mwanamke alitubu sawa na jinsi Yesu alivyomwambia. Kama ndivyo alivyofanya, basi aliokolewa kwa neema kwa njia ya imani. Aliokolewa kwa neema kwa sababu kama mwenye dhambi, asingeweza kuokoka bila neema ya Mungu. Asingweza kusema kweli kwamba ameupata wokovu wake kwa matendo yake. Na aliokolewa kwa njia ya imani kwa sababu alimwamini Yesu na akaamini alichomwambia – yaani, akajali maonyo Yake, akageuka na kuiacha dhambi yake kabla hajachelewa sana. Yeyote mwenye kumwamini Yesu kweli kweli atatubu, kwa sababu, Yesu alionya kwamba, kama watu wasipotubu, watapotea (ona Luka 13:3). Pia Yesu alitangaza kwa dhati kabisa kwamba wale tu watendao mapenzi ya Baba ndiyo watakaoingia mbinguni (Mathayo 7:21). Basi, kama mtu anamwamini Yesu, ataamini na kujali maonyo Yake pia.

Lakini, hebu tudhani kwamba yule mwanamke hakutubu dhambi yake. Tuseme aliendelea kutenda dhambi, kisha akafa na kusimama mbele ya kiti cha hukumu cha Yesu. Hebu tudhani kwamba amemwambia Yesu hivi: “Aha Yesu! Nimefurahi sana kukuona! Nakumbuka hukunihukumu kwa dhambi yangu nilipofikishwa mbele Zako duniani. Bila shaka bado wewe ni mwenye neema vile vile. Hukunihukumu wakati ule, kwa hiyo bila shaka hutanihukumu hata sasa!”

Unafikirije? Je, Yesu angemkaribisha aingie mbinguni? Jibu ni dhahiri. Paulo alionya hivi: “Msidanganyike – hakuna wazinzi … wala waasherati … watakaourithi ufalme wa Mungu” (1Wakor. 6:9-10. TLR)

Hayo yote ni ili kusema hivi: Matakwa ya Yesu kwa uanafunzi hayana tofauti na matakwa kuhusu kumwamini kwa dhati – ambayo ni sawa na kuwa na imani yenye kuokoa. Na kila mwenye imani yenye kuokoa ameokolewa kwa neema kwa njia ya imani. Hakuna msingi KiBiblia wa kudai kwamba, kwa kuwa wokovu ni kwa neema, masharti ya Yesu kuhusuuanafunzi hayalingani na masharti Yake kwa habari ya wokovu. Uanafunzi si hatua nyingine ya hiari inayochukuliwa na waamini waendao mbinguni. Uanafunzi ni ushahidi wa imani ya kweli yenye kuokoa. [5]

Kwa kuwa mambo ni hivyo, ili mtumishi aweze kufanikiwa mbele za Mungu, anatakiwa aanze sawasawa zile harakati za kuwafanya watu kuwa wanafunzi kwa kuhubiri Injili ya kweli, akiwaita watu kuwa na imani tiifu. Wakati watumishi wanapohubiri fundisho la uongo kwamba uanafunzi ni hatua ya kujitoa zaidi – lakini ya hiari – kwa ajili ya waamini waendao mbinguni, wanafanya kazi kinyume cha amri ya Kristo ya kuwafanya watu kuwa wanafunzi, na wanatangaza neema ya uongo na injili ya uongo. Wanafunzi wa kweli wa Kristo ndiyo wenye imani yenye kuokoa, na ndiyo wanaokwenda mbinguni, sawa tu na ahadi ya Yesu, hivi: “Si kila aniitaye, ‘Bwana! Bwana!’ atakayeingia katika ufalme wa mbinguni, bali ni yule atendaye mapenzi ya Baba Yangu aliye mbinguni” (Mathayo 7:21).

Injili Mpya Ya Uongo

Kwa sababu ya mawazo ya uongo kuhusu neema ya Mungu katika wokovu, injili ya kisasa mara nyingi imevuliwa dondoo zile muhimu za KiBiblia, ambazo zinahesabiwa hazilingani na ujumbe wa neema. Shida ni kwamba, injili ya uongo huzaa Wakristo wa uongo, ambayo ndiyo sababu idadi kubwa ya “waongofu” wapya wa siku hizi hawapatikani makanisani majuma kadhaa baada ya “kumpokea Kristo”. Tena, wengi wanaohudhuria ibada kanisani mara nyingi hawana tofauti na watu wasio-okoka, kwa sababu ya kufuata tabia zile zile na kutenda mambo yale yale mabaya kama jirani zao wasiokuwa wabaya sana. Hii ni kwa sababu kwa kweli hawamwamini Bwana Yesu Kristo, na hawajazaliwa upya kweli kweli.

Kitu kimoja muhimu sana ambacho sasa kimeondolewa katika injili ya kisasa ni wito watu watubu. Watumishi wengi wanajisikia kwamba wakiwaambia watu waache kutenda dhambi (kama Yesu alivyofanya na yule mwanamke aliyeshikwa katika uzinzi), itakuwa ni sawa na kuwaambia kwamba wokovu si kwa neema bali ni kwa matendo. Lakini huo si ukweli, kwa sababu Yohana Mbatizaji, na Yesu, na Petro na Paulo wote walitangaza kwamba toba ni kitu muhimu sana kwa ajili ya wokovu. Kama kuhubiri toba kunaua neema ya Mungu katika wokovu kwa namna fulani, basi Yohana Mbatizaji, na Yesu, na Petro, na Paulo wote waliua neema ya Mungu katika wokovu. Sivyo. Wao walielewa vizuri kabisa kwamba neema ya Mungu huwapa watu nafasi fupi tu ya kutubu – sio nafasi ya kuendelea kutenda dhambi.

Kwa mfano: Wakati Yohana Mbatizaji alipotangaza kile ambacho Luka anakiita “Injili”, ujumbe wake mkuu ulikuwa toba (tazama Luka 3:1-18). Wale ambao hawangetubu wangekwenda jehanamu (ona Mathayo 3:10-12; Luka 3:17).

Yesu alihubiri toba tangu mwanzo wa huduma Yake (ona Mathayo 4:17). Aliwaonya watu kwamba, kama wasingetubu, wangeangamia (tazama Luka 13:3, 5).

Alipowatuma wanafunzi Wake kumi na mbili kuhubiri katika miji mbalimbali, “wakatoka, wakahubiri kwamba watu watubu” (Marko 6:12 – maneno mepesi kukazia).

Baada ya kufufuka Kwake, Yesu aliwaambia wale Thenashara wapeleke ujumbe wa toba duniani kote kwa sababu ndiyo ufunguo wa mlango wa kusamehewa.

Akawaambia, ‘Ndivyo ilivyoandikwa, kwamba Kristo atateswa na kufufuka siku ya tatu; na kwamba mataifa yote watahubiriwa kwa jina Lake habari ya toba na ondoleo la dhambi, kuanza tangu Yerusalemu’ (Luka 24:46-47. Maneno mepesi kukazia).

Mitume walitii agizo la Yesu. Petro alipokuwa anahubiri Siku ya Pentekoste, baada ya kutambua ukweli juu ya Yule waliyemsulubisha, wasikilizaji wake waliokuwa wanajisikia hukumu walimwuliza wafanye nini. Aliwajibu kwamba kwanza kabisa walitakiwa watubu (ona Matendo 2:38).

Mahubiri ya pili ya Petro mbele ya watu, katika ukumbi wa Sulemani, yalikuwa na ujumbe unaofanana hivyo hivyo. Dhambi zisingefutwa pasipo kutubu.[6]

Tubuni basi, mrejee, ili dhambi zenu zifutwe (Matendo 3:19a – maneno mepesi kukazia).

Paulo aliposhuhudia mbele za Mfalme Agripa, alitangaza kwamba injili yake ilikuwa na ujumbe wa toba daima, kama ifuatavyo:

Kwa hiyo, Ee Mfalme Agripa, sikuyaasi yale maono ya mbinguni, bali kwanza niliwahubiri wale wa Dameski na Yerusalemu, na katika nchi yote ya Uyahudi, na watu wa Mataifa, kwamba watubu na kumwelekea Mungu, wakiyatenda matendo yanayopatana na kutubu kwao (Matendo 26:19-20. Maneno mepesi kukazia).

Huko Athene, Paulo aliwaonya wasikilizaji wake kwamba kila mtu lazima asimame kuhukumiwa mbele za Kristo, na wale wasiotubu hawatakuwa tayari kwa ajili ya siku hiyo kuu. Alisema hivi:

Basi, zamani zile za ujinga Mungu alijifanya kama hazioni; bali sasa anawaagiza watu wote wa kila mahali watubu. Kwa maana ameweka siku atakayowahukumu walimwengu kwa haki, kwa mtu yule aliyemchagua; naye amewapa watu wote uthabiti wa mambo haya kwa kumfufua katika wafu (Matendo 17:30-31. Maneno mepesi kukazia).

Alipokuwa anaagana na wazee wa Efeso, Paulo, katika mahubiri yake, aliorodhesha toba na imani kama sehemu muhimu sana ya ujumbe wake, kama ifuatavyo:

Sikujiepusha … nikiwashuhudia Wayahudi na Wayunani wamtubie Mungu, na kumwamini Bwana wetu Yesu Kristo (Matendo 20:20a, 21 – maneno mepesi kukazia).

Hii orodha ya Maandiko ambayo ni kama ushahidi wa hoja inapaswa kumfanya yeyote yule aamini kwamba umuhimu wa toba usipotangazwa, Injili ya kweli haijahubiriwa. Mahusiano na Mungu huanza kwa toba. Hakuna msamaha wa dhambi bila hiyo kuwepo.

Toba Inafafanuliwa

Pamoja na mwanga wa Maandiko mengi kuthibitisha kwamba wokovu hutegemea toba, watumishi wengine bado wanatafuta njia ya kuua umuhimu wake kwa kupindisha maana iliyo wazi na kutoa yao yenye kukubaliana na mawazo ya makosa waliyo nayo kuhusu neema ya Mungu. Kwa tafsiri yao mpya – toba si kitu zaidi ya kubadilisha mawazo kuhusu Yesu ni nani – tena cha ajabu – jambo hilo halipaswi kuathiri tabia ya mtu.

Sasa – wahubiri wa Agano Jipya walitazamia nini walipowaita watu kutubu? Je, walikuwa wanawaita wabadilishe tu mawazo yao kuhusu Yesu, au walikuw awanawaita watu kubadilisha tabia?

Paulo aliamini kwamba toba ya kweli ilidai mabadiliko ya tabia. Tumekwisha soma tayari ushuhuda wake juu ya miaka mingi ya huduma yake, alipotamka mbele ya Mfalme Agripa hivi:

Kwa hiyo, Ee Mfalme Agripa, sikuyaasi yale maono ya mbinguni, bali kwanza niliwahubiri wale wa Dameski na Yerusalemu, na katika nchi yote ya Uyahudi, na watu wa Mataifa, kwamba watubu na kumwelekea Mungu, wakiyatenda matendo yanayopatana na kutubu kwao (Matendo 26:19-20. Maneno mepesi kukazia).

Yohana Mbatizaji naye aliamini kwamba toba ilikuwa zaidi ya kubadili mawazo juu ya kweli fulani za kitheolojia. Wasikilizaji wake walipoitikia mwito wake wa toba kwa kumwuliza wafanye nini, aliorodhesha mabadiliko fulani ya tabia (ona Luka 3:3, 10-14). Pia aliwalaumu Mafarisayo na Masadukayo kwa kuigiza toba, na kuwaonya juu ya moto wa jehanamu kama wasingetubu kwa kweli.

Enyi wazao wa nyoka, ni nani aliyewaonya ninyi kuikimbia hasira itakayokuja? Basi zaeni matunda yapasayo toba …Na shoka limekwisha kuwekwa penye mashina ya miti; basi kila mti usiozaa matunda mazuri hukatwa na kutupwa motoni (Mathayo 3:7-10. Maneno mepesi kukazia).

Yesu alihubiri ujumbe wa toba aina hiyo hiyo kama Yohana (ona Mathayo 3:2; 4:17). Kuna wakati mmoja alipsema kwamba Ninawi walitubu kwa mahubiri ya Yona (ona Luka 11:32). Yeyote aliyewahi kusoma kitabu cha Yona anajua kwmaba watu wa Ninawi walifanya kitu zaidi ya kubadili mawazo yao tu. Walibadili tabia zao pia, wakaacha dhambi. Yesu anasema hiyo ni toba.

Toba ya KiBiblia ni badiliko la makusudi la tabia, kama itikio la dhati la imani ya kweli iliyozaliwa moyoni mwa mtu. Mtumishi anapohubiri Injili bila ya kutaja haja ya kuwepo kwa mabadiliko halisi ya tabia yenye kuonyesha toba, kwa kweli anafanya kazi kinyume cha shauku ya Kristo kwa wanafunzi. Tena, anawadanganya wasikilizaji wake kuamini kwamba wanaweza kuokoka bila ya kutubu. Kufanya hivyo kunawahakikishia kupotea kama watamwamini. Yeye anatenda kazi kinyume cha Mungu, na anamtumikia Shetani – ajue au asijue.

Mtumishi akitaka kufanya watu kuwa wanafunzi kama Yesu alivyoagiza, ni lazima aanze harakati hizo kisawasawa. Asipohubiri Injili ya kweli yenye kuwataka watu watubu na kuwa na imani tiifu, ni kwamba anaelekea kushindwa, hata ingawa anaweza kuonekana anafanikiwa sana machoni pa watu. Anaweza kuwa na kusanyiko kubwa, lakini anajenga nyumba yake kwa mbao, majani na manyasi, na kazi yake itakapopitishwa katika ule moto wa siku zijazo, thamani ya kazi yake itapimwa. Na itateketea (ona 1Wakor. 3:12-15).

Yesu Aita Watu Kujitoa

Yesu hakuita wasi-okoka wageuke na kuziacha dhambi tu – aliwaita pia wajitoe kumfuata na kumtii mara moja. Hakuwahi kueleza habari za wokovu kwa lugha nyepesi au rahisi, kama inavyofanyika siku hizi. Hakuwahi kuwaalika watu “kumkubali”, akiwaahidi msamaha, kisha baadaye apendekeze kwamba pengine wangetaka kujitoa wenyewe kumtii. Hapana. Yesu alidai kwamba hatua ya kwanza kabisa iwe ndiyo hatua ya kujitoa kwa moyo wote.

Cha kusikitisha ni kwamba, mwito wa Yesu kwamba watu wajitoe kikamilifu hupuuzwa mara nyingi na watu wanaokiri Ukristo. Au kama mwito ukitiliwa maanani, hufafanuliwa kwamba ni mwito wa kuingia katika mahusiano ya ndani zaidi ambao unatolewa kwa wale waliokwisha pokea neema ya Mungu ya wokovu – si mwito kwa wasio-okoka. Lakini, wengi katika hawa “waaminio” wanaodai kwamba ndiyo wameambiwa kujitoa kikamilifu na Yesu hawajali mwito Wake kama wanavyoufasiri. Wanadhani kwamba wana uchaguzi kuuitikia kwa kutokutii. Hivyo, hawauitikii kabisa.

Hebu tatazame mwito mmoja wa wokovu ambao Yesu anautoa, ambao mara nyingi hufasiriwa kuwa ni mwito wa kumkaribia Yeye zaidi, unaodhaniwa kutolewa kwa wale waliokwisha okolewa.

Akawaita mkutano pamoja na wanafunzi wake, akawaambia, ‘Mtu yeyote akitaka kunifuata na ajikane mwenyewe, ajitwike na msalaba wake, anifuate. Kwa kuwa mtu atakaye kuiponya nafsi yake, ataiangamiza, na mtu atakayeiangamiza nafsi yake kwa ajili yangu na kwa ajili ya Injili, huyu ataisalimisha. Kwa kuwa itamfaidia mtu nini kuupata ulimwengu wote, akipata hasara ya nafsi yake? Ama mtu atoe nini badala ya nafsi yake? Maana kila mtu atakayenionea haya mimi, na maneno yangu, katika kizazi hiki cha uzinzi na dhambi, Mwana wa Adamu atamwonea haya mtu huyo, atakapokuja katika utukufu wa Baba yake pamoja na malaika watakatifu’ (Marko 8:34-38).

Tuulize hivi: Je, huo ni mwito wa kuokolewa unaotolewa kwa wasioamini, au ni mwaliko wa kuingia katika mahusiano ya karibu zaidi, unaotolewa kwa waamini? Tukisoma kwa kumaanisha, jibu ni wazi kabisa.

Kwanza: Ona kwamba kundi ambalo Yesu alizungumza nao lilikuwa na wafuatao: “mkutano pamoja na wanafunzi Wake” (ms. 34 – maneno mepesi kukazia). Basi ni kwamba “mkutano” haukuwa wanafunzi Wake. Wao waliitwa na Yeye ili wasikie anachotaka kusema. Yesu alitaka kila mmoja – wafuasi na watafutaji – waelewe ukweli aliokuwa anataka kufundisha. Ona kwamba alianza kwa maneno haya: “Mtu yeyote” (ms. 34 – maneno mepesi kukazia). Maneno ya Yesu yanamhusu yeyote na kila mtu.

Tunapoendelea kusoma, inakuwa dhahiri zaidi kwamba Yesu alikuwa anasema na nani. Maneno Yake yalilengwa kwa kila mtu ambaye alitaka (1) kumfuata, (2) “kuiponya nafsi yake”, (3) kuto”pata hasara ya nafsi yake”, na (4) kuwa miongoni mwa wale ambao hatawaonea aibu, “atakapokuja katika utukufu wa Baba yake pamoja na malaika watakatifu”. Hayo maneno manne yanaonyesha kwamba Yesu alikuwa anawaelezea watu waliotamani kuokolewa. Je, ni sawa tufikiri kwamba kuna mtu anayekwenda mbinguni asiyetaka “kumfuata” Yesu na “kuponya nafsi yake”? Je, ni sawa kwetu kufikiri kwamba wapo waamini wa kweli ambao wata”pata hasara” ya nafsi zao, wenye kumwonea Yesu aibu na maneno Yake, na ambao Yesu atawaonea aibu atakaporudi? Ni dhahiri kwamba Yesu alikuwa anazungumza juu ya kupata wokovu wa milele katika fungu hili la Maandiko.

Ona kwamba zile sentensi nne za mwisho katika fungu hili lenye sentensi tano zinaanza na neno “kwa kuwa”. Ni kwamba kila sentensi husaidia kufafanua ile iliyotangulia. Hakuna sentensi katika fungu hili inayofaa kufasiriwa bila ya kufikiri zile nyingine zinaipa mwanga gani. Hebu tutazame maneno ya Yesu sentensi kwa sentensi, tukizingatia kweli hiyo hapo juu.

Sentensi Ya Kwanza

Mtu yeyote akitaka kunifuata na ajikane mwenyewe, ajitwike na msalaba wake, anifuate (Marko 8:34).

Ona tena kwamba maneno ya Yesu yalielekezwa kwa yeyote aliyetaka kumfuata Yeye – aliyetaka kuwa mfuasi Wake. Huu ndiyo uhusiano wa pekee ambao Yesu anautoa mwanzoni kabisa – kuwa mfuasi Wake.

Wengi wanapenda kuwa rafiki tu bila ya kuwa mfuasi, lakini uchaguzi wa aina hiyo haupo. Yesu hakumhesabu yeyote kuwa rafki Yake kama hakumtii. Aliwahi kusema hivi: “Ninyi ni rafiki zangu, mkitenda niwaamuruyo” (Yohana 15:14 – TLR).

Wengi wangependa kuwa ndugu Zake bila kuwa wafuasi Wake, lakini tena, Yesu hakutoa nafasi hiyo. Hakumhesabu yeyote kuwa ndugu kama hakuwa mtii. “Yeyote afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni, huyo ndiye ndugu yangu” (Mathayo 12:50 – TLR. Maneno mepesi kukazia).

Wengi wanapenda kujiunga na Yesu mbinguni bila ya kuwa wafuasi Wake, lakini Yesu alionyesha kutowezekana kwa jambo hilo. Wanaotii tu ndiyo wanaokwenda mbinguni, hivi: “Si kila aniambiaye, ‘Bwana! Bwana!’ ataingia katika ufalme wa mbinguni, bali ni wale watendaop mapenzi ya Baba yangu wa mbinguni” (Mathayo 7:21).

Katika sentensi hii tunayotazama, Yesu aliwaambia waliotaka kumfuata kwamba wasingeweza bila kujikana. Lazima wawe tayari kuweka shauku zao pembeni, na kuziweka chini ya mapenzi Yake. Kujikana na kujinyenyekeza ndiyo kiini cha kumfuata Yesu. Hiyo ndiyo maana ya “jitwike msalaba wako”.

Sentensi Ya Pili

Sentensi ya pili ya Yesu inasaidia kuelewa zaidi ile ya kwanza. Inasema hivi:

Kwa kuwa mtu atakaye kuiponya nafsi yake, ataiangamiza, na mtu atakayeiangamiza nafsi yake kwa ajili yangu na kwa ajili ya Injili, huyu ataisalimisha (Marko 8:35).

Ona tena kwamba sentensi hii inaanza hivi: “Kwa kuwa”. Hii inaiunganisha na sentensi ya kwanza, na kufafanua zaidi. Hapa Bwana Yesu anawalinganisha watu wawili – wale wale wanaotajwa katika sentensi ya kwanza – mmoja atakayejikana na kujitwika msalaba wake na kumfuata, na mwingine ambaye hatajikana. Sasa wanalinganishwa kwa habari ya mmoja kupoteza maisha yake kwa ajili ya Kristo na Injili, na mwingine kutopoteza. Tukitazama mahusiano kati ya hao wawili hatuna budi kuamua kwamba yule wa sentensi ya kwanza asiyejikana anafanana na yule wa sentensi yapili anayetaka kuokoa maisha yake, atakayeyapoteza. Na yule wa sentensi ya kwanza aliyekuwa tayari kujikana anafanana na yule katika sentensi ya pili anayekubali kupoteza maisha yake, lakini mwishowe anayaokoa.

Yesu hakuwa anazungumza juu ya mtu kupoteza au kuokoa uhai wake kimwili. Sentensi za baadaye katika fungu hili zinaonyesha kwamba Yesu alikuwa anazungumzia juu ya kupoteza na kupata katika umilele. Maneno kama hayo hayo yanatamkwa na Yesu katika Yohana 12:25, hivi: “Yeye aipendaye nafsi yake ataiangamiza; naye aichukiaye nafsi yake katika ulimwengu huu ataisalimisha hata uzima wa milele” (maneno mepesi kukazia).

Yule mtu wa sentensi ya kwanza ambaye hakutaka kujikana ndiye huyo huyo katika sentensi ya pili aliyetamani kuokoa nafsi yake. Basi tunaweza kusema hivi: kuokoa nafsi ya mtu maana yake ni kuokoa mipango ya mtu kwa ajili ya maisha yake binafsi. Hii ni dhahiri zaidi tunapomtazama yule mtu aliye tayari “kupoteza nafsi yake kwa ajili ya Kristo na Injili”. Yeye ndiye anayejikana, anayejitwika msalaba, anayeachilia mipango yake mwenyewe, ambaye sasa anaishi kwa kusudi la kuendeleza mipango ya Kristo na kuenea kwa Injili. Huyo ndiye atakayeokoa maisha yake. Yule anayetafuta kumpendeza Kristo badala ya kujipendeza mwenyewe atajikuta akifurahi mbinguni mwisho wa siku, huku yule anaye-endelea kujipendeza mwenyewe atajikuta akiteseka jehanamu mwisho wa siku, na huko atapoteza uhuru wote wa kufuata mipango yake.

Sentensi Ya Tatu Na Ya Nne

Sasa tutazame sentensi ya tatu na ya nne.

Kwa kuwa itamfaidia mtu nini kuupata ulimwengu wote, akipata hasara ya nafsi yake? Ama mtu atoe nini badala ya nafsi yake? (Marko 8:36-37).

Hapo tunaonyeshwa yule ambaye hatajikana mwenyewe. Tene huyu ndiye anayetaka kuokoa maisha yake, lakini mwishoni anayapoteza. Sasa anatajwa kwamba ni mwenye kutafuta kinachotolewa na dunia, ambaye mwishoni “anapoteza nafsi yake”. Yesu anaonyesha upumbavu wa mtu huyo kwa kulinganisha thamani ya dunia nzima na nafsi ya mtu. Ni kwamba wala havilinganishwi. Mtu anaweza kupata yote yatolewayo na dunia hii, lakini kama matokeo ya mwisho ni yeye kukaa milele jehanamu, anakuwa amefanya kosa kubwa sana.

Kutokana na sentensi ya tatu na ya nne tunapata pia kuona undani wa kinachowavuta watu wasijikane ili kuwa wafuasi wa Kristo. Ni shauku yao ya kujitosheleza, itolewayo na dunia. Wakisukumwa na ubinafsi, wale wanaokataa kumfuata Kristo hutafuta starehe za dhambi, ambazo wafuasi wa kweli wa Kristo huzikataa kwa sababu ya kumpenda na kumtii. Wanaojaribu kupata vyote vitolewavyo na dunia hutafuta mali, uwezo na sifa. Wafuasi wa kweli wa Kristo hutafuta kwanza ufalme Wake na haki Yake. Utajiri wowote, uwezo au sifa vinavyopatikana kwa sababu hiyo huhesabiwa kuwa ni nafasi ya uwakili toka kwa Mungu, ili kutumiwa kwa ajili ya utukufu Wake.

Sentensi Ya Tano

Hatimaye tunafikia sentensi ya tano katika fungu tunalotazama. Ona tena jinsi inavyounganishwa na zile nyingine kwa neno la kwanza – “maana”.

Maana kila mtu atakayenionea haya mimi, na maneno yangu, katika kizazi hiki cha uzinzi na dhambi, Mwana wa Adamu atamwonea haya mtu huyo, atakapokuja katika utukufu wa Baba yake pamoja na malaika watakatifu” (Marko 8:38).

Hapa tena tunamwona yule asiyejikana bali alitamani kufuata mipango na mapenzi yake, na kutafuta kile kinachotolea na dunia. Mwishoni anapoteza maisha yake na kupata hasara ya nafsi yake. Hapa sasa anaonyeshwa kama mtu ambaye anamwonea Kristo aibu na maneno Yake. Aibu yake inatokana na kutoamini kwake. Kama kweli angeamini kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu, asingemwonea aibu Yeye wala maneno Yake. Lakini, ni mmoja katika “kizazi cha uzinzi na dhambi”, na Yesu atamwonea aibu atakaporudi. Bila shaka Yesu hapo hazungumzi juu ya mtu aliyeokoka!

Jumla ya hayo yote ni nini? Ni hivi: Fungu hilo haliwezi kuwa mwito wa watu kujitoa zaidi – watu ambao wanaelekea mbinguni tayari. Bila shaka linaeleza njia ya kupata wokovu kwa kuwalinganisha wale ambao wameokoka kweli, na wale ambao bado. Walio-okoka kweli wanamwamini Bwana Yesu Kristo na wanajikana kwa ajili Yake. Wasio-okoka hawana imani ya aina hiyo, yenye utiifu.

Mwito Mwingine Kujitoa

Tunaweza kutazama miito mingi, lakini hebu tutazame mwingine tena unaotolea na Bwana Yesu ambao ni mwito wa wokovu.

Njooni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi (Mathayo 11:28-30).

Mara nyingi wainjilisti hutumia fungu hili la Maandiko katika mialiko yao, na ni sawa. Maneno hayo ni mwaliko wa wokovu. Hapa Yesu anatoa pumziko kwa “wasumbukao na wenye kulemewa na mizigo”. Si pumziko la kimwili kwa wale waliolemewa kimwili, bali ni pumziko la nafsi zo. Wasio-okoka wamelemewa na kujisikia hatia, hofu na dhambi, na wanapochoshwa na vitu hivyo, wanafaa sana kuokoka.

Kama watu aina hiyo wanahitaji kupokea pumziko ambalo Yesu anatoa, lazima wafanye mambo mawili kulingana na Yeye Mwenyewe. (1) Wamjie Yeye, na (2) wajitie nira Yake.

Waalimu wanaofundisha neema ya ungo wanabadilisha maana halisi ya “kujitia nira” ya Yesu. Wengine wanadai kwamba Yesu alikuwa anazungumza juu ya nira iliyoko shingoni Kwake mwenyewe. Ndiyo maana akaiita “nira yangu”. Wanasema hivi: Bila shaka Yesu alikuwa anazungumzia nira yenye pande mbili, ambayo nusu moja iko shingano mwa Yesu na nyingine iko wazi, ikingojea sisi tuivae kwenye shingo zetu. Wanasema kwamba Yesu anaahidi kwamba ndiye atakayehusika na kuvuta plau maana alisema nira Yake ni laini na mzigo ni mwepesi. Kwa hiyo, kazi yetu sisi ni kuhakikisha kwamba tumeunganishwa na Yesu kwa nira ya imani, tukimwachia Yeye afanye kazi yote kwa ajili ya wokovu wetu huku sisi tunafurahia faida zote zitokanazo na neema Yake! Nadhani mtakubaliana nami kwamba tafsiri hiyo ni ya kulazimisha – sivyo maandiko hayo yanavyosema!

Ni hivi: Wakati Yesu aliposema watu waliochoka wajitie nira Yake, alimaanisha kwamba wanapaswa kujinyenyekeza Kwake na kumfanya Yeye bwana wao na kumruhusu atawale au aongoze maisha yao. Hiyo ndiyo sababu Yesu alisema tunapaswa kujitia nira Yake na kujifunza kutoka Kwake. Wasio-okoka wako kama ng’ombe dume wasiofugwa – wanajiendea wanakotaka na kutawala maisha yao. Wanapojitia nira ya Yesu, wanamwachia Yeye utawala. Na sababu ya nira ya Yesu kuwa laini na mzigo Wake kuwa mwepesi ni kwamba Yeye hutuwezesha kumtii kwa Roho Wake akaaye ndani yetu.

Hapa tena tunaona kwamba Yesu aliwaita watu waokolewe, na mfano wa kufafanua wokovu hapa ni pumziko kwa waliochoka. Unapatikana kwa watu kujinyenyekeza Kwake na kumfanya Yesu kuwa Bwana wao.

Kuhitimisha

Yote hayo yamesemwa ili kuleta ujumbe huu: Mtumishi aliyefanikiwa kweli ni yule anayetii amri ya Yesu kwamba awafanye watu kuwa wanafunzi, anayejua kwamba kutubu, kujitoa na uanafunzi si vitu vya hiari kwa wanaokwenda mbinguni. Badala yake, ni maonyesho ya dhati kabisa ya imani yenye kuokoa. Basi, mtumishi mwenye mafanikio ni yule anayehubiri Injili ya KiBiblia kwa wasio-okolewa. Anawaita wasio-okoka watubu na kumfuata Yesu, naye hawahakikishii watu wasiojitoa kwamba wameokoka.


[1] Tafsiri hii inatokana na yale ambayo tumekwisha soma katika Mathayo 28:18-20, Yohana 8:31-32 na Luka 14:25-33.

[2] Wanafunzi wanatajwa katika Matendo 6:1, 2, 7; 9:1, 10, 19, 25, 26, 36, 38; 11:26, 29; 13:52; 14:20, 21, 22, 28; 15:10; 16:1; 18:23, 27; 19:1, 9, 30; 20:1, 30; 21:4, 16. Waamini wanatajwa katika Matendo 5:14; 10:45 na 16:1 tu. Kwa mfano: Katika Matendo 14:21, Luka aliandika hivi: “Hata [Paulo na Barnaba] walipokwisha kuihubiri Injili katika mji ule, na kupata wanafunzi wengi …” Basi Paulo na Barnaba walifanya watu kuwa wanafunzi kwa kuhubiri Injili, na watu wakawa wanafunzi mara tu walipookoka – sio baadaye walipoamua wenyewe!.

[3] Maandiko haya pia yanaonyesha kosa katika tabia ya kisasa ya kuwahakikishia waongofu wapya wokovu wao. Yesu hakuwahakikishia hao waamini wapya kwamba wameokoka kwa sababu waliomba sala fupi tu ya kumpokea, au kwa kuwa walitamka kwamba wanamwamini. Aliwahimiza kufikiri ikiwa ukiri wao ulikuwa halisi na kweli. Sisi pia tufuate mfano Wake.

[4] Tena, Yakobo anasema kwamba hatuwezi kuokolewa kwa imani iliyo peke yake, kinyume na wale wanaodai kwamba tumeokolewa kwa imani hata kama hatuna matendo. “Basi, mtu huhesabiwa haki kwa matendo, wala si imani peke yake” – TLR. Imani ya kweli haiko peke yake; kila mara inaambatana na matendo.

[5] Inasaidia pia kukumbuka kwamba sababu ya Paulo kusema mara nyingi sana kwamba wokovu ni kwa neema na si kwa matendo ni mapambano yake mara kwa mara na washika sheria wa siku zake. Paulo hakuwa anawasahihisha waliofundisha kwamba wokovu ni kitu cha lazima ili watu wafike mbinguni, kwa sababu yeye mwenyewe aliamini hivyo na mara nyingi alisema hivyo. Ila, aliandika ili kuwasahihisha Wayahudi ambao, kwa kukosa kutambua swala la neema ya Mungu katika wokovu, hawakuona sababu yoyote ya kufa kwa Yesu. Wengi hawakuamini kwamba watu wa Mataifa wangeweza kuokoka, kwa sababu hawakuwa na wazo la neema ya Mungu kuwezesha wokovu kupatikana. Baadhi yao walifikiri kwamba tohara, ukoo wa kimwili au kushika Torati (kitu ambacho wala hawakukifanya pia) vilimfanya mtu kupata wokovu. Hilo lilibatilisha neema ya Mungu na sababu ya Kristo kufa.

[6] Vivyo hivyo, wakati Roho Mtakatifu alipomfunulia Petro kwamba watu wa Mataifa wangeokolewa kwa kumwamini Yesu tu, Petro alitangaza kwa watu waliokuwa nyumbani mwa Kornelio hivi: “Sasa natambua kwamba Mungu hana upendeleo, bali katika kila taifa, yule amchaye Yeye na kutenda yaliyo sawa, hupokelewa Naye” (Matendo 10:34b na 35 – maneno mepesi kukazia). Petro pia alitangaza katika Matendo 5:32 kwamba Mungu alimtoa Roho Mtakatifu “kwa wale wenye kumtii”. Wakristo wote wa kweli wanaye Roho Mtakatifu akikaa ndani yao (ona Warumi 8:9; Wagalatia 4:6).

Kuendelea Sawasawa

Sura Ya Tatu

Kwa miaka mingi na kwa njia nyingi sana nilifuata – bila ya kujua – kawaida ambazo zilikuwa kinyume cha lengo ambalo Mungu alitaka nilifuate – lengo la kuwafanya watu kuwa wanafunzi. Lakini Roho Mtakatifu kwa neema Yake alianza kunifungua macho taratibu, nikaona makosa yangu. Kitu kimoja nilichojifunza ni hiki: Ninatakiwa kuhoji kila kitu nilichofundishwa na kuamini, kwa mwangaza wa Neno la Mungu. Desturi zetu zinapofusha macho yetu tusione kile ambacho Mungu amesema. Halafu kibaya sana ni kwamba, tunajivunia sana desturi zetu, tukiwa na uhakika kwamba tunasimama miongoni mwa kundi la kipekee sana ambalo lina ufahamu mkubwa zaidi wa kweli kuliko Wakristo wengine. Mwalimu mmoja alisema hivi, kwa dharau sana: “Kuna madhehebu elfu thelathini na mbili duniani leo. Ninyi mna bahati kwamba ni washirika wa lile ambalo ndiyo la kweli!”

Matokeo ya kiburi chetu ni kwamba Mungu hutupinga, maana Yeye huwapinga wenye kiburi. Tukitaka kuwa na maendeleo ya aina yoyote na kuwa tayari kusimama mbele za Yesu, lazima tujinyenyekeze wenyewe. Mungu huwapa neema wanyenyekevu.

Tutazame Nafasi Ya Mchungaji

Lengo la mtumishi kuwafanya watu kuwa wanafunzi linatakiwa kutawala kila kitu anachofanya katika huduma. Daima ajiulize hivi: “Je, ninachofanya kinachangia vipi katika mpango wa kuwafanya watu kuwa wanafunzi watakaotii amri zote za Yesu?” Swali hilo rahisi tu la kujipima, likiulizwa kwa kumaanisha, litaondoa vitu vingi sana vinavyofanywa kama shughuli za Kikristo.

Hebu tufikiri kidogo juu ya huduma ya mchungaji au mzee au mwangalizi,[1] mtu ambaye kazi yake kihuduma humweka kwenye kanisa moja la mahali. Kama huyo anataka kuwafanya watu kuwa wanafunzi watakaotii amri zote za Yesu, kazi yake moja ni ipi? Kufundisha. Yesu alisema kwamba wanafunzi hupatikana kwa kufundisha (ona Mathayo 28:19-20). Sharti moja la mtu kuwa mzee au mchungaji au mwangalizi ni kwamba “aweze kufundisha” (1Timo. 3:2). Wale “wafanyao bidii katika kuhubiri na kufundisha” wapewe “heshima mara dufu” (1Timo. 5:17).

Basi – mchungaji atathmini kila mahubiri kwa kujiuliza swali hili: “Je, mahubiri haya yanasaidiaje kufanikisha kazi ya kufanya watu kuwa wanafunzi?”

Lakini je, wajibu wa mchungaji kufundisha unakamilika kwa mahubiri yake ya Jumapili au katikati ya wiki? Kama anafikiri ndiyo, anasahau ukweli kwamba Maandiko yanasema wajibu wake wa kufundisha unakamilika kwa maisha anayoishi na mfano anao-onyesha. Mfano wenye kufundisha wa maisha yake ya kila siku huongezewa tu kwa ile huduma ya kufundisha. Hii ndiyo sababu masharti kwa ajili ya wazee au wachungaji au waangalizi yanahusu zaidi tabia ya mtu na jinsi anavyoishi kuliko uwezo wake wa kusema. Kati ya masharti kumi na tano kwa ajili ya waangalizi yanayotajwa katika 1Timotheo 3:1-7, kumi na nne yanahusiana na tabia, na moja tu linahusu uwezo wa kufundisha. Katika masharti kumi na nane yanayotajwa kwa ajili ya wazee katika Tito 1:5-9, kumi na saba yanahusiana na tabia na moja tu linahusu uwezo wa kufundisha. Paulo alianza kwa kumkumbusha Timotheo hivi: “Uwe mfano kwao waaminio, katika usemi na mwenendo, na katika upendo na imani na usafi” (1Timo. 4:12 – maneno mepesi kukazia). Ndipo akasema, “Hata nitakapokuja, ufanye bidii katika kusoma na kuonya na kufundisha” (1Timo. 4:13). Basi tunaona kwamba mfano wa tabia ya Timotheo unatajwa kabla ya huduma yake ya kufundisha, kuonyesha jinsi maisha yalivyo muhimu zaidi.

Petro naye aliandika hivi:

Nawasihi wazee walio kwenu, mimi niliye mzee mwenzenu, na shahidi wa mateso ya Kristo, na mshirika wa utukufu utakaofunuliwa baadaye; lichungeni kundi la Mungu lililo kwenu na kulisimamia, si kwa kulazimishwa, bali kwa hiari kama Mungu atakavyo; si kwa kutaka fedha ya aibu, bali kwa moyo. Wala si kama wajifanyao mabwana juu ya mitaa yao, bali kwa kuwa mifano kwa lile kundi (1Petro 5:1-3. Maneno mepesi kukazia).

Nani anayetuhamasisha kujikana na kumtii Kristo? Je, ni wale ambao mahubiri yao tunayafurahia, au ni wale ambao tunatamani maisha yao? Wachungaji wasiojitoa, wenye maneno laini, hawamvuti yeyote ajitwike msalaba wake. Kama wachungaji hao watahubiri mara moja moja ujumbe wa kujitoa kwa Kristo, inabidi wahubiri kwa kufunika-funika, maana wasikilizaji wao watahoji ukweli wa maneno yao. Viongozi wengi Wakristo wa siku zilizopita hawakumbukwi kwa mahubiri yao bali kwa kujitoa kwao. Mifano yao inatuhamasisha kwa muda mrefu baada ya kuondoka kwao.

Kama mchungaji haonyeshi mfano wa utii kama mfuasi wa kweli wa Yesu Kristo, anapoteza wakati wake kuhubiri. Ee Mchungaji: Mfano wa maisha yako unazungumza kwa sauti mara kumi zaidi kuliko mahubiri yako. Je, unawahamasisha watu kujikana na kumfuata Kristo kwa kujikana mwenyewe na kumfuata Kristo?

Lakini – mchungaji anawezaje – kwa mfano wa maisha yake – kufundisha watu ambao wanamjua kama msemaji fundi wa Jumapili asubuhi? Kama wanampata na kumwona kwa karibu akiishi maisha yake, ni kule kusalimiana kwa sekunde tano wanapotoka ibadani. Labda kuna kitu ambacho si sahihi katika utaratibu wa siku hizi wa uchungaji.

Mahubiri Ya Jumapili Asubuhi Kila Juma

Kosa lingine analoweza kufanya mchungaji ni kufikiri kwamba wajibu wake wa kufundisha ni ule wa kutoa mihadhara mbele za watu kila juma. Huduma ya Yesu ya kufundisha haikuwa mahubiri mbele za watu tu, bali pia mazungumzo binafsi yaliyosababishwa na maswali ya wanafunzi Wake. Tena, mengi ya mahubiri Yake mbele za watu hayakuwa marefu sana – ukichunguza kwa makini. Halafu, mazungumzo Yake na wanafunzi hayakuwa ni nusu saa kila siku kwa juma katika kanisa, bali yalifanywa pembeni ya bahari, ndani ya nyumba, na wakati wanatembea njiani kwenye vumbi nyingi. Yesu aliishi maisha Yake kikamilifu mbele ya macho ya wanafunzi Wake. Mtindo huo huo wa kufundisha ulifuatwa na mitume. Baada ya Pentekoste, wale Thenashara walifundisha “hekaluni na nyumba kwa nyumba” (Matendo 5:42 – maneno mepesi kukazia). Kila siku walikuwa wanakutana na kuhusiana na waaminio. Hata Paulo alifundisha “hadharani na nyumba kwa nyumba” (Matendo 20:20 – maneno mepesi kukazia).

Kama wewe ni mchungaji, bila shaka kufikia hapa umekwisha anza kulinganisha huduma yako ya kufundisha na ile ya Yesu, au mitume wa kwanza. Pengine umeanza hata kujiuliza kama kile ambacho umekuwa ukifanya ndicho Mungu anakusudia ufanye, au pengine unafanya yale ambayo ni mapokeo ya kanisa lenu kwa miaka mamia na mamia. Kama umeanza kujihoji hivyo, ni vizuri – tena vizuri sana. Hiyo ni hatua ya kwanza kuelekea upande unaofaa.

Labda hata umefikiri zaidi. Pengine umejiuliza hivi: “Nitapata wapi muda unaohitajika kufanya huduma kama hiyo – yaani, kuwafundisha watu nyumba kwa nyumba, au kuwahusisha katika maisha yangu ya kila siku ili niweze kuwashawishi kwa mfano wa maisha yangu?” Hilo ni swali zuri sana, kwa sababu linaweza kukufanya uzidi kujiuliza kama kuna kitu kingine kisichokuwa sahihi katika mtindo wa kisasa wa nafasi ya mchungaji.

Yawezekana umefikiri hivi: “Sidhani kama ningetaka kuishi maisha yangu kwa ukaribu kiasi hicho na washirika wangu. Nilifundisha Shule ya Biblia kwamba mchungaji hapaswi kuwa karibu sana na washirika wake. Kwamba lazima ajitenge kidogo ili waweze kumheshimu kama kiongozi. Kwamba hapaswi kuwa na marafiki wa karibu katika washirika wake.”

Wazo la aina hiyo linaonyesha kwamba kuna kasoro katika jinsi mambo yanavyofanywa katika kanisa la kisasa. Bwana Yesu alikuwa karibu mno na wale Thenashara kiasi cha mmoja kujisikia huru kabisa kuegemeza kichwa kifuani Pake wakati wa chakula (ona Yohana 13:23-25). Waliishi pamoja kwa miaka kadhaa. Unaonaje hapo – Yesu alikuwa anajitahidi kujitenga ili aweze kuwahudumia vizuri zaidi?

Kulinganisha Mbinu – Za Zamani Na Za Kisasa

Kama lengo ni kumtii Yesu na kuwafanya watu kuwa wanafunzi, si ingekuwa busara sisi kufuata mbinu Zake? Zilifaulu sana alipozitumia Yeye, na hata mitume waliomfuata walifaulu sana walipozitumia.

Je, mbinu za kisasa zinafanikiwa kwa kiasi gani kuwafanya watu kuwa wanafunzi ambao wanatii amri zote za Kristo? Wakati matokeo ya utafiti katika Wakristo unapo-onyesha tena na tena kwamba hakuna tofauti katika mitindo ya maisha ya Wakristo wengi ikilinganisha na wasiokuwa Wakristo, labda wakati umefika kujiuliza maswali na kuchunguza Maandiko upya.

Angalia swali hili – lenye kufunua mengi – tunalotakiwa kujiuliza: Kanisa la kwanza lilifanikiwaje – tena vizuri sana – kuwafanya watu kuwa wanafunzi – pasipo kuwa na majengo, wachungaji waliosomea kazi yao, shule za Biblia, vitabu vya nyimbo na mitambo ya kuonyesha nyimbo ukutani, mashine za kupaza sauti na kutoa nakala za kanda, taratibu za Shule ya Jumapili na huduma kwa vijana, vikundi vya kuongoza sifa, kwaya, mashine kama kompyuta na fotokopi, vituo vya Kikristo vya redio na televisheni, maelfu kwa maelfu ya vitabu vya Kikristo na Biblia za watu binafsi? Hawakuhitaji hata kimoja katika vitu hivyo ili kuwafanya watu kuwa wanafunzi, na hata Yesu hakuhitaji. Na kwa sababu vitu hivyo havikuwa muhimu wakati ule, hakuna hata kimoja kilicho muhimu hata sasa. Vinaweza kuwa msaada, lakini hakuna kilicho cha muhimu. Ukweli ni huu: vingi katika hivyo vinaweza kutuzuia sisi kufanya watu kuwa wanafunzi. Hebu nitoe mifano miwili.

Tutazame kwanza kitu ambacho siku hizi kimekuwa cha muhimu sana – kuwa na wachungaji waliosoma Vyuo vya Biblia kama viongozi makanisani. Paulo hakuwahi kusikia jambo hilo. Kuna miji ambayo, baada ya kuanzisha makanisa, Paulo aliondoka na hakuwepo kwa majuma au miezi kadhaa. Kisha alirudi na akawaweka wazee wa kuyasimamia (tazama mfano katika Matendo 13:14 hadi 14:32). Maana yake ni kwamba makanisa hayo – bila ya kuwepo kwa Paulo – hayakuwa na uongozi rasmi wa wazee kwa majuma kadhaa au hata miezi, na kwamba wazee wengi walikuwa ni waamini wapya bado walipochaguliwa. Hawakuwa wamepitia kitu kinachofanana na mafunzo ya miaka miwili au mitatu yaliyowatayarisha kufanya kazi yao.

Ni hivi: Biblia inafundisha kwamba wachungaji au wazee au waangalizi hawahitaji elimu ya miaka miwili hadi mitatu ili wafanikiwe katika huduma. Hakuna awezaye kutoa hoja kinyume cha hilo. Lakini masharti ya siku hizi daima yanatuma ujumbe ufuatao kwa kila aaminiye: “Ukitaka kuwa kiongozi kanisani, unahitaji kusoma miaka kadhaa.”[2] Jambo hili linapunguza kasi ya kuzaa viongozi, na kupunguza kasi ya kufanya watu kuwa wanafunzi, na kupunguza kasi ya kukua kwa kanisa. Sijui makampuni yenye kuuza bidhaa yangefanikiwaje kufikia masoko yao kama wangedai kwamba kila muuzaji wao ahamishe familia yake kwenda mji fulani ili kupata mafunzo ya miaka mitatu kabla ya kuruhusiwa kuuza bidhaa!

Kuna hoja hapa – “Lakini, uchungaji ni kazi ngumu sana, yenye mambo mengi! Biblia inasema tusimweke mwongofu mpya katika nafasi ya usimamizi” (ona 1Timo. 3:6).

Sawa – lakini cha kwanza ni hiki: Nini tafsiri ya mwongofu mpya? Mtazamo wa Paulo ulikuwa tofauti na wetu, kwa sababu yeye aliwaweka watu kuwa wazee au wachungaji au waangalizi baada ya miezi michache tu ya wokovu.

Pili ni hivi: Sababu moja ya uchungaji wa kisasa kuwa mgumu na wenye mambo mengi ni kwamba, utaratibu mzima wa kanisa na wa huduma umetofautiana sana na jinsi Biblia inavyofundisha. Tumeufanya kuwa wa hali ya juu na mgumu kiasi cha kwamba wanaoweza kufaulu tu na kuwezana na matakwa yake ni watu ambao si wa kawaida!

Hoja nyingine – “Mungu apishe mbali kanisa lisije likasimamiwa na mtu ambaye hana elimu ya Chuo cha Biblia. Huyo mwangalizi ataongoza kundi lake liingie kwenye mafundisho ya uongo!”

Inaonekana jambo hilo halikumsumbua Paulo. Ukweli ni kwamba siku hizi tunao watumishi waliosoma Vyuo vya Biblia ambao hawaamini Yesu alizaliwa na bikira. Wanaunga mkono ushoga, wanafundisha kwamba Mungu anataka kila mtu awe na gari la kifahari, na kusema kwamba Mungu amechagua watu wa kuokoka na wa kupotea. Tena wanasema – bila hata kuogopa – kwamba mtu anaweza kuingia mbinguni bila ya kumtii Kristo. Vyuo vya Biblia vya siku hizi vimefanya kazi ya kukuza mafundisho ya uongo, na watumishi watokanao na vyuo hivyo wamezidisha kasi ya mafundisho hayo.

“Washirika wa kawaida” wanaogopa kuwahoji hao, kwa sababu wamepitia vyuoni na wanaweza kutoa maandiko mengi “ya kuthibitisha hoja” zao. Tena, hao watumishi wametengeneza na kugawa makanisa yao na kuyatenga na mwili wa Kristo kwa sababu ya mafundisho yao ya kipekee mpaka kufikia kutangaza tofauti zao kwa majina kwenye vibao mbele ya makanisa. Ujumbe wanaotuma kwa dunia ni huu: “Sisi si kama Wakristo wale wengine.” Tena – kibaya zaidi ni kwamba wanamwita ‘muasi’ kila asiyekubaliana na mafundisho yao potofu na yenye kugawa watu. Mateso Kikanisa bado yapo, na yanaongozwa na watu wenye vyeti kutoka vyuoni. Je, huo ndio mfano ambao Yesu anataka uwekwe na wanaofanya watu kuwa wanafunzi, wanaojulikana kwa kupendana wao kwa wao?

Siku hizi Wakristo wanachagua makanisa kutokana na mafundisho fulani. Kuwa na mafundisho sahihi kimekuwa kitu cha maana zaidi kuliko kuwa na mtindo sahihi wa maisha. Yote hayo ni kwa sababu utaratibu wa KiBiblia umeachwa.

Njia Mbadala Ya KiBiblia

Je, ninajaribu kusukuma kwamba waamini wenye miezi mitatu katika wokovu wachukuliwe na kupewa usimamizi wa makanisa – kama alivyofanya Paulo? Ndiyo – lakini ni kama hao waamini wanatimiza masharti yatolewayo na Biblia kuhusu wazee au wasimamizi – na, ikiwa watapewa kusimamia makanisa ambayo yanafuata utaratibu wa KiBiblia. Yaani – hayo makanisa lazima yawe mapya kabisa, yenye kuwa chini ya mamlaka ya mtumishi aliyekomaa kama vile mtume, anayeweza kuyasimamia.[3] Kwa hali hiyo, hao viongozi wapya hawatakuwa peke yao.

Jambo la pili ni kwamba, makusanyiko hayo yawe madogo kiasi cha kutosha kukutanikia nyumbani, kama ilivyokuwa kwa makanisa ya mwanzo.[4] Hiyo inarahisisha usimamizi. Pengine ndiyo sababu sharti moja la wazee au waangalizi ni kwamba waweze kusimamia nyumba zao vizuri (ona 1Timo. 3:4-5). Kusimamia nyumba ndogo ya waamini si kazi sana – ni sawa na kusimamia familia tu.

Jambo la tatu ni kwamba hilo kusanyiko liwe na watu ambao wamepokea Injili ya KiBiblia na kutubu. Jambo hilo huwafanya kuwa wafuasi halisi wa Bwana Yesu Kristo. Hilo linaondoa changamoto zote zinazotokana na kujaribu kuchunga kondoo ambao kwa kweli ni mbuzi.

Na jambo la nne ni kwamba, wachungaji au wazee au waangalizi husika lazima wafuate na kutekeleza nafasi yao KiBiblia – sio ile iliyozoeleka. Yaani – wasiwe ndiyo nyota – ndiyo watu muhimu – ndiyo wakuu – kama ilivyo kawaida katika makanisa mengi ya siku hizi.[5] Badala yake, wawe ni sehemu katika mwili, watumishi wanyenyekevu wenye kufundisha kwa mfano na kwa masomo, ambao lengo lao ni kuwafanya watu kuwa wanafunzi – si kuwa wasemaji mabingwa wa Jumapili asubuhi, bali wafuate mbinu za Yesu.

Utaratibu huo ukifuatwa, basi baadhi ya waamini wenye miezi mitatu katika wokovu wanaweza kusimamia makanisa.

Majengo

Vipi kuhusu majengo? Hili nalo ni jambo “muhimu” la kisasa ambalo kanisa la kwanza halikuwa nalo, lakini wakafaulu sana. Je, majengo husaidia katika mpango mzima wa kufanya watu kuwa wanafunzi?

Mimi nilipokuwa mchungaji, mara nyingi nilijisikia kama muuza kiwanja, mfanya kazi benki, fundi ujenzi na mtaalamu wa kukusanya fedha. Nimewahi mpaka kuota majengo usiku, nimetafuta majengo, nimerekebisha majengo yaliyozeeka, nimekodisha majengo, nimejenga majengo mapya na kuyakarabati wakati Mungu alipoleta mvua kubwa. Majengo hutumia muda na nguvu nyingi sana. Sababu ya kufanya mengi sana kwa habari ya majengo ni kwamba nilikuwa na uhakika – kama wachungaji wengi – kwamba hakuna kufanikiwa bila ya jengo – mahali pa kanisa kukutania.

Majengo pia yanakula fedha nyingi sana. (Huko Marekani, kuna makusanyiko yenye kutumia mamilioni ya dola kwa ajili ya majengo.) Baada ya ndoto yangu kupata majengo ilipotimia, nikawa ninaota kuhusu siku ambapo madeni yote tuliyokopa kwa ajili ya majengo yangemalizika, ili tuweze kutumia fedha hiyo katika huduma. Kuna wakati nilitambua – nikiwa nafundisha washirika kuhusu uwakili na jinsi ya kutoka kwenye madeni – kwamba, mimi nilikuwa nimehusika kutuingiza sote kwenye madeni! (Kweli, nilifundisha kwa mfano hai.)

Majengo mengi ya kanisa hutumiwa kwa masaa machache tu, tena mara moja au mbili kwa juma. Ni shirika gani lingine duniani kote lenye kujenga majengo yasiyotumiwa sana? (Jibu ni: dini za uongo.)

Hilo shimo la kumeza fedha huleta matatizo mengi. Mchungaji mwenye jengo anahitaji fedha kila wakati, na hilo huathiri anachofanya. Anajaribiwa kuwajali sana matajiri (ambao mara nyingi wanatoa bila ya kujitoa), anajaribiwa kubadilisha mafundisho yoyote yanayoweza kuwakwaza watu wengine, na wakati mwingine kugeuza Maandiko ili yatosheleze haja yake. Mahubiri yake mengi yanahusu mada ambazo hazizuii fedha kuja, bali hutia moyo kuongezeka kwake. Kwa sababu hiyo, wakati mwingine Wakristo wanaanza kufikiri kwamba mambo muhimu kwa mwamini ni (1) kulipa zaka (kitu ambacho Yesu alisema ni kidogo) na (2) kuhudhuria ibada (ambapo zaka zinakusanywa kila Jumapili). Hiyo si picha ya kufanya watu kuwa wanafunzi. Lakini wachungaji wengi wanaota ndoto za kupata makusanyiko ambayo kila mtu atafanya hayo mambo mawili tu. Ikiwa mchungaji angekuwa na kusanyiko ambalo nusu yake wanafanya hayo mambo mawili tu, basi angeweza kuandika vitabu na kuuza siri yake kwa wachungaji wengine mamilioni!

Ukweli ni huu: Katika kitabu cha Matendo, hatuambiwi juu ya kusanyiko lolote likinunua au kujenga jengo. Waamini walikutania nyumbani.[6] Hawakuwa na michango kwa ajili ya mfuko wa ujenzi. Katika nyaraka hatusomi maagizo yoyote kusimamia ujenzi wa makanisa. Tena, hakuna mtu aliyefikiri juu ya kuwa na jengo mpaka Ukristo ulipotimiza miaka mia tatu – wakati kanisa lilipofunga ndoa na dunia chini ya agizo la mfalme Konstantino. Miaka mia tatu? Hebu fikiri ni muda mrefu kiasi gani huo! Na kanisa likakua na kuongezeka sana – hata nyakati za mateso makali sana – pasipo kuwa na majengo. Jambo hilo limerudiwa mara nyingi tu katika karne zilizopita. Hivi karibuni jambo hilo limetokea huko Uchina. Yawezekana yapo makanisa zaidi ya milioni moja huko Uchina yanayokutania nyumbani.

Saa Tano Jumapili Asubuhi Ndiyo Saa Yenye Ubaguzi Mkubwa

Majengo ya kisasa yenye kuiga mfano wa KiMarekani yanatazamiwa kuwa na nafasi ya kutosha kwa ajili ya huduma kwa watu wa umri zote. Kanisa la mwanzo halikuwa hivyo – halikuwa na huduma maalum za kibinafsi kwa ajili ya wanaume, wanawake, na umri mbalimbali wa watoto. Kanisa lilikuwa na umoja katika kila hali, sio matengano. Familia ililindwa, na wajibu wa wazazi kiroho ulikaziwa na mfumo wa kanisa badala ya kumalizwa, kama ilivyo katika mpango wa kisasa wa majengo ya kanisa.

Je, jengo la kanisa huchangia katika kuwafanya watu kuwa wanafunzi, au huzuia? Kulingana na historia, kuwafanya watu kuwa wanafunzi kumefaulu sana katika karne nyingi pasipo majengo, na kwa sababu nyingi tu nzuri.

Kukutania nyumbani – kama kanisa la kwanza lilivyofanya kwa karne tatu za kwanza – kulijenga mazingira mazuri kwa ajili ya waamini kukua kweli kiroho. Wewe fikiri: unaingia mahali ambapo kwa masaa matatu hadi matano kuna mlo wenye furaha, mafundisho, nyimbo na karama za kiroho.Washirika hao – viungo vya mwili wa Kristo – walijisikia ni wahusika kwa jinsi walivyoketi wakitazamana, badala ya jinsi washirika wa makanisa ya kisasa wanavyojisikia – kama watazamaji kwenye viwanja vya michezo, huku wakitazamana visogo na kujitahidi wasikose onyesho linaloendelea ukumbini! Ile hali ya kawaida tu ya mlo wa pamoja ilisababisha watu kufunguka na kuanzisha mahusiano halisi ya kujaliana na kushirikiana kweli kweli – wala hakuna mfano wake katika “faragha” za kisasa – ambazo ni kupeana mkono kijuu-juu tu kwa watu wasiojuana kabisa walioketi pamoja, wakati mchungaji anaposema iwe hivyo.

Mafundisho yalikuwa ni kama vipindi vya maswali na majibu, na majadiliano kati ya watu wanaofanana, badala ya kuwa kama mihadhara itolewayo na watu waliovalia mavazi ya kitofauti, waliosema kwa sauti tofauti, na waliosimama juu sana ya wasikilizaji waungwana (japo waliochoka!). Wachungaji hawakuandaa “mahubiri ya wiki.” Yeyote (pamoja na wazee, wachungaji na waangalizi) angeweza kupokea fundisho kutoka kwa Roho Mtakatifu.

Watu walipokuwa wengi katika nyumba, wazee wasingewaza juu ya kutafuta jengo kubwa. Kila mtu alijua kwamba iliwapasa kugawanyika na kuwa makusanyiko mawili katika nyumba mbili. Ikawa ni kazi ya kutafuta uongozi wa Roho Mtakatifu kwamba mkutano mpya ufanyikie wapi, na msimamizi awe nani. Wala hawakuwa na haja ya kuanza kukusanya sifa za wageni na kutafuta maelekezo kwa wataalamu wa kukua kwa kanisa ili watazame itikadi zao na filosofia zao. Tayari miongoni mwao walikuwepo waangalizi watarajiwa, ambao walikwisha pata mafunzo kazini, na ambao walijua wanachama wa kundi lao la baadaye. Hilo kanisa jipya la nyumbani lilipata nafasi ya kufanya uinjilisti katika eneo jipya na kuwaonyesha wasioamini Wakristo ni nani – ni watu waliopendana. Ilikuwa ni rahisi tu kwao kuwakaribisha wasioamini kwenye mikutano, kama kuwakaribisha kula chakula.

Mchungaji Aliyebarikiwa – Mwenye Heri

Hakuna mchungaji wa kanisa la nyumbani au mzee au mwangalizi aliyefikia mahali pa “kumalizika” kihuduma kutokana na kuzidiwa na majukumu ya kichungaji – jambo ambalo katika kanisa la kisasa lime-enea sana. (Kuna utafiti uliofanywa huko Marekani wenye kuonyesha kwamba wachungaji elfu moja na mia nane wanaacha huduma kila mwezi!) Alikuwa na kundi dogo tu la kusimamia, na kama hilo kundi dogo liliweza kumpa fedha za kukidhi mahitaji yake ili afanye huduma moja kwa moja, basi alipata nafasi ya kuomba, kutafakari, kuhubiri Injili kwa wasioamini, kusaidia maskini, kutembelea wagonjwa na kuwaombea, na kuwa na muda mzuri kabisa na wanafunzi wapya ili kuwawezesha kufanya hayo aliyokuwa anafanya wakiwa pamoja. Utawala kanisani ulikuwa kitu rahisi tu.

Alishirikiana na wazee wengine au wachungaji au waangalizi katika eneo lake la kazi. Hapakuwa na haja ya kushindana ili kuwa na “kanisa kubwa” hapo mjini au “huduma bora ya vijana” hapo mjini au “mipango mizuri kwa ajili ya ibada ya watoto” katika mji huo. Watu hawakwenda kanisani ili kupima uzuri wa kundi la kuongoza sifa na ibada, au jinsi mchungaji alivyokuwa anavutia watu. Walikuwa wamezaliwa mara ya pili, na walimpenda Yesu na watu Wake. Walipenda kula pamoja na kushirikiana karama zozote ambazo Mungu aliwapa. Lengo lao lilikuwa kumtii Yesu na kuwa tayari kusimama mbele ya kiti Chake cha hukumu.

Ndiyo – makanisa ya nyumbani yalikuwa na matatizo, na ndiyo yanayotajwa katika nyaraka. Lakini matatizo mengi yanayokumba makanis aya kisasa na kuzuia watu kuwa wanafunzi hayakuwepo katika kanisa la kwanza kwa sababu utaratibu wao wa kanisa la mahali pamoja ulikuwa tofauti na jinsi ilivyo sasa. Tafadhali tafakari hili: Hayakuwepo majengo mpaka mwanzo wa karne ya nne. Kama ungeishi wakati wa zile karne tatu za kwanza, huduma yako ingekuwaje tofauti na jinsi ilivyo leo?

Tumalize hivi: Tukiwa makini kufuata taratibu za KiBiblia, tutafanikiwa sana kutimiza lengo la Mungu la kuwafanya watu kuwa wanafunzi. Vizuizi vikubwa katika kuwafanya watu kuwa wanafunzi makanisani siku hizi hutokana na taratibu na mipango isiyokuwa ya KiBiblia.


[1] Inaonekana wazi kabisa kwamba mchungaji ni sawa na mzee au mwangalizi. Kwa Kiyunani, neno linalotafsiriwa mchungaji ni poimain. Neno presbuteros ndiyo mzee, na neno episkopos ndiyo askofu au mwangalizi. Kwa mfano: Paulo aliwashauri wazee wa Efeso (presbuteros), ambao alisema wamefanywa kuwa wasimamizi au waangalizi (episkopos) na Roho Mtakatifu, walichunge (poimaino) kundi la Mungu (tazama Matendo 20:28). Pia alitumia neno wazee (presbuteros) na wasimamizi au waangalizi (episkopos) pamoja katika Tito 1:5-7. Petro naye aliwashauri wazee (presbuteros) walichunge (poimaino) kundi (ona 1Petro 5:1-2). Kwamba askofu ni cheo cha juu kuliko mchungaji au mzee, na ni mwangalizi wa makanisa mengi ni kitu kilichotungwa tu na wanadamu.

 

[2] Mkazo wa siku hizi kuhusu watenda kazi kanisani waliosomea kazi yao ni dalili ya ugonjwa mkubwa zaidi – kudhani kwamba kupatikana kwa maarifa ni sawa na kukua kiroho. Sisi hufikiri kwamba mtu anayejua mengi amekomaa zaidi kiroho – kumbe, inaweza kuwa kinyume chake, akajawa na kiburi kwa sababu ya yote aliyosomea. Paulo aliandika hivi: “Maarifa huleta kiburi” (1Wakor. 8:1 TLR). Tena – kwa hakika – mtu anayesikiliza mihadhara yenye kuchosha kwa miaka miwili au mitatu, anakuwa tayari na yeye kutoa mihadhara inayochosha kila juma!

[3] Katika barua yake ya kwanza kwa Timotheo, na barua yake kwa Tito, Paulo anataja kwamba aliwaacha hao ili waweke wazee au waangalizi katika makanisa. Maana yake ni kwamba Timotheo na Tito wangewasimamia hao wazee na waangalizi kwa muda. Bila shaka walikuwa wanakutana nao mara kwa mara ili kuwafundisha, kama Paulo alivyoandika:- “Na mambo yale uliyoyasikia kwangu mbele ya mashahidi wengi, uwakabidhi watu waaminifu ambao wataweza kuwafundisha na wengine pia” (2Timo. 2:2 – TLR).

[4] Tazama Matendo 2:2, 46; 5:42; 8:3; 12:12; 16:40; 20:20; Warumi 16:5; 1Wakor. 16:19; Wakolosai 4:15; Filemoni mstari wa 2; 2Yohana 1:10.

[5] Ni kitu cha kushangaza kuona kwamba barua za Paulo kwa makanisa zimeandikwa kwa wote hapo kanisani – si kwa wazee au waangalizi tu. Wazee au wachungaji au waangalizi wanatajwa katika barua mbili tu. Katika moja, wanatajwa kwenye salamu – ni kama wameongezwa ili wasidhani kwamba wametengwa (ona Wafilipi 1:1). Katika nyingine, Paulo anawataja wachungaji katika orodha ya watumishi wenye kuwakamilisha watakatifu (ona Waefeso 4:11-12). Pia, ni kitu cha kushangaza kuona jinsi ambavyo Paulo hataji nafasi ya wazee wakati anapotoa maagizo kuhusu maswala ambayo sisi tungedhani yanawahusu, kama vile kuendesha Meza ya Bwana na kutatua matatizo kati ya Wakristo. Hayo yote yanaonyesha kwamba wazee au wachungaji hawakushika nafasi kuu – muhimu sana – ambayo wanashika siku hizi katika makanisa.

 

[6] Ona Matendo 2:2, 46; 5:42; 8:3; 12:12; 16:40; 20:20; Warumi 16:5; 1Wakor. 16:19; Wakolosai 4:15; Filemoni mstari wa 2; 2Yohana 1:10.